Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 25

“Ninakata Rufaa kwa Kaisari!”

“Ninakata Rufaa kwa Kaisari!”

Paulo aweka kielelezo katika kuitetea habari njema

Matendo 25:1–26:32

1, 2. (a) Paulo anajikuta katika hali gani? (b) Rufaa ya Paulo kwa Kaisari inatokeza swali gani?

 PAULO bado yuko chini ya ulinzi mkali jijini Kaisaria. Miaka miwili mapema alipokuwa amerudi Yudea, siku chache tu baada ya kufika kwake Wayahudi walijaribu kumuua mara tatu hivi. (Mdo. 21:27-36; 23:10, 12-15, 27) Kufikia sasa, adui zake hawajafanikiwa, hata hivyo, hawakati tamaa. Paulo anapoona kwamba huenda akakabidhiwa mikononi mwao, anamwambia Festo, Gavana Mroma: “Ninakata rufaa kwa Kaisari!”​—Mdo. 25:11.

2 Je, Yehova aliunga mkono uamuzi wa Paulo wa kukata rufaa kwa maliki wa Roma? Jibu la swali hilo ni muhimu kwetu leo, sisi tunaotoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu. Tunahitaji kujua ikiwa tunaweza kuiga mfano wa Paulo “katika kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema.”​—Flp. 1:7.

“Nimesimama Mbele ya Kiti cha Hukumu” (Mdo. 25:1-12)

3, 4. (a) Kwa nini Wayahudi wanaomba Paulo apelekwe Yerusalemu, naye anaepuka kifo jinsi gani? (b) Kama alivyomtegemeza Paulo, Yehova huwategemeza jinsi gani watumishi wake leo?

3 Siku tatu baada ya kuteuliwa, Festo, gavana mpya wa Roma katika mkoa wa Yudea, anaenda Yerusalemu. a Akiwa huko, anawasikiliza wakuu wa makuhani na wakuu kati ya Wayahudi wakitoa mashtaka mazito dhidi ya Paulo. Wanajua kwamba gavana huyo mpya anataka sana kudumisha amani kati yake nao na Wayahudi wengine wote. Kwa hiyo wanamwomba Festo ampeleke Paulo Yerusalemu, na kumhukumu huko. Hata hivyo, adui hao walikuwa wamepanga njama ya kumuua Paulo akiwa njiani kutoka Kaisaria kwenda Yerusalemu. Festo akataa ombi lao na kusema: “Wale walio na mamlaka kati yenu washuke pamoja nami [mpaka Kaisaria] na kumshtaki, ikiwa kwa kweli mtu huyu amefanya kosa lolote.” (Mdo. 25:5) Hivyo, kwa mara nyingine tena, Paulo anaepuka kifo.

4 Katika kesi zote za Paulo, Yehova alimtegemeza kupitia Bwana Yesu Kristo. Kumbuka kwamba katika maono, Yesu alimwambia mtume wake: “Jipe moyo!” (Mdo. 23:11) Leo, watumishi wa Mungu hukabili upinzani na vitisho. Yehova hatulindi kutokana na kila tatizo, lakini hutupatia hekima na nguvu za kuvumilia. Sikuzote tunaweza kutegemea “nguvu zinazopita zile za kawaida” ambazo Mungu wetu mwenye upendo hutoa.​—2 Kor. 4:7.

5. Festo alishughulikiaje kesi ya Paulo?

5 Siku kadhaa baadaye, Festo “akaketi kwenye kiti cha hukumu” jijini Kaisaria. b Paulo na wanaomshitaki walikuwa wamesimama mbele yake. Akijibu mashtaka yao yasiyo na msingi, Paulo akasema: “Sijatenda dhambi yoyote dhidi ya Sheria ya Wayahudi wala dhidi ya hekalu wala dhidi ya Kaisari.” Mtume huyo hakuwa na hatia na alistahili kuachiliwa huru. Festo atatoa uamuzi gani? Akitamani kukubaliwa na Wayahudi, anamuuliza Paulo: “Je, ungependa kupanda kwenda Yerusalemu ukahukumiwe huko mbele yangu kuhusu mambo haya?” (Mdo. 25:6-9) Pendekezo la kipumbavu sana. Ikiwa Paulo angerudishwa Yerusalemu, watu wanaomshtaki ndio ambao wangemhukumu, na bila shaka angeuawa. Katika kisa hiki, Festo alikuwa akihangaikia manufaa yake ya kisiasa badala ya kuzingatia haki. Pontio Pilato, gavana aliyemtangulia, alitenda vivyo hivyo katika kesi iliyomhusu Yesu. (Yoh. 19:12-16) Leo pia, huenda mahakimu wakatenda isivyo haki ili kuwapendeza wanasiasa. Kwa hiyo, tusishangae mahakama zinapotoa uamuzi usiopatana hata kidogo na ushahidi uliotolewa katika kesi zinazowahusu watu wa Mungu.

6, 7. Kwa nini Paulo alikata rufaa kwa Kaisari, naye aliwawekea Wakristo wa kweli leo mfano gani?

6 Tamaa ya Festo ya kuwapendeza Wayahudi ingeweza kufanya Paulo auawe. Kwa hiyo, Paulo akatumia haki yake akiwa raia wa Roma. Alimwambia Festo: “Mimi nimesimama mbele ya kiti cha hukumu cha Kaisari, ambapo ninapaswa kuhukumiwa. Sijawakosea Wayahudi, nawe pia umegundua jambo hilo. . . . Ninakata rufaa kwa Kaisari!” Baada ya rufaa kukatwa, lazima ingesikilizwa. Festo alikazia hilo kwa kusema: “Umekata rufaa kwa Kaisari; nawe utaenda kwa Kaisari.” (Mdo. 25:10-12) Paulo aliwawekea Wakristo wa kweli leo mfano wa kuiga. Wapinzani wanapojaribu kutunga “matatizo kwa kutumia sheria,” Mashahidi wa Yehova hutumia maandalizi ya kisheria yaliyopo ili kuitetea habari njema. cZab. 94:20.

7 Hivyo, baada ya kufungwa kwa zaidi ya miaka miwili kwa sababu ya makosa ambayo hakuwa amefanya, Paulo alipewa nafasi ya kujitetea jijini Roma. Hata hivyo, kabla ya kuondoka, mtawala mwingine alitaka kumwona.

Tunapohukumiwa isivyofaa, tunakata rufaa

“Sikukosa Kutii” (Mdo. 25:13–26:23)

8, 9. Kwa nini Mfalme Agripa alienda Kaisaria?

8 Siku kadhaa baada ya Paulo kumwambia Festo kwamba anakata rufaa kwa Kaisari, Mfalme Agripa na dada yake, Bernike walifika kwa “ziara ya kumsalimia” gavana huyo mpya. d Katika siku za Waroma, ilikuwa kawaida kwa maofisa kuwatembelea magavana wapya. Kwa kumpongeza Festo, ni wazi kwamba Agripa alikuwa akijaribu kujenga urafiki wa kibinafsi na kisiasa kati yao kwa ajili ya wakati ujao.​—Mdo. 25:13.

9 Festo alimwambia mfalme kumhusu Paulo, naye Agripa akataka kumwona. Siku iliyofuata, watawala hao wawili wakaketi juu ya kiti cha hukumu. Hata hivyo, jambo la kuvutia zaidi lilikuwa maneno ya mfungwa aliyekuwa mbele yao wala si nguvu au fahari yao.​—Mdo. 25:22-27.

10, 11. Paulo alimwonyesha Agripa heshima kwa njia gani, na Paulo alimwambia nini mfalme kuhusu maisha yake ya awali?

10 Paulo alimshukuru kwa heshima Mfalme Agripa kwa kumpa nafasi ya kujitetea, akikiri kwamba mfalme ana ujuzi juu ya desturi zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi. Kisha, Paulo akasimulia maisha yake ya wakati uliopita: “Niliishi nikiwa Farisayo kulingana na madhehebu yetu yenye msimamo mkali zaidi katika ibada yetu.” (Mdo. 26:5) Akiwa Farisayo, Paulo alitazamia kuja kwa Masihi. Sasa akiwa Mkristo, alimtambulisha kwa ujasiri Yesu Kristo kuwa yule aliyekuwa akisubiriwa kwa muda mrefu. Paulo alishtakiwa kwa sababu ya jambo ambalo yeye na wale waliokuwa wakimshtaki waliamini, lile tumaini la ahadi ya Mungu kwa mababu zao. Maelezo ya Paulo yalimchochea Agripa atake kusikia zaidi. e

11 Akikumbuka jinsi alivyokuwa akiwatendea Wakristo kwa ukatili hapo awali, Paulo alisema: “Mimi niliamini kwamba ninapaswa kufanya matendo mengi ili kulipinga jina la Yesu Mnazareti . . . kwa sababu nilikuwa nimewakasirikia sana [wafuasi wa Kristo], nilifikia hatua ya kuwatesa hata katika majiji yaliyo mbali.” (Mdo. 26:9-11) Paulo hakuwa akitia chumvi. Watu wengi walijua jinsi alivyokuwa amewatendea Wakristo kwa ujeuri. (Gal. 1:13, 23) Huenda Agripa alitaka kujua: ‘Ni nini kilichombadili mtu huyu?’

12, 13. (a) Paulo alieleza jinsi gani kugeuzwa kwake? (b) Ni kwa njia gani Paulo alikuwa ‘akiipiga teke michokoo’?

12 Maneno yafuatayo ya Paulo yanatoa jibu: “Nikiwa safarini kwenda Damasko pia nikiwa na mamlaka na maagizo kutoka kwa wakuu wa makuhani, katikati ya mchana niliona barabarani, ewe Mfalme, nuru kutoka mbinguni inayozidi mwangaza wa jua ikimulika kunizunguka mimi na wale waliokuwa wakisafiri pamoja nami. Sisi sote tulipoanguka chini, nikasikia sauti ikiniambia katika lugha ya Kiebrania: ‘Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa? Kuendelea kuipiga teke michokoo kunafanya iwe vigumu kwako.’ Lakini nikauliza: ‘Wewe ni nani Bwana?’ Naye Bwana akajibu: ‘Mimi ni Yesu, ambaye unamtesa.’” fMdo. 26:12-15.

13 Kabla ya tukio hilo lisilo la kawaida, Paulo alikuwa ‘akiipiga teke michokoo.’ Kama vile mnyama wa kubeba mizigo angejiumiza kwa kupiga teke sehemu yenye ncha kali ya mchokoo, Paulo alijiumiza kiroho kwa kupinga mapenzi ya Mungu. Kwa kumtokea Paulo barabarani alipokuwa akielekea Damasko, Yesu aliyekuwa amefufuliwa alimchochea mtu huyo mnyoofu aliyetenda bila kujua, abadili maoni yake.​—Yoh. 16:1, 2.

14, 15. Paulo alisema nini kuhusu mabadiliko aliyokuwa amefanya maishani?

14 Bila shaka Paulo alifanya mabadiliko makubwa maishani. Alimwambia Agripa: “Mimi sikukosa kutii maono hayo kutoka mbinguni, lakini kwanza kwa wale walio huko Damasko kisha kwa wale walio Yerusalemu, na katika nchi yote ya Yudea, na pia kwa mataifa, nilikuwa nikipeleka ujumbe kwamba wanapaswa kutubu na kumgeukia Mungu kwa kufanya matendo yanayoonyesha toba.” (Mdo. 26:19, 20) Kwa miaka mingi, Paulo alikuwa akitimiza mgawo ambao Yesu Kristo alimpatia katika maono hayo aliyopata katikati ya mchana. Alipata matokeo gani? Waliokubali habari njema aliyohubiri Paulo, walitubu mwenendo wao mpotovu na usio mnyoofu, kisha wakamgeukia Mungu. Watu hao wakawa raia wazuri, wanaoheshimu sheria na mamlaka.

15 Hata hivyo, matokeo hayo hayakuwa na maana yoyote kwa Wayahudi waliompinga Paulo. Paulo alisema hivi: “Hiyo ndiyo sababu Wayahudi walinikamata hekaluni na kujaribu kuniua. Hata hivyo, kwa sababu nimepata msaada kutoka kwa Mungu, mpaka leo hii ninaendelea kutoa ushahidi kwa wadogo na wakubwa pia.”​—Mdo. 26:21, 22.

16. Tunaweza kumwigaje Paulo tunapozungumza na mahakimu na watawala kuhusu imani yetu?

16 Tukiwa Wakristo wa kweli, tunapaswa ‘sikuzote kuwa tayari kuitetea’ imani yetu. (1 Pet. 3:15) Tunapozungumza na mahakimu na watawala kuhusu imani yetu, huenda ikafaa kuiga njia ambayo Paulo alitumia alipokuwa akizungumza na Agripa na Festo. Kwa kuwaeleza kwa heshima jinsi kweli za Biblia zimebadili maisha ya watu—yetu wenyewe na ya wale ambao wamekubali ujumbe wetu—huenda tukagusa mioyo ya watu hao wenye mamlaka.

“Ungenishawishi Niwe Mkristo” (Mdo. 26:24-32)

17. Baada ya kumsikiliza Paulo, Festo alisema nini, na ni mtazamo gani kama huo unaoonekana leo?

17 Walipokuwa wakisikiliza ushahidi wenye kusadikisha wa Paulo, watawala hao wawili walichochewa sana. Ona jinsi mambo yalivyokuwa: “Paulo alipokuwa akijitetea kwa kusema mambo hayo, Festo akasema kwa sauti kubwa: ‘Unarukwa na akili, Paulo! Kusoma kwingi kunafanya urukwe na akili!’” (Mdo. 26:24) Huenda maneno ya Festo yanalingana sana na mtazamo unaoonekana leo. Machoni mwa wengi, wale wanaofundisha kweli za Biblia wamerukwa na akili. Wenye hekima ya ulimwengu huona vigumu kukubali fundisho la Biblia kuhusu ufufuo wa wafu.

18. Paulo alimjibuje Festo, na hilo lilimfanya Agripa aseme nini?

18 Hata hivyo, Paulo alimjibu gavana huyo: “Mimi sirukwi na akili, ewe Mtukufu Festo, bali ninasema maneno ya kweli na ya akili timamu. Kwa kweli, mfalme ninayezungumza naye kwa uhuru anajua vizuri mambo haya . . . Je, wewe, Mfalme Agripa, unawaamini Manabii? Ninajua unawaamini.” Agripa akamwambia Paulo: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” (Mdo. 26:25-28) Maneno hayo, yawe yalitoka moyoni au la, yanaonyesha kwamba ushahidi wa Paulo ulikuwa na matokeo makubwa kwa mfalme.

19. Festo na Agripa walifikia mkataa gani kuhusu Paulo?

19 Kisha Agripa na Festo wakasimama, kuonyesha kwamba mahojiano yamefikia mwisho. “Walipokuwa wakiondoka wakaanza kuambiana: ‘Mtu huyu hafanyi lolote linalostahili kifo au vifungo vya gereza.’ Kisha Agripa akamwambia Festo: ‘Mtu huyu angefunguliwa kama hangekuwa amekata rufaa kwa Kaisari.’” (Mdo. 26:31, 32) Walijua kwamba mtu aliyesimama mbele yao hakuwa na hatia. Huenda tangu wakati huo na kuendelea wangekuwa na maoni yanayofaa kuhusu Wakristo.

20. Ushahidi ambao Paulo alitoa mbele ya watu wenye mamlaka ulikuwa na matokeo gani?

20 Hakuna yeyote kati ya watawala hao wawili wenye nguvu aliyekubali habari njema ya Ufalme wa Mungu. Je, kulikuwa na manufaa yoyote kwa Paulo kujitetea mbele ya watu hao? Ndiyo. Kwa kuwa Paulo ‘alipelekwa mbele ya wafalme na magavana’ huko Yudea, habari njema iliwafikia maofisa Waroma ambao huenda hawangehubiriwa kamwe. (Luka 21:12, 13) Pia, mambo yaliyompata na uaminifu wake chini ya majaribu yaliwatia moyo ndugu na dada zake Wakristo.​—Flp. 1:12-14.

21. Tunaweza kupata matokeo gani mazuri tukiendelea na kazi yetu ya Ufalme?

21 Ndivyo ilivyo leo. Tukiendelea na kazi ya Ufalme licha ya majaribu na upinzani, tunaweza kupata matokeo mazuri. Huenda tukawahubiria maofisa ambao hawapatikani kwa urahisi. Kuvumilia kwetu kwa uaminifu kunaweza kuwatia moyo ndugu na dada zetu Wakristo na kuwachochea wawe na ujasiri zaidi katika kazi ya kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu.

a Ona sanduku lenye kichwa “ Porkio Festo—Gavana wa Roma Katika Mkoa wa Yudea.”

b “Kiti cha hukumu” ni kiti kilichokuwa juu ya jukwaa lililoinuliwa. Kwa kuwa kiti hicho kilikuwa juu, basi ilionekana kana kwamba uamuzi wa hakimu unapaswa kuheshimiwa na hauwezi kupingwa. Pilato aliketi juu ya kiti hicho aliposikiliza kesi ya Yesu.

c Ona sanduku lenye kichwa “ Kukata Rufaa kwa Ajili ya Ibada ya Kweli Leo.”

d Ona sanduku lenye kichwa “ Mfalme Herode Agripa wa Pili.”

e Akiwa Mkristo, Paulo aliamini kwamba Yesu ndiye Masihi. Wayahudi, waliomkataa Yesu, walimwona Paulo kuwa mwasi imani.​—Mdo. 21:21, 27, 28.

f Kuhusu kusafiri kwa Paulo “katikati ya mchana,” msomi mmoja wa Biblia anasema hivi: “Isipokuwa iwe kwamba msafiri alikuwa na jambo la dharura sana, alipumzika mchana wakati ambao joto lilikuwa kali sana. Hivyo, Paulo alifanya jitihada nyingi sana ili kuwatesa Wakristo.”