Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 28

“Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia”

“Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia”

Mashahidi wa Yehova wanaendeleza kazi iliyoanzishwa na wafuasi wa Yesu Kristo katika karne ya kwanza

1. Kuna ulinganifu gani kati ya hali ya Wakristo wa karne ya kwanza na Mashahidi wa Yehova leo?

 WALITOA ushahidi kwa bidii. Mioyo yao iliwachochea kukubali msaada na mwongozo wa roho takatifu. Mateso hayakuwanyamazisha. Naye Mungu aliwabariki sana. Hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa kwa Wakristo wa karne ya kwanza, kama vile ilivyo kwa Mashahidi wa Yehova leo.

2, 3. Kwa nini kitabu cha Matendo ni cha pekee?

2 Bila shaka, umetiwa moyo na masimulizi yenye kuimarisha imani na yenye kusisimua ya kitabu cha Biblia cha Matendo ya Mitume! Kitabu hicho ni cha pekee. Ndicho kitabu pekee kilichoongozwa na roho ya Mungu, ambacho kinaeleza historia ya Wakristo wa karne ya kwanza.

3 Kitabu cha Matendo kinataja watu 95 kutoka nchi 32, majiji 54, na visiwa 9. Ni masimulizi yenye kusisimua kuhusu watu wa kawaida, wafuasi wa dini wenye majivuno, wanasiasa wenye kiburi, na watesaji wakatili. Lakini zaidi ya yote, kinasimulia kuhusu ndugu na dada zako wa karne ya kwanza, ambao licha ya hali ngumu ambazo ni kawaida maishani, waliendelea kuhubiri habari njema kwa bidii.

4. Ni nini kinachofanya tuwe na uhusiano wa karibu pamoja na watu kama vile mtume Paulo, Tabitha, na Mashahidi wengine wengi waaminifu wa zamani?

4 Miaka 2,000 hivi imepita tangu siku za mitume wenye bidii Petro na Paulo, daktari mpendwa Luka, Barnaba aliyekuwa mkarimu, Stefano mwenye ujasiri, Tabitha mwenye fadhili, Lidia mkaribishaji wageni, na Mashahidi wengine wengi waliokuwa waaminifu. Ingawa waliishi miaka mingi iliyopita, tunahisi tuna uhusiano wa karibu pamoja nao. Kwa nini? Kwa sababu sisi pia tuna mgawo wa kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Tuna pendeleo kubwa sana la kushiriki katika kazi hiyo!

“. . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—Matendo 1:8

5. Wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza walianza kuhubiri wapi?

5 Hebu fikiria kazi ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake. Aliwaambia: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Kwanza, roho takatifu iliwawezesha wanafunzi kutoa ushahidi “katika Yerusalemu.” (Mdo. 1:1–8:3) Halafu, wakiongozwa na roho, wakatoa ushahidi “katika Yudea yote na Samaria.” (Mdo. 8:4–13:3) Kisha wakaanza kuhubiri “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”​—Mdo. 13:4–28:31.

6, 7. Katika huduma yetu, tuna nini ambacho waamini wenzetu wa karne ya kwanza hawakuwa nacho?

6 Waamini wenzako wa karne ya kwanza hawakuwa na Biblia nzima ili kuitumia katika kazi ya kuhubiri. Injili ya Mathayo haikuwa imeandikwa mpaka karibu mwaka wa 41 W.K. Baadhi ya barua za Paulo ziliandikwa kabla ya kitabu cha Matendo kukamilishwa, karibu mwaka wa 61 W.K. Lakini Wakristo wa karne ya kwanza hawakuwa na nakala za kibinafsi za Maandiko yote Matakatifu wala vitabu na magazeti ya kuwapatia watu wanaopendezwa. Kabla ya kuwa wanafunzi wa Yesu, Wakristo Wayahudi walikuwa wamesikia Maandiko ya Kiebrania yakisomwa katika sinagogi. (2 Kor. 3:14-16) Hata hivyo, wao pia walipaswa kujifunza kwa bidii, kwa kuwa huenda walihitaji kukariri maandiko.

7 Leo, wengi wetu tuna nakala yetu wenyewe ya Biblia na vitabu vingi vinavyotegemea Biblia. Tunafanya wanafunzi kwa kuhubiri habari njema katika nchi 240 na katika lugha nyingi.

Kutiwa Nguvu na Roho Takatifu

8, 9. (a) Roho takatifu iliwawezesha wanafunzi wa Yesu kufanya nini? (b) Mtumwa mwaminifu anatokeza nini kwa msaada wa roho ya Mungu?

8 Yesu alipowaamuru wanafunzi wake wawe mashahidi, aliwaambia: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu.” Wakiongozwa na roho ya Mungu, au nguvu zake za utendaji, hatimaye wafuasi wa Yesu wangekuwa mashahidi duniani pote. Kwa msaada wa roho takatifu, Petro na Paulo waliponya wagonjwa, wakawafukuza roho waovu, na hata kufufua wafu! Hata hivyo, nguvu walizopata kupitia roho takatifu zilikuwa na kusudi muhimu zaidi. Ziliwawezesha mitume na wale wanafunzi wengine kuwapa watu ujuzi sahihi ili wapate uzima wa milele.​—Yoh. 17:3.

9 Katika siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wa Yesu walisema “katika lugha mbalimbali, kama roho ilivyowawezesha kusema.” Hivyo, wakatoa ushahidi kuhusu “mambo makuu ya Mungu.” (Mdo. 2:1-4, 11) Leo, hatuzungumzi kimuujiza katika lugha mbalimbali. Hata hivyo, chini ya mwelekezo wa roho ya Mungu, mtumwa mwaminifu anatoa vitabu na magazeti yanayotegemea Biblia katika lugha nyingi. Kwa mfano, mamilioni ya magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yanachapishwa kila mwezi, na pia katika tovuti yetu ya jw.org, kuna machapisho yanayotegemea Biblia na video katika lugha zaidi ya 1,000. Yote hayo yanatusaidia kutangaza “mambo makuu ya Mungu” kwa watu wa mataifa yote, makabila, na lugha.​—Ufu. 7:9.

10. Tangu mwaka wa 1989, ni nini kimefanywa kuhusiana na kutafsiri Biblia?

10 Tangu mwaka wa 1989, mtumwa mwaminifu ameongeza jitihada za kuhakikisha kwamba Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana katika lugha nyingi. Tayari Biblia hiyo imetafsiriwa katika lugha zaidi ya 200, na mamilioni ya nakala yamechapishwa—nyingine nyingi zikiwa njiani. Mungu tu, kupitia roho yake, ndiye amefanikisha jitihada hizo.

11. Ni mambo gani yametimizwa kuhusiana na kutafsiriwa kwa machapisho ya Mashahidi wa Yehova?

11 Kazi ya kutafsiri inafanywa na maelfu ya Wakristo wanaojitolea katika nchi na maeneo zaidi ya 150. Hilo halitushangazi kwa kuwa hakuna tengenezo lingine lolote duniani linaloongozwa na roho takatifu katika “kutoa ushahidi kamili” ulimwenguni pote kumhusu Yehova Mungu, Mfalme wake wa Kimasihi, na Ufalme uliosimamishwa mbinguni!—Mdo. 28:23.

12. Ni nini kilichomsaidia Paulo na Wakristo wengine kutoa ushahidi?

12 Paulo alipowahubiria Wayahudi na Watu wa Mataifa katika Antiokia ya Pisidia, “wote waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini.” (Mdo. 13:48) Luka anapokamilisha kuandika kitabu cha Matendo, Paulo angali ‘akihubiri ufalme wa Mungu . . . kwa uhuru mwingi wa kusema, bila kizuizi.’ (Mdo. 28:31) Mtume huyo anahubiri wapi? Katika jiji la Roma—makao makuu ya serikali kuu ya ulimwengu! Iwe ni kupitia hotuba au njia nyingine, wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza walifanya kazi yao ya kutoa ushahidi kwa msaada na mwongozo wa roho takatifu.

Uvumilivu Licha ya Mateso

13. Kwa nini tunapaswa kusali tunapokabili mateso?

13 Wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza walipoteswa, walimwomba Yehova awape ujasiri. Ikawaje? Walijazwa roho takatifu na kuwezeshwa kusema neno la Mungu kwa ujasiri. (Mdo. 4:18-31) Sisi pia husali ili tupate hekima na nguvu za kuendelea kutoa ushahidi licha ya mateso. (Yak. 1:2-8) Kwa kuwa tuna baraka za Mungu na msaada wa roho yake, tunaendelea kutangaza Ufalme. Hakuna chochote kinachoweza kuzuia kazi ya kutoa ushahidi—iwe ni upinzani mkali au mateso ya kikatili. Tunapoteswa, tunahitaji kumwomba Yehova atupatie roho takatifu, hekima, na ujasiri wa kutangaza habari njema.​—Luka 11:13.

14, 15. (a) Mambo yalikuwaje baada ya “dhiki iliyotokea kwa sababu ya Stefano”? (b) Katika siku zetu, watu wengi katika eneo la Siberia walipataje kweli?

14 Stefano alitoa ushahidi kwa ujasiri kabla ya kuuawa na adui zake. (Mdo. 6:5; 7:54-60) Kutaniko lilipoanza “kuteswa sana,” wanafunzi wote isipokuwa mitume walitawanyika kotekote katika maeneo ya Yudea na Samaria. Lakini hilo halikuzuia kazi ya kutoa ushahidi. Filipo alienda Samaria ‘kuwahubiria kumhusu Kristo,’ naye alipata matokeo mazuri. (Mdo. 8:1-8, 14, 15, 25) Isitoshe, tunaambiwa: “Wale waliokuwa wametawanyika kwa sababu ya dhiki iliyotokea kuhusiana na Stefano, wakaenda mpaka Foinike, Kipro, na Antiokia, lakini walitangaza lile neno kwa Wayahudi tu. Hata hivyo, wanaume fulani kati yao kutoka Kipro na Kirene walikuja Antiokia na kuanza kuongea na watu waliozungumza Kigiriki, wakitangaza habari njema ya Bwana Yesu.” (Mdo. 11:19, 20) Wakati huo, mateso yalichangia kuenezwa kwa ujumbe wa Ufalme.

15 Katika siku zetu, jambo kama hilo lilitokea katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti. Hasa katika miaka ya 1950, maelfu ya Mashahidi wa Yehova walipelekwa uhamishoni Siberia. Kwa kuwa walipelekwa katika kambi mbalimbali, habari njema iliendelea kuenea katika eneo hilo kubwa. Bila shaka, Mashahidi wengi hivyo hawangeweza kamwe kupata pesa za kusafiri kilomita zaidi ya 10,000 ili kutangaza habari njema! Hata hivyo, serikali yenyewe iliwapeleka sehemu mbalimbali za nchi hiyo. Ndugu mmoja alisema: “Wenye mamlaka wenyewe waliwasaidia maelfu ya watu wanyoofu katika eneo la Siberia kujua kweli.”

Baraka Nyingi za Yehova

16, 17. Kitabu cha Matendo kinataja mambo gani yanayoonyesha kwamba Yehova anabariki kazi ya kutoa ushahidi?

16 Bila shaka Yehova aliwabariki sana Wakristo wa karne ya kwanza. Paulo na wengine walipanda na kutilia maji, “lakini Mungu akaendelea kuikuza.” (1 Kor. 3:5, 6) Kitabu cha Matendo kina mifano mingi ya ukuzi huo unaopatikana kwa sababu ya baraka za Yehova katika kazi ya kutoa ushahidi. Kwa mfano, “Neno la Mungu likazidi kuenea, na idadi ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana huko Yerusalemu.” (Mdo. 6:7) Kadiri kazi ya kutoa ushahidi ilivyoenea, “kutaniko katika eneo lote la Yudea, Galilaya, na Samaria likaingia katika kipindi cha amani, huku likijengwa; nalo lilipokuwa likitembea katika kumwogopa Yehova na katika faraja ya roho takatifu, likaendelea kuongezeka.”​—Mdo. 9:31.

17 Katika Antiokia ya Siria, Wayahudi na watu waliozungumza Kigiriki walihubiriwa na mashahidi wenye ujasiri. Masimulizi yanasema: “Isitoshe, mkono wa Yehova ulikuwa pamoja nao, na idadi kubwa wakawa waamini na kumgeukia Bwana.” (Mdo. 11:21) Tunasoma hivi kuhusu maendeleo zaidi katika jiji hilo: “Neno la Yehova likazidi kukua na kuenea.” (Mdo. 12:24) Na kwa sababu ya bidii ya Paulo na wengine katika kazi ya kutoa ushahidi kwa Watu wa Mataifa, “kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova likazidi kukua na kusitawi.”​—Mdo. 19:20.

18, 19. (a) Tunajuaje kwamba “mkono wa Yehova” uko pamoja nasi? (b) Toa mfano unaoonyesha kwamba Yehova huwategemeza watu wake.

18 Bila shaka, “mkono wa Yehova” uko pamoja nasi leo. Ndiyo sababu watu wengi sana wanakuwa wanaamini na kuonyesha wakfu wao kwa Mungu kwa kubatizwa. Isitoshe, msaada na baraka za Mungu zinatuwezesha kuvumilia upinzani—au hata mateso makali—na kuendelea kuitimiza huduma yetu kwa mafanikio, kama vile Paulo na Wakristo wengine wa karne ya kwanza walivyofanya. (Mdo. 14:19-21) Yehova Mungu atatusaidia sikuzote. “Mikono [yake] ya milele” inaendelea kutusaidia katika majaribu yetu yote. (Kum. 33:27) Na pia tusisahau kwamba kwa sababu ya jina lake kuu, Yehova hatawaacha kamwe watu wake.​—1 Sam. 12:22; Zab. 94:14.

19 Kwa mfano: Maofisa wa Nazi walimpeleka Ndugu Harald Abt katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu kwa sababu ya kazi yake ya kutoa ushahidi. Mnamo Mei 1942, polisi wapelelezi walienda alipokuwa akikaa mke wake, Elsa, wakamchukua binti yao mdogo, na kumkamata Elsa. Alipelekwa katika kambi mbalimbali za mateso. Dada Abt alisema: “Muda niliokaa katika kambi za mateso za Ujerumani, ulinifundisha jambo fulani muhimu. Kwamba roho ya Yehova inaweza kukutia nguvu unapokuwa chini ya jaribu kali! Kabla ya kukamatwa nilikuwa nimesoma barua ya dada mmoja aliyeandika kwamba wakati wa majaribu makali, roho ya Yehova hutusaidia kuwa watulivu. Nilifikiri kwamba alikuwa akitia chumvi. Lakini mimi mwenyewe nilipokuwa nikijaribiwa, nilitambua ukweli wa mambo aliyosema. Kwa kweli, ndivyo inavyokuwa. Si rahisi kuwazia, ikiwa wewe binafsi hujapatwa na majaribu. Lakini kwangu, ndivyo ilivyokuwa.”

Endelea Kutoa Ushahidi Kamili!

20. Paulo alifanya nini alipokuwa katika kifungo cha nyumbani, na hilo linawezaje kuwatia moyo baadhi ya ndugu na dada zetu?

20 Masimulizi ya kitabu cha Matendo yanamalizika Paulo ‘akihubiri Ufalme wa Mungu,’ kwa bidii. (Mdo. 28:31) Kwa sababu alikuwa katika kifungo cha nyumbani, hakuwa na uhuru wa kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba katika jiji la Roma. Hata hivyo, aliendelea kuwahubiria waliomtembelea. Leo, baadhi ya ndugu na dada zetu hawawezi kutoka nyumbani, labda ni wagonjwa kitandani, au wako katika makao ya kuwatunzia wazee, wagonjwa, au walemavu. Hata hivyo, upendo wao kwa Mungu na tamaa yao ya kutoa ushahidi bado ni yenye nguvu. Tunasali kwa ajili yao na tunaweza kumwomba Baba yetu wa mbinguni awasaidie wakutane na watu wanaotaka kujifunza kumhusu na kuhusu makusudi yake mazuri.

21. Kwa nini tunapaswa kutoa ushahidi haraka?

21 Wengi wetu tunaweza kushiriki katika utumishi wa nyumba kwa nyumba na katika njia nyingine za kufanya wanafunzi. Kwa hiyo, kila mmoja wetu na afanye kila awezalo ili tutimize wajibu wetu tukiwa watangazaji wa Ufalme, na kushiriki kutoa ushahidi “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” Lazima kazi hii ifanywe haraka, kwa sababu “ishara” ya kuwapo kwa Kristo inaonekana wazi. (Mt. 24:3-14) Hatuna wakati wa kupoteza. Tuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.”​—1 Kor. 15:58.

22. Tunapaswa kuazimia kufanya nini tunaipongojea siku ya Yehova?

22 Tunapongojea “kuja kwa ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha,” na tuazimie kuendelea kutoa ushahidi kwa ujasiri na kwa uaminifu. (Yoe. 2:31) Bado tutapata watu wengi walio kama Waberoya ambao “walilikubali neno kwa hamu kubwa ya akili.” (Mdo. 17:10, 11) Kwa hiyo, na tuendelee kutoa ushahidi mpaka tutakapoambiwa: “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu!” (Mt. 25:23) Tukitimiza sehemu yetu kwa bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi leo na kudumisha uaminifu wetu kwa Yehova, bila shaka, tutafurahi milele kwamba tulishiriki katika “kutoa ushahidi kamili” kuhusu Ufalme wa Mungu!