Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 27

“Kutoa Ushahidi Kamili”

“Kutoa Ushahidi Kamili”

Paulo afungwa Roma, aendelea kuhubiri

Matendo 28:11-31

1. Paulo na wenzake wana uhakika gani, na kwa nini?

 MELI yenye sanamu ya “Wana wa Zeu,” ambayo huenda ni meli kubwa ya nafaka, inasafiri kutoka kisiwani Malta katika Bahari ya Mediterania kwenda Italia. Ni mwaka wa 59 hivi W.K. Mtume Paulo—mfungwa aliye chini ya ulinzi wa askari—pamoja na Wakristo wenzake, Luka na Aristarko, wako katika meli hiyo. (Mdo. 27:2) Tofauti na mafundi wa mitambo wa meli hiyo, waeneza injili hao hawahitaji ulinzi wa ndugu pacha Castor na Pollux, wana wa Zeu, mungu wa Wagiriki. (Mdo. 28:11) Paulo na wenzake ni waabudu wa Yehova, aliyetabiri kwamba Paulo atatoa ushahidi kuhusu ile kweli jijini Roma na kwamba atasimama mbele ya Kaisari.​—Mdo. 23:11; 27:24.

2, 3. Meli ya Paulo inaelekea wapi, na anategemezwa jinsi gani katika safari yake?

2 Siku tatu baada ya kutia nanga Sirakusa, jiji lenye kupendeza la Sisili na maarufu kama Athene na Roma, meli yang’oa nanga na kuelekea Regiamu katika rasi ya Italia. Kisha, ikisukumwa na upepo wa kusi, meli hiyo yasafiri umbali wa kilomita 320 hadi bandari ya Italia inayoitwa Puteoli (karibu na mahali panapoitwa Naples leo), na kufika huko siku ya pili, haraka kuliko ilivyo kawaida.​—Mdo. 28:12, 13.

3 Sasa, Paulo anaanza sehemu ya mwisho ya safari ya kuelekea Roma, ambapo atasimama mbele ya Maliki Nero. Katika safari yake yote, “Mungu wa faraja yote” amekuwa pamoja na Paulo. (2 Kor. 1:3) Kama tutakavyoona, Yehova hakumwacha kamwe; naye Paulo hakupunguza bidii yake akiwa mmishonari.

“Paulo. . . Akamshukuru Mungu na Kujipa Moyo” (Mdo. 28:14, 15)

4, 5. (a) Ni ukarimu gani ambao Paulo na wenzake walionyeshwa walipofika Puteoli, na kwa nini Paulo alipewa uhuru mwingi? (b) Hata wanapofungwa gerezani, Wakristo wanaweza kunufaikaje kutokana na mwenendo wao mzuri?

4 Walipofika Puteoli, Paulo na wenzake ‘waliwakuta akina ndugu huko, wakawasihi wakae pamoja nao kwa siku saba.’ (Mdo. 28:14) Huo ni mfano mzuri sana wa ukarimu wa Kikristo! Bila shaka ndugu hao wakarimu walibarikiwa hata zaidi kwa kuwa Paulo na wenzake waliwatia moyo kiroho. Hata hivyo, mfungwa anayelindwa angewezaje kupata uhuru mwingi hivyo? Huenda kwa sababu walinzi hao Waroma walimwamini kabisa mtume huyo.

5 Vivyo hivyo leo, watumishi wa Yehova, wanapokuwa katika magereza na kambi za mateso, mara nyingi hupewa uhuru zaidi na kuruhusiwa kufanya mambo ambayo wafungwa wengine hawawezi kwa sababu wakiwa Wakristo, ni wanyoofu na wenye kutegemeka. Kwa mfano, nchini Romania, mtu aliyehukumiwa kifungo cha miaka 75 kwa kosa la wizi, alianza kujifunza Neno la Mungu na kufanya mabadiliko makubwa maishani. Kwa sababu ya mabadiliko aliyokuwa amefanya, wenye mamlaka gerezani walimpa kazi ya kwenda mjini—akiwa peke yake—na kununua vitu vinavyohitajiwa gerezani! Zaidi ya yote, mwenendo wetu mzuri humtukuza Yehova.​—1 Pet. 2:12.

6, 7. Akina ndugu wa Roma walionyeshaje ukarimu wa pekee?

6 Kutoka Puteoli, yawezekana kwamba Paulo na wenzake walitembea kwa miguu kilomita 50 hivi hadi Kapua kwenye Njia ya Apio, inayoenda Roma. Ikiwa imetandazwa kwa mawe, njia hiyo maarufu ilikuwa na mandhari zenye kuvutia za nchi ya Italia, na mtu akiwa sehemu fulani katika njia hiyo, angeweza hata kuiona Bahari ya Mediterania. Pia, njia hiyo ilipitia Pontine Marshes, eneo lenye majimaji, kilomita 60 hivi kutoka Roma, ambapo Soko la Apio lilikuwa. Ndugu wa Roma “waliposikia habari zetu,” aandika Luka, baadhi yao walikuja mpaka Soko la Apio, na wengine wakasubiri mahali pa kupumzika panapoitwa Mikahawa Mitatu, umbali wa kilomita 50 hivi kutoka Roma. Walimpenda sana Paulo.​—Mdo. 28:15.

7 Soko la Apio halikuwa mahali pa kustarehesha, hasa kwa wasafiri waliohitaji kupumzika baada ya safari ndefu yenye kuchosha. Horace, mshairi Mroma, anataja kwamba soko hilo lilikuwa “limesongamana na wenye mashua na wenye mikahawa wajeuri.” Aliandika kwamba “maji yalikuwa yenye kuchukiza.” Naye hata alikataa kula mahali hapo! Bila kujali yote hayo, akina ndugu kutoka Roma walimngoja Paulo na wenzake ili kuwasindikiza katika sehemu ya mwisho ya safari yao.

8. Kwa nini Paulo alimshukuru Mungu “alipowaona” ndugu zake?

8 “Alipowaona” ndugu zake, masimulizi yanasema, “Paulo . . . akamshukuru Mungu na kujipa moyo.” (Mdo. 28:15) Ndiyo, alipowaona tu ndugu hao wapendwa, ambao huenda mtume huyo aliwajua baadhi yao kibinafsi, alihisi kwamba amepata nguvu mpya na kufarijiwa. Kwa nini Paulo alimshukuru Mungu? Alijua kwamba upendo usio na ubinafsi ni sehemu ya tunda la roho. (Gal. 5:22) Leo pia, roho takatifu huwachochea Wakristo kujitoa kwa ajili ya wengine na kuwafariji wenye uhitaji.​—1 The. 5:11, 14.

9. Tunaweza kuigaje roho iliyoonyeshwa na ndugu waliokuja kumpokea Paulo?

9 Kwa mfano, roho takatifu huwachochea akina ndugu kuwaonyesha ukarimu waangalizi wa mzunguko, wamishonari, na watumishi wengine wa wakati wote, ambao wengi wao wamejinyima mengi ili kumtumikia Yehova kikamili zaidi. Jiulize: ‘Kuna lolote ninaloweza kufanya ili kutegemeza ziara ya mwangalizi wa mzunguko, labda kwa kumwonyesha ukarimu yeye na mke wake ikiwa ameoa? Ninaweza kupanga kuhubiri pamoja nao?’ Ukifanya hivyo utapata baraka nyingi. Kwa mfano, wazia shangwe ambayo ndugu wa Roma walipata walipokuwa wakimsikiliza Paulo na wenzake wakisimulia mambo mengi waliyojionea yenye kujenga imani.​—Mdo. 15:3, 4.

“Yanasemwa Vibaya Kila Mahali” (Mdo. 28:16-22)

10. Hali ya Paulo ilikuwaje huko Roma, na mtume huyo alifanya nini mara tu baada ya kufika huko?

10 Mwishowe, kikundi hicho cha wasafiri kilipoingia Roma, “Paulo aliruhusiwa kukaa peke yake akiwa na mwanajeshi aliyemlinda.” (Mdo. 28:16) Kwa kawaida, wafungwa wa makosa madogo walizuiliwa kwa kufungwa kwa minyororo pamoja na askari walinzi. Hata hivyo, kwa kuwa Paulo alikuwa mtangazaji wa Ufalme, minyororo hiyo haikumfunga kinywa. Kwa hiyo, baada ya kupumzika kwa siku tatu, akawaita wakuu wa Wayahudi waliokuwa Roma ili ajitambulishe na kuwatolea ushahidi.

11, 12. Alipokuwa akizungumza na Wayahudi wenzake, Paulo alijaribu jinsi gani kuondoa chuki yoyote ambayo huenda walikuwa nayo kumwelekea?

11 Paulo akasema hivi: “Wanaume, akina ndugu, ingawa sikuwa nimefanya jambo lolote kinyume cha watu au desturi za mababu zetu, nilikabidhiwa nikiwa mfungwa kutoka Yerusalemu na kutiwa mikononi mwa Waroma. Na baada ya kufanya uchunguzi, walitaka kuniacha huru, kwa maana hawakuwa na sababu yoyote ya kuniua. Lakini Wayahudi walipopinga, nililazimika kukata rufaa kwa Kaisari, lakini si kwa sababu nilikuwa na shtaka lolote dhidi ya taifa langu.”​—Mdo. 28:17-19.

12 Kwa kuwaita Wayahudi hao “ndugu,” Paulo alijaribu kujenga urafiki na kuondoa chuki yoyote ambayo huenda ilikuwa kati yao. (1 Kor. 9:20) Pia, aliwajulisha wazi kwamba hakuja kuwalaumu Wayahudi wenzake, bali ili kukata rufaa kwa Kaisari. Hata hivyo, Wayahudi hao walishangaa kusikia kwamba amekuja kukata rufaa. (Mdo. 28:21) Kwa nini Wayahudi wa Yudea hawakuwajulisha lolote? Kitabu kimoja kinasema: “Inaonekana kwamba meli ya Paulo ilikuwa miongoni mwa meli za kwanza kufika Italia baada ya majira ya baridi kali, nao wawakilishi wa wenye mamlaka miongoni mwa Wayahudi wa Yerusalemu hawakuwa wamefika, wala barua zozote kuhusu kesi hiyo hazikuwa zimewasili.”

13, 14. Paulo alianzaje kuzungumzia Ufalme, na tunawezaje kuiga mfano wake?

13 Kisha, Paulo akaanza kuzungumza kuhusu Ufalme. Alianza kwa kutaja jambo ambalo bila shaka liliamsha hamu ya Wayahudi waliokuwa wamekuja. Alisema: “Kwa sababu hii niliomba kuwaona na kuzungumza nanyi, kwa maana nimefungwa mnyororo huu kwa sababu ya tumaini la Israeli.” (Mdo. 28:20) Tumaini hilo lilitegemea Masihi na Ufalme wake uliokuwa ukitangazwa na kutaniko la Kikristo. Wazee hao Wayahudi wakamjibu: “Tunaona inafaa kusikia kutoka kwako maoni yako, kwa maana kwa kweli kuhusu madhehebu haya, tunajua yanasemwa vibaya kila mahali.”​—Mdo. 28:22.

14 Tunapopata nafasi ya kutangaza habari njema, tunaweza kufuata mfano wa Paulo kwa kutumia maneno yanayoamsha hamu ya wasikilizaji wetu. Tunaweza kupata mapendekezo mazuri katika vitabu kama vile Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Boresha Uwezo Wako wa Kusoma na Kufundisha. Je, unavitumia vizuri vitabu hivyo vya kujifunzia Biblia?

“Kutoa Ushahidi Kamili”​—Mfano Tunaoweza Kufuata (Mdo. 28:23-29)

15. Ni mambo gani manne yanayojitokeza wazi kuhusiana na njia ya Paulo ya kuhubiri?

15 Siku iliyopangwa, Wayahudi wenyeji “wakaja wakiwa wengi hata zaidi,” mahali alipoishi Paulo. Naye akawafafanulia jambo hilo “kuanzia asubuhi mpaka jioni . . . na kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu, ili kuwashawishi kumhusu Yesu kwa kutumia Sheria ya Musa na pia Manabii.” (Mdo. 28:23) Mambo manne yanajitokeza wazi kuhusiana na njia ya Paulo ya kuhubiri. Kwanza, alikazia Ufalme wa Mungu. Pili, alijitahidi kuchochea mioyo ya wasikilizaji wake kwa kuwashawishi. Tatu, alijadiliana nao kwa kutumia Maandiko. Nne, alijitolea kwa nafsi yote, akiwahubiria “kuanzia asubuhi mpaka jioni.” Alituwekea mfano mzuri sana! Alipata matokeo gani? “Baadhi yao wakaanza kuamini,” lakini wengine hawakuamini. Mgawanyiko ukazuka, nao watu “wakaanza kuondoka,” asema Luka.​—Mdo. 28:24, 25a.

16-18. Kwa nini kutoitikia kwa Wayahudi wa Roma hakukumshangaza Paulo, na tunapaswa kuhisije ujumbe wetu unapokataliwa?

16 Hilo halikumshangaza Paulo, kwa kuwa lilipatana na unabii wa Biblia, isitoshe haikuwa mara ya kwanza kwake kujionea hilo. (Mdo. 13:42-47; 18:5, 6; 19:8, 9) Kwa hiyo, Paulo akawaambia wale waliokuwa wakiondoka: “Kwa kufaa roho takatifu ilisema kupitia Isaya nabii kwa mababu zenu, ikisema, ‘Nenda kwa watu hawa uwaambie: “Kwa kweli mtasikia lakini hamtaelewa kamwe, na kwa kweli mtatazama, lakini hamtaona kamwe. Kwa maana mioyo ya watu hawa imekuwa migumu.”’” (Mdo. 28:25b-27) Neno la lugha ya awali linalotafsiriwa “mgumu” hurejelea moyo “mnene” au “wenye mafuta mengi,” hivi kwamba ujumbe wa Ufalme haungeweza kupenya. (Mdo. 28:27) Ilikuwa hali yenye kusikitisha sana!

17 Tofauti na Wayahudi hao, Paulo alisema kwamba, ‘mataifa wangesikiliza.’ (Mdo. 28:28; Zab. 67:2; Isa. 11:10) Bila shaka, mtume huyo angeweza kusema hivyo akiwa na uhakika, kwa sababu alijionea Watu wa Mataifa wakikubali ujumbe wa Ufalme!—Mdo. 13:48; 14:27.

18 Kama Paulo, hatupaswi kuvunjika moyo watu wanapokataa habari njema. Tayari tunajua kwamba ni wachache watakaoipata barabara inayoongoza kwenye uzima. (Mt. 7:13, 14) Pia, watu wenye mwelekeo unaofaa wanapojiunga na ibada ya kweli, tunapaswa kufurahi na kuwakaribisha kwa moyo wote.​—Luka 15:7.

“Akiwahubiria Ufalme wa Mungu” (Mdo. 28:30, 31)

19. Ni kwa njia gani Paulo alitumia hali zake vizuri?

19 Luka anamalizia masimulizi yake kwa jambo lenye kutia moyo sana. Anasema hivi: “[Paulo] akakaa huko kwa miaka miwili kamili katika nyumba yake ya kukodi, naye alikuwa akiwakaribisha kwa fadhili wale wote waliomtembelea, akiwahubiria Ufalme wa Mungu na kuwafundisha kumhusu Bwana Yesu Kristo kwa uhuru mwingi wa kusema, bila kizuizi.” (Mdo. 28:30, 31) Hicho ni kielelezo kizuri sana cha ukarimu, imani, na bidii!

20, 21. Taja watu mbalimbali walionufaika na huduma ya Paulo katika jiji la Roma.

20 Mmoja wa watu waliopokewa na Paulo kwa fadhili ni Onesimo, mtumwa aliyetoroka Kolosai. Paulo alimsaidia Onesimo kuwa Mkristo, naye Onesimo akawa “ndugu . . . mwaminifu na mpendwa” kwa Paulo. Paulo anamwita “mwanangu . . . ambaye nimekuwa baba yake.” (Kol. 4:9; Flm. 10-12) Bila shaka Onesimo alimtia moyo sana Paulo! a

21 Wengine pia walinufaika na mfano mzuri wa Paulo. Aliwaandikia hivi Wafilipi: “Hali yangu kwa kweli imesaidia kuendeleza habari njema, hivi kwamba vifungo vyangu vya gereza kwa ajili ya Kristo vimejulikana wazi kati ya Walinzi wote wa Mfalme na watu wengine wote. Sasa akina ndugu wengi katika Bwana wamekuwa na uhakika kwa sababu ya vifungo vyangu vya gereza, nao wanaonyesha uhodari mwingi wa kulisema neno la Mungu bila woga.”​—Flp. 1:12-14.

22. Paulo alitumia wakati wake jinsi gani alipokuwa mfungwa jijini Roma?

22 Paulo alitumia wakati wake akiwa mfungwa jijini Roma kuandika barua muhimu ambazo sasa ni sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. b Barua hizo walizoandikiwa Wakristo wa karne ya kwanza, ziliwanufaisha sana. Sisi pia tunanufaika na barua za Paulo kwa sababu ushauri aliotoa ulioongozwa na roho unatufaa leo pia.​—2 Tim. 3:16, 17.

23, 24. Kama Paulo, Wakristo wengi leo wamedumishaje shangwe yao na kuendelea kuhubiri ijapokuwa wamefungwa isivyo haki?

23 Kufikia wakati ambapo alifunguliwa, ijapokuwa hautajwi katika kitabu cha Matendo, Paulo alikuwa amekaa gerezani miaka minne—miwili Kaisaria na miwili Roma. c (Mdo. 23:35; 24:27) Hata hivyo, hakupoteza shangwe, bali aliendelea kufanya yote aliyoweza katika utumishi wa Mungu. Vivyo hivyo pia, watumishi wengi wa Yehova leo, ijapokuwa wanatiwa gerezani isivyo haki kwa sababu ya imani yao, wao huendelea kuwa na shangwe na kuendelea kuhubiri. Fikiria mfano wa Adolfo, aliyefungwa huko Hispania kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi. “Unatushangaza,” akasema ofisa mmoja. “Tumekuwa tukifanya maisha yako yawe magumu, na kadiri tunavyozidi ndivyo unavyozidi kutabasamu na kuzungumza nasi kwa fadhili.”

24 Baada ya muda, Adolfo aliaminika kiasi cha kwamba mlango wa chumba chake cha gereza ulikuwa ukiachwa wazi. Askari walikuwa wakija kumuuliza maswali ya Biblia. Hata mlinzi mmoja alikuwa akiingia katika chumba cha Adolfo ili kuisoma Biblia, huku Adolfo akimlinda asikamatwe. Kwa hiyo, mfungwa akawa “akimlinda” mlinzi! Mfano mzuri wa Mashahidi kama hao na utuchochee kuonyesha “uhodari mwingi wa kulisema neno la Mungu bila woga,” hata chini ya hali ngumu.

25, 26. Paulo alijionea utimizo wa unabii gani miaka isiyozidi 30 baadaye, na hali hiyo inalingana jinsi gani na siku zetu?

25 Mtume wa Kristo aliye katika kifungo cha nyumbani “akiwahubiria Ufalme wa Mungu” wote wanaomtembelea—mwisho wenye kutia moyo sana wa kitabu cha Matendo! Katika sura ya kwanza, tulisoma kuhusu mgawo ambao Yesu aliwapa wafuasi wake aliposema: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Sasa, miaka isiyozidi 30 baadaye, tayari ujumbe wa Ufalme ulikuwa umehubiriwa “katika uumbaji wote chini ya mbingu.” d (Kol. 1:23) Huo ni ushahidi mkubwa wa nguvu za roho ya Mungu!—Zek. 4:6.

26 Leo, roho hiyo imewawezesha ndugu za Kristo na waandamani wao, “kondoo wengine,” kuendelea “kutoa ushahidi kamili kuhusiana na ufalme wa Mungu” katika nchi zaidi ya 240! (Yoh. 10:16; Mdo. 28:23) Je, unashiriki kikamili katika kazi hiyo?

a Paulo alitaka Onesimo akae naye, lakini hilo lingevunja sheria za Roma na vilevile haki za Mkristo Filemoni, bwana mkubwa wa Onesimo. Kwa hiyo, Onesimo akarudi kwa Filemoni, akiwa na barua kutoka kwa Paulo iliyomhimiza Filemoni ampokee kwa fadhili, kama ndugu yake wa kiroho.​—Flm. 13-19.

c Ona sanduku lenye kichwa “ Maisha ya Paulo Baada ya Mwaka wa 61 W.K.

d Ona sanduku lenye kichwa “ Habari Njema ‘Ilihubiriwa Katika Uumbaji Wote.’”