Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 9

“Mungu Hana Ubaguzi”

“Mungu Hana Ubaguzi”

Watu wa Mataifa wasiotahiriwa waanza kuhubiriwa

Matendo 10:1–11:30

1-3. Petro aliona nini katika njozi, na kwa nini tunahitaji kuelewa maana yake?

 NI MWAKA wa 36 W.K. Petro anasali kwenye paa ya nyumba iliyo karibu na bahari, katika bandari ya Yopa. Amekuwa akiishi katika nyumba hiyo kwa siku kadhaa sasa. Kwa kiasi fulani, kukaa kwake hapo kunaonyesha kwamba hana ubaguzi. Mwenye nyumba hiyo anayeitwa Simoni ni mtengenezaji wa ngozi. Kwa kweli, si kila Myahudi angekubali kukaa na mtu kama huyo. a Hata hivyo, Petro ataelewa vizuri zaidi maoni ya Yehova kuhusu ubaguzi.

2 Petro anaposali anaanza kuona njozi. Mambo anayoona katika maono hayo yangeweza kumchukiza Myahudi yeyote. Anaona kitu fulani, kama shuka kubwa, kikishuka kutoka mbinguni kikiwa na wanyama ambao kulingana na Sheria si safi. Anapoambiwa achinje na kula, Petro anajibu hivi: “Sijawahi kula kitu chochote kilicho najisi na kisicho safi.” Mara tatu anaambiwa: “Acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu amevitakasa.” (Mdo. 10:14-16) Baada ya maono hayo, Petro anachanganyikiwa, ijapokuwa si kwa muda mrefu.

3 Mambo aliyoona Petro yanamaanisha nini? Maono hayo ni muhimu kwa kuwa yanatusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyowaona watu. Tukiwa Wakristo wa kweli, tutaweza kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu ikiwa tutakuwa na maoni kama ya Mungu kuelekea watu. Ili kuelewa maana ya mambo hayo, acheni tuchunguze matukio fulani yaliyotukia karibu na wakati huo.

“Aliomba Dua Sikuzote kwa Mungu” (Mdo. 10:1-8)

4, 5. Kornelio ni nani, na ni nini kilichotokea alipokuwa akisali?

4 Petro hakuwa na habari kwamba siku moja kabla, kilomita 50 hivi upande wa kaskazini huko Kaisaria, mtu anayeitwa Kornelio alikuwa pia amepata maono kutoka kwa Mungu. Kornelio, ofisa katika jeshi la Roma, alikuwa mtu ‘aliyemwogopa Mungu.’ b Pia, aliisimamia nyumba yake vizuri kwa sababu alikuwa “mtu aliyemheshimu na kumwogopa Mungu, yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake.” Kornelio hakuwa Myahudi mgeuzwa imani; bali alikuwa Mtu wa Mataifa asiyetahiriwa. Hata hivyo, aliwahurumia Wayahudi wenye uhitaji, na aliwasaidia kimwili. Mtu huyo mnyoofu “aliomba dua sikuzote kwa Mungu.”​—Mdo. 10:2.

5 Karibu saa 9 hivi mchana, Kornelio alikuwa akisali. Kisha akaanza kuona maono, na katika maono hayo malaika anamwambia: “Mungu amesikia sala zako na kuona zawadi zako za rehema, naye anazikumbuka.” (Mdo. 10:4) Kornelio anatii agizo la malaika na kuwatuma watu wakamwite mtume Petro. Kornelio angekuwa wa kwanza kati ya Watu wa Mataifa wasiotahiriwa kupata pendeleo la pekee. Angepata pendeleo la kusikia ujumbe wa wokovu.

6, 7. (a) Simulia jambo lililoonwa linaloonyesha kwamba Mungu anajibu sala za watu wanyoofu ambao wanataka kujua ukweli kumhusu. (b) Tunaweza kusema nini kuhusu mambo kama hayo yaliyoonwa?

6 Je, Mungu anasikiliza sala za watu wanyoofu wanaotaka kujua ukweli kumhusu? Fikiria jambo hili lililoonwa. Mwanamke mmoja huko Albania alipewa gazeti la Mnara wa Mlinzi linalozungumzia jinsi ya kulea watoto. c Alimwambia hivi Shahidi aliyemtembelea: “Kwa kweli nilikuwa nikisali kwa Mungu ili anisaidie kujua jinsi ya kulea binti zangu! Bila shaka amekutuma! Nimepata ninachohitaji!” Mwanamke huyo na binti zake wakaanza kujifunza, baadaye mume wake pia akaanza kujifunza.

7 Je, hicho ni kisa cha pekee? Hapana! Mambo kama hayo hutokea sehemu mbalimbali duniani, na yanatokea mara nyingi sana. Tuseme nini? Kwanza, Yehova hujibu sala za watu wanaomtafuta. (1 Fal. 8:41-43; Zab. 65:2) Pili, malaika wanatusaidia katika kazi yetu ya kuhubiri.​—Ufu. 14:6, 7.

“Petro Akiwa . . . Anashangaa” (Mdo. 10:9-23a)

8, 9. Roho ilimjulisha nini Petro, na aliitikiaje?

8 Watumishi waliotumwa na Kornelio walipofika, Petro alikuwa juu ya paa, “akiwa bado anashangaa” kuhusu maana ya maono hayo. (Mdo. 10:17) Je, Petro, ambaye mara tatu alikataa kula vyakula vilivyokuwa najisi kulingana na Sheria, atakubali kwenda na watu hao na kuingia kwenye nyumba ya Mtu wa Mataifa? Roho takatifu ilifunua kusudi la Mungu katika kisa hicho. Petro aliambiwa hivi: “Tazama! Wanaume watatu wanakutafuta. Basi simama, ushuke na kwenda pamoja nao, usiwe na shaka kamwe, kwa sababu nimewatuma.” (Mdo. 10:19, 20) Bila shaka, maono ambayo Petro aliona yalimtayarisha kutii mwongozo wa roho takatifu.

9 Baada ya kujua kwamba Mungu alimwelekeza Kornelio awatume watu waje kumchukua, Petro akawakaribisha “na kukaa nao.” (Mdo. 10:23a) Tayari mtume huyo mtiifu ameanza kubadili maoni yake yapatane na mapenzi ya Mungu.

10. Yehova anawaongozaje watu wake, na ni maswali gani tunayohitaji kujiuliza?

10 Hadi leo hii, Yehova amekuwa akiwaongoza watu wake hatua kwa hatua. (Met. 4:18) Kupitia roho takatifu, anamwongoza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Mara kwa mara, huenda tukapokea marekebisho fulani katika uelewaji wetu wa Neno la Mungu au mabadiliko fulani katika utaratibu wa tengenezo. Ingefaa kujiuliza: ‘Ninaitikiaje mabadiliko hayo yanapotokea? Ninakubali kwa unyenyekevu mwongozo wa roho ya Mungu katika mambo hayo?’

Petro “Akawaamuru Wabatizwe” (Mdo. 10:23b-48)

11, 12. Petro alifanya nini alipofika Kaisaria, na alijifunza jambo gani?

11 Siku iliyofuata, Petro na wengine tisa—watatu waliotumwa na Kornelio na “ndugu sita” Wayahudi kutoka Yopa—wakafunga safari kuelekea Kaisaria. (Mdo. 11:12) Akiwa anamtarajia Petro, Kornelio aliwakusanya “watu wake wa ukoo na rafiki zake wa karibu”​—inaonekana wote walikuwa Watu wa Mataifa. (Mdo. 10:24) Anapofika, Petro anafanya jambo ambalo awali asingeweza kufanya: Anaingia kwenye nyumba ya Mtu wa Mataifa ambaye hajatahiriwa! Petro anaeleza hivi: “Mnajua jinsi ilivyo kinyume cha sheria kwa Myahudi kushirikiana au kumkaribia mtu wa jamii nyingine, lakini Mungu amenionyesha kwamba sipaswi kumwita mtu yeyote najisi au asiye safi.” (Mdo. 10:28) Kufikia sasa, Petro anaelewa kwamba maono aliyopata yalikusudiwa kumfundisha kanuni ambayo haikuhusu tu vyakula ambavyo mtu anaweza kula. Hapaswi “kumwita mtu yeyote [hata wa Mataifa] najisi.”

“Bila shaka, Kornelio alikuwa akiwatarajia naye alikuwa amekusanya watu wake wa ukoo na rafiki zake wa karibu.”—Matendo 10:24

12 Kila mtu aliyekuwapo alitaka kumsikiliza Petro. Kornelio akasema: “Sote tupo mbele za Mungu ili kuyasikia mambo yote ambayo Yehova amekuamuru useme.” (Mdo. 10:33) Hebu wazia jinsi ambavyo ungehisi ikiwa mtu anayependezwa angekuambia hivyo! Petro anaanza kwa kusema hivi kwa usadikisho: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.” (Mdo. 10:34, 35) Petro alikuwa amejifunza kwamba Mungu haangalii rangi, taifa, au jinsi mtu alivyo kwa nje. Kisha Petro akaendelea kuwahubiria kuhusu huduma, kifo, na ufufuo wa Yesu.

13, 14. (a) Kugeuzwa imani kwa Kornelio na watu wengine wa Mataifa mwaka wa 36 W.K. kuliashiria nini? (b) Kwa nini hatupaswi kuwahukumu watu kwa jinsi wanavyoonekana?

13 Sasa jambo fulani lisilo la kawaida latokea: “Petro alipokuwa akizungumza,” roho takatifu ikamiminwa juu ya “watu wa mataifa.” (Mdo. 10:44, 45) Hiki ndicho kisa cha pekee kinachotajwa katika Maandiko cha kumiminwa kwa roho kabla ya ubatizo. Akiwa ametambua hiyo ni ishara kwamba Mungu amewakubali, Petro “akawaamuru [kikundi hicho cha Watu wa Mataifa] wabatizwe.” (Mdo. 10:48) Kugeuzwa kwa Watu hao wa Mataifa mwaka wa 36 W.K. kuliashiria mwisho wa nyakati za kupendelewa kwa Wayahudi. (Dan. 9:24-27) Katika pindi hiyo, Petro aliutumia ufunguo wa tatu na wa mwisho wa Ufalme. (Mt. 16:19) Ufunguo huo ulitoa nafasi kwa Watu wa Mataifa wasiotahiriwa kuwa Wakristo watiwa-mafuta.

14 Tukiwa watangazaji wa Ufalme leo, tunatambua kwamba “Mungu hana ubaguzi.” (Rom. 2:11) Ni mapenzi yake kwamba “watu wa namna zote waokolewe.” (1 Tim. 2:4) Hivyo, tusiwahukumu watu kwa kutegemea jinsi wanavyoonekana. Jukumu letu ni kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu, na hilo linatia ndani kuwahubiria watu wote, bila kujali rangi, taifa, jinsi wanavyoonekana, au dini zao.

“Wakaacha Kupinga, Nao Wakamtukuza Mungu” (Mdo. 11:1-18)

15, 16. Kwa nini baadhi ya Wakristo Wayahudi walimkosoa Petro, naye alitoa sababu gani?

15 Bila shaka, akiwa na hamu ya kuripoti yaliyotokea, Petro anafunga safari kuelekea Yerusalemu. Habari hizo kwamba Watu wa Mataifa wasiotahiriwa walikuwa “wamelikubali neno la Mungu,” zilikuwa zimefika Yerusalemu. Muda mfupi baada ya Petro kufika, “wale waliounga mkono kutahiriwa wakaanza kumkosoa.” Walichukizwa kwa sababu aliingia ‘ndani ya nyumba ya watu ambao hawajatahiriwa naye akala pamoja nao.’ (Mdo. 11:1-3) Tatizo halikuwa ikiwa Watu wa Mataifa wangeweza kuwa wafuasi wa Kristo au la. Badala yake, wanafunzi hao Wayahudi walisisitiza kwamba Watu wa Mataifa wanapaswa kushika Sheria—kutia ndani sheria ya kutahiriwa—ili waweze kumwabudu Yehova kwa njia inayokubalika. Ni wazi kwamba haikuwa rahisi kwa baadhi ya wanafunzi Wayahudi kuacha kufuata Sheria ya Musa.

16 Petro alitoa sababu gani? Kulingana na Matendo 11:4-16, alizungumzia mambo manne yanayothibitisha kwamba huo ulikuwa mwongozo kutoka mbinguni: (1) maono aliyopokea kutoka kwa Mungu (Mstari 4-10); (2) amri aliyopewa na roho (Mstari 11, 12); (3) malaika kumtembelea Kornelio (Mstari 13, 14); na (4) Watu wa Mataifa kumiminiwa roho takatifu. (Mstari 15, 16) Petro alimalizia hotuba yake kwa kuuliza swali hili lenye kuchochea: “Kwa hiyo, ikiwa Mungu aliwapa [Watu wa Mataifa walioamini] zawadi ileile ya bure [roho takatifu] kama alivyotupatia sisi [Wayahudi] ambao tumemwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani hata niweze kumzuia Mungu?”​—Mdo. 11:17.

17, 18. (a) Kwa nini ushahidi wa Petro ulikuwa mtihani mkubwa kwa Wakristo Wayahudi? (b) Kwa nini huenda ikawa vigumu kudumisha umoja kutanikoni, na tunapaswa kujiuliza maswali gani?

17 Ushahidi huo wa Petro ulikuwa mtihani mkubwa kwa Wakristo Wayahudi. Je, wataondoa ubaguzi wowote walio nao na kuwakubali wanafunzi wapya wa Mataifa wawe Wakristo wenzao? Simulizi hilo linatuambia: “[Mitume na Wakristo wengine Wayahudi] Waliposikia mambo hayo, wakaacha kupinga, nao wakamtukuza Mungu wakisema: ‘Kwa hiyo basi, Mungu pia ameruhusu watu wa mataifa watubu ili wapate uzima.’” (Mdo. 11:18) Maoni hayo mazuri yalidumisha umoja wa kutaniko.

18 Leo, huenda isiwe rahisi kudumisha umoja, kwa sababu waabudu wa kweli wametoka “mataifa yote na makabila na jamii na lugha.” (Ufu. 7:9) Kwa sababu hiyo, katika makutaniko mengi kuna watu wa rangi, tamaduni na malezi mbalimbali. Tunapaswa kujiuliza: ‘Je, nimeondoa dalili zozote za ubaguzi moyoni mwangu? Je, nimeazimia kutoruhusu mambo yanayowagawanya watu leo—kama vile utaifa, ukabila, utamaduni, na ubaguzi—yaongoze jinsi ninavyowatendea Wakristo wenzangu?’ Kumbuka jinsi Petro (Kefa) alivyotenda miaka kadhaa baada ya Watu wa Mataifa kugeuzwa imani. Ubaguzi wa watu wengine ulifanya ‘ajitenge’ na Wakristo wa Mataifa mengine, naye alirekebishwa na Paulo. (Gal. 2:11-14) Na tuendelee kuwa macho sikuzote ili tusinaswe na mtego huo wa kuwa na ubaguzi.

“Idadi Kubwa Wakawa Waamini” (Mdo. 11:19-26a)

19. Wakristo Wayahudi huko Antiokia walianza kuwahubiria nani, nao walipata matokeo gani?

19 Je, wafuasi wa Yesu walianza kuwahubiria Watu wa Mataifa wasiotahiriwa? Fikiria kilichotokea baadaye huko Antiokia ya Siria. d Jiji hilo lilikuwa na idadi kubwa ya Wayahudi, hata hivyo hakukuwa na uadui mkubwa kati ya Wayahudi na Watu wa Mataifa. Hivyo, haikuwa vigumu kuwahubiria Watu wa Mataifa waliokuwa wakiishi Antiokia. Hapo ndipo baadhi ya wanafunzi Wayahudi walipoanza kuwahubiria habari njema “watu waliozungumza Kigiriki.” (Mdo. 11:20) Waliwahubiria Wayahudi waliozungumza Kigiriki na Watu wa Mataifa wasiotahiriwa. Yehova alibariki kazi hiyo, na “idadi kubwa wakawa waamini.”​—Mdo. 11:21.

20, 21. Barnaba alionyeshaje unyenyekevu, na tunaweza kuonyeshaje unyenyekevu tunapokuwa katika huduma?

20 Ili kuhakikisha kwamba watu katika eneo la Antiokia wanahubiriwa, kutaniko la Yerusalemu lilimtuma Barnaba aende huko. Bila shaka hangeweza kuwahudumia watu wote wanaopendezwa katika eneo hilo akiwa peke yake. Sauli, ambaye baadaye angekuwa mtume kwa mataifa, alikuwa katika nafasi nzuri zaidi ya kumsaidia. (Mdo. 9:15; Rom. 1:5) Je, Barnaba alianza kushindana na Sauli? Hapana, badala yake, Barnaba alionyesha unyenyekevu. Alienda Tarso kumtafuta Sauli, na kwenda naye Antiokia. Walikaa huko mwaka mzima wakiwaimarisha wanafunzi katika kutaniko hilo.​—Mdo. 11:22-26a.

21 Tunawezaje kuonyesha unyenyekevu katika huduma yetu? Tukiwa wanyenyekevu tutajua mipaka yetu. Tuna uwezo na vipawa mbalimbali. Kwa mfano, huenda wengine wakawa na ustadi wa kuhubiri isivyo rasmi au nyumba kwa nyumba lakini ikawa vigumu kwao kufanya ziara za kurudia au kuanzisha mafunzo ya Biblia. Kwa nini usiombe msaada ikiwa ungependa kuboresha sehemu fulani ya utumishi wako? Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia kupata matokeo mazuri katika huduma na shangwe zaidi.​—1 Kor. 9:26.

‘Walituma Msaada’ (Mdo. 11:26b-30)

22, 23. Ndugu wa Antiokia walionyeshaje upendo wa kindugu, na watu wa Mungu leo wanaigaje mfano wao?

22 Antiokia ndipo ambapo kwa mara ya kwanza “wanafunzi waliitwa Wakristo kupitia mwongozo wa Mungu.” (Mdo. 11:26b) Jina hilo lililotolewa kwa mwongozo wa Mungu liliwafaa watu hao waliofuata mfano wa Kristo katika maisha yao. Kadiri Watu wa Mataifa walivyokuwa wakijiunga na kutaniko la Kikristo, je, kulikuwa na umoja wa kindugu kati yao na Wayahudi? Fikiria kilichotokea wakati wa njaa kali ya karibu mwaka wa 46 W.K. e Wakati huo, njaa iliwaathiri hasa maskini ambao hawakuwa na akiba ya fedha wala chakula. Wakati huo wa njaa, Wakristo Wayahudi walioishi Yudea, ambao wengi wao walikuwa maskini, walihitaji msaada. Walipojua kwamba kuna uhitaji huo, akina ndugu huko Antiokia—kutia ndani Watu wa Mataifa waliokuwa Wakristo, ‘walituma msaada’ kwa akina ndugu walioishi Yudea. (Mdo. 11:29) Huo ulikuwa upendo wa kindugu!

23 Ndivyo ilivyo pia miongoni mwa watu wa Mungu leo. Tunaposikia kwamba ndugu zetu—katika nchi nyingine au eneo letu—wana uhitaji fulani, tunajitoa kwa hiari ili kuwasaidia. Halmashauri za Tawi huunda Halmashauri za Kutoa Misaada ili kuwasaidia ndugu ambao wameathiriwa na majanga ya asili, kama vile vimbunga, matetemeko ya nchi, na tsunami. Jitihada hizo zote za kutoa misaada zinaonyesha kwamba tuna undugu wa kweli.​—Yoh. 13:34, 35; 1 Yoh. 3:17.

24. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunazingatia maana ya maono ambayo Petro aliona?

24 Tukiwa Wakristo wa kweli, tunazingatia maana ya maono ambayo Petro aliona akiwa kwenye paa ya nyumba huko Yopa katika karne ya kwanza. Tunamwabudu Mungu asiye na ubaguzi. Mapenzi yake ni kwamba tutoe ushahidi kamili kuhusu Ufalme wake. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwahubiria watu bila kujali rangi, taifa au hali yao. Na tuazimie kuwapa nafasi watu wote wanaotaka kusikiliza habari njema.​—Rom. 10:11-13.

Ndugu zetu wanapokuwa na uhitaji, tunakuwa tayari kuwasaidia

a Baadhi ya Wayahudi waliwadharau watengenezaji wa ngozi kwa sababu walikuwa wakishika ngozi, mizoga ya wanyama na vitu vingine vyenye kuchukiza katika kazi yao. Watengenezaji wa ngozi walionwa kuwa hawastahili kuingia hekaluni, nao walipaswa kufanyia kazi yao umbali usiopungua mita 22 kutoka mjini. Huenda hiyo ndiyo sababu nyumba ya Simoni ilikuwa “kando ya bahari.”​—Mdo. 10:6.

b Ona sanduku lenye kichwa “ Kornelio na Jeshi la Roma.”

c Makala yenye kichwa “Mashauri Yenye Kutegemeka Kuhusu Kulea Watoto,” toleo la Novemba 1, 2006, ukurasa wa 4 hadi 7.

d Ona sanduku lenye kichwa “ Antiokia ya Siria.”

e Mwanahistoria Myahudi Yosefo, aliandika kuhusu “njaa kali” iliyotokea wakati wa utawala wa Maliki Klaudio (41-54 W.K.).