Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 10

“Neno la Yehova Likazidi Kukua”

“Neno la Yehova Likazidi Kukua”

Petro aokolewa; habari njema yaenea licha ya mateso

Matendo 12:1-25

1-4. Petro anakabili hali gani ngumu, na ungefanya nini ikiwa ungekuwa katika hali hiyo?

 BAADA ya Petro kutiwa gerezani, lango kubwa ya chuma likafungwa kwa kishindo. Akiwa amefungwa minyororo katikati ya walinzi wawili Waroma, mmoja upande huu na mwingine upande ule, anapelekwa na kuingizwa katika chumba cha gereza. Anakaa humo kwa muda mrefu huenda hata kwa siku kadhaa akisubiri kujua kitakachompata. Akiwa huko, hakuna kitu kingine alichoona zaidi ya minyororo aliyofungwa, kuta, nondo za chumba cha gereza, na walinzi walio kando yake.

2 Hukumu inayotolewa ni kali sana. Mfalme Herode Agripa wa Kwanza aliazimia kumuua Petro. a Alipanga kumleta Petro mbele ya watu baada ya Pasaka, na kumhukumu adhabu ya kifo ili kuwafurahisha. Hicho si kitisho tu kwa kuwa muda mfupi uliopita, mtawala huyo alikuwa amemuua mtume Yakobo.

3 Ni usiku wa kuamkia siku ambayo angeuawa. Petro anafikiria nini akiwa gerezani? Je, inawezekana anakumbuka miaka kadhaa iliyopita, wakati ambapo Yesu alitabiri kwamba siku moja Petro angefungwa na kupelekwa asikotaka, yaani, angeuawa? (Yoh. 21:18, 19) Huenda Petro anafikiri kwamba wakati huo umefika.

4 Kama ungekuwa Petro, ungefanya nini? Wengi wangekata tamaa wakifikiri kwamba hakuna tumaini lolote. Hata hivyo, je, kuna hali yoyote inayoweza kuwafanya wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo wakose kuwa na tumaini? Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Petro na Wakristo wenzake walivyotenda walipoteswa? Acheni tuone.

“Kutaniko Lilikuwa Likisali kwa Mungu kwa Bidii Sana” (Mdo. 12:1-5)

5, 6. (a) Mfalme Herode Agripa wa Kwanza alilishambulia kutaniko la Kikristo jinsi gani na kwa nini? (b) Kwa nini kifo cha Yakobo kilikuwa pigo kubwa kwa kutaniko?

5 Kama tulivyojifunza katika sura ya tisa ya kitabu hiki, kutaniko la Kikristo lilifurahia sana kugeuzwa imani kwa Kornelio na familia yake. Lakini lazima Wayahudi wasiokuwa waamini walishangaa sana kuona Wakristo wengi Wayahudi wakiabudu pamoja na watu wasio Wayahudi.

6 Herode, mwanasiasa mwenye hila, aliona hiyo kuwa nafasi nzuri ya kujitafutia sifa miongoni mwa Wayahudi, naye akaanza kuwatesa Wakristo. Bila shaka alikuwa amesikia kwamba mtume Yakobo alikuwa rafiki wa karibu wa Yesu Kristo. Kwa hiyo, Herode “alimuua kwa upanga Yakobo ndugu ya Yohana.” (Mdo. 12:2) Hilo lilikuwa pigo kubwa sana kwa kutaniko! Yakobo alikuwa mmoja kati ya mitume watatu walioshuhudia sura ya Yesu ilipogeuka na alijionea miujiza mingine ambayo wale mitume wengine hawakuiona. (Mt. 17:1, 2; Marko 5:37-42) Yesu alimwita Yakobo na ndugu yake Yohana, “Wana wa Ngurumo” kwa sababu ya bidii yao. (Marko 3:17) Kwa hiyo Yakobo alipouawa, kutaniko lilipoteza shahidi mwaminifu, mwenye ujasiri, na mtume mpendwa.

7, 8. Kutaniko lilifanya nini Petro alipokuwa gerezani?

7 Kama Agripa alivyotazamia, kuuawa kwa Yakobo kuliwafurahisha Wayahudi. Hivyo, akapata ujasiri wa kupanga njama ya kumwua Petro. Kama inavyosimuliwa mwanzoni mwa sura hii, aliagiza Petro akamatwe. Hata hivyo, kama tulivyoona katika Sura ya 5 ya kitabu hiki, huenda Agripa alikumbuka kutokana na matukio ya wakati uliopita kwamba magereza hayangeweza kuwazuia mitume. Ili kuhakikisha kwamba hatoroki, Herode anaagiza Petro afungwe minyororo katikati ya walinzi 2 na kuagiza walinzi wengine 16 wamlinde kwa zamu usiku na mchana. Akitoroka, walinzi hao watapata adhabu kali. Katika hali hizo, Wakristo wenzake wangefanya nini?

8 Kutaniko lilijua jambo la kufanya. Andiko la Matendo 12:5 linasema: “Petro alikuwa gerezani lakini kutaniko lilikuwa likisali kwa Mungu kwa bidii sana kwa ajili yake.” Walisali kwa bidii na kutoka moyoni kwa ajili ya ndugu yao mpendwa. Kifo cha Yakobo hakikuwavunja moyo wala kuwafanya wapuuze sala. Yehova anathamini sana sala za watumishi wake naye huzijibu ikiwa zinapatana na mapenzi yake. (Ebr. 13:18, 19; Yak. 5:16) Wakristo leo wanapaswa kukumbuka hilo.

9. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano uliowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza kuhusu sala?

9 Je, unajua waabudu wenzako wanaokabili majaribu? Huenda wanavumilia mateso, wamepigwa marufuku na serikali, au wamepatwa na majanga ya asili. Unaweza kuwakumbuka katika sala zako. Labda unawajua wengine wanaokabili hali ngumu kama vile matatizo ya familia, kuvunjika moyo, au mambo yanayojaribu imani yao. Ukitafakari kabla ya kusali, unaweza kukumbuka ndugu na dada ambao utawataja unaposali kwa Yehova, “Msikiaji wa sala.” (Zab. 65:2) Bila shaka wewe pia ungependa ndugu na dada zako wafanye hivyo unapokabili hali ngumu.

Tunasali kwa ajili ya ndugu zetu walio gerezani kwa sababu ya imani yao

“Uendelee Kunifuata” (Mdo. 12:6-11)

10, 11. Eleza jinsi malaika wa Yehova alivyomtoa Petro gerezani.

10 Je, Petro alikuwa na wasiwasi? Hatujui. Hata hivyo, usiku wa mwisho akiwa gerezani, alikuwa amelala usingizi mzito huku akilindwa na walinzi wawili. Bila shaka mwanamume huyo mwenye imani alijua kwamba hata nini kitokee, yuko salama mikononi mwa Yehova. (Rom. 14:7, 8) Vyovyote vile, Petro hakutazamia kamwe mambo yaliyotokea muda mfupi baadaye. Ghafla, nuru ikang’aa katika chumba cha gereza. Malaika akasimama kwenye chumba hicho bila kuonekana na walinzi na kumwamsha Petro. Minyororo aliyofungwa—iliyoonekana haiwezi kukatika—ikaanguka!

“Wakafika kwenye lango la chuma linaloelekea jijini, nalo likafunguka lenyewe mbele yao.”—Matendo 12:10

11 Malaika huyo aanza kumhimiza Petro: “Simama upesi! . . . Vaa nguo na uvae viatu vyako . . . Vaa vazi lako la nje.” Petro akafanya hivyo bila kusita. Mwishowe malaika akamwambia: “Uendelee kunifuata,” naye Petro akafanya hivyo. Wakatoka katika chumba hicho, wakawapita walinzi waliokuwa nje kimyakimya hadi kwenye lango kubwa la chuma. Watapitaje? Ikiwa Petro alijiuliza swali hilo, alipata jibu mara moja. Walipokaribia, lango likafunguka “lenyewe.” Ghafla, wakatoka nje na kuingia barabarani, kisha malaika akamwacha. Baada ya Petro kuachwa, alitambua kwamba jambo hilo halikuwa ndoto wala maono, bali alikuwa huru.​—Mdo. 12:7-11.

12. Kwa nini tunaweza kufarijika tunapotafakari jinsi Yehova alivyomkomboa Petro?

12 Bila shaka tunafarijika sana tunapotafakari nguvu za Yehova zisizo na mipaka za kuwakomboa watumishi wake. Petro alifungwa na mfalme wa serikali iliyokuwa na nguvu zaidi katika ulimwengu wa wakati huo. Hata hivyo, Petro aliokolewa kutoka gerezani. Ni kweli kwamba Yehova hafanyi miujiza kama hiyo kwa watumishi wake wote. Hakufanya hivyo kwa Yakobo, wala baadaye wakati unabii wa Yesu kumhusu mtume Petro ulipotimia. Leo, Wakristo hawatazamii kukombolewa kimuujiza. Hata hivyo, tunajua kwamba Yehova hajabadilika. (Mal. 3:6) Hivi karibuni, atamtumia Mwana wake kuwaweka huru mamilioni ya watu kutoka katika gereza kuu zaidi, yaani, kifo. (Yoh. 5:28, 29) Ahadi kama hizo zinaweza kututia moyo tunapokabili majaribu.

“Wakamwona Nao Wakashangaa” (Mdo. 12:12-17)

13-15. (a) Washiriki wa kutaniko waliokutanika katika nyumba ya Maria walitendaje Petro alipofika? (b) Kitabu cha Matendo kinaanza kuzungumzia nini, na Petro aliendelea kuwasaidiaje ndugu na dada zake wa kiroho?

13 Petro alisimama barabarani usiku huku akifikiria aende wapi. Kisha akaamua. Maria, mwanamke Mkristo alikuwa akiishi karibu na eneo hilo. Huenda alikuwa mjane mwenye mali na nyumba kubwa ambayo ingeweza kutumiwa na kutaniko. Maria alikuwa mama ya Yohana Marko, anayetajwa hapa kwa mara ya kwanza katika kitabu cha Matendo na ambaye baadaye Petro alimwita mwanangu. (1 Pet. 5:13) Usiku huo, washiriki wengi wa kutaniko walikuwa nyumbani kwa Maria wakisali kwa bidii, ingawa ilikuwa usiku sana. Walikuwa wakisali ili Petro afunguliwe, hata hivyo hawakutazamia kwamba Yehova angejibu sala yao mara moja!

14 Petro anapiga hodi kwenye lango la kuingia kwenye ua wa nyumba hiyo. Kijakazi anayeitwa Roda—jina la Kigiriki ambalo humaanisha “Waridi”​—akaenda kumfungulia. Haamini anachosikia. Alisikia sauti ya Petro. Badala ya kufungua lango, msichana huyo mwenye shangwe anarudi haraka ndani ya nyumba na kuwaambia washiriki wa kutaniko kwamba Petro amekuja. Wanasema amerukwa na akili, lakini anaendelea kusisitiza. Haachi kusema ukweli. Wakiwa hawamwamini, baadhi yao wanasema huenda ni malaika anayemwakilisha Petro. (Mdo. 12:12-15) Wakati huo wote, Petro anaendelea kupiga hodi, na mwishowe wanaenda langoni na kumfungulia.

15 Walipofungua mlango, “wakamwona nao wakashangaa”! (Mdo. 12:16) Petro analazimika kuwanyamazisha ili awaeleze yaliyokuwa yametokea. Kisha anawaagiza wamwambie Yakobo na akina ndugu, naye anaondoka kabla hajakamatwa na askari wa Herode. Halafu anaenda eneo lingine lililo salama na kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Petro anatajwa kwenye sura ya 15 wakati suala la tohara lilipokuwa likizungumziwa, na baada ya hapo hatajwi tena katika kitabu cha Matendo. Sasa kitabu hicho kinazungumzia kazi na safari za mtume Paulo. Hata hivyo, tuna uhakika kwamba popote alipoenda, Petro aliimarisha imani ya ndugu na dada. Alipoondoka, alikiacha kikundi kilichokuwa katika nyumba ya Maria kikiwa na furaha.

16. Kwa nini tunaweza kutazamia kufurahia mambo mengi wakati ujao?

16 Nyakati nyingine Yehova hujibu sala za watumishi wake kuliko walivyotarajia, nao huwa na shangwe nyingi sana. Hivyo ndivyo ndugu na dada walivyohisi usiku huo, Petro alipoachiliwa. Sisi pia, huenda tukahisi hivyo tunapopata baraka nyingi za Yehova. (Met. 10:22) Wakati ujao, tutaona ahadi zote za Yehova zikitimizwa duniani pote. Ahadi hizo zitatimizwa kwa kiwango kikubwa kuliko tunavyowazia. Kwa hiyo, tukiendelea kuwa waaminifu, tunaweza kutazamia kufurahia mambo mengi wakati ujao.

“Malaika wa Yehova Akampiga” (Mdo. 12:18-25)

17, 18. Kwa nini umati ulianza kumsifu Herode?

17 Herode alishangaa sana kwamba Petro alitoka gerezani lakini hakufurahishwa na jambo hilo. Mara moja akaamuru Petro atafutwe na walinzi waliokuwa wakimlinda wahojiwe. ‘Wakapelekwa kuadhibiwa.’ Huenda waliuawa. (Mdo. 12:19) Herode Agripa hakuwa na huruma wala rehema. Je, mtu huyo mkatili alipata adhabu anayostahili?

18 Huenda Agripa aliaibika kwa sababu hakufaulu kumuua Petro, hata hivyo, baada ya muda mfupi alipata nafasi nyingine ya kujitukuza. Kulikuwa na mkutano na adui zake ambao walitaka kufanya amani. Bila shaka alikuwa na hamu ya kutoa hotuba mbele ya umati huo. Luka anasema kwamba “Herode alivaa mavazi ya kifalme” ili kujitayarisha kwa ajili ya mkutano huo. Yosefo, mwanahistoria Myahudi aliandika kwamba vazi la Herode lilikuwa la fedha, naye mfalme alipopigwa na jua, vazi hilo lilionekana liking’aa kwa utukufu. Kisha mwanasiasa huyo mwenye kiburi akatoa hotuba. Umati uliokuwa ukimsifu ukapaaza sauti na kusema: “Hii ni sauti ya mungu, si ya mwanadamu!”​—Mdo. 12:20-22.

19, 20. (a) Kwa nini Yehova alimwadhibu Herode? (b) Kwa nini tunaweza kupata faraja kutokana na kilichompata Herode Agripa?

19 Mungu tu ndiye anayestahili utukufu huo, naye alikuwa akitazama! Herode angeweza kuepuka msiba. Angeweza kuukemea umati huo au kukataa sifa hizo. Badala yake, alionyesha waziwazi ukweli wa methali hii: “Kiburi hutangulia kuanguka kwa kishindo.” (Met. 16:18) “Papo hapo malaika wa Yehova akampiga,” na kusababisha mtu huyo mbinafsi na mwenye kiburi afe kifo chenye maumivu. Herode “akaliwa na wadudu akafa.” (Mdo. 12:23) Yosefo anasema kuwa Agripa alishambuliwa ghafla, na mfalme huyo alitambua kwamba anakufa kwa sababu ya kukubali kusifiwa na umati. Kulingana na Yosefo, Agripa aliendelea kuteseka katika hali hiyo kwa siku tano kabla ya kufa. b

20 Wakati mwingine huenda ikaonekana kwamba watu wasiomwogopa Mungu wanaendelea kufanya uovu bila kuadhibiwa. Hilo halipaswi kutushangaza, kwa kuwa “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) Hata hivyo, watumishi waaminifu wa Mungu huumia sana wanapowaona waovu wakiendelea kufanya uovu bila kuadhibiwa. Ndiyo sababu masimulizi kama haya yanawafariji sana. Ni kana kwamba tunamwona Yehova akiingilia kati, na kuwakumbusha watumishi wake wote kwamba anapenda haki. (Zab. 33:5) Hivi karibuni, Yehova ataleta haki duniani pote.

21. Matendo sura ya 12 inahusu nini hasa, na kwa nini kujua jambo hilo kunatufariji?

21 Masimulizi hayo yanamalizia kwa kitia moyo hiki: “Neno la Yehova likazidi kukua na kuenea.” (Mdo. 12:24) Ripoti hiyo kuhusu kuenea kwa kazi ya kuhubiri inatukumbusha jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi yetu ya kuhubiri. Habari zilizo katika Matendo sura ya 12 si masimulizi tu ya kifo cha mtume mmoja na kuokolewa kwa mwingine. Masimulizi hayo pia yanahusu jinsi Yehova anavyovunja mipango ya Shetani ya kujaribu kuangamiza kutaniko la Kikristo na kukomesha kazi ya kuhubiri. Mashambulizi yote ya Shetani hayakufanikiwa kama tu ambavyo hila zake zote hazitafanikiwa. (Isa. 54:17) Hata hivyo, wale walio upande wa Yehova na Yesu Kristo hawatashindwa kamwe. Jambo hilo linatia moyo sana. Leo, tuna pendeleo kubwa la kueneza “neno la Yehova.”

a Ona sanduku lenye kichwa “ Mfalme Herode Agripa wa Kwanza.”

b Daktari mmoja ambaye pia ni mwandishi wa vitabu, aliandika kwamba huenda ugonjwa ambao Yosefo na Luka wanataja ulisababishwa na minyoo iliyoziba utumbo. Nyakati nyingine mtu mwenye ugonjwa huo hutapika minyoo au, anapokaribia kufa, minyoo hiyo hutoka. Kitabu kimoja kinasema: “Maneno hususa ya kidaktari anayotumia Luka yanafafanua vizuri kifo chenye maumivu kilichompata [Herode].”