Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 7

Kutangaza “Habari Njema Kumhusu Yesu”

Kutangaza “Habari Njema Kumhusu Yesu”

Filipo aweka mfano mzuri katika kueneza Injili

MATENDO 8:4-40

1, 2. Ni kwa njia gani jitihada za kuzuia kazi ya kuhubiri habari njema katika karne ya kwanza hazikufanikiwa?

 MATESO makali yameanza, na Sauli akaanza “kulishambulia” kutaniko—maneno ambayo katika lugha ya awali, yanamaanisha kulitesa kutaniko kikatili. (Mdo. 8:3) Wanafunzi wanatawanyika. Huenda kwa watu fulani ikaonekana kwamba lengo la Sauli la kuumaliza Ukristo litatimia. Hata hivyo, kwa sababu ya kutawanyika kwa Wakristo jambo fulani lisilotarajiwa linatokea. Jambo gani?

2 Wakristo hao waliotawanyika wakaanza ‘kutangaza habari njema ya lile neno’ katika nchi ambazo wamekimbilia. (Mdo. 8:4) Hebu wazia! Mateso hayakuzuia habari njema bali yalichangia kuenea kwa ujumbe huo! Kwa kuwatawanya wanafunzi, bila kukusudia, watesaji hao wamesaidia kazi ya kuhubiri Ufalme ienee katika maeneo ya mbali. Kama tutakavyoona, jambo fulani linalofanana na hilo limetokea katika siku zetu.

“Wale Waliotawanyika” (Mdo. 8:4-8)

3. (a) Filipo alikuwa nani? (b) Kwa nini Samaria haikuwa imehubiriwa sana, na Yesu alitabiri nini kuhusu eneo hilo?

3 Filipo ni mmoja wa “wale waliotawanyika.” a (Mdo. 8:4; ona sanduku “ Filipo ‘Mweneza-Injili,’”) Alienda Samaria, jiji ambalo halikuwa limehubiriwa sana kwa sababu wakati fulani Yesu aliwaagiza mitume hivi: “Msiingie katika jiji lolote la Wasamaria; badala yake, nendeni kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mt. 10:5, 6) Hata hivyo, Yesu alijua kwamba baada ya muda fulani ushahidi kamili ungetolewa Samaria, kwa sababu kabla ya kurudi mbinguni, alisema: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”​—Mdo. 1:8.

4. Wasamaria walipokeaje habari njema alizowatangazia Filipo, na huenda ni kwa sababu gani?

4 Filipo aliona kwamba shamba la Samaria lilikuwa ‘jeupe kwa ajili ya kuvunwa.’ (Yoh. 4:35) Ujumbe wake uliwaburudisha watu waliokuwa wakiishi huko, na tunaweza kuelewa sababu. Wayahudi hawakuchangamana na Wasamaria, na wengi wao walionyesha chuki yao waziwazi. Kinyume na hilo, Wasamaria waliona kwamba ujumbe wa habari njema uliwapa tumaini watu wote bila ubaguzi, nao ulikuwa kinyume kabisa na mtazamo wa ubaguzi wa Mafarisayo. Kwa kuwahubiria Wasamaria kwa bidii na bila ubaguzi, Filipo alionyesha kwamba hakuathiriwa na maoni ya ubaguzi ya wale waliokuwa wanawadharau. Kwa hiyo, haishangazi kwamba umati wote wa Wasamaria ulikuwa ukimsikiliza Filipo “kwa pamoja.”​—Mdo. 8:6.

5-7. Toa mifano inayoonyesha jinsi kutawanywa kwa Wakristo kumesaidia kueneza habari njema.

5 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, mateso hayajawazuia watu wa Mungu kuendelea na kazi yao ya kuhubiri leo. Wakristo waliolazimika kuhama, iwe kwa sababu ya kufungwa gerezani au kuhamishiwa nchi nyingine, wametumia fursa hiyo kuhubiri ujumbe wa Ufalme katika maeneo hayo mapya. Kwa mfano, wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi wa Yehova waliwahubiria wafungwa wenzao katika kambi za mateso za Nazi. Myahudi mmoja aliyekutana na Mashahidi katika kambi hizo alisema hivi: “Ujasiri wa wafungwa waliokuwa Mashahidi wa Yehova ulinihakikishia kwamba imani yao ilikuwa na msingi wa Kimaandiko—nami nikawa Shahidi.”

6 Katika visa fulani hata wale waliowatesa walihubiriwa na kukubali ujumbe. Kwa mfano, Ndugu Franz Desch alipokuwa katika kambi ya mateso ya Gusen nchini Austria, alijifunza Biblia na ofisa mmoja wa Nazi. Wazia shangwe yao, miaka mingi baadaye, wanaume hao wawili walipokutana kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, wote wakiwa wahubiri wa habari njema!

7 Ndivyo ilivyokuwa wakati mateso yaliposababisha Wakristo katika nchi moja wakimbilie nchi nyingine. Miaka ya 1970, ushahidi mkubwa ulitolewa nchini Msumbiji wakati Mashahidi kutoka Malawi walipolazimika kukimbilia huko. Baadaye upinzani ulipotokea nchini Msumbiji, kazi ya kuhubiri iliendelea. Francisco Coana anasema: ‘Baadhi yetu tulikamatwa mara kadhaa kwa sababu ya kazi yetu ya kuhubiri. Lakini, tulipoona wengi wakiitikia ujumbe wa Ufalme, tulikuwa na hakika kwamba Mungu anatusaidia, kama alivyowasaidia Wakristo wa karne ya kwanza.’

8. Mabadiliko ya kisiasa na ya kiuchumi yamekuwa na matokeo gani katika kazi ya kuhubiri?

8 Bila shaka, si mateso tu yaliyochangia kuenea kwa Ukristo katika maeneo mengine. Mabadiliko ya kisiasa na ya kiuchumi yamewezesha ujumbe wa Ufalme uhubiriwe kwa watu wa lugha na mataifa mengi. Watu fulani kutoka katika maeneo yenye vita na hali ngumu za kiuchumi wamehamia katika nchi zenye utulivu na kujifunza Biblia wakiwa huko. Ongezeko la wakimbizi limefungua maeneo mapya ya lugha za kigeni. Je, unafanya yote uwezayo ili kuwahubiria watu “kutoka mataifa yote na makabila na jamii na lugha” walio katika eneo lenu?​—Ufu. 7:9.

“Nipeni Mimi Pia Mamlaka Hii” (Mdo. 8:9-25)

“Simoni alipoona kwamba watu walipokea roho takatifu mitume walipoweka mikono juu yao, akawatolea pesa.”—Matendo 8:18

9. Simoni alikuwa nani, na kwa nini alivutiwa na Filipo?

9 Filipo alifanya ishara nyingi jijini Samaria. Aliwaponya walemavu na kuwafukuza roho waovu. (Mdo. 8:6-8) Mtu mmoja alivutiwa sana na uwezo wa Filipo wa kufanya miujiza. Aliitwa Simoni, naye alikuwa mchawi ambaye aliheshimiwa sana hivi kwamba watu walikuwa wakisema: “Mtu huyu ndiye Nguvu za Mungu.” Simoni alijionea mwenyewe nguvu za kweli za Mungu kutokana na miujiza iliyofanywa na Filipo, naye akawa mwamini. (Mdo. 8:9-13) Hata hivyo, baadaye nia ya Simoni ilijaribiwa. Jinsi gani?

10. (a) Petro na Yohana walifanya nini jijini Samaria? (b) Simoni alifanya nini alipoona wapya wakipokea roho takatifu baada ya Petro na Yohana kuwawekea mikono?

10 Mitume walipoona kwamba kulikuwa na ongezeko kubwa jijini Samaria, waliwatuma Petro na Yohana huko. (Ona sanduku “ Petro Atumia ‘Funguo za Ufalme.’”) Mitume hao wawili walipofika waliweka mikono yao juu ya wanafunzi wapya, na kila mmoja wao akapokea roho takatifu. b Simoni alipoona hivyo, alistaajabu. Akawaambia mitume hao: “Nipeni mimi pia mamlaka hii, ili yeyote nitakayeweka mikono juu yake apokee roho takatifu.” Simoni hata alitaka kuwapa pesa wamuuzie pendeleo hilo takatifu!—Mdo. 8:14-19.

11. Petro alimwambia Simoni nini, naye Simoni aliitikiaje?

11 Petro alimkaripia Simoni na kumwambia: “Fedha yako na iangamie pamoja nawe, kwa sababu ulidhani utanunua zawadi ya bure ya Mungu kwa kutumia pesa. Wewe huna sehemu wala fungu katika jambo hili, kwa maana moyo wako si mnyoofu machoni pa Mungu.” Kisha, Petro akamhimiza Simoni atubu na kuomba msamaha. Petro akasema: ‘Mwombe Yehova dua, ili ikiwezekana, usamehewe nia mbaya ya moyo wako.’ Inaonekana kwamba Simoni hakuwa mtu mwovu; alitaka kufanya yaliyo sawa, lakini kwa muda hakuwa na maoni yanayofaa. Kwa hiyo, akawasihi mitume: “Mwombeni Yehova dua kwa ajili yangu ili nisipatwe na lolote kati ya mambo mliyosema.”​—Mdo. 8:20-24.

12. “Usimoni” ni nini, na dini zinazodai kuwa za Kikristo zimetumbukiaje katika mtego huo?

12 Karipio hilo lapaswa pia kuwa onyo kwa Wakristo leo. Neno “usimoni” latokana na kisa hicho nalo linamaanisha kununua au kuuza vyeo, hasa vya kanisa. Usimoni umeenea sana katika dini zinazodai kuwa za Kikristo. Kitabu kimoja kinasema: ‘Historia ya mabaraza ya siri ya Mapapa inaonyesha wazi kwamba hakujawahi kuwa na uchaguzi wowote wa kanisa usiokuwa na usimoni, na katika visa vingi, usimoni wenyewe ulikuwa usimoni mbaya sana, wenye kuaibisha, tena ulifanywa waziwazi.’​—The Encyclopædia Britannica (1878).

13. Wakristo wanapaswa kuepuka usimoni kwa njia gani?

13 Wakristo wanapaswa kujihadhari na dhambi ya usimoni. Kwa mfano, hawapaswi kujaribu kupata mapendeleo kutanikoni kwa kuwapa zawadi au kuwasifu kupita kiasi ndugu wenye madaraka. Kwa upande mwingine, ndugu hao wenye madaraka wanapaswa kuwa waangalifu wasiwaonyeshe watu wenye mali upendeleo. Yote hayo ni usimoni. Watumishi wote wa Mungu wanapaswa kujiendesha kama ‘walio wadogo,’ na kuonyesha subira huku wakiiruhusu roho takatifu ya Yehova iweke rasmi wale wanaostahili. (Luka 9:48) Katika tengenezo la Mungu, hakuna nafasi kwa ajili ya watu wanaojaribu ‘kujitafutia utukufu wao wenyewe.’​—Met. 25:27.

“Je, Kweli Unajua Unayosoma?” (Mdo. 8:26-40)

14, 15. (a) “Towashi Mwethiopia” alikuwa nani, na Filipo alikutana naye jinsi gani? (b) Mwethiopia huyo aitikiaje ujumbe wa Filipo, na kwa nini uamuzi wake wa kubatizwa haukutokana tu na msisimko? (Ona maelezo ya chini.)

14 Malaika wa Yehova anamwambia Filipo aende kwenye barabara inayoshuka kutoka Yerusalemu mpaka Gaza. Muda mfupi baadaye, Filipo anaelewa sababu ya kutumwa baada ya kukutana na towashi Mwethiopia ambaye “alikuwa akimsoma kwa sauti kubwa nabii Isaya.” (Ona sanduku “ ‘Towashi’ Katika Maana Gani?”) Roho takatifu ya Yehova ilimwongoza Filipo alikaribie gari la mtu huyo. Huku akikimbia kandokando ya gari hilo, Filipo alimuuliza Mwethiopia huyo: “Je, kweli unajua unayosoma?” Mwethiopia akajibu: “Ninawezaje kuyaelewa mtu fulani asiponiongoza?”​—Mdo. 8:26-31.

15 Mwethiopia akamsihi Filipo apande kwenye gari. Wazia mazungumzo yaliyofuata! Kwa muda mrefu, haikujulikana ni nani anayezungumziwa katika unabii unaohusu “kondoo,” au “mtumishi,” katika kitabu cha Isaya. (Isa. 53:1-12) Hata hivyo, walipokuwa wakiendelea na safari, Filipo alimfafanulia kwamba Yesu Kristo ndiye anayezungumziwa katika unabii huo. Kama wale waliobatizwa siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., Mwethiopia huyo ambaye tayari alikuwa Myahudi mgeuzwa imani akajua mara moja jambo analopaswa kufanya. Kisha akamwambia Filipo. “Tazama! Hapa kuna maji; ni nini kinachonizuia kubatizwa?” Bila kukawia, Filipo akambatiza Mwethiopia huyo! c (Ona sanduku “ Kubatizwa ‘Mahali Penye Maji.’”) Kisha, roho ya Mungu ikamwongoza Filipo kwenda katika mgawo mwingine huko Ashdodi, ambako aliendelea kutangaza habari njema.​—Mdo. 8:32-40.

16, 17. Malaika wanahusika jinsi gani katika kazi ya kuhubiri leo?

16 Wakristo leo wana pendeleo la kushiriki kazi kama iliyofanywa na Filipo. Mara nyingi, wanaposafiri wanatumia nafasi hiyo kuwahubiria watu ujumbe wa Ufalme. Katika visa vingi, wanapopata mtu mnyoofu, hawashangai kwa sababu Biblia inaonyesha wazi kwamba malaika wanaelekeza kazi ya kuhubiri ili ujumbe huo ufikie “kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufu. 14:6) Yesu alitabiri kwamba malaika wangeelekeza kazi ya kuhubiri. Katika mfano wa ngano na magugu, Yesu alisema kwamba wakati wa mavuno, au umalizio wa mfumo wa mambo, “wavunaji ni malaika.” Pia, alisema, viumbe hao wa kiroho “watakusanya kutoka katika Ufalme wake vitu vyote vinavyosababisha kukwazika na watu wenye mazoea ya kuasi sheria.” (Mt. 13:37-41) Wakati huohuo, malaika watakusanya watu watakaorithi Ufalme wa mbinguni, kisha watakusanya “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” ambao Yehova anawavuta katika tengenezo lake.​—Ufu. 7:9; Yoh. 6:44, 65; 10:16.

17 Jambo moja linalothibitisha kwamba malaika wanaelekeza kazi yetu ni kwamba watu fulani tunaowapata katika huduma yetu husema kwamba wamekuwa wakisali ili wapate mwongozo wa kiroho. Fikiria jambo moja lililoonwa: Wahubiri wawili wa Ufalme walikuwa wakihubiri pamoja na mtoto mdogo. Ilipofika mchana, wahubiri hao walipotaka kuondoka kwenye eneo, yule mtoto alitaka sana waende nyumba inayofuata. Alienda kubisha mlango huo! Mwanamke alipoufungua mlango, Mashahidi hao wawili wakakaribia ili kuzungumza naye. Walishangaa kusikia kwamba mwanamke huyo alikuwa ametoka tu kusali mtu amtembelee na kumsaidia kuelewa Biblia. Funzo la Biblia likaanzishwa!

“Mungu, ikiwa upo, tafadhali nisaidie”

18. Kwa nini hatupaswi kamwe kuipuuza huduma yetu?

18 Ukiwa mmoja wa wahubiri katika kutaniko la Kikristo, una pendeleo la kushiriki bega kwa bega katika kazi ya kuhubiri ambayo leo inafanywa kwa kiwango kikubwa zaidi. Usilipuuze kamwe pendeleo hilo. Ukidumu katika kazi hiyo, utapata shangwe kubwa inayotokana na kutangaza “habari njema kumhusu Yesu.”​—Mdo. 8:35.

a Filipo huyu si mtume Filipo. Badala yake, ni Filipo ambaye, kama Sura ya 5 ya kitabu hiki inavyoeleza, alikuwa mmoja wa “wanaume saba wenye sifa nzuri” ambao waliwekwa rasmi kusimamia ugawaji wa kila siku wa chakula kati ya Wakristo wajane waliozungumza Kigiriki na waliozungumza Kiebrania katika jiji la Yerusalemu.​—Mdo. 6:1-6.

b Inaonekana kwamba kwa kawaida wanafunzi wapya walitiwa mafuta, au kupokea roho takatifu walipobatizwa. Baada ya kupokea roho hiyo, wakawa na tumaini la kutawala wakiwa wafalme na makuhani pamoja na Yesu mbinguni. (2 Kor. 1:21, 22; Ufu. 5:9, 10; 20:6) Hata hivyo, katika kisa hiki, Wakristo wapya hawakutiwa mafuta walipobatizwa. Walipokea roho takatifu pamoja na uwezo wa kufanya miujiza walipowekewa mikono na Petro na Yohana.

c Huo haukuwa msisimko tu. Kwa kuwa alikuwa Myahudi mgeuzwa imani, tayari alikuwa na ujuzi wa Maandiko, kutia ndani unabii kuhusu Masihi. Baada ya kuelewa jukumu la Yesu katika mpango wa Mungu, hakuna jambo lililomzuia kubatizwa.