Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 8

Kutaniko “Likaingia Katika Kipindi cha Amani”

Kutaniko “Likaingia Katika Kipindi cha Amani”

Sauli, aliyekuwa mtesaji mkatili awa mhubiri mwenye bidii

Matendo 9:1-43

1, 2. Sauli alikusudia kufanya nini Damasko?

 WASAFIRI wenye hasira kali wanakaribia Damasko, ambapo wanakusudia kutekeleza njama yao. Wanawachukia wanafunzi wa Yesu. Wanataka kuwakamata kwa nguvu, kuwafunga, kuwaaibisha, na kuwapeleka Yerusalemu mbele ya Sanhedrini.

2 Tayari kiongozi wa kikundi hicho, Sauli, ana hatia ya damu ya mmoja wa wanafunzi hao. a Siku chache zilizopita, wenzake walipokuwa wakimuua Stefano, mwanafunzi mwenye bidii wa Yesu kwa kumpiga mawe, Sauli alikuwa akiwatazama na kuunga mkono jambo hilo. (Mdo. 7:57–8:1) Sauli hajatosheka kuwatesa wafuasi wa Yesu wanaoishi Yerusalemu, naye anachochea zaidi mateso. Alitaka kuangamiza kabisa kikundi hicho cha dini kinachoitwa “Ile Njia.”​—Mdo. 9:1, 2; ona sanduku lenye kichwa “ Mamlaka ya Sauli Jijini Damasko,”.

3, 4. (a) Ni nini kilimpata Sauli? (b) Tutachunguza maswali gani?

3 Ghafla, nuru nyangavu yamfunika Sauli. Wasafiri wenzake wanaiona nuru hiyo na kushangaa sana. Sauli apigwa kwa upofu na kuanguka. Kisha, akasikia sauti kutoka mbinguni ikisema: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?” Sauli akauliza hivi kwa mshangao: “Wewe ni nani, Bwana?” Anapata jibu lenye kushangaza: “Mimi ni Yesu, ambaye unamtesa.”​—Mdo. 9:3-5; 22:9.

4 Tunaweza kujifunza nini kutokana na swali ambalo Yesu alimwuliza Sauli? Tunaweza kunufaikaje kwa kuchunguza mambo yaliyotokea pindi hiyo? Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na jinsi kutaniko lilivyotumia kipindi cha amani kilichofuata baada ya kugeuzwa imani kwa Sauli?

“Kwa Nini Unanitesa?” (Mdo. 9:1-5)

5, 6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na swali ambalo Yesu alimuuliza Sauli?

5 Yesu alipomsimamisha Sauli akiwa njiani kuelekea Damasko, hakumuuliza: “Kwa nini unawatesa wanafunzi wangu?” Badala yake, alimuuliza: “Kwa nini unanitesa?” (Mdo. 9:4) Naam, majaribu yanayowapata wafuasi wake, ni kana kwamba yanampata Yesu mwenyewe.​—Mt. 25:34-40, 45.

6 Ikiwa unateswa kwa sababu ya kumwamini Kristo, uwe na hakika kwamba Yehova na Yesu wanaelewa hali yako. (Mt. 10:22, 28-31) Kwa sasa, huenda jaribu hilo lisiondolewe. Kumbuka, Stefano alipokuwa akiuawa, na pia wanafunzi waaminifu walipokuwa wakikokotwa kutoka katika nyumba zao huko Yerusalemu, Yesu alikuwa akimtazama Sauli na kuona yote aliyokuwa akifanya. (Mdo. 8:3) Lakini, Yesu hakuingilia kati wakati huo. Badala yake, Yehova, kupitia Kristo, alimpa Stefano na wanafunzi wengine nguvu walizohitaji ili waendelee kuwa waaminifu.

7. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuvumilia mateso?

7 Wewe pia unaweza kuvumilia mateso ikiwa utafanya mambo yafuatayo: (1) Azimia kuendelea kuwa mshikamanifu, hata hali iweje. (2) Mwombe Yehova akusaidie. (Flp. 4:6, 7) (3) Mwachie Yehova alipize kisasi. (Rom. 12:17-21) (4) Uwe na uhakika kwamba Yehova atakupatia nguvu za kuvumilia mpaka wakati ambapo yeye mwenyewe ataona inafaa kuliondoa jaribu.​—Flp. 4:12, 13.

“Sauli, Ndugu, Bwana . . . Amenituma” (Mdo. 9:6-17)

8, 9. Anania aliuonaje mgawo wake?

8 Baada ya kujibu swali la Sauli, “Wewe ni nani, Bwana?” Yesu anamwambia: “Inuka uende jijini, nawe utaambiwa unachopaswa kufanya.” (Mdo. 9:6) Kisha, Sauli asiyeweza kuona anaongozwa hadi mahali atakapokaa katika jiji la Damasko, ambapo anafunga na kusali kwa siku tatu. Wakati huohuo, Yesu anamwambia mwanafunzi anayeishi katika mji huo kuhusu Sauli. Mwanafunzi huyo anaitwa Anania, naye ‘alishuhudiwa vema na Wayahudi wote’ walioishi Damasko.​—Mdo. 22:12.

9 Wazia jinsi Anania alivyochanganyikiwa! Kiongozi wa kutaniko, Yesu Kristo aliyefufuliwa alikuwa akizungumza naye na akampatia mgawo wa pekee. Ni pendeleo kubwa sana ijapokuwa mgawo wenyewe haukuwa rahisi! Alipoambiwa kwamba anapaswa kuzungumza na Sauli, Anania alijibu hivi: “Bwana, nimesikia kutoka kwa watu wengi kuhusu mtu huyu, jinsi alivyowatesa watakatifu wako huko Yerusalemu. Na sasa amepewa mamlaka na wakuu wa makuhani ili awakamate wote wanaoliitia jina lako.”​—Mdo. 9:13, 14.

10. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyoshughulika na Anania?

10 Yesu hakumkaripia Anania kwa kutoa maoni yake. Hata hivyo, Yesu alimpa maagizo yaliyo wazi. Naye alionyesha anamjali Anania kwa kumweleza ni kwa nini anataka ashughulikie mgawo huo usio wa kawaida. Yesu alimwambia hivi: “Mtu huyu ni chombo nilichokichagua ili kupeleka jina langu kwa mataifa na pia kwa wafalme na wana wa Israeli. Kwa maana nitamwonyesha waziwazi mateso mengi yatakayompata kwa sababu ya jina langu.” (Mdo. 9:15, 16) Anania hakusita kutii maagizo ya Yesu. Alimtafuta Sauli, aliyekuwa mtesaji, na kumwambia: “Sauli, ndugu, Bwana Yesu aliyekutokea barabarani ulipokuwa ukija, amenituma ili uweze kuona tena na ujazwe roho takatifu.”​—Mdo. 9:17.

11, 12. Tunajifunza nini kutokana na matukio yaliyowahusisha Yesu, Anania, na Sauli?

11 Kuna mambo mengi tunayoweza kujifunza kutokana na matukio hayo yaliyowahusisha Yesu, Anania, na Sauli. Kwa mfano, Yesu ndiye anayeongoza kazi ya kuhubiri kama alivyoahidi. (Mt. 28:20) Ingawa hazungumzi moja kwa moja na watu leo, Yesu anaongoza kazi ya kuhubiri kupitia mtumwa mwaminifu, ambaye sasa amewekwa rasmi juu ya watumishi wake. (Mt. 24:45-47) Chini ya mwongozo wa Baraza Linaloongoza, wahubiri na mapainia hutumwa kwenda kuwatafuta wale wanaotaka kujua mengi kumhusu Kristo. Kama ilivyotajwa katika sura ya saba, watu wengi wametembelewa na Mashahidi wa Yehova baada ya kusali wapate mwongozo.​—Mdo. 9:11.

12 Anania aliukubali mgawo aliopewa naye akapata baraka. Namna gani wewe? Unatii amri ya kutoa ushahidi kikamili, hata ikiwa una mashaka fulani kuhusu mgawo wako? Kwa wengine, kwenda nyumba kwa nyumba na kukutana na watu wasiowafahamu huwatia wasiwasi. Wengine huona ni vigumu kuwahubiria watu katika sehemu za biashara, barabarani, au kupitia simu au barua. Anania aliushinda woga wake naye akapata pendeleo la kumsaidia Sauli kuipokea roho takatifu. b Anania alifanikiwa kwa sababu alimwamini Yesu na kumwona Sauli kama ndugu yake. Kama alivyofanya Anania, sisi pia tunaweza kushinda woga wetu, kwa kutambua kwamba Yesu ndiye anayeongoza kazi ya kuhubiri, kuwajali watu na kuwaona kuwa wanaweza kuwa ndugu zetu hata wale wanaoonekana kuwa wenye kutisha.​—Mt. 9:36.

“Akaanza Kuhubiri . . . Kuhusu Yesu” (Mdo. 9:18-30)

13, 14. Ikiwa unajifunza Biblia lakini hujabatizwa, unaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Sauli?

13 Sauli hakusita kutenda kulingana na mambo aliyojifunza. Baada ya kuponywa, alibatizwa na kuanza kushirikiana kwa ukaribu na wanafunzi huko Damasko. Si hayo tu, “mara moja akaanza kuhubiri katika masinagogi kuhusu Yesu, kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu.”​—Mdo. 9:20.

14 Ikiwa unajifunza Biblia lakini hujabatizwa, je, utakuwa kama Sauli kwa kutenda kulingana na mambo unayojifunza? Ni kweli kwamba muujiza uliofanywa na Kristo, ulimchochea Sauli kutenda. Hata hivyo, wengine walijionea miujiza iliyofanywa na Yesu. Kwa mfano, kikundi kimoja cha Mafarisayo kilishuhudia wakati ambapo Yesu alimponya mtu aliyepooza mkono, na Wayahudi wengi walijua kwamba Yesu alimfufua Lazaro. Lakini, wengi wao hawakuchukua hatua yoyote, na hata wengine walimpinga. (Marko 3:1-6; Yoh. 12:9, 10) Tofauti nao, Sauli alifanya mabadiliko. Kwa nini Sauli alichukua hatua ingawa wengine hawakufanya hivyo? Kwa sababu alimwogopa Mungu kuliko wanadamu naye alithamini sana rehema aliyoonyeshwa na Kristo. (Flp. 3:8) Wewe pia, kama alivyofanya Sauli, usiruhusu chochote kikuzuie kufanya kazi ya kuhubiri au kubatizwa.

15, 16. Sauli alifanya nini katika masinagogi, na Wayahudi huko Damasko walichukua hatua gani?

15 Wazia jinsi watu walivyoshangaa na kushtuka huku wengine wakikasirika Sauli alipoanza kuhubiri kumhusu Yesu katika masinagogi. Waliuliza: “Je, huyu si yule mtu aliyewashambulia wale wanaoliitia jina hilo huko Yerusalemu?” (Mdo. 9:21) Alipokuwa akieleza sababu iliyomfanya abadilike, Sauli ‘alithibitisha kupatana na akili kwamba huyu ndiye Kristo.’ (Mdo. 9:22) Hata hivyo, si watu wote wanaoweza kusadikishwa kwa njia hiyo. Kwa mfano, si wote wanaoshikilia desturi au wenye kiburi wanaoweza kusadikishwa kwa kuwathibitishia mambo “kupatana na akili.” Hata hivyo, Sauli hakukata tamaa.

16 Miaka mitatu baadaye, bado Wayahudi mjini Damasko walikuwa wakimpinga Sauli. Mwishowe, wakapanga kumuua. (Mdo. 9:23; 2 Kor. 11:32, 33; Gal. 1:13-18) Njama yao ilipojulikana, Sauli alitenda kwa busara na kuondoka jijini kwa kushushwa katika kapu kupitia shimo lililokuwa katika ukuta wa jiji. Luka anasema kwamba waliomsaidia Sauli kutoroka usiku huo walikuwa “wanafunzi” wa Sauli. (Mdo. 9:25) Maneno hayo yanaonyesha kwamba watu fulani waliomsikiliza Sauli huko Damasko, walichukua hatua na kuwa wafuasi wa Kristo.

17. (a) Watu huitikiaje kweli ya Biblia? (b) Tunapaswa kuendelea kufanya nini, na kwa nini?

17 Ulipoanza kuzungumza na watu wa familia, marafiki, na wengine kuhusu mambo mazuri uliyokuwa unajifunza, huenda ulitazamia kwamba kila mmoja angekubali kweli ya Biblia kwa sababu ni habari inayopatana na akili. Ijapokuwa huenda baadhi yao walikubali, wengi walikataa. Huenda hata watu wa nyumbani kwako mwenyewe walikuona kuwa adui. (Mt. 10:32-38) Hata hivyo, ukiendelea kukuza uwezo wako wa kujadiliana kwa kutumia Maandiko na ukiwa na mwenendo mzuri wa Kikristo, huenda mwishowe hata wale wanaokupinga wakabadili maoni yao.​—Mdo. 17:2; 1 Pet. 2:12; 3:1, 2, 7.

18, 19. (a) Barnaba alipomtetea Sauli, matokeo yalikuwa nini? (b) Tunawezaje kuwaiga Barnaba na Sauli?

18 Sauli alipoingia Yerusalemu, inaeleweka ni kwa nini wanafunzi hawakuamini kwamba sasa yeye ni mwanafunzi. Hata hivyo, Barnaba alipomtetea Sauli, mitume walimkubali naye akakaa nao kwa muda. (Mdo. 9:26-28) Ingawa Sauli hakuionea aibu habari njema, nyakati nyingine alilazimika kutenda kwa busara. (Rom. 1:16) Alihubiri kwa ujasiri katika jiji la Yerusalemu, ambapo aliwatesa vikali wanafunzi wa Yesu Kristo. Wakiwa na hofu, Wayahudi katika jiji la Yerusalemu wanatambua kwamba mtu waliyetegemea aangamize Ukristo, amewakimbia, nao wanataka kumuua. “Akina ndugu walipogundua hilo, wakampeleka [Sauli] Kaisaria na kumtuma aende Tarso.” (Mdo. 9:30) Sauli alinyenyekea mwongozo ambao Yesu alitoa kupitia kutaniko. Hivyo, Sauli na kutaniko likanufaika.

19 Kumbuka kwamba Barnaba hakusita kumtetea Sauli. Bila shaka, tendo hilo la fadhili lilichangia urafiki wa karibu kati ya watumishi hao wa Yehova wenye bidii. Kama alivyofanya Barnaba, je, wewe hujitolea kuwasaidia wapya kutanikoni, kwa kuhubiri pamoja nao na kuwasaidia kufanya maendeleo ya kiroho? Utabarikiwa sana ukifanya hivyo. Ikiwa wewe ni mhubiri mpya wa habari njema, je, unamwiga Sauli kwa kukubali msaada wa wengine? Ukishirikiana na wahubiri wenye uzoefu, utapata ustadi katika kazi ya kuhubiri, shangwe nyingi na marafiki wa kudumu.

“Wengi Wakamwamini” (Mdo. 9:31-43)

20, 21. Watumishi wa Mungu, wa zamani na wa sasa, wametumia jinsi gani ‘vipindi vya amani’?

20 Baada ya Sauli kugeuzwa-imani na kuondoka akiwa salama, “kutaniko katika eneo lote la Yudea, Galilaya, na Samaria likaingia katika kipindi cha amani.” (Mdo. 9:31) Wanafunzi walitumiaje ‘nyakati hizo zinazofaa?’ (2 Tim. 4:2) Maandiko yanasema kwamba walikuwa ‘wakijengwa.’ Mitume na ndugu wengine wenye kutegemeka kutanikoni waliimarisha imani ya wanafunzi na kutoa mwongozo uliohitajika huku kutaniko “likitembea katika kumwogopa Yehova na katika faraja ya roho takatifu.” Kwa mfano, Petro alitumia kipindi hicho kuwatia nguvu wanafunzi katika mji wa Lida katika Nchi Tambarare ya Sharoni. Bidii yake iliwafanya wengi waliokuwa wakiishi karibu na mahali hapo ‘wamgeukie Bwana.’ (Mdo. 9:32-35) Mitume hawakukengeushwa na shughuli za kimwili, bali walijitahidi sana kusaidiana na kuhubiri habari njema, nalo kutaniko “likaendelea kuongezeka.”

21 Kufikia mwisho wa karne ya 20, Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingi waliingia katika “kipindi cha amani.” Serikali zilizokuwa zikiwatesa watu wa Mungu kwa miaka mingi zilitoka mamlakani, na marufuku katika nchi fulani zikapunguzwa au kuondolewa. Makumi ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova walitumia nafasi hiyo kuhubiri, nao wakapata matokeo mazuri.

22. Unaweza kutumia jinsi gani uhuru ulio nao?

22 Je, unatumia vizuri uhuru ulio nao? Ikiwa unaishi katika nchi iliyo na uhuru wa kidini, huenda Shetani akakushawishi utafute utajiri badala ya kumtumikia Yehova. (Mt. 13:22) Usikengeushwe. Tumia vizuri vipindi vyovyote vya amani ambavyo huenda vipo kwa sasa. Vione kuwa nafasi za kutoa ushahidi kikamili na kujenga kutaniko. Kumbuka kwamba hali zinaweza kubadilika ghafla.

23, 24. (a) Ni mambo gani tunayojifunza kutokana na masimulizi kumhusu Tabitha? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

23 Fikiria kilichompata mwanafunzi anayeitwa Tabitha, au Dorkasi. Alikuwa akiishi Yopa, mji uliokuwa karibu na Lida. Dada huyo mwaminifu alitumia wakati na mali zake kwa hekima, “alikuwa akitenda matendo mema na kutoa zawadi za rehema.” Hata hivyo, aliugua na kisha akafa ghafla. c Wanafunzi wa Yopa, hasa wajane ambao alikuwa amewatendea kwa fadhili walihuzunika sana. Petro alipofika katika nyumba ambamo mwili wa Tabitha ulikuwa unatayarishwa kwa ajili ya maziko, alifanya muujiza ambao ulikuwa wa kwanza kufanywa na mitume wa Yesu Kristo. Petro alisali, kisha akamfufua Tabitha! Wazia jinsi wajane na wanafunzi wengine walivyoshangilia Petro alipowaita na kuwakabidhi Tabitha akiwa hai! Tukio hilo liliwaimarisha sana kukabiliana na majaribu yaliyokuwa mbele yao! Muujiza huo ‘ukajulikana kotekote huko Yopa, na wengi wakamwamini Bwana.’​—Mdo. 9:36-42.

Unawezaje kumwiga Tabitha?

24 Tunajifunza mambo mawili muhimu kutokana na masimulizi yenye kutia moyo kumhusu Tabitha. (1) Maisha ni mafupi hivyo ni muhimu tujifanyie jina zuri na Mungu tukiwa hai. (Mhu. 7:1) (2) Tumaini la ufufuo ni hakika. Yehova aliona matendo mengi yenye fadhili aliyofanya Tabitha, naye alimthawabisha. Yehova hatasahau bidii yetu na atatufufua ikiwa tutakufa kabla ya Har–Magedoni. (Ebr. 6:10) Kwa hiyo, iwe tunavumilia “nyakati ngumu” au tunaishi katika “kipindi cha amani,” na tuendelee kutoa ushahidi kamili kumhusu Kristo.​—2 Tim. 4:2.

a Ona sanduku lenye kichwa “ Sauli Aliyekuwa Farisayo,” katika ukurasa wa 62.

b Kwa kawaida, zawadi za roho takatifu zilipitishwa kupitia mitume. Hata hivyo, katika hali hii isiyo ya kawaida, inaonekana Yesu alimwamuru Anania apitishe zawadi za roho takatifu kwa Sauli. Baada ya kugeuzwa imani, kwa muda fulani, Sauli alikuwa peke yake, mbali na wale mitume wengine 12. Hata hivyo, inaonekana kwamba aliendelea kuwa mtendaji katika kipindi hicho. Inaonekana kwamba Yesu alihakikisha Sauli amepata nguvu zinazohitajika ili kuutimiza mgawo wake wa kuhubiri.

c Ona sanduku lenye kichwa “ Tabitha—‘Alikuwa Akitenda Matendo Mema,’”.