Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 6

Stefano—“Amejaa Kibali cha Mungu na Nguvu”

Stefano—“Amejaa Kibali cha Mungu na Nguvu”

Ujasiri wa Stefano akiwa mbele ya Sanhedrini

MATENDO 6:8–8:3

1-3. (a) Stefano anakabili hali gani ngumu, naye anatendaje? (b) Tutachunguza maswali gani?

 STEFANO yuko mahakamani, mbele ya wanaume 71 katika jumba kubwa ambalo huenda liko karibu na hekalu la Yerusalemu. Mahakama hiyo inayoitwa Sanhedrini, imekutana ili kusikiliza kesi ya Stefano. Mahakimu wenyewe ni watu mashuhuri, wenye mamlaka, na wengi wao wanamdharau mwanafunzi huyo wa Yesu. Kuhani Mkuu Kayafa, ambaye alikuwa mkuu wa mahakama hiyo Yesu Kristo ilipohukumiwa kifo miezi michache iliyopita, ndiye aliyeitisha kikao hicho. Je, Stefano anaogopa?

2 Sura ya Stefano inaonekana tofauti kabisa. Mahakimu wanapomkazia macho, wanaona kwamba uso wake ni “kama uso wa malaika.” (Mdo. 6:15) Malaika ni wajumbe wa Yehova Mungu, nao hawana sababu yoyote ya kuogopa bali huwa watulivu na wenye amani. Ndivyo alivyo Stefano—hata mahakimu hao wenye chuki kali wanaona hilo wazi. Ni nini kinachomwezesha kuwa mtulivu hivyo?

3 Leo, Wakristo wanaweza kujifunza mengi kutokana na jibu la swali hilo. Pia, tunahitaji kujua jinsi Stefano alivyojikuta katika hali hiyo mbaya. Alikuwa ameiteteaje imani yake awali? Nasi tunaweza kumwiga jinsi gani?

“Wakawachochea Watu” (Mdo. 6:8-15)

4, 5. (a) Kwa nini Stefano alithaminiwa sana kutanikoni? (b) Stefano alikuwa “amejaa kibali cha Mungu na nguvu” jinsi gani?

4 Tayari tumejifunza kwamba Stefano alithaminiwa sana katika kutaniko changa la Kikristo. Katika sura ya tano ya kitabu hiki, tuliona kwamba alikuwa miongoni mwa wanaume saba wanyenyekevu waliojitolea kuwasaidia mitume walipoombwa wafanye hivyo. Unyenyekevu wake unaonekana wazi unapozingatia vipawa alivyokuwa navyo. Andiko la Matendo 6:8 linasema kwamba alikuwa akifanya “mambo makubwa ya ajabu na ishara,” kama baadhi ya mitume. Pia, tunaambiwa kwamba alikuwa “amejaa kibali cha Mungu na nguvu.” Maneno hayo yanamaanisha nini?

5 Neno la Kigiriki “kibali cha Mungu” linaweza kutafsiriwa pia “neema.” Inaonekana watu wengi walivutiwa sana na Stefano kwa sababu alishughulika nao kwa fadhili na heshima. Alizungumza kwa usadikisho sana hivi kwamba wasikilizaji wake waliona unyoofu wake wa moyoni na kweli muhimu alizokuwa akizungumzia. Alikuwa na nguvu nyingi kwa sababu alikuwa na roho ya Yehova, naye alikubali mwongozo wake. Badala ya kuwa na kiburi kwa sababu ya vipawa na uwezo wake, alielekeza sifa zote kwa Yehova na kuwahangaikia kwa upendo watu aliokuwa akizungumza nao. Si ajabu kwamba hata wapinzani wake walimwogopa!

6-8. (a) Stefano alishtakiwa nini, na kwa nini? (b) Kwa nini mfano wa Stefano ni muhimu kwa Wakristo leo?

6 Wanaume kadhaa walisimama ili kubishana na Stefano, lakini “hawakuweza kumshinda kwa sababu ya hekima yake na roho iliyomwongoza kusema.” a Wakiwa wamekasirika, “wakawashawishi watu kwa siri” walete mashtaka dhidi ya mfuasi huyo wa Kristo asiye na hatia. Pia, “wakawachochea watu,” wazee na waandishi, ili Stefano akamatwe kwa nguvu na kumpeleka kwenye Sanhedrini. (Mdo. 6:9-12) Washtaki hao walidai kwamba anamkufuru Mungu na Musa. Jinsi gani?

7 Washtaki hao wa uwongo walidai kwamba Stefano amemkufuru Mungu na kwamba amesema makufuru dhidi ya “mahali hapa patakatifu,” yaani, hekalu la Yerusalemu. (Mdo. 6:13) Pia, walidai amemkufuru Musa, kwa kuwa aliidharau Sheria ya Musa, kwa kubadili desturi na mapokeo yaliyoanzishwa na Musa. Hilo lilikuwa shtaka zito sana, kwa sababu Wayahudi wa wakati huo walikazia sana hekalu, Sheria ya Musa, na mapokeo mengi yaliyopitishwa kwa mdomo, waliyoyaongeza kwenye Sheria. Kwa sababu hiyo, Stefano alionwa kuwa mtu hatari, anayestahili kifo!

8 Kwa kusikitisha, watu wengi wa dini hutumia mbinu hizo kuwasumbua watumishi wa Mungu. Leo, wafuasi wa dini huwachochea wenye mamlaka wawatese Mashahidi wa Yehova. Tunaweza kufanya nini tunapokabili mashtaka ya uwongo? Tunaweza kujifunza mengi kutokana na mfano wa Stefano.

Kutoa Ushahidi kwa Ujasiri Kuhusu “Mungu wa Utukufu” (Mdo. 7:1-53)

9, 10. Wachambuzi fulani hudai nini, na ni jambo gani tunalopaswa kukumbuka?

9 Kama ilivyotajwa mwanzoni, uso wa Stefano ulikuwa mtulivu kama wa malaika, alipokuwa akisikiliza mashtaka dhidi yake. Kwa hiyo Kayafa akamgeukia na kumwuliza: “Je, mambo hayo ni ya kweli?” (Mdo. 7:1) Sasa ulikuwa wakati wa Stefano kuongea, naye hakusita kufanya hivyo!

10 Wachambuzi fulani hudai kwamba Stefano aliongea kwa muda mrefu na hakujibu mashtaka aliyoshtakiwa. Lakini, ukweli ni kwamba Stefano alituwekea mfano mzuri sana wa ‘kutetea’ habari njema. (1 Pet. 3:15) Kumbuka, alishtakiwa kwamba amemkufuru Mungu kwa kulivunjia heshima hekalu na amemkufuru Musa kwa kuidharau Sheria. Stefano alijibu kwa kuzungumzia vipindi vitatu katika historia ya taifa la Israeli, akikazia mambo fulani hususa. Acheni tuzungumzie vipindi hivyo.

11, 12. (a) Stefano aliutumiaje vizuri mfano wa Abrahamu? (b) Kwa nini Stefano alimtaja Yosefu?

11 Kipindi cha wazee wa ukoo. (Mdo. 7:1-16) Stefano alianza kwa kuzungumza kuhusu Abrahamu, aliyeheshimiwa na Wayahudi kwa sababu ya imani yake. Akianza kwa kuzungumzia jambo ambalo wote walikubaliana, Stefano alikazia kwamba Yehova, “Mungu wa utukufu,” alimtokea Abrahamu alipokuwa Mesopotamia. (Mdo. 7:2) Abrahamu alikuwa mkaaji mgeni katika Nchi ya Ahadi. Wakati huo, hakukuwa na hekalu wala Sheria ya Musa. Hivyo, mtu anawezaje kusisitiza kwamba uaminifu wa mtu kwa Mungu unategemea hekalu na Sheria ya Musa?

12 Yosefu, aliyezaliwa katika ukoo wa Abrahamu, aliheshimiwa sana pia na baraza hilo lililokuwa likimsikiliza Stefano. Hata hivyo, Stefano aliwakumbusha kwamba ndugu za Yosefu, mababa wa makabila ya Israeli, walimtesa mtu huyo mwadilifu na kumuuza utumwani. Hata hivyo, Mungu alimtumia kuokoa Israeli wakati wa njaa kali. Inaonekana kwamba Stefano aliona ulinganisho huo ulio wazi kati ya maisha ya Yosefu na ya Yesu Kristo. Lakini, ili umati huo uendelee kumsikiliza kwa makini, hakutaja jambo hilo wakati huo.

13. Mazungumzo kuhusu Musa yalijibu jinsi gani mashtaka yaliyoletwa dhidi ya Stefano, na ni jambo gani linalojitokeza wazi katika mazungumzo ya Stefano?

13 Nyakati za Musa. (Mdo. 7:17-43) Stefano alisema mengi kuhusu Musa. Alikuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo kwa kuwa wengi katika Sanhedrini walikuwa Masadukayo, waliokataa vitabu vingine vyote vya Biblia isipokuwa vile vilivyoandikwa na Musa. Pia, kumbuka Stefano alishtakiwa kwamba amemkufuru Musa. Maneno ya Stefano yalijibu shtaka hilo moja kwa moja, kwa kuwa yalionyesha wazi kwamba anamheshimu sana Musa na Sheria. (Mdo. 7:38) Alitaja kwamba Musa pia alikataliwa na watu aliokuwa akijaribu kuwaokoa. Walimkataa alipokuwa na umri wa miaka 40. Zaidi ya miaka 40 baadaye, walipinga uongozi wake mara kadhaa. b Jambo moja linajitokeza wazi katika mazungumzo ya Stefano: Mara kwa mara, watu wa Mungu waliwakataa watu waliowekwa rasmi na Yehova kuwaongoza.

14. Stefano alitumia masimulizi ya Musa jinsi gani ili kutegemeza hoja yake?

14 Stefano aliwakumbusha wasikilizaji wake kuwa Musa alikuwa ametabiri kwamba nabii kama Musa angetokea katika Israeli. Nabii huyo ni nani, naye angepokewa jinsi gani? Stefano aliamua kutojibu swali hilo hadi mwisho wa mazungumzo yake. Alitaja jambo lingine muhimu: Musa alijua kwamba mahali popote panaweza kuwa patakatifu, kama vile mahali palipokuwa na kichaka kinachowaka moto, ambapo Yehova alizungumza naye. Basi, je, ni lazima Yehova aabudiwe katika jengo fulani hususa, kama vile hekalu la Yerusalemu? Acheni tuone.

15, 16. (a) Kwa nini hoja ya hema la ibada ilikuwa muhimu katika mazungumzo ya Stefano? (b) Stefano alisema nini kuhusu hekalu la Sulemani?

15 Hema la ibada na hekalu. (Mdo. 7:44-50) Stefano aliikumbusha mahakama hiyo kwamba kabla hekalu lolote lile halijajengwa Yerusalemu, Mungu alimwagiza Musa ajenge hema la ibada ambalo lingeweza kuhamishwa. Kwa kuwa Musa mwenyewe aliabudu kwenye hema la ibada, hakuna yeyote kati yao angeweza kudai kwamba hema hilo la ibada halikufaa kwa sababu halikuwa hekalu.

16 Baadaye, Sulemani alijenga hekalu Yerusalemu. Roho ya Mungu ilimchochea kusema jambo muhimu katika sala yake. Kama Stefano alivyosema, “Aliye Juu Zaidi haishi katika nyumba zilizojengwa kwa mikono.” (Mdo. 7:48; 2 Nya. 6:18) Yehova anaweza kutumia hekalu kutimiza makusudi yake, lakini si kwamba hana njia nyingine. Basi, mbona waabudu wake wahisi kwamba ibada ya kweli inategemea jengo fulani lililojengwa kwa mikono ya wanadamu? Stefano alimalizia hoja yake kwa kishindo kwa kunukuu kitabu cha Isaya: “Mbingu ni kiti changu cha ufalme, nayo dunia ni kiti cha miguu yangu. Mtanijengea nyumba ya aina gani? Asema Yehova. Au pako wapi mahali pangu pa kupumzikia? Mkono wangu uliumba vitu hivi vyote, sivyo?”​—Mdo. 7:49, 50; Isa. 66:1, 2.

17. Katika mazungumzo yake, Stefano (a) alionyesha nini kuhusu mtazamo wa wasikilizaji wake na (b) alijibuje mashtaka dhidi yake?

17 Unapochunguza mambo ambayo Stefano alisema mbele ya Sanhedrini, je, huoni kwamba alijibu kwa ustadi mambo aliyoshtakiwa? Alionyesha kwamba sikuzote kusudi la Yehova hutimizwa, na halizuiwi na mapokeo au desturi za wanadamu. Wale waliokuwa wakiabudu katika jengo hilo lenye kuvutia lililokuwa Yerusalemu na kushikilia desturi na mapokeo yaliyohusiana na Sheria ya Musa hawakuelewa kusudi la Sheria na hekalu! Ni kana kwamba Stefano alikuwa akisema: Njia bora zaidi ya kuheshimu Sheria na hekalu ni kumtii Yehova. Ni wazi kwamba maneno ya Stefano yalitetea vizuri matendo yake mwenyewe, kwa kuwa alifanya yote awezayo ili kumtii Yehova.

18. Tunawezaje kumwiga Stefano?

18 Tunaweza kujifunza nini kutokana na hotuba ya Stefano? Aliyajua Maandiko vizuri. Sisi pia tunapaswa kujifunza kwa bidii Neno la Mungu ili tuweze kulitumia “sawasawa neno la kweli.” (2 Tim. 2:15) Lazima pia tujifunze kuwa na neema na kutumia busara kama alivyofanya Stefano. Watu waliokuwa wakimsikiliza walikuwa wabishi sana! Hata hivyo, aliweza kuzungumza nao kwa muda mrefu, akizungumzia mambo ambayo hata wao waliyakubali na kuyathamini. Pia, alizungumza nao kwa heshima, akiwaita wazee wa mahakama hiyo, “akina baba.” (Mdo. 7:2) Sisi pia tunapaswa kutangaza kweli za Neno la Mungu “kwa upole na heshima kubwa.”​—1 Pet. 3:15.

19. Stefano alitangaza hukumu za Yehova mbele ya Sanhedrini jinsi gani?

19 Hata hivyo, hatuepuki kutangaza kweli za Neno la Mungu ili tu tusiwakasirishe watu; wala hatupunguzi uzito wa ujumbe wa hukumu za Yehova. Stefano alituwekea mfano mzuri. Bila shaka, aliona wazi kwamba uthibitisho wote aliotoa mbele ya Sanhedrini haukuwa na maana yoyote machoni pa mahakimu hao wenye mioyo migumu. Kwa hiyo, akichochewa na roho takatifu, alimalizia mazungumzo yake kwa kuwaambia bila woga kwamba walikuwa tu kama baba zao waliomkataa Yosefu, Musa, na manabii wote. (Mdo. 7:51-53) Isitoshe, mahakimu hao wa Sanhedrini walikuwa wamemuua Masihi, ambaye Musa na manabii wengine wote walitabiri kuja kwake. Kwa kweli, walikuwa wameivunja kabisa Sheria ya Musa!

“Bwana Yesu, Pokea Roho Yangu” (Mdo. 7:54–8:3)

“Waliposikia mambo hayo wakawaka hasira moyoni na kuanza kumsagia meno yao.”—Matendo 7:54

20, 21. Sanhedrini ilitendaje iliposikia maneno ya Stefano, naye Yehova alimtia nguvu jinsi gani?

20 Mahakimu hao walikasirishwa sana na mambo ya kweli ambayo Stefano aliwaambia. Bila kukawia, wakaanza kumsagia meno yao. Haikosi mwanamume huyo mwadilifu alikumbuka jinsi Bwana wake Yesu alivyotendewa kikatili, naye alijua kwamba hataonyeshwa rehema hata kidogo.

21 Stefano alihitaji ujasiri ili kukabili hali iliyokuwa mbele yake. Bila shaka alitiwa moyo sana na maono ambayo Yehova alimwonyesha. Stefano aliuona utukufu wa Mungu, akamwona Yesu akiwa amesimama upande wa kulia wa Yehova! Stefano alipokuwa akisimulia maono hayo, mahakimu hao waliziba masikio kwa mikono yao. Kwa nini? Mapema, Yesu alikuwa ameiambia mahakama hiyo kwamba yeye ndiye Masihi na kwamba angeketi upande wa kulia wa Baba yake. (Marko 14:62) Maono ya Stefano yalithibitisha kwamba Yesu alisema kweli. Hakuna shaka kwamba mahakama hiyo ilikuwa imemsaliti na kumuua Masihi! Kwa pamoja wakamrukia wamtoe nje ili apigwe kwa mawe na kufa. c

22, 23. Kifo cha Stefano kilifanana jinsi gani na kifo cha Bwana wake, na kwa nini Wakristo leo wanaweza kuwa na usadikisho kama wa Stefano?

22 Stefano alikufa kama vile Bwana wake alivyokufa, akiwa na amani moyoni, akimtumaini kabisa Yehova na hakuwa na kinyongo chochote kuelekea waliomuua. Alisema, “Bwana Yesu, pokea roho yangu,” labda kwa sababu bado angeweza kumwona Mwana wa binadamu pamoja na Yehova katika maono. Huenda Stefano alijua maneno haya yenye kutia moyo yaliyosemwa na Yesu: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” (Yoh. 11:25) Mwishowe, Stefano alisali moja kwa moja kwa Mungu kwa sauti kubwa: “Yehova, usiwahesabie dhambi hii.” Baada ya kusema hayo, akalala usingizi katika kifo.​—Mdo. 7:59, 60.

23 Hivyo, Stefano akawa mfia-imani wa kwanza kati ya wafuasi wa Kristo. (Ona sanduku lenye kichwa “ Stefano—Alikuwa Shahidi au Mfia-Imani?”) Hata hivyo, jambo la kusikitisha ni kwamba hakuwa wa mwisho. Leo, watumishi waaminifu wa Yehova wameuawa na wafuasi wa dini, wanasiasa, na wapinzani wengine wakatili. Hata hivyo, tuna sababu nzuri ya kuwa na usadikisho kama aliokuwa nao Stefano. Sasa, Yesu anatawala akiwa Mfalme, na ana nguvu nyingi alizopewa na Baba yake. Hakuna kitakachomzuia kuwafufua wafuasi wake waaminifu.​—Yoh. 5:28, 29.

24. Sauli alichangiaje kuuawa kwa Stefano, na kifo cha Stefano kilikuwa na matokeo gani mazuri baadaye?

24 Kijana Sauli alikuwa akitazama mambo yote yaliyokuwa yakiendelea. Aliunga mkono kuuawa kwa Stefano, hata alitunza mavazi ya nje ya wale waliokuwa wakimpiga kwa mawe. Muda mfupi baadaye aliongoza katika kuwanyanyasa vikali Wakristo. Lakini kifo cha Stefano kingekuwa na matokeo mazuri baadaye. Mfano wake uliwaimarisha Wakristo wengine waendelee kuwa waaminifu mpaka mwisho kama alivyofanya. Isitoshe, Sauli, ambaye baadaye alikuja kujulikana kama Paulo, alisikitishwa sana baadaye kwa sababu ya msimamo wake Stefano alipokuwa akiuawa. (Mdo. 22:20) Alichangia kumwua Stefano, lakini baadaye alitambua makosa yake na kukiri hivi: “Nilikuwa mkufuru na mtesaji na mtu mwenye dharau.” (1 Tim. 1:13) Ni wazi kwamba, Paulo hakumsahau kamwe Stefano, na mambo yenye kuchochea sana aliyosema siku hiyo. Isitoshe, katika baadhi ya hotuba zake na barua alizoandika, Paulo alitia ndani mambo ambayo Stefano alitaja. (Mdo. 7:48; 17:24; Ebr. 9:24) Baadaye, Paulo aliiga imani na ujasiri wa Stefano, mtu aliyekuwa “amejaa kibali cha Mungu na nguvu.” Je, sisi pia tutafanya hivyo?

a Baadhi ya wapinzani hao walikuwa sehemu ya “Sinagogi la Watu Waliowekwa Huru.” Huenda walikuwa watu waliokuwa wamekamatwa na Waroma kisha wakaachiliwa, au huenda walikuwa watumwa waliowekwa huru kisha wakawa Wayahudi wageuzwa imani. Baadhi yao walikuwa wenyeji wa Kilikia, alikotoka Sauli wa Tarso. Masimulizi hayo hayataji iwapo Sauli alikuwa miongoni mwa Wakilikia waliokuwa wameshindwa kuthibitisha kwamba walikuwa sahihi kuhusu madai yao dhidi ya Stefano.

b Stefano anazungumzia habari ambazo hazipatikani kwingineko katika Biblia. Habari hizo zinatia ndani elimu ambayo Musa alipata alipokuwa Misri, umri aliokuwa nao alipokimbia Misri, na muda aliokaa Midiani.

c Chini ya sheria ya Roma, inaelekea kwamba Sanhedrini haikuwa na mamlaka ya kumhukumu mtu kifo. (Yoh. 18:31) Vyovyote vile, inaonekana kwamba Stefano aliuawa na umati uliokuwa na hasira, bali si hukumu ya kifo iliyokuwa ikitekelezwa.