Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 17

“Akajadiliana Nao Akitumia Maandiko”

“Akajadiliana Nao Akitumia Maandiko”

Msingi mzuri wa kufundisha; mfano mzuri uliowekwa na Waberoya

Matendo 17:1-15

1, 2. Ni nani wanaosafiri kutoka Filipi kwenda Thesalonike, na huenda wanafikiria nini?

 BARABARA nzuri sana iliyojengwa na wahandisi stadi kutoka Roma. Barabara hiyo iliyojipinda inapitia milimani. Kuna kelele nyingi—milio ya punda, kelele za magurudumu ya magari ya kukokotwa, na kelele za wasafiri. Huenda wasafiri walitia ndani wanajeshi, wafanyabiashara, na mafundi. Paulo, Sila na Timotheo wanatumia barabara hiyo kusafiri kutoka Filipi kwenda Thesalonike, umbali wa zaidi ya kilomita 130. Safari hiyo si rahisi, hasa kwa Paulo na Sila kwa kuwa bado walikuwa na majeraha waliyopata Filipi, ambako walipigwa kwa fimbo.​—Mdo. 16:22, 23.

2 Ni nini kitakachowasaidia wasivunjwe moyo na safari ndefu iliyo mbele yao? Ni mazungumzo yao wanapokuwa njiani. Bado wanakumbuka vizuri jambo la kustaajabisha lililotokea huko Filipi, jinsi yule mlinzi wa jela pamoja na familia yake walivyokuwa waamini. Tukio hilo limewachochea waazimie hata zaidi kuendelea kutangaza neno la Mungu. Hata hivyo, wanapokaribia jiji la Thesalonike lililo pwani, hawajui jinsi watakavyotendewa na Wayahudi katika jiji hilo. Je, watashambuliwa, na hata kupigwa kama ilivyokuwa Filipi?

3. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Paulo wa kujipa ujasiri ili kuhubiri?

3 Baadaye Paulo alieleza hisia zake alipowaandikia Wakristo katika jiji la Thesalonike: “Ingawa kwanza tulikuwa tumeteseka na kudharauliwa huko Filipi, kama mnavyojua, tulijipa ujasiri kupitia Mungu wetu ili tuwatangazie ninyi habari njema ya Mungu licha ya upinzani.” (1 The. 2:2) Inaonekana Paulo alisitasita kwenda Thesalonike, hasa baada ya mambo yaliyotokea Filipi. Je, unaweza kuelewa hisia za Paulo? Je, kuna wakati unahisi ni vigumu kuhubiri habari njema? Paulo alimtegemea Yehova ili apate nguvu, na kumwezesha kujipa ujasiri. Mfano wake unaweza kukusaidia kufanya hivyo pia.​—1 Kor. 4:16.

“Akajadiliana . . . Akitumia Maandiko” (Mdo. 17:1-3)

4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Paulo alikaa jijini Thesalonike kwa zaidi ya majuma matatu?

4 Masimulizi yanasema kwamba Paulo alipokuwa Thesalonike, alihubiri katika sinagogi kwa Sabato tatu. Hilo halimaanishi kwamba alikaa jijini humo kwa majuma matatu tu. Huenda Paulo hakuweza kwenda kwenye sinagogi mara tu alipofika Thesalonike. Isitoshe, barua za Paulo zinaonyesha kwamba wakiwa Thesalonike, yeye na wenzake walifanya kazi ili kupata mahitaji yao. (1 The. 2:9; 2 The. 3:7, 8) Akiwa huko, Paulo alipokea vitu fulani mara mbili kwa ajili ya mahitaji yake kutoka kwa akina ndugu wa Filipi. (Flp. 4:16) Hivyo inaonekana alikaa jijini Thesalonike kwa zaidi ya majuma matatu.

5. Paulo alichocheaje fikira za wasikilizaji wake?

5 Baada ya kujipa ujasiri wa kuhubiri, Paulo alizungumza na watu waliokuwa wamekusanyika katika sinagogi. Kulingana na desturi yake, ‘akajadiliana nao akitumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu, akisema: “Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ninayewatangazia ninyi.”’ (Mdo. 17:2, 3) Lengo la Paulo halikuwa kuwasisimua tu wasikilizaji wake bali kuchochea fikira zao. Alijua kwamba watu waliokuwa katika sinagogi waliyajua Maandiko na kuyaheshimu lakini hawakuyaelewa. Hivyo, Paulo alijadili, akafafanua, na kuthibitisha kwa kutumia Maandiko kwamba Yesu wa Nazareti ndiye Masihi, au Kristo, aliyeahidiwa.

6. Yesu aliwathibitishiaje wanafunzi wake kwa kutumia Maandiko, na matokeo yalikuwa nini?

6 Paulo alifuata mfano wa Yesu wa kutumia Maandiko kama msingi wa mafundisho yake. Kwa mfano, katika huduma yake, Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba kulingana na Maandiko, lazima Mwana wa binadamu ateseke na kufa, kisha afufuliwe. (Mt. 16:21) Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatokea wanafunzi wake, na hivyo kuthibitisha kwamba alikuwa amesema kweli. Hata hivyo, Yesu aliwapa uthibitisho zaidi. Tunasoma hivi kuhusu mazungumzo yake na wanafunzi fulani: “Akawafafanulia kuanzia Musa na Manabii wote, mambo yote ambayo Maandiko yalisema kumhusu.” Ikawaje? Wanafunzi wakasema hivi kwa mshangao: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akizungumza nasi barabarani, na alipokuwa akitufungulia Maandiko waziwazi?”​—Luka 24:13, 27, 32.

7. Kwa nini ni muhimu kutumia Maandiko kama msingi wa mafundisho yetu?

7 Ujumbe wa Neno la Mungu una nguvu. (Ebr. 4:12) Kama Yesu, Paulo, na mitume wengine, Wakristo leo hutegemea Neno la Mungu wanapowafundisha watu. Sisi pia hujadili, hufafanua Maandiko, na kuwathibitishia watu mambo tunayowafundisha kwa kuwafungulia Biblia na kuwaonyesha kile ambacho inasema. Ujumbe tunaohubiri si wetu. Tunapotumia Biblia, tunawasaidia kutambua kwamba hatufundishi maoni yetu, bali mafundisho ya Mungu. Pia, tunakumbuka kwamba msingi wa ujumbe wetu ni Neno la Mungu. Neno hilo linategemeka kabisa. Kwa kuwa tunajua kwamba ujumbe wetu unategemeka, tunahubiri kwa ujasiri kama Paulo.

“Baadhi . . . Wakaamini” (Mdo. 17:4-9)

8-10. (a) Watu jijini Thesalonike waliitikiaje habari njema? (b) Kwa nini baadhi ya Wayahudi walimwonea wivu Paulo? (c) Wapinzani Wayahudi walitendaje?

8 Tayari Paulo alikuwa amejionea ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia; ikiwa wamelishika neno langu, watalishika lenu pia.” (Yoh. 15:20) Jijini Thesalonike, Paulo alikutana na watu wenye maoni mbalimbali, baadhi yao walikuwa tayari kutii neno na wengine walipinga. Kuhusu wale waliokubali, Luka anaandika hivi: “Baadhi yao [Wayahudi] wakaamini [wakawa Wakristo] na kujiunga na Paulo na Sila, pia umati mkubwa wa Wagiriki waliomwabudu Mungu, vilevile wanawake wengi mashuhuri.” (Mdo. 17:4) Wanafunzi hao wapya walifurahi kusaidiwa kuyaelewa Maandiko.

9 Ingawa baadhi yao walithamini maneno ya Paulo, wengine walimkasirikia sana. Wayahudi fulani jijini Thesalonike walimwonea wivu Paulo kwa sababu “umati mkubwa wa Wagiriki” ulikubali ujumbe wake. Wayahudi hao, wakiwa na lengo la kupata wafuasi, waliwafundisha Watu wa Mataifa waliokuwa Wagiriki mafundisho kutoka katika Maandiko ya Kiebrania, na waliwaona Wagiriki hao kuwa mali yao. Hata hivyo, ilianza kuonekana kana kwamba Paulo anawanyakua Wagiriki hao, tena hapohapo kwenye sinagogi! Wayahudi hao walikasirika sana.

‘Walitaka Paulo na Sila waletwe nje kwenye kile kikundi.’—Matendo 17:5

10 Luka anatueleza kilichofuata: “Wayahudi wakawa na wivu, wakakusanya wanaume fulani waovu waliokuwa wakizurura sokoni, wakafanyiza kikundi chenye ghasia kisha wakazusha fujo jijini. Wakaishambulia nyumba ya Yasoni wakitaka Paulo na Sila waletwe nje kwenye kile kikundi. Walipowakosa wakamkokota Yasoni na baadhi ya akina ndugu mpaka kwa watawala wa jiji, wakisema kwa sauti kubwa: ‘Watu hawa ambao wameipindua dunia inayokaliwa wako hapa pia, naye Yasoni amewakaribisha. Watu hao wote wanapinga maagizo ya Kaisari, wakisema kuna mfalme mwingine, Yesu.’” (Mdo. 17:5-7) Mashambulizi hayo yangewaathirije Paulo na wenzake?

11. Paulo na wenzake walishtakiwa kwa makosa gani, na huenda waliowashtaki walidai wamevunja amri gani? (Ona maelezo ya chini)

11 Kikundi chenye ghasia ni kama mto uliovunja kingo zake, wenye nguvu nyingi na usiozuilika. Wayahudi walitumia kikundi hicho ili kujaribu kuwafukuza Paulo na Sila. Baada ya “kuzusha fujo jijini,” wakajaribu kuwasadikisha watawala kwamba mashtaka yao yalikuwa mazito. Shtaka la kwanza lilikuwa kwamba Paulo na wenzake “wameipindua dunia inayokaliwa,” ingawa Paulo na wenzake hawakusababisha fujo jijini Thesalonike! Shtaka la pili lilikuwa zito zaidi. Wayahudi walidai kwamba wamishonari hao wanamtangaza Mfalme mwingine, Yesu, na hivyo wanavunja sheria ya maliki. a

12. Ni nini kinachoonyesha kwamba mashtaka dhidi ya Wakristo jijini Thesalonike yangeweza kuwa na matokeo mabaya?

12 Kumbuka kwamba viongozi wa kidini walimshtaki Yesu kwa madai yanayofanana na hayo. Walimwambia Pilato: “Tulimkuta mtu huyu akipindua taifa letu . . . akisema kwamba yeye mwenyewe ni Kristo mfalme.” (Luka 23:2) Huenda Pilato aliogopa kuwa maliki angefikiri ameachilia kosa kubwa la uhaini, ndio sababu alimhukumu Yesu kwamba anastahili kufa. Vivyo hivyo, mashtaka dhidi ya Wakristo jijini Thesalonike yangekuwa na matokeo mabaya. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema: “Mashtaka hayo yalikuwa hatari sana. Ikiwa mtu angetuhumiwa kuwa anataka kumsaliti Maliki, angeweza kuhukumiwa kifo.’” Je, mashtaka hayo yenye chuki yangefanikiwa?

13, 14. (a) Kwa nini kikundi chenye ghasia hakikufanikiwa? (b) Paulo alifuata jinsi gani ushauri wa Kristo wa kuwa waangalifu, nasi tunawezaje kuiga mfano wake?

13 Umati huo wenye ghasia ulishindwa kukomesha kazi ya kuhubiri jijini Thesalonike. Kwa nini? Kwanza, Paulo na Sila hawakupatikana. Isitoshe, inaonekana kwamba watawala wa jiji hilo hawakuamini mashtaka hayo. Baada ya kuchukua “dhamana ya kutosha,” walimwachilia Yasoni na ndugu wengine waliofikishwa mbele yao. (Mdo. 17:8, 9) Paulo alifuata ushauri wa Yesu wa kuwa ‘mwangalifu kama nyoka na asiye na hatia kama njiwa.’ (Mt. 10:16) Alifanya hivyo kwa kuondoka kwa busara mahali penye hatari na kwenda kuhubiri mahali pengine. Bila shaka, ujasiri wa Paulo haukuwa wa kijinga. Wakristo wanawezaje kuiga mfano wake?

14 Leo, mara nyingi viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo huwachochea watu wawafanyie fujo Mashahidi wa Yehova. Wamewachochea watawala wawatese kwa kudai kwamba Mashahidi wanaipinga serikali au si wazalendo. Kama karne ya kwanza, wapinzani wa leo huchochewa na wivu. Wakristo wa kweli hawajihatarishi bila sababu. Sisi huepuka kubishana na watu wenye hasira na wakaidi, badala yake tunaendelea kufanya kazi yetu kwa amani, na ikiwezekana tunawarudia baadaye wanapokuwa wametulia.

“Walikuwa Wasikivu” (Mdo. 17:10-15)

15. Waberoya waliitikiaje habari njema?

15 Kwa ajili ya usalama wao, Paulo na Sila walitumwa Beroya, kilomita 65 hivi kutoka Thesalonike. Walipofika huko, Paulo alienda katika sinagogi na kuanza kuzungumza na watu waliokusanyika huko. Walifurahi sana kwa sababu walipata watu waliosikiliza. Luka aliandika kwamba Wayahudi wa Beroya walikuwa “wasikivu kuliko wale wa Thesalonike, kwa maana walilikubali neno kwa hamu kubwa ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.” (Mdo. 17:10, 11) Hili halimaanishi kwamba Wathesalonike waliokubali kweli walikuwa na mtazamo mbaya. Baadaye Paulo aliwaandikia: “Tunamshukuru Mungu bila kuacha, kwa kuwa mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali si kama neno la wanadamu, bali kama lilivyo kwa kweli, neno la Mungu, ambalo pia linafanya kazi ndani yenu waamini.” (1 The. 2:13) Hata hivyo, ni nini kilichowafanya Wayahudi waliokuwa Beroya kuwa wasikivu zaidi?

16. Kwa nini Waberoya waliitwa “wasikivu”?

16 Ingawa ilikuwa habari mpya kwa Waberoya, hawakutilia shaka au kuichambua. Haimaanishi walidanganyika kwa urahisi. Kwanza walimsikiliza Paulo kwa makini. Kisha, wakahakikisha mambo waliyojifunza kwa kusoma Maandiko ambayo Paulo aliwasaidia kuyaelewa. Isitoshe, walikuwa wakijifunza Neno la Mungu kila siku, si siku ya Sabato tu. Na walifanya hivyo “kwa hamu kubwa ya akili,” wakijitahidi kujua mambo ambayo Maandiko yanasema kuhusu mafundisho hayo mapya. Pia, walionyesha unyenyekevu kwa kufanya mabadiliko na “wengi wao wakawa waamini.” (Mdo. 17:12) Ndiyo sababu Luka anasema kwamba walikuwa “wasikivu”!

17. Kwa nini Waberoya ni mfano mzuri wa kuigwa, na tunawezaje kudumisha mtazamo huo hata ikiwa tumekuwa katika kweli kwa muda mrefu?

17 Waberoya hao hawakujua kwamba mtazamo wao mzuri kuelekea habari njema ungeandikwa katika Neno la Mungu kwa faida ya wengine. Walifanya kama vile Paulo alivyotarajia na jinsi Yehova Mungu alivyotaka wafanye. Leo, sisi huwatia moyo watu wachunguze Biblia kwa makini ili imani yao itegemee Neno la Mungu. Hata hivyo, baada ya kuwa waamini, je, huo ndio mwisho wa kuwa wasikivu? Hapana, usikivu ni muhimu hata zaidi nasi tunapaswa kuwa na hamu kubwa zaidi ya kujifunza kutoka kwa Yehova na kutumia mambo tunayojifunza maishani. Kwa kufanya hivyo, tunamruhusu Yehova atufinyange na kutuzoeza kulingana na mapenzi yake. (Isa. 64:8) Hivyo, tunampendeza Baba yetu wa mbinguni naye ataendelea kututumia kutimiza makusudi yake.

18, 19. (a) Kwa nini Paulo aliondoka Beroya, na tunajifunza nini kutokana na mfano wake? (b) Paulo anapaswa kuwahubiria nani sasa, na wapi?

18 Paulo hakukaa Beroya kwa muda mrefu. Tunasoma hivi: “Wayahudi kutoka Thesalonike waliposikia kwamba Paulo alikuwa akitangaza pia neno la Mungu huko Beroya, wakaja huko ili kuchochea na kuuvuruga umati. Mara moja akina ndugu wakamsindikiza Paulo mpaka baharini, lakini Sila na Timotheo wakabaki huko. Hata hivyo, wale waliomsindikiza Paulo wakaenda naye mpaka Athene, kisha wakarudi baada ya kupokea maagizo kwamba Sila na Timotheo wamfuate Paulo haraka iwezekanavyo.” (Mdo. 17:13-15) Adui hao wa habari njema hawakukata tamaa! Hawakutosheka kwamba Paulo ameondoka Thesalonike; walimfuata mpaka Beroya na kujaribu kuwachochea watu wa huko pia, lakini hawakufanikiwa. Paulo alijua kwamba eneo ni kubwa, kwa hiyo alienda kuhubiri eneo lingine. Sisi pia, tuazimie kusimama imara dhidi ya wale wanaotaka kukomesha kazi yetu ya kuhubiri!

19 Baada ya kutoa ushahidi kamili kwa Wayahudi wa Thesalonike na Beroya, Paulo alikuwa amejifunza mengi kuhusu umuhimu wa kuhubiri kwa ujasiri na kujadiliana na watu kwa kutumia Maandiko. Sisi pia tumejifunza mengi. Hata hivyo, sasa Paulo anakutana na wasikilizaji tofauti—Watu wa Mataifa jijini Athene. Mambo yatakuwaje katika jiji hilo? Tutaona katika sura inayofuata.

a Kulingana na msomi mmoja, wakati huo kulikuwa na sheria ya Kaisari iliyokataza utabiri wowote kuhusu “kuja kwa mfalme au ufalme mpya, hasa mfalme anayeweza kumwondoa au kumhukumu maliki anayetawala.” Huenda adui za Paulo walifanya ujumbe wa mtume huyo uonekane kana kwamba unakiuka sheria hiyo. Ona sanduku lenye kichwa “ Kaisari Wanaotajwa Katika Kitabu cha Matendo.”