Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 15

“Kuyaimarisha Makutaniko”

“Kuyaimarisha Makutaniko”

Waangalizi wa mzunguko huyasaidia makutaniko yawe na imani yenye nguvu

Matendo 15:36–16:5

1-3. (a) Paulo anasafiri na nani, na mwandamani huyo ni mtu wa aina gani? (b) Tutajifunza nini katika sura hii?

 WANAPOVUKA milima na mabonde kutoka mji mmoja hadi mwingine, mtume Paulo anamfikiria kijana anayesafiri pamoja naye. Kijana huyo ni Timotheo mwenye umri wa miaka 20 hivi. Kadiri kijana huyo anavyotembea katika safari hii ndivyo anavyokuwa mbali zaidi na nyumbani kwao. Kadiri siku inavyopita, ndivyo wanavyozidi kuwa mbali na majiji ya Listra na Ikoniamu. Ni mambo gani yatakayotokea? Huenda Paulo alijua kwa sababu hii ni safari yake ya pili ya umishonari. Anajua kwamba kutakuwa na hatari na matatizo mengi. Timotheo atatendaje atakapokabili hali hizo?

2 Paulo anamwamini Timotheo, labda kuliko Timotheo anavyojiamini. Matukio ya karibuni yalimfanya Paulo aone umuhimu wa kuchagua mwandamani anayefaa. Paulo anajua kwamba kazi ya kutembelea makutaniko na kuyatia nguvu, inahitaji waangalizi walio thabiti na wenye nia moja. Kwa nini? Huenda sababu moja ni kutoelewana kati ya Paulo na Barnaba kulikosababisha mgawanyiko.

3 Katika sura hii tutajifunza mengi kuhusu njia bora ya kutatua kutoelewana. Pia, tutajua ni kwa nini Paulo alichagua kusafiri na Timotheo, nasi tutajifunza mengi kuhusu kazi muhimu inayotimizwa na waangalizi wa mzunguko.

“Turudi Tukawatembelee Akina Ndugu” (Mdo. 15:36)

4. Paulo alikusudia kufanya nini katika safari yake ya pili ya umishonari?

4 Katika sura iliyotangulia tuliona jinsi ndugu wanne, Paulo, Barnaba, Yuda, na Sila, walivyolitia nguvu kutaniko la Antiokia kwa kulijulisha uamuzi wa baraza linaloongoza kuhusu suala la tohara. Paulo alifanya nini baadaye? Alimwendea Barnaba akiwa na mikakati mipya ya safari, akamwambia: “Turudi tukawatembelee akina ndugu katika kila jiji ambalo tulitangaza neno la Yehova tuone jinsi wanavyoendelea.” (Mdo. 15:36) Paulo hakuwa akipendekeza wawatembelee Wakristo hao wapya kirafiki tu. Kitabu cha Matendo kinaonyesha wazi kusudi halisi la safari ya pili ya umishonari ya Paulo. Kwanza, kuyajulisha makutaniko maagizo yaliyotolewa na baraza linaloongoza. (Mdo. 16:4) Pili, akiwa mwangalizi wa mzunguko, Paulo alikuwa ameazimia kuyajenga makutaniko kiroho, na kusaidia kuimarisha imani yao. (Rom. 1:11, 12) Tengenezo la Mashahidi wa Yehova linafanyaje hivyo leo?

5. Baraza Linaloongoza huwasiliana na makutaniko na kuyatia moyo jinsi gani?

5 Leo, Kristo anatumia Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova kuongoza kutaniko lake. Kupitia barua, machapisho ya mtandaoni na yaliyochapishwa, mikutano, na njia nyingine, ndugu hao watiwa-mafuta huyaongoza na kuyatia moyo makutaniko ulimwenguni pote. Pia, Baraza Linaloongoza hujitahidi kudumisha mawasiliano pamoja na kila kutaniko. Ili kufanya hivyo, wanatumia waangalizi wa mzunguko. Baraza Linaloongoza huwaweka rasmi maelfu ya wazee wanaostahili ulimwenguni pote kuwa waangalizi wa mzunguko.

6, 7. Waangalizi wa mzunguko wana majukumu gani?

6 Waangalizi wa mzunguko leo huwahangaikia na kuwatia moyo wote katika makutaniko wanayotembelea. Jinsi gani? Kwa kufuata kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza kama Paulo. Alimhimiza hivi mwangalizi mwenzake: “Lihubiri neno; fanya hivyo kwa uharaka katika nyakati zinazofaa na nyakati ngumu; karipia, kemea, himiza, kwa subira yote na ustadi wa kufundisha. . . . Fanya kazi ya mweneza-injili.”​—2 Tim. 4:2, 5.

7 Waangalizi wa mzunguko—pamoja na wake zao ikiwa wameoa—hutii maneno hayo kwa kushiriki katika huduma ya shambani pamoja na wahubiri wa kutaniko wanalotembelea. Kwa sababu wao ni walimu stadi, na wanapenda huduma, mfano wao unawachochea ndugu na dada. (Rom. 12:11; 2 Tim. 2:15) Waangalizi wa mzunguko huonyesha upendo usio na ubinafsi na kujidhabihu. Huwatumikia wengine kwa hiari, nyakati nyingine wanasafiri wakati ambapo kuna hali mbaya ya hewa na hata katika maeneo yenye hatari. (Flp. 2:3, 4) Pia, waangalizi wa mzunguko hutia moyo, hufundisha, na kuonya makutaniko kupitia hotuba zinazotegemea Biblia. Ni vizuri kwa wote kutanikoni kutafakari mfano mzuri wa waangalizi hao na kujitahidi kuiga imani yao.​—Ebr. 13:7.

“Wakagombana kwa Ukali” (Mdo. 15:37-41)

8. Barnaba aliitikiaje mwaliko wa Paulo?

8 Barnaba alikubali pendekezo la Paulo la ‘kuwatembelea akina ndugu.’ (Mdo. 15:36) Wawili hao walifanya kazi bega kwa bega wakisafiri pamoja, na tayari walijua maeneo na watu waliohitaji kutembelewa. (Mdo. 13:2–14:28) Kwa hiyo, huenda waliona ingefaa wasafiri pamoja kwa ajili ya mgawo huo. Hata hivyo, tatizo likatokea. Andiko la Matendo 15:37 linasema: “Barnaba alikuwa ameazimia kwenda na Yohana, aliyeitwa Marko.” Barnaba hakuwa akitoa pendekezo. “Alikuwa ameazimia” waende pamoja binamu yake, Marko, katika safari hiyo ya umishonari.

9. Kwa nini Paulo na Barnaba hawakuelewana?

9 Paulo hakukubali. Kwa nini? Masimulizi yanasema: “Lakini Paulo hakutaka waende pamoja naye [Marko], kwa sababu alikuwa amewaacha huko Pamfilia na hakuenda pamoja nao kwenye kazi.” (Mdo. 15:38) Marko alikuwa amesafiri pamoja na Paulo na Barnaba katika safari yao ya kwanza ya umishonari lakini hakuendelea na safari hiyo mpaka mwisho. (Mdo. 12:25; 13:13) Mwanzoni katika safari yao ya kwanza, wakiwa Pamfilia, Marko aliuacha mgawo wake na kurudi nyumbani Yerusalemu. Biblia haisemi ni kwa nini aliondoka, lakini inaonekana kwamba mtume Paulo alimwona Marko kuwa mtu asiyechukua mambo kwa uzito. Huenda Paulo alikuwa na mashaka kuhusu kutegemeka kwa Marko.

10. Kutoelewana kati ya Paulo na Barnaba kulisababisha nini, na matokeo yalikuwa nini?

10 Hata hivyo, Barnaba alikuwa ameazimia kwenda na Marko. Na Paulo alikataa kwenda naye. Matendo 15:39 inasema: “Ndipo wakagombana kwa ukali hivi kwamba wakaachana.” Barnaba akapanda meli kuelekea Kipro, kisiwa cha nyumbani kwao, akiwa pamoja na Marko. Naye Paulo akaenda zake. Masimulizi hayo yanasema: “Paulo akamchagua Sila na kuondoka baada ya akina ndugu kumkabidhi kwenye fadhili zisizostahiliwa za Yehova.” (Mdo. 15:40) Wakasafiri pamoja ‘kupitia Siria na Kilikia, wakiyaimarisha makutaniko.’​—Mdo. 15:41.

11. Ni sifa gani zinazohitajiwa ili kudumisha urafiki na mtu aliyetukosea?

11 Huenda masimulizi hayo yakatukumbusha hali yetu ya kutokamilika. Paulo na Barnaba walikuwa wamewekwa rasmi kuwa wawakilishi wa pekee wa baraza linaloongoza. Inaonekana baadaye Paulo aliwekwa rasmi kuwa mshiriki wa baraza hilo. Hata hivyo, ingawa Paulo na Barnaba walikuwa ndugu wazuri sana, wakati huu walishindwa kudhibiti hasira yao. Je, wangeruhusu hali hiyo ivunje kabisa urafiki wao? Ingawa hawakuwa wakamilifu, Paulo na Barnaba walikuwa wanyenyekevu, na walikuwa na akili ya Kristo. Ndiyo sababu baada ya muda mfupi, walionyesha roho ya undugu wa Kikristo na kusameheana. (Efe. 4:1-3) Baadaye, Paulo na Marko walifanya kazi pamoja katika migawo mingine ya Kikristo. aKol. 4:10.

12. Kama Paulo na Barnaba, waangalizi wanapaswa kuwa na sifa gani?

12 Tukio hilo moja halimaanishi kwamba Barnaba na Paulo walikuwa na utu huo. Barnaba alikuwa mwenye upendo na mkarimu sana hivi kwamba badala ya mitume kumwita kwa jina lake, Yosefu, walikuwa wakimwita Barnaba, yaani, “Mwana wa Faraja.” (Mdo. 4:36) Paulo alikuwa mpole na mwenye upendo mwororo. (1 The. 2:7, 8) Waangalizi Wakristo leo, kutia ndani waangalizi wa mzunguko, wanapaswa kujitahidi kuwa wanyenyekevu na kuwatendea wazee wenzao na kundi zima kwa wororo.​—1 Pet. 5:2, 3.

“Alishuhudiwa Vema” (Mdo. 16:1-3)

13, 14. (a) Timotheo alikuwa nani, na alikutana jinsi gani na Paulo? (b) Kwa nini Paulo alipendezwa na Timotheo? (c) Timotheo alipewa mgawo gani?

13 Katika safari yake ya pili ya umishonari, Paulo alienda Galatia, mkoa wa Roma, ambako makutaniko kadhaa yalikuwa yameanzishwa. Mwishowe, “akafika Derbe na pia Listra.” Simulizi hilo linaendelea kusema hivi: “Huko kulikuwa na mwanafunzi aliyeitwa Timotheo, mama yake alikuwa Myahudi aliyekuwa mwamini, lakini baba yake alikuwa Mgiriki.”​—Mdo. 16:1. b

14 Inaonekana kwamba, Paulo alikuwa amekutana na familia ya Timotheo alipotembelea eneo hilo karibu mwaka wa 47 W.K. Baada ya miaka miwili au mitatu hivi, wakati wa safari yake ya pili, Paulo alipendezwa kwa njia ya pekee na kijana Timotheo. Kwa nini? Kwa sababu Timotheo “alishuhudiwa vema na akina ndugu.” Sifa nzuri za Timotheo zilijulikana kutanikoni kwao na hata katika makutaniko mengine. Masimulizi ya Matendo yanasema kwamba akina ndugu wa Listra na Ikoniamu, waliokuwa umbali wa kilomita 30 hivi, walijua sifa nzuri za Timotheo. (Mdo. 16:2) Wakiongozwa na roho takatifu, wazee walimpa kijana Timotheo mgawo mzito wa kusafiri pamoja na Paulo na Sila ili kufanya kazi nao.​—Mdo. 16:3.

15, 16. Timotheo aliwezaje kupata sifa nzuri?

15 Timotheo alipataje sifa nzuri hivyo akiwa kijana? Je, ni kwa sababu alikuwa na akili nyingi, sura nzuri, au vipawa vyake? Mara nyingi wanadamu huvutiwa na mambo kama hayo. Hata nabii Samweli alidanganyika wakati fulani kwa kuangalia mwonekano wa nje. Hata hivyo, Yehova alimkumbusha: “Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona ndani ya moyo.” (1 Sam. 16:7) Timotheo alikuwa na sifa za ndani zilizowavutia Wakristo wenzake.

16 Miaka kadhaa baadaye, mtume Paulo alirejelea sifa fulani za Timotheo. Paulo alitaja mtazamo wake mzuri, upendo wake wa kujidhabihu, na bidii yake katika kushughulikia migawo ya kiroho. (Flp. 2:20-22) Timotheo alijulikana pia kwa kuwa na ‘imani isiyo na unafiki.’​—2 Tim. 1:5.

17. Vijana wanawezaje kumwiga Timotheo?

17 Leo, vijana wengi humwiga Timotheo kwa kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu. Wanajifanyia jina zuri pamoja na Yehova na watu wake, hata wakiwa na umri mdogo. (Met. 22:1; 1 Tim. 4:15) Wanaonyesha imani isiyo na unafiki. (Zab. 26:4) Hivyo, vijana wengi, kama Timotheo, wanaweza kutimiza mengi katika kutaniko. Wanapostahili kuwa wahubiri wa habari njema na hatimaye kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, wao huwatia moyo wote wanaompenda Yehova!

“Kuimarishwa Katika Imani” (Mdo. 16:4, 5)

18. (a) Paulo na Timotheo walilisaidiaje baraza linaloongoza wakiwa wahudumu wanaosafiri? (b) Makutaniko yalipata baraka gani?

18 Paulo na Timotheo walifanya kazi pamoja kwa miaka mingi. Wakiwa wahudumu wanaosafiri, walifanya mambo mbalimbali waliyoagizwa na baraza linaloongoza. Biblia inasema: “Walipokuwa wakipita katika majiji, walikuwa wakiwapa maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu ili wayashike.” (Mdo. 16:4) Bila shaka makutaniko yalifuata mwongozo wa mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu. Kwa sababu ya kutii “makutaniko yakaendelea kuimarishwa katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”​—Mdo. 16:5.

19, 20. Kwa nini Wakristo wanapaswa kuwatii “wale wanaoongoza”?

19 Leo pia Mashahidi wa Yehova hupata baraka nyingi wanapofuata mwongozo wa “wale wanaoongoza” kati yao. (Ebr. 13:17) Kwa kuwa tamasha ya ulimwengu huu inabadilika, Wakristo wanapaswa kukubali na kujitiisha chini ya mwongozo wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45; 1 Kor. 7:29-31) Tukifanya hivyo tutaepuka madhara ya kiroho na kubaki bila doa kutokana na ulimwengu.​—Yak. 1:27.

20 Waangalizi Wakristo leo kutia ndani washiriki wa Baraza Linaloongoza si wakamilifu kama walivyokuwa Paulo, Barnaba, Marko na wazee wengine watiwa mafuta wa karne ya kwanza. (Rom. 5:12; Yak. 3:2) Hata hivyo, Baraza Linaloongoza linategemeka kwa sababu linashikamana kabisa na Neno la Mungu na kufuata mfano uliowekwa na mitume. (2 Tim. 1:13, 14) Matokeo ni kwamba makutaniko yanatiwa nguvu na kuimarishwa katika imani.

a Ona sanduku lenye kichwa “ Marko Apata Mapendeleo Mengi.”

b Ona sanduku lenye kichwa “ Timotheo Atumika ‘Kuendeleza Habari Njema’.”