Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 18

“Wamtafute Mungu, . . . na kwa Kweli Wampate”

“Wamtafute Mungu, . . . na kwa Kweli Wampate”

Paulo aweka msingi mzuri wa mazungumzo na kubadilika kulingana na hali ya wasikilizaji wake

Matendo 17:16-34

1-3. (a) Ni nini kilichomkasirisha mtume Paulo akiwa Athene? (b) Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza mfano wa Paulo?

 PAULO amekasirika sana. Yuko jijini Athene, kitovu cha elimu nchini Ugiriki, ambako wakati fulani wanafalsafa kama vile Sokratesi, Plato, na Aristoto walifundisha. Athene ni jiji la kidini. Pande zote—mahekaluni, katika viwanja vya watu wote, na barabarani—Paulo anaona sanamu nyingi, kwa sababu Waathene huabudu miungu mingi sana. Paulo anajua maoni ya Mungu wa kweli, Yehova, kuhusiana na ibada ya sanamu. (Kut. 20:4, 5) Mtume huyo mwaminifu ana maoni kama ya Yehova—anachukia sanamu!

2 Paulo anashangazwa sana na mambo anayoona anapoingia sokoni. Kuna sanamu nyingi za mungu Herme zenye umbo la kiungo cha uzazi cha kiume zilizowekwa upande wa kaskazini-magharibi, karibu na lango kuu. Soko hilo lina madhabahu nyingi. Mtume huyo mwenye bidii atahubiri jinsi gani katika jiji hilo ambalo ibada ya sanamu imekita mizizi? Je, ataonyesha sifa ya kujizuia na kuweka msingi mzuri wa mazungumzo kwa wasikilizaji wake? Je, atafaulu kumsaidia yeyote amtafute Mungu wa kweli na kumwabudu?

3 Hotuba ya Paulo, iliyo katika Matendo 17:22-31, ambayo aliitoa mbele za watu hao wenye elimu inaonyesha kwamba alitumia ushawishi, busara, na utambuzi. Mfano wa Paulo unaweza kutusaidia sana kujua jinsi ya kuweka msingi mzuri wa mazungumzo na kuwasaidia wasikilizaji wetu kufikiri.

Kufundisha “Sokoni” (Mdo. 17:16-21)

4, 5. Paulo alihubiri wapi akiwa Athene, naye alikutana na watu wa aina gani?

4 Katika safari yake ya pili ya umishonari, mwaka wa 50 hivi W.K., Paulo alitembelea jiji la Athene. a Alipokuwa akiwasubiri Sila na Timotheo wafike kutoka Beroya, Paulo “akaanza kujadiliana katika sinagogi pamoja na Wayahudi,” kama ilivyokuwa desturi yake. Pia alienda “sokoni,” mahali ambapo angeweza kuwapata watu wa Athene wasio Wayahudi. (Mdo. 17:17) Soko hilo lililokuwa na ukubwa wa ekari 12 hivi, lilikuwa upande wa kaskazini-magharibi mwa Ngome ya Athene. Halikuwa mahali pa kuuza na kununua tu, bali pia uwanja wa watu wote. Kitabu fulani cha marejeo kinasema kwamba mahali hapo palikuwa “kituo cha kibiashara, kisiasa na kitamaduni jijini humo.” Waathene walipenda kukusanyika hapo na kuzungumzia mambo mbalimbali ya kitaalamu.

5 Akiwa sokoni, Paulo alikutana na watu ambao hawakuwa tayari kumsikiliza. Baadhi ya wasikilizaji wake walikuwa Waepikurea na Wastoa, ambao waliamini falsafa mbili tofauti. b Waepikurea waliamini kwamba uhai ulijitokeza wenyewe tu. Kwa ufupi, waliamini hivi: “Mungu hawezi kutufanya lolote; Hakuna maumivu yoyote katika kifo; Mambo mema yanaweza kufanywa; Mambo mabaya yanaweza kuvumiliwa.” Wastoa walikazia falsafa za kibinadamu nao hawakuamini kwamba kuna Mungu. Waepikurea na Wastoa hawakuamini ufufuo ambao wanafunzi wa Kristo walifundisha. Ni wazi kwamba maoni ya kifalsafa ya vikundi hivyo viwili hayakupatana hata kidogo na Ukristo wa kweli, ambao Paulo alikuwa akitangaza.

6, 7. Wasomi Wagiriki waliyaonaje mafundisho ya Paulo, na hali ikoje leo?

6 Wasomi Wagiriki walionaje mafundisho ya Paulo? Baadhi yao walimwita “mpigadomo.” (Mdo. 17:18) Kuhusu neno la Kigiriki linalotumika katika mstari huo, msomi mmoja anasema hivi: “Mwanzoni neno hilo lilitumiwa kurejelea ndege mdogo anayerukaruka akiokota punje, pia lilitumiwa kurejelea watu waliokuwa wakiokota masalio ya vyakula na vitu vingine vilivyoanguka sokoni. Baadaye, neno hilo lilianza kutumiwa kwa njia ya mfano kurejelea mtu anayekusanya habari hapa na pale, na hasa yule ambaye haelewi habari zenyewe.” Kwa kumwita “mpiga-domo,” ni kana kwamba wasomi hao walisema kwamba Paulo ni mtu anayerudia-rudia mambo asiyoelewa, ambayo amesikia kutoka kwa wengine. Kama tutakavyoona, Paulo hakuvunjika moyo kwa kuitwa jina hilo.

7 Ndivyo ilivyo leo. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, mara nyingi tunasemwa vibaya kwa sababu ya imani yetu inayotegemea Biblia. Kwa mfano, walimu fulani hudai kwamba fundisho la mageuzi ni la kweli na kwamba ikiwa una akili, utaliamini. Ni kana kwamba wanadai wote wanaopinga fundisho hilo ni wajinga. Wasomi hao wanataka watu wengine watuone sisi kuwa wajinga kwa sababu tunafundisha mambo ambayo Biblia inasema na kuthibitisha kwamba vitu vyote viliumbwa. Hata hivyo, hilo halituvunji moyo. Badala yake, tunasema tukiwa na uhakika kwamba uhai uliopo duniani ulitokana na Muumba mwenye akili, Yehova Mungu.​—Ufu. 4:11.

8. (a) Baadhi ya watu waliomsikia Paulo akihubiri walikuwa na maoni gani? (b) Kwa nini Paulo alipelekwa Areopago? (Ona maelezo ya chini katika ukurasa wa 142.)

8 Wengine waliomsikiliza Paulo akihubiri sokoni walikuwa na maoni tofauti. Walisema: “Inaonekana anatangaza miungu ya kigeni.” (Mdo. 17:18) Je, ni kweli Paulo alikuwa akiwatangazia Waathene miungu ya kigeni? Hilo lilikuwa jambo zito. Karne kadhaa mapema, Sokratesi alihukumiwa kifo kwa mashtaka kama hayo. Hivyo, haishangazi kwamba Paulo alipelekwa Areopago na kuambiwa afafanue mafundisho hayo yaliyokuwa mageni kwa Waathene. c Paulo angeuteteaje ujumbe wake mbele ya watu hao wasiojua Maandiko?

“Wanaume wa Athene, Ninaona” (Mdo. 17:22, 23)

9-11. (a) Paulo aliwekaje msingi mzuri wa mazungumzo? (b) Tunawezaje kufuata mfano wa Paulo katika huduma?

9 Kumbuka kwamba Paulo alikasirika kwa sababu ya ibada ya sanamu aliyojionea, ambayo ilienea sana. Badala ya kuanza kuishambulia ibada ya sanamu, alikuwa mtulivu. Alitumia busara, na kujitahidi kuwavutia wasikilizaji wake kwa kuweka msingi mzuri wa mazungumzo. Alianza kwa kusema hivi: “Wanaume wa Athene, ninaona kwamba katika mambo yote mnaonekana kuwa mnaogopa sana miungu kuliko watu wengine.” (Mdo. 17:22) Ni kana kwamba Paulo alikuwa akisema ‘Naona mnapenda sana mambo ya dini.’ Paulo alitenda kwa hekima alipowapongeza kwa sababu walipendezwa na mambo ya dini. Alitambua kwamba baadhi ya watu waliopofushwa na imani za uwongo wanaweza kusikiliza. Isitoshe, alijua kwamba wakati fulani hata yeye mwenyewe ‘alitenda bila ujuzi na hakuwa na imani.’​—1 Tim. 1:13.

10 Baada ya kuweka msingi mzuri, Paulo alieleza kwamba ameona jambo linalothibitisha kuwa watu wa Athene wanapenda mambo ya dini. Aliona madhabahu iliyotengwa kwa ajili ya “Mungu Asiyejulikana.” Kulingana na kitabu kimoja, “Wagiriki walikuwa na mazoea ya kutenga madhabahu kwa ajili ya ‘miungu isiyojulikana,’ ili wasimsahau mungu fulani katika ibada yao, na hivyo kumkasirisha.” Kwa kutenga madhabahu hiyo, Waathene walikiri kwamba kuna Mungu ambaye hawamjui. Paulo alitumia madhabahu hiyo kuwa msingi wa kuwahubiria habari njema. Alieleza: “Kile mnachoabudu bila kujua, hicho ndicho ninachowatangazia.” (Mdo. 17:23) Paulo alitoa hoja zenye nguvu kwa busara. Hakuwa akiwahubiria mungu mpya au wa kigeni, kama watu fulani walivyodai. Alikuwa akiwaeleza kuhusu Mungu ambaye hawakumjua—Mungu wa kweli.

11 Tunawezaje kumwiga Paulo katika huduma yetu? Tukiwa wenye utambuzi, tunaweza kugundua ikiwa mtu anapendezwa na mambo ya dini, labda kwa kuona vitu fulani vya kidini ambavyo amevaa au vilivyo katika nyumba yake au kwenye uwanja wake. Tunaweza kusema: ‘Naona unapendezwa na mambo ya dini. Nilitaka kuzungumza na mtu kama wewe.’ Kwa kumpongeza, tunaweza kuweka msingi mzuri wa mazungumzo. Kumbuka kwamba lengo letu si kuwahukumu watu kwa sababu ya imani yao. Wakati fulani, baadhi ya waabudu wenzetu waliamini mafundisho ya uwongo kwa kutojua.

Jitahidi kuweka msingi mzuri wa mazungumzo

Mungu “Hayuko Mbali na Kila Mmoja Wetu” (Mdo. 17:24-28)

12. Paulo alibadili mazungumzo yake jinsi gani ili yawafae wasikilizaji wake?

12 Tayari Paulo aliweka msingi mzuri wa mazungumzo, lakini je, alijenga vizuri juu ya msingi huo? Akijua kwamba wasikilizaji wake wamefunzwa falsafa za Kigiriki na hawayajui Maandiko, alitumia mbinu mbalimbali. Kwanza alitaja mafundisho ya Biblia bila kunukuu Maandiko moja kwa moja. Pili, alijihusisha kwenye mazungumzo, nyakati nyingine alitumia maneno kama vile “sisi,” na “tuna-.” Tatu, alinukuu vitabu vya Kigiriki ili kuonyesha kwamba mambo fulani aliyokuwa akifundisha yalikuwa katika vitabu vyao wenyewe. Acheni sasa tuchanganue hotuba ya Paulo iliyokuwa na matokeo mazuri. Aliwajulisha Waathene kweli gani muhimu kuhusu Mungu ambaye hawakumjua?

13. Paulo alieleza nini kuhusu ulimwengu, na maneno yake yalikuwa na ujumbe gani?

13 Mungu aliumba ulimwengu. Paulo alisema hivi: “Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, akiwa, kama alivyo, Bwana wa mbingu na dunia, hakai katika mahekalu yaliyotengenezwa kwa mikono.” d (Mdo. 17:24) Ulimwengu haukujitokeza wenyewe. Mungu wa kweli ndiye Muumba wa vitu vyote. (Zab. 146:6) Tofauti na Athena au miungu mingine ambayo utukufu wao ulitegemea mahekalu na madhabahu, mahekalu yaliyojengwa na mikono ya wanadamu hayawezi kumtosha Bwana Mwenye Enzi Kuu wa mbingu na dunia. (1 Fal. 8:27) Ujumbe wa Paulo ulikuwa wazi: Mungu wa kweli ni mkuu kuliko sanamu yoyote iliyotengenezwa na mwanadamu iliyo katika mahekalu yaliyojengwa na wanadamu.​—Isa. 40:18-26.

14. Paulo alionyeshaje kwamba Mungu hawategemei wanadamu?

14 Mungu hawategemei wanadamu. Waabudu-sanamu walipamba sanamu zao kwa nguo maridadi, walizipatia zawadi za bei ghali, au kuzipelekea vyakula na vinywaji—kana kwamba sanamu zilihitaji vitu hivyo! Hata hivyo, huenda baadhi ya wanafalsafa Wagiriki waliomsikiliza Paulo hawakuamini kwamba mungu anahitaji chochote kutoka kwa wanadamu. Ikiwa ndivyo, basi walikubaliana na maneno ya Paulo kwamba Mungu “hatumikiwi kwa mikono ya binadamu kana kwamba anahitaji kitu chochote.” Hakuna kitu chochote cha kimwili ambacho wanadamu wanaweza kumpa Muumba! Badala yake, Mungu huwapa wanadamu wanachohitaji—“uhai na pumzi na vitu vyote,” kutia ndani jua, mvua, na udongo wenye rutuba. (Mdo. 17:25; Mwa. 2:7) Kwa hiyo, Mungu aliye Mpaji, hawezi kuwategemea wanadamu ambao ni wapokeaji.

15. Paulo alishughulikiaje maoni ya Waathene kwamba wao ni bora kuliko watu wasio Wagiriki, nasi tunajifunza nini kutokana na mfano wake?

15 Mungu alimuumba mwanadamu. Waathene waliamini kwamba wao ni bora kuliko watu wasio Wagiriki. Lakini ubaguzi haupatani na kweli ya Biblia. (Kum. 10:17) Paulo alizungumzia kwa busara na ustadi jambo hilo ambalo lingeweza kutokeza ubishi. Huenda waliomsikiliza walitulia na kufikiri aliposema, “[Mungu] alifanyiza kila taifa la watu kutoka kwa mtu mmoja.” (Mdo. 17:26) Alikuwa akirejelea masimulizi ya Mwanzo kuhusu Adamu, baba ya wanadamu wote. (Mwa. 1:26-28) Kwa kuwa wanadamu wote wana baba mmoja, hakuna jamii au taifa bora kuliko lingine. Wasikilizaji wa Paulo walielewa vizuri hoja yake. Mfano huu unatufundisha jambo muhimu. Ingawa tunapaswa kutumia busara na kuwa wenye usawaziko katika kazi yetu ya kuhubiri, hatupaswi kamwe kupunguza uzito wa kweli ya Biblia ili kufanya watu wakubali ujumbe wetu.

16. Muumba ana kusudi gani kwa wanadamu?

16 Mungu alikusudia wanadamu wawe na uhusiano wa karibu pamoja naye. Hata ikiwa wanafalsafa waliomsikiliza Paulo walikuwa wamejadiliana kwa muda mrefu kuhusu kusudi la uhai wa binadamu, hawangeweza kamwe kutoa jibu sahihi na linaloeleweka. Hata hivyo, Paulo alieleza waziwazi kusudi la Muumba kwa wanadamu, kwamba “wamtafute Mungu, ikiwa watapapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate, ingawa, kwa hakika, hayuko mbali na kila mmoja wetu.” (Mdo. 17:27) Mungu ambaye Waathene hawakumjua anaweza kujulikana. Hayuko mbali na wale ambao kwa kweli wanataka kumtafuta na kumjua. (Zab. 145:18) Ona kwamba Paulo anatumia maneno “kila mmoja wetu,” akijitia ndani kati ya wale wanaohitaji ‘kumtafuta’ na ‘kupapasa-papasa wakimtafuta’ Mungu.

17, 18. Kwa nini wanadamu wanapaswa kumkaribia Mungu, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Paulo alivyozungumza na wasikilizaji wake?

17 Wanadamu wanapaswa kumkaribia Mungu. Paulo alisema kwamba, kwa sababu ya Mungu “tuko hai, tunatembea, na tunaishi.” Wasomi fulani husema kwamba Paulo alikuwa akirejelea maneno ya Epimenide, mshairi Mgiriki wa karne ya sita K.W.K. “aliyeheshimiwa sana katika utamaduni wa dini ya Waathene.” Paulo alitaja sababu nyingine inayopaswa kuwafanya wanadamu wahisi wako karibu na Mungu, aliposema: “Baadhi ya washairi wenu wamesema, ‘Kwa maana sisi pia ni watoto wake.’” (Mdo. 17:28) Wanadamu wanapaswa kujiona kuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu, kwa kuwa Yeye ndiye Baba ya mwanadamu wa kwanza ambaye wanadamu wote walitoka kwake. Ili kuwavutia wasikilizaji wake, Paulo alitumia busara kwa kunukuu moja kwa moja vitabu vya Kigiriki ambavyo bila shaka watu waliomsikiliza waliviheshimu sana. e Kama Paulo, nyakati nyingine tunaweza kunukuu vitabu vya historia, ensaiklopedia, au vitabu vingine vya marejeo vinavyoheshimika. Kwa mfano, nukuu inayofaa kutoka katika chanzo kinachotegemeka, inaweza kumsaidia mtu ambaye si Shahidi kujua chanzo cha mazoea au maadhimisho fulani ya dini za uwongo.

18 Kufikia hapa, Paulo ameeleza kweli za msingi kumhusu Mungu, akitumia maneno yake kwa ustadi ili yawafae wasikilizaji wake. Mtume huyo alitaka Waathene hao watumie jinsi gani habari hizo muhimu? Bila kukawia, aliendelea kutoa hotuba yake na kuwaambia wanalopaswa kufanya.

“Wanadamu Wote Kila Mahali . . . Wanapaswa Kutubu” (Mdo. 17:29-31)

19, 20. (a) Paulo alitumia busara jinsi gani kuonyesha ubatili wa kuabudu sanamu zilizotengenezwa na wanadamu? (b) Waliomsikiliza Paulo walihitaji kuchukua hatua gani?

19 Paulo alikuwa tayari kuwahimiza wasikilizaji wake wachukue hatua. Akirejelea tena nukuu kutoka kwa waandishi Wagiriki, alisema: “Kwa hiyo, kwa kuwa sisi ni watoto wa Mungu, hatupaswi kufikiri kwamba Mungu ni kama dhahabu au fedha au jiwe, kama kitu kilichochongwa kwa ufundi na ubunifu wa wanadamu.” (Mdo. 17:29) Kwa kweli, ikiwa wanadamu wametoka kwa Mungu, inawezekanaje Mungu awe sanamu zinazotengenezwa na wanadamu? Njia ya Paulo ya kujadiliana nao ilionyesha ubatili wa kuabudu sanamu zilizotengenezwa na wanadamu. (Zab. 115:4-8; Isa. 44:9-20) Huenda Paulo alifanya iwe rahisi kwa wasikilizaji wake kukubali ushauri wake kwa kujihusisha katika mazungumzo na kusema, “hatupaswi.”

20 Paulo alionyesha wazi kabisa kwamba wanahitaji kuchukua hatua. Alisema: “Mungu ameachilia nyakati hizo za kutojua [za kufikiri kwamba Mungu angependezwa na watu wanaoabudu sanamu]; lakini sasa anawatangazia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu.” (Mdo. 17:30) Huenda baadhi wa wasikilizaji wa Paulo walishangaa kusikia kwamba wanapaswa kutubu. Hata hivyo, hotuba yake yenye nguvu ilionyesha wazi kwamba Mungu ndiye chanzo cha uhai wao na kwa sababu hiyo wanawajibika mbele Zake. Wanahitaji kumtafuta Mungu, kujifunza ukweli kumhusu, na kupatanisha maisha yao na ukweli huo. Kwa Waathene, hilo lilimaanisha kutambua na kuacha kabisa dhambi ya kuabudu sanamu.

21, 22. Paulo alimaliza hotuba yake kwa maneno gani yenye kuchochea, nayo yanatuhusu jinsi gani?

21 Paulo alimaliza hotuba yake kwa maneno yenye kuchochea sana: “[Mungu] ameweka siku ambayo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.” (Mdo. 17:31) Siku ya Hukumu inayokuja—hiyo ni sababu nzuri ya kumtafuta na kumpata Mungu wa kweli! Paulo hakutaja jina la Hakimu huyo aliyewekwa rasmi. Badala yake, alisema jambo la kustaajabisha kumhusu Hakimu huyo: Aliishi akiwa mwanadamu, akafa, na kufufuliwa na Mungu!

22 Umalizio huo wenye kuchochea una umuhimu mkubwa kwetu. Tunajua kwamba Yesu Kristo aliyefufuliwa ndiye Hakimu aliyewekwa rasmi na Mungu. (Yoh. 5:22) Pia tunajua kwamba Siku ya Hukumu ina urefu wa miaka elfu moja, nayo inakaribia sana. (Ufu. 20:4, 6) Hatuogopi Siku ya Hukumu, kwa kuwa tunajua itawaletea baraka nyingi wale watakaohukumiwa kuwa waaminifu. Kufufuliwa kwa Yesu Kristo kunatuhakikishia kwamba tumaini letu la kuwa na maisha bora ya wakati ujao litatimia hakika!

“Wanaume . . . [Wakawa] Waamini” (Mdo. 17:32-34)

23. Watu waliitikia hotuba ya Paulo katika njia gani mbalimbali?

23 Watu waliitikia hotuba ya Paulo kwa njia mbalimbali. Waliposikia kuhusu ufufuo, “baadhi yao wakaanza kumdhihaki.” Wengine walikuwa watulivu lakini hawakutaka kuchukua hatua yoyote, nao wakamwambia: “Tutakusikiliza kuhusu jambo hili wakati mwingine.” (Mdo. 17:32) Hata hivyo, wachache kati yao waliitikia vizuri: “Wanaume fulani wakajiunga naye na kuwa waamini. Miongoni mwao kulikuwa na Dionisio, aliyekuwa mwamuzi wa mahakama ya Areopago, na mwanamke aliyeitwa Damari, na wengineo.” (Mdo. 17:34) Ndivyo inavyokuwa pia katika huduma yetu. Huenda watu fulani wakatudhihaki, na wengine ingawa wanatuheshimu, lakini hawataki kuchukua hatua yoyote. Hata hivyo, sisi hufurahi sana baadhi yao wanapokubali ujumbe wa Ufalme na kuwa waamini.

24. Tunaweza kujifunza nini kutokana na hotuba aliyotoa Paulo alipokuwa amesimama Areopago?

24 Tunapochanganua hotuba ya Paulo, tunaweza kujifunza mengi kuhusu mpangilio mzuri wa habari, hoja zenye kusadikisha, na jinsi ya kubadilika kulingana na hali za wasikilizaji wetu. Pia, tunaweza kujifunza faida ya kuwa na subira na busara tunapozungumza na watu ambao wamepofushwa na imani za uwongo za kidini. Pia, tunaweza kujifunza somo hili muhimu: Hatupaswi kamwe kupunguza uzito wa kweli za Biblia ili tu kuwafurahisha wasikilizaji wetu. Hata hivyo, tukifuata mfano wa Paulo, tunaweza kuwa walimu wenye matokeo mazuri katika utumishi wa shambani. Isitoshe, waangalizi wanaweza kuwa walimu stadi kutanikoni. Hivyo, tutakuwa tayari kuwasaidia wengine “wamtafute Mungu . . . na kwa kweli wampate.”​—Mdo. 17:27.

b Ona sanduku lenye kichwa “ Waepikurea na Wastoa.”

c Kilima cha Areopago kilikuwa upande wa kaskazini-magharibi mwa Ngome ya Athene, mahali ambapo baraza kuu la Athene lilikutana. Huenda jina “Areopago” lilirejelea baraza hilo au kilima chenyewe. Hivyo, wasomi hawajui kihususa ikiwa Paulo alipelekwa kwenye kilima hicho au karibu na eneo, au mahali pengine ambapo baraza hilo lilikutana, labda sokoni.

d Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ulimwengu” ni koʹsmos. Ijapokuwa Wagiriki walilitumia neno hilo kurejelea ulimwengu halisi, neno koʹsmos kwa kawaida hutumika katika Biblia kurejelea watu. Inawezekana kwamba Paulo, aliyekuwa akijaribu kuweka msingi mzuri wa mazungumzo kati yake na Wagiriki waliomsikiliza, alitumia neno hilo katika maana hiyo.

e Paulo alinukuu shairi linaloitwa Phaenomena, la Arato, mshairi Mstoa. Maneno kama hayo yanapatikana katika vitabu vingine vya Kigiriki kutia ndani wimbo unaoitwa Hymn to Zeus, uliotungwa na Kleanthe, mwandikaji Mstoa.