Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 4

“Watu Wasio na Elimu na wa Kawaida Tu”

“Watu Wasio na Elimu na wa Kawaida Tu”

Mitume watenda kwa ujasiri, Yehova awabariki

Matendo 3:1–5:11

1, 2. Petro na Yohana walifanya muujiza gani karibu na lango la hekalu?

 JUA la alasiri laangaza huku umati ukisongamana. Wayahudi wenye kumwogopa Mungu na wanafunzi wa Yesu wanamiminika kuingia katika ua wa hekalu. “Saa ya sala” inakaribia. a (Mdo. 2:46; 3:1) Wakiwa kati ya umati huo, Petro na Yohana wanaingia kuelekea lango la hekalu lililoitwa Lango Zuri. Katikati ya kelele za umati huo na vishindo vya miguu, mwombaji mwenye umri wa zaidi ya miaka 40, aliyezaliwa akiwa kilema, anaomba zawadi za rehema.​—Mdo. 3:2; 4:22.

2 Petro na Yohana wanapokaribia, mwombaji huyo anawaomba pesa kama ilivyo kawaida yake. Mitume hao wanasimama, jambo linalompa mtu huyo matumaini. “Sina fedha wala dhahabu,” Petro akamwambia, “lakini kile nilicho nacho ndicho ninachokupa. Katika jina la Yesu Kristo Mnazareti, tembea!” Hebu wazia jinsi umati ulivyoshangaa ulipomwona Petro akimshika mkono, na kwa mara ya kwanza maishani mwake, anasimama wima! (Mdo. 3:6, 7) Wazia mtu huyo akitazama miguu yake iliyoponywa na kupiga hatua za kwanza maishani! Ndiyo sababu anaanza kurukaruka na kumsifu Mungu kwa sauti kubwa!

3. Ni zawadi gani ambayo mtu aliyeponywa na umati ungepata?

3 Umati huo wenye msisimko unawakimbilia Petro na Yohana walio kwenye safu ya nguzo za Sulemani. Wakiwa hapo, mahali ambapo wakati mmoja Yesu alisimama na kufundisha, Petro anawaambia maana ya mambo ambayo wamejionea. (Yoh. 10:23) Anasema kwamba umati huo, kutia ndani mtu aliyeponywa, wanaweza kupata zawadi yenye thamani zaidi kuliko fedha na dhahabu. Zawadi hiyo inatia ndani mengi zaidi kuliko afya nzuri. Anawapa nafasi ya kutubu ili dhambi zao zifutiliwe mbali, kisha wawe wafuasi wa Yesu Kristo, “Wakili Mkuu wa uzima,” aliyewekwa rasmi na Yehova.​—Mdo. 3:15.

4. (a) Muujiza wa uponyaji ulitokeza mzozo gani? (b) Ni maswali gani mawili yatakayojibiwa?

4 Ni siku ya furaha sana! Mtu mmoja ameponywa kimwili na sasa anaweza kutembea. Maelfu ya watu wamepewa nafasi ya kuponywa kiroho, ili waweze kutembea kwa kumstahili Mungu. (Kol. 1:9, 10) Isitoshe, mambo yaliyotokea siku hiyo yalitokeza mzozo kati ya wafuasi waaminifu wa Kristo na watu wenye mamlaka waliokuwa wakijaribu kuwazuia wasitimize amri ya Yesu ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme. (Mdo. 1:8) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mtazamo na mbinu ambazo Petro na Yohana—“watu wasio na elimu na wa kawaida tu”​—walitumia walipouhubiria umati uliokuwa umekusanyika? b (Mdo. 4:13) Na tunapokabili upinzani, tunawezaje kuwaiga wanafunzi?

Si “kwa Nguvu Zetu” (Mdo. 3:11-26)

5. Petro aliuhubiria umati jinsi gani, nasi tunaweza kujifunza nini?

5 Petro na Yohana walisimama mbele ya umati. Walijua kwamba huenda baadhi ya watu katika umati huo, ndio waliokuwa wakipiga kelele wakitaka Yesu atundikwe siku chache tu zilizopita. (Marko 15:8-15; Mdo. 3:13-15) Wazia ujasiri wa Petro alipotangaza kwamba mtu huyo aliyekuwa kilema ameponywa katika jina la Yesu. Petro hakujaribu kuficha ukweli. Maneno yake yalionyesha waziwazi kwamba umati huo ulikuwa na hatia ya kumuua Kristo. Hata hivyo, Petro hakuwa na kinyongo chochote kuelekea watu hao, kwa kuwa ‘walitenda kwa kutojua.’ (Mdo. 3:17) Aliwasihi kama ndugu zake na kukazia fikira mambo yenye kupendeza ya ujumbe wa Ufalme. Ikiwa wangetubu na kumwamini Kristo, wangepata “majira yenye kuburudisha” kutoka kwa Yehova. (Mdo. 3:19) Sisi pia tunapaswa kuwa na ujasiri, na kusema mambo waziwazi tunapotangaza hukumu ya Mungu inayokaribia. Hata hivyo, hatupaswi kuwa wakali, wasiojali hisia za watu, au kuwahukumu. Badala yake, tunawaona watu hao kuwa ndugu zetu wa wakati ujao. Na kama alivyofanya Petro, tunakazia hasa mambo yenye kupendeza ya ujumbe wa Ufalme.

6. Petro na Yohana walionyesha unyenyekevu jinsi gani?

6 Mitume hao walikuwa na sifa ya kiasi. Hawakudai kwamba walifanya muujiza huo kwa uwezo wao. Petro aliuliza umati huo: “Kwa nini mnatutazama kana kwamba tumemfanya atembee kwa nguvu zetu au kwa sababu ya ujitoaji-kimungu?” (Mdo. 3:12) Petro na wale mitume wengine walijua kwamba huduma yao ilikuwa na matokeo mazuri, si kwa sababu ya nguvu zao wenyewe, bali kwa sababu ya nguvu za Mungu. Walionyesha unyenyekevu kwa kumpa sifa Yehova na Yesu kwa sababu ya mafanikio waliyopata.

7, 8. (a) Ni zawadi gani tunayoweza kuwapa watu? (b) Ahadi ya “kurudishwa kwa mambo yote” inatimizwa jinsi gani leo?

7 Sisi pia tunapaswa kuonyesha unyenyekevu tunapotangaza Ufalme. Ni kweli kwamba leo roho ya Mungu haiwapi Wakristo nguvu za kuwaponya watu kimuujiza. Hata hivyo, tunaweza kuwasaidia watu kumwamini Mungu na Kristo na kupokea zawadi ileile ambayo Petro aliahidi—wasamehewe dhambi na kuburudishwa na Yehova. Kila mwaka, mamia ya maelfu hupokea zawadi hiyo, na kuwa wanafunzi waliobatizwa wa Kristo.

8 Kwa kweli tunaishi nyakati ambazo Petro aliziita nyakati za “kurudishwa kwa mambo yote.” Mambo ambayo “Mungu alisema kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu walioishi zamani” yalitimia Ufalme ulipoanza kutawala mbinguni mwaka wa 1914. (Mdo. 3:21; Zab. 110:1-3; Dan. 4:16, 17) Muda mfupi baadaye, kazi ya kurudisha au kuwaponya watu kiroho ilianza hapa duniani, Kristo akiwa msimamizi. Mamilioni ya watu wameingizwa katika paradiso ya kiroho, na hivyo kuwa raia wa Ufalme wa Mungu. Wamevua utu wa zamani uliopotoka na “kuvaa utu mpya ulioumbwa kupatana na mapenzi ya Mungu.” (Efe. 4:22-24) Kama yule kilema aliyeponywa, kazi hiyo imetimizwa kwa nguvu za roho ya Mungu, bali si kwa nguvu za wanadamu. Kama alivyofanya Petro, lazima tulitumie Neno la Mungu kwa ujasiri na kwa njia inayofaa tunapowafundisha wengine. Mafanikio yoyote tunayopata tunapowasaidia watu wawe wanafunzi wa Kristo yanatokana na nguvu za Mungu, bali si zetu wenyewe.

“Hatuwezi Kuacha Kusema” (Mdo. 4:1-22)

9-11. (a) Viongozi wa Wayahudi walifanyaje walipousikia ujumbe wa Petro na Yohana? (b) Mitume waliazimia kufanya nini?

9 Hotuba ya Petro, zile kelele na kurukaruka kwa yule mtu aliyekuwa kilema, kulileta vurugu. Basi, kapteni wa hekalu—aliyekuwa na wajibu wa kuhakikisha usalama hekaluni—pamoja na wakuu wa makuhani, wakaja haraka kuona kilichokuwa kikiendelea. Inawezekana kwamba walikuwa Masadukayo, kikundi cha matajiri chenye uwezo kisiasa kilichojitahidi kudumisha uhusiano mzuri na Waroma, ambacho kilikataa sheria ya mdomo iliyopendwa sana na Mafarisayo, na kilichodhihaki imani ya ufufuo. c Walikasirika sana walipowakuta Petro na Yohana hekaluni wakifundisha bila woga kwamba Yesu amefufuliwa!

10 Wapinzani hao wenye hasira waliwaweka Petro na Yohana kizuizini, kisha siku iliyofuata wakawaburuta hadi mahakama kuu ya Wayahudi. Machoni pa watawala hao wenye cheo, Petro na Yohana walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu” ambao hawakuwa na haki ya kufundisha hekaluni. Hawakusomea katika shule zozote za kidini zilizokuwa maarufu. Hata hivyo, mahakama hiyo ilishangazwa na maneno yao yaliyo wazi na yenye usadikisho. Ni nini kilichowasaidia Petro na Yohana? Sababu moja ni kwamba “walikuwa pamoja na Yesu.” (Mdo. 4:13) Bwana wao alikuwa mwalimu stadi, tofauti kabisa na waandishi.​—Mt. 7:28, 29.

11 Mahakama hiyo iliwaagiza mitume hao waache kuhubiri. Siku hizo, amri za mahakama zilichukuliwa kwa uzito. Majuma machache yaliyotangulia, Yesu alipopelekwa kwenye mahakama hiyo, washiriki wa mahakama hiyo walisema: “Anastahili kufa.” (Mt. 26:59-66) Licha ya mambo hayo yote, Petro na Yohana hawaogopi. Wakiwa wamesimama mbele za wanaume hao matajiri, wenye elimu, na uvutano mkubwa, Petro na Yohana wanajibu kwa heshima lakini bila woga wowote: “Kama ni sawa machoni pa Mungu kuwasikiliza ninyi badala ya Mungu, hukumuni ninyi wenyewe. Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.”​—Mdo. 4:19, 20.

12. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa na ujasiri na usadikisho?

12 Je, unaweza kuonyesha ujasiri kama huo? Inakuwaje unapopata nafasi ya kuwahubiria watu matajiri, wenye elimu ya juu, au watu mashuhuri? Namna gani wakati ambapo watu wa familia yako, wanafunzi, au wafanyakazi wenzako wanapokashifu imani yako? Unaogopa? Ikiwa wewe huogopa, jipe moyo. Alipokuwa duniani, Yesu aliwafundisha mitume wake jinsi ya kutetea imani yao kwa usadikisho na kwa heshima. (Mt. 10:11-18) Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwaahidi wanafunzi wake kwamba angeendelea kuwa pamoja nao “sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Chini ya mwelekezo wa Yesu, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anatufundisha jinsi ya kutetea imani yetu. (Mt. 24:45-47; 1 Pet. 3:15) Anafanya hivyo kupitia mikutano ya kutaniko kama vile Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo, na kupitia machapisho yanayotegemea Biblia, kama vile makala za “Majibu ya Maswali ya Biblia,” zinazopatikana kwenye tovuti ya jw.org. Je, unatumia vizuri maandalizi hayo? Ukifanya hivyo, utakuwa na ujasiri na usadikisho hata zaidi. Na kama walivyofanya mitume, hutakubali chochote kikuzuie kuzungumza kuhusu kweli za kiroho zenye thamani ambazo umeona na kusikia.

Usikubali chochote kikuzuie kusema kuhusu kweli za kiroho zenye thamani ambazo umejifunza

‘Wakasema kwa Sauti Kubwa kwa Mungu’ (Mdo. 4:23-31)

13, 14. Tukikabili upinzani, tunapaswa kufanya nini, na kwa nini?

13 Mara tu baada ya kuachiliwa, Petro na Yohana walijiunga na washiriki wengine wa kutaniko. Wote kwa pamoja, ‘wakasema kwa sauti kubwa kwa Mungu’ na kumwomba awape ujasiri wa kuendelea kuhubiri. (Mdo. 4:24) Petro alijua vizuri ubatili wa kujaribu kufanya mapenzi ya Mungu kwa kutegemea nguvu zake mwenyewe. Majuma kadhaa yaliyopita, alikuwa amemwambia Yesu kwa kimbelembele: “Hata wengine wote wakikwazika kuhusiana nawe, mimi sitakwazika kamwe!” Lakini kama Yesu alivyokuwa ametabiri, Petro aliwaogopa wanadamu na kumkana rafiki na mwalimu wake. Hata hivyo, Petro alijifunza kutokana na kosa lake.​—Mt. 26:33, 34, 69-75.

14 Huwezi kutimiza utume wako wa kuhubiri kuhusu Kristo kwa kuwa tu umeazimia kufanya hivyo. Wapinzani wanapojaribu kuvunja imani yako, au kukuzuia usihubiri, fuata mfano wa Petro na Yohana. Mwombe Yehova akupe nguvu. Tafuta msaada wa kutaniko. Waambie wazee na wengine wakomavu kutanikoni hali ngumu unazokabili. Sala za wengine zinaweza kukutia nguvu.​—Efe. 6:18; Yak. 5:16.

15. Kwa nini wale ambao wakati fulani waliacha kuhubiri kwa muda hawapaswi kuvunjika moyo?

15 Ikiwa wakati fulani uliacha kuhubiri kwa muda kwa sababu ya upinzani, jipe moyo. Kumbuka kwamba, Yesu alipokufa, mitume wote waliacha kuhubiri kwa muda, lakini upesi wakawa watendaji tena. (Mt. 26:56; 28:10, 16-20) Badala ya kuruhusu makosa ya wakati uliopita yakulemee, je, unaweza kujifunza kutokana na hali hiyo na kutumia mambo hayo kuwaimarisha wengine?

16, 17. Sala ambayo wafuasi wa Kristo walitoa huko Yerusalemu inatufundisha nini?

16 Tunapoonewa na wenye mamlaka, tunapaswa kusali kuhusu nini? Kumbuka kwamba wanafunzi hawakuomba waepushwe na majaribu. Walikumbuka vizuri maneno ya Yesu: “Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yoh. 15:20) Wanafunzi hao washikamanifu walimwomba Yehova ‘aangalie’ vitisho vya wapinzani. (Mdo. 4:29) Ni wazi kwamba wanafunzi hao walielewa mambo yote yaliyohusika, wakitambua kwamba unabii ulikuwa ukitimia. Walijua kwamba, kama vile Yesu alivyowafundisha kusali, mapenzi ya Mungu ‘yangetendeka duniani,’ hata watawala wa kibinadamu waseme nini.​—Mt. 6:9, 10.

17 Ili kufanya mapenzi ya Mungu, wanafunzi walisali kwa Yehova hivi: “Uwawezeshe watumwa wako waendelee kutangaza neno lako kwa ujasiri wote.” Yehova alijibuje sala yao? “Mahali walipokuwa wamekusanyika pakatikiswa, na kila mmoja wao akajazwa roho takatifu nao walikuwa wakitangaza neno la Mungu kwa ujasiri.” (Mdo. 4:29-31) Hakuna chochote kinachoweza kuzuia mapenzi ya Mungu yasitimizwe. (Isa. 55:11) Hata hali ziwe ngumu kadiri gani, au adui awe mwenye nguvu kadiri gani, tukimwinulia Mungu sauti zetu katika sala, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atatupatia nguvu za kuendelea kutangaza neno lake kwa ujasiri.

Hawakuwajibika Mbele za “Wanadamu, Bali Mungu” (Mdo. 4:32–5:11)

18. Washiriki wa kutaniko la Yerusalemu walisaidiana jinsi gani?

18 Washiriki wa kutaniko hilo dogo lililokuwa Yerusalemu waliongezeka na kuwa zaidi ya 5,000. d Ijapokuwa walikuwa watu wenye malezi mbalimbali, wanafunzi walikuwa na “moyo na nafsi moja.” Walikuwa wameunganishwa katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri. (Mdo. 4:32; 1 Kor. 1:10) Baada ya wanafunzi hao kumwomba Yehova abariki jitihada zao hawakuketi tu. Walitegemezana kiroho na, ilipohitajika, kimwili pia. (1 Yoh. 3:16-18) Kwa mfano, mwanafunzi Yosefu, ambaye mitume walikuwa wakimwita Barnaba, aliuza shamba lake, na pasipo ubinafsi, akachanga fedha zote ziwasaidie waliokuwa wametoka mbali wakae Yerusalemu kwa muda mrefu zaidi ili wajifunze mengi zaidi kuhusu imani yao mpya.

19. Kwa nini Yehova alimwangamiza Anania na Safira?

19 Anania na Safira pia waliuza mali yao na kutoa mchango. Walijifanya kwamba wametoa kiasi chote, lakini kumbe walikuwa ‘wamejiwekea kisiri kiasi fulani.’ (Mdo. 5:2) Yehova aliwaangamiza, si kwa sababu mchango wao haukutosha, bali nia yao ya kutoa ilikuwa mbaya na pia kwa sababu walisema uwongo. Walidanganya, “si wanadamu, bali Mungu.” (Mdo. 5:4) Anania na Safira walitaka sana kusifiwa na watu badala ya kupata kibali cha Mungu, kama walivyofanya wale wanafiki walioshutumiwa na Yesu.​—Mt. 6:1-3.

20. Tunajifunza nini kuhusu michango tunayotoa?

20 Leo, kama walivyofanya wanafunzi waaminifu wa karne ya kwanza huko Yerusalemu, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova huonyesha roho ya ukarimu kwa kutegemeza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote kwa michango yao ya hiari. Hakuna anayewalazimisha watumie wakati wao au pesa zao kutegemeza kazi ya Ufalme. Kwa kweli, Yehova hapendi tumtumikie kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa. (2 Kor. 9:7) Tunapotoa michango yetu, Yehova hapendezwi na kiasi tunachotoa, bali hupendezwa na nia yetu. (Marko 12:41-44) Hatungetaka kamwe kuwa kama Anania na Safira kwa kumtumikia Mungu kwa sababu za kibinafsi au kujitafutia sifa. Badala yake, kama Petro, Yohana, na Barnaba, upendo wa kweli kwa Mungu na wanadamu wenzetu na utuchochee kumtumikia Yehova.​—Mt. 22:37-40.

a Katika hekalu, sala zilikuwa zikitolewa wakati wa dhabihu za asubuhi na za jioni. Dhabihu ya jioni ilikuwa ikitolewa “saa tisa,” au karibu saa 9 alasiri.

c Ona sanduku lenye kichwa “ Kuhani Mkuu na Wakuu wa Makuhani,”.

d Mwaka wa 33 W.K., huenda kulikuwa na Mafarisayo 6,000 hivi na Masadukayo wachache katika jiji la Yerusalemu. Huenda ndiyo sababu vikundi hivyo viwili vilianza kuyaona mafundisho ya Yesu kuwa tishio.