Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 2

“Mtakuwa Mashahidi Wangu”

“Mtakuwa Mashahidi Wangu”

Yesu awatayarisha mitume wake kwa ajili ya kazi ya kuhubiri

Matendo 1:1-26

1-3. Yesu aliondoka duniani jinsi gani, na ni maswali gani yanayotokea?

 KWA majuma kadhaa sasa mitume wana shangwe sana! Majuma machache yaliyopita walikuwa na huzuni na majonzi, lakini kwa kuwa sasa Yesu amefufuka, wana furaha sana. Kwa siku 40 Yesu amewatokea wafuasi wake katika pindi mbalimbali, akawafundisha na kuwatia moyo. Hata hivyo, leo anawatokea kwa mara ya mwisho.

2 Wakiwa wamesimama pamoja naye katika Mlima wa Mizeituni, mitume wake wanasikiliza kwa makini sana kila neno analosema. Anapomaliza kuzungumza, wanaona kana kwamba wakati umepita haraka sana. Kisha, baada ya kuinua mikono yake na kuwabariki, Yesu anaanza kupaa kutoka duniani! Huku wafuasi wake wakiendelea kumtazama, anaingia mawinguni. Mwishowe, anafunikwa na wingu hivi kwamba hawawezi kumwona tena. Ingawa hawamwoni bado wanatazama mbinguni.​—Luka 24:50; Mdo. 1:9, 10.

3 Huo ni mwanzo wa badiliko kubwa maishani mwa mitume wa Yesu. Kwa kuwa sasa Bwana wao, Yesu Kristo, amerudi mbinguni, watafanya nini? Bwana wao amewatayarisha vizuri kwa ajili ya kazi aliyoanzisha. Yesu aliwapa maagizo gani? Je, waliyafuata? Wakristo leo wanawezaje kunufaika na habari hiyo? Majibu ya maswali hayo yanapatikana katika sura ya kwanza ya kitabu cha Matendo.

“Uthibitisho Mwingi Wenye Kusadikisha” (Mdo. 1:1-5)

4. Katika kitabu cha Matendo, Luka anaanza masimulizi yake jinsi gani?

4 Luka anaanza masimulizi yake kwa kuzungumza na Theofilo. a Kwa kuwa Theofilo ndiye aliyeandikiwa kitabu cha Luka, ni wazi kwamba masimulizi haya ni mwendelezo wa Injili hiyo. Katika kitabu cha Matendo, Luka anaanza kwa kutoa muhtasari wa mambo yanayotajwa mwishoni mwa Injili yake, akitumia maneno tofauti kidogo na kuongezea habari mpya.

5, 6. (a) Ni nini kilichoimarisha imani ya wafuasi wa Yesu? (b) Ni kwa njia gani imani ya Wakristo leo inategemea “uthibitisho mwingi wenye kusadikisha”?

5 Ni nini kilichoimarisha imani ya wafuasi wa Yesu? Andiko la Matendo 1:3 linasema hivi kumhusu Yesu: “Alijionyesha kwao akiwa hai kupitia uthibitisho mwingi wenye kusadikisha.” Katika Biblia, Luka peke yake, yule “daktari mpendwa,” ndiye anayetumia maneno ‘uthibitisho wenye kusadikisha.’ (Kol. 4:14) Maneno hayo yalitumiwa katika maandishi ya kitiba, na yanamaanisha uthibitisho unaoonekana wazi, uliohakikishwa, na wenye kutegemeka. Yesu alitoa uthibitisho wa aina hiyo. Aliwatokea wafuasi wake mara nyingi. Nyakati fulani alimtokea mmoja au wawili, nyakati nyingine akawatokea mitume wote, na pindi moja aliwatokea ndugu zaidi ya 500. (1 Kor. 15:3-6) Uthibitisho wenye kusadikisha kwelikweli!

6 Imani ya Wakristo wa kweli leo pia inategemea “uthibitisho mwingi wenye kusadikisha.” Je, kuna uthibitisho wowote kwamba Yesu aliishi duniani, akafa kwa ajili ya dhambi zetu, kisha akafufuliwa? Ndiyo! Masimulizi yenye kutegemeka ya watu waliojionea matukio hayo yaliyo katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho, yanatoa uthibitisho wa kutosha wenye kusadikisha. Kusoma masimulizi hayo na kumwomba Yehova atusaidie kutumia mambo tunayojifunza maishani kutaimarisha sana imani yetu. Imani ya kweli hutegemea uthibitisho ulio wazi nayo ni muhimu ili kupata uzima wa milele.​—Yoh. 3:16.

7. Yesu aliwawekea wafuasi wake mfano gani katika kazi ya kuhubiri na kufundisha?

7 Yesu alikuwa ‘akizungumza nao kuhusu Ufalme wa Mungu.’ Kwa mfano, alieleza unabii mbalimbali ulioonyesha kwamba Masihi angeteseka na kufa. (Luka 24:13-32, 46, 47) Akiwa Mfalme Aliyechaguliwa, Yesu aliwasaidia watu kuelewa jukumu lake akiwa Masihi, kwa kuukazia Ufalme wa Mungu. Sikuzote, kichwa kikuu cha mahubiri yake kilikuwa Ufalme. Leo pia wafuasi wake hukazia Ufalme huo wanapohubiri.​—Mt. 24:14; Luka 4:43.

“Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia” (Mdo. 1:6-12)

8, 9. (a) Ni mambo gani mawili ambayo mitume wa Yesu hawakuelewa vizuri? (b) Yesu aliwasaidia jinsi gani, na Wakristo leo wanaweza kujifunza nini?

8 Yesu alifanya mkutano wa mwisho na mitume wake katika Mlima wa Mizeituni. Wakiwa na hamu kubwa ya kujua walimuuliza: “Bwana, je, unaurudisha ufalme kwa Israeli wakati huu?” (Mdo. 1:6) Swali hilo lilifunua mambo mawili ambayo hawakuelewa vizuri. Kwanza, walifikiri kwamba Ufalme wa Mungu ungerudishwa kwa Waisraeli. Pili, walitarajia Ufalme ulioahidiwa uanze kutawala ‘wakati huo.’ Yesu aliwasaidiaje?

9 Kuhusu jambo la kwanza, yaelekea Yesu alijua wangelielewa vizuri baada ya siku chache. Kwa kweli, siku kumi tu baadaye, wafuasi wake wangejionea kuzaliwa kwa taifa jipya, Israeli la kiroho! Baada ya muda mfupi, Mungu angeacha kushughulika na taifa la Israeli. Kuhusu jambo la pili, Yesu aliwakumbusha hivi kwa fadhili: “Si juu yenu kujua nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.” (Mdo. 1:7) Yehova ndiye huamua nyakati na majira. Kabla ya kufa, Yesu mwenyewe alisema kwamba hata Mwana hakujua “siku hiyo na saa hiyo” ambayo mwisho ungekuja. Aliyejua ni “Baba tu.” (Mt. 24:36) Leo pia, Wakristo wakihangaikia kupita kiasi kuhusu wakati ambapo mwisho utakuja, watakuwa wanajihangaisha na jambo ambalo haliwahusu.

10. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani ulioonyeshwa na mitume, na kwa nini?

10 Hata hivyo, haimaanishi kwamba mitume wa Yesu hawakuwa na imani. Walionyesha unyenyekevu kwa kukubali kurekebishwa. Isitoshe, ijapokuwa waliuliza kwa kutojua, swali hilo lilifunua mtazamo mzuri waliokuwa nao. Yesu alikuwa amewahimiza wafuasi wake mara nyingi ‘waendelee kukesha.’ (Mt. 24:42; 25:13; 26:41) Hivyo, swali lao lilionyesha kwamba walikuwa macho kiroho, wakitafuta kwa hamu uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba Yehova yuko karibu kuchukua hatua. Tunapaswa kuwa na mtazamo kama huo leo, hasa kwa kuwa tunaishi mwishoni mwa “siku za mwisho.”​—2 Tim. 3:1-5.

11, 12. (a) Yesu aliwapa wafuasi wake kazi gani? (b) Kwa nini Yesu alitaja roho takatifu alipokuwa akiwapa wafuasi wake kazi ya kuhubiri?

11 Yesu aliwakumbusha mitume wake jambo kuu wanalopaswa kuhangaikia. Alisema: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Habari za kufufuliwa kwa Yesu zingetangazwa kwanza katika jiji la Yerusalemu, ambapo aliuawa. Kisha, ujumbe huo ungeenezwa sehemu zote za Yudea, Samaria, na maeneo ya mbali zaidi.

12 Yesu aliwapa kazi ya kuhubiri baada ya kuwakumbusha ahadi yake kwamba atatuma roho takatifu iwasaidie. Maneno “roho takatifu” yanatajwa katika kitabu cha Matendo zaidi ya mara 40. Kitabu hiki cha Biblia kinaonyesha wazi kwamba hatuwezi kutimiza mapenzi ya Yehova bila msaada wa roho takatifu. Hivyo, tunapaswa kusali kwa ukawaida ili tupate roho hiyo. (Luka 11:13) Leo, kuliko wakati mwingine wowote tunaihitaji sana roho hiyo.

13. Kazi ya kuhubiri ambayo watu wa Mungu wamepewa leo ni kubwa kadiri gani, na kwa nini tunapaswa kuikubali kwa moyo wote?

13 Katika siku zetu, “sehemu ya mbali zaidi ya dunia” inatia ndani maeneo mengi zaidi kuliko ilivyokuwa katika karne ya kwanza. Hata hivyo, kama tulivyoona katika sura ya kwanza, Mashahidi wa Yehova wamekubali mgawo huo kwa moyo wote, wakijua kwamba Mungu anataka watu wa namna zote wahubiriwe habari njema ya Ufalme wake. (1 Tim. 2:3, 4) Je, unafanya kazi hiyo ya kuokoa uhai kwa bidii? Hiyo ndiyo kazi yenye kuridhisha sana! Yehova atakupa nguvu unazohitaji kutimiza kazi hiyo. Kitabu cha Matendo kitakueleza mbinu zinazofaa na mtazamo unaopaswa kuwa nao ili ufanikiwe.

14, 15. (a) Malaika walisema Kristo atarudi jinsi gani, nao walimaanisha nini? (Ona pia maelezo ya chini.) (b) Ni katika maana gani Kristo alirudi “vivyo hivyo” alivyoondoka?

14 Kama ilivyotajwa mwanzoni mwa sura hii, Yesu alipokuwa akipaa kuelekea mbinguni, mitume wake 11 walibaki wakiwa wamesimama huku wakikaza macho yao kuelekea mbinguni. Mwishowe, malaika wawili wakatokea na kuwashauri hivi kwa fadhili: “Wanaume wa Galilaya, kwa nini mnasimama mkitazama angani? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda angani atakuja vivyo hivyo kama vile ambavyo mmemwona akienda angani.” (Mdo. 1:11) Je, walimaanisha kwamba Yesu angerudi katika mwili uleule kama vile viongozi fulani wa dini wanavyofundisha? Hapana. Tunajuaje?

15 Malaika hao hawakusema kwamba Yesu angerudi katika umbo au mwili uleule, bali kwamba angerudi “vivyo hivyo,” au kwa njia hiyohiyo. b Aliondoka jinsi gani? Tayari alikuwa amefunikwa na mawingu malaika hao walipokuwa wakizungumza. Ni watu wachache tu, yaani mitume, ndio waliojua kwamba Yesu ameondoka duniani na kurudi mbinguni kwa Baba yake. Kristo angerudi vivyo hivyo. Na ndivyo alivyorudi. Leo, ni wale tu walio na utambuzi wa kiroho ndio wanaotambua kwamba Yesu amerudi katika maana ya kwamba sasa anatawala. (Luka 17:20) Tunahitaji kuwa macho ili kuona mambo mbalimbali yanayothibitisha kuwapo kwake na kuwaeleza wengine ili wao pia watambue kwamba mwisho unakaribia sana.

“Onyesha Ni Nani . . . Ambaye Umemchagua” (Mdo. 1:13-26)

16-18. (a) Tunajifunza nini katika Matendo 1:13, 14, kuhusu mikutano ya Kikristo? (b) Ni kwa njia gani Maria mama ya Yesu ni mfano mzuri kwetu leo? (c) Kwa nini mikutano ya Kikristo ni muhimu leo?

16 Ni wazi kwamba mitume ‘walirudi Yerusalemu wakiwa na shangwe kubwa.’ (Luka 24:52) Hata hivyo, walitumia jinsi gani mwongozo na maagizo ya Kristo? Matendo 1:13, 14, inasema kwamba walikuwa wamekusanyika katika “chumba cha juu.” Tunaweza kujifunza mengi kutokana na mistari hiyo kuhusu mikutano. Nyumba za Palestina zilikuwa na vyumba vya juu. Mtu angeweza kuingia katika chumba cha juu kwa kutumia ngazi iliyojengwa nje ya nyumba. Je, inawezekana kwamba “chumba cha juu” kinachotajwa katika mistari hiyo kilikuwa juu ya nyumba ya mama ya Marko ambayo inatajwa katika Matendo 12:12? Vyovyote vile, palikuwa mahali panapofaa kwa ajili ya mikutano ya wafuasi wa Kristo. Ni nani waliokutanika hapo, nao walifanya nini?

17 Mkutano huo haukuhudhuriwa na mitume, au wanaume tu. Ulihudhuriwa pia na “wanawake fulani” kutia ndani Maria mama ya Yesu. Hii ndiyo mara ya mwisho Maria huyo anatajwa moja kwa moja katika Biblia. Inapendeza kuona Maria hatafuti umashuhuri, bali ni mnyenyekevu na amekusanyika ili kuabudu pamoja na ndugu na dada zake wa kiroho. Lazima alifurahi sana kuona watoto wake wanne ambao hawakumwamini Yesu alipokuwa duniani, wakiwa pamoja naye. (Mt. 13:55; Yoh. 7:5) Walibadili mtazamo wao baada ya Yesu kufa na kufufuliwa.​—1 Kor. 15:7.

18 Pia, usisahau kusudi la mkutano huo: “Wote hawa walidumu katika sala kwa kusudi moja.” (Mdo. 1:14) Wakristo huiona mikutano kuwa sehemu muhimu ya ibada yao. Sisi hukutana ili kutiana moyo, kufundishwa na kupata mashauri, na zaidi ya yote, kumwabudu pamoja Baba yetu wa mbinguni, Yehova. Sala na nyimbo zetu humpendeza sana, na ni muhimu. Tusikose kamwe kuhudhuria pindi hizo takatifu na zenye kujenga!—Ebr. 10:24, 25.

19-21. (a) Tunajuaje kwamba Petro alifanya maendeleo ya kiroho, na hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova? (b) Kwa nini nafasi ya Yuda ilihitaji kujazwa, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi jambo hilo lilivyoshughulikiwa?

19 Sasa, suala muhimu lilitokea katika kutaniko la Kikristo, naye mtume Petro akalishughulikia. (Mstari wa 15-26) Inatia moyo sana kuona kwamba Petro alikuwa amepiga hatua kubwa kiroho hasa tunapokumbuka kwamba majuma kadhaa yaliyotangulia alikuwa amemkana Bwana wake mara tatu! (Marko 14:72) Sote ni watenda dhambi, na mara kwa mara tunahitaji kukumbushwa kwamba Yehova ni mwema na yuko tayari kusamehe’ wale wanaotubu kutoka moyoni.​—Zab. 86:5.

20 Petro alitambua kwamba mtu mwingine anapaswa kuchukua mahali pa Yuda, mtume aliyemsaliti Yesu. Lakini ni nani angechukua mahali pake? Mtume atakayechaguliwa anapaswa kuwa mfuasi wa Yesu tangu mwanzo wa huduma yake na ambaye alishuhudia ufufuo wake. (Mdo. 1:21, 22) Hilo lapatana na ahadi hii ya Yesu: “Ninyi ambao mmenifuata mtaketi katika viti vya ufalme 12, mkiyahukumu makabila 12 ya Israeli.” (Mt. 19:28) Inaonekana Yehova alikusudia kwamba kati ya wafuasi wa Yesu, kuwe na mitume 12 ambao baadaye wangekuja kuwa “mawe ya msingi 12” ya Yerusalemu Jipya. (Ufu. 21:2, 14) Hivyo, Mungu alimwezesha Petro kutambua kwamba unabii unaosema “mtu mwingine na achukue cheo chake cha uangalizi,” unamhusu Yuda.​—Zab. 109:8.

21 Mtu huyo angechaguliwa jinsi gani? Kwa kupiga kura, kama ilivyokuwa kawaida katika nyakati za Biblia. (Met. 16:33) Hata hivyo, hii ndiyo mara ya mwisho katika Biblia ambapo kura ilitumiwa kwa njia hiyo. Inaonekana kwamba baadaye, roho takatifu ilipomiminwa, zoea hilo lilikoma. Hata hivyo, kwa nini kura zilitumiwa? Mitume walisali: “Wewe, Ee Yehova, unayejua mioyo ya wote, onyesha ni nani kati ya watu hawa wawili ambaye umemchagua.” (Mdo. 1:23, 24) Walitaka Yehova achague. Mathia, ambaye yaelekea alikuwa mmoja wa wale wanafunzi 70 ambao Yesu aliwatuma kuhubiri, alichaguliwa. Hivyo, Mathia akawa mmoja wa “wale 12.” cMdo. 6:2.

22, 23. Kwa nini tunapaswa kunyenyekea na kuwatii wale wanaoongoza katika kutaniko leo?

22 Kisa hicho kinatukumbusha kwamba watu wa Mungu wanapaswa kufanya mambo kitengenezo. Leo pia, wanaume wanaostahili huwekwa rasmi kutumikia wakiwa waangalizi katika makutaniko. Wazee huchunguza kwa makini sifa ambazo waangalizi hao wanapaswa kutimiza, nao huomba mwongozo wa roho takatifu. Hivyo, kutaniko huwaona wanaume hao kuwa wamewekwa rasmi na roho takatifu. Sisi hufuata mwongozo wao na kuchochea roho ya ushirikiano kutanikoni.​—Ebr. 13:17.

Sisi hunyenyekea na kuwatii waangalizi waliowekwa rasmi

23 Kwa kuwa sasa wanafunzi hao walikuwa wameimarishwa kwa kutokewa na Yesu baada ya ufufuo wake na kutiwa nguvu na mabadiliko ya kitengenezo, walikuwa tayari kabisa kwa ajili ya mambo ambayo yangetokea. Sura inayofuata itazungumzia tukio hilo la pekee.

a Watu fulani huamini kwamba Theofilo alikuwa mtu mashuhuri ambaye hakuwa mwamini wakati huo, kwa kuwa katika Injili yake, Luka anamwita “mheshimiwa Theofilo.” (Luka 1:3) Lakini kwa sababu katika kitabu cha Matendo, Luka anamwita, “Ewe Theofilo,” wasomi fulani wanasema kwamba Theofilo alikuja kuwa mwamini baada ya kusoma Injili ya Luka; na ndiyo sababu Luka anaacha kumwita “mheshimiwa” na kumwandikia kama ndugu Mkristo.

b Biblia inatumia neno la Kigiriki troʹpos, linalomaanisha “jinsi,” bali si neno mor·pheʹ, linalomaanisha “umbo.”

c Baadaye Paulo alichaguliwa kuwa “mtume kwa mataifa,” lakini hakuhesabiwa kamwe miongoni mwa wale Kumi na Wawili. (Rom. 11:13; 1 Kor. 15:4-8) Kwa kuwa hakuwa mfuasi wa Yesu wakati wa huduma yake hapa duniani, hakustahili pendeleo hilo la pekee.