Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 9

Furahia Maisha Yenye Kuridhisha Sasa na Milele!

Furahia Maisha Yenye Kuridhisha Sasa na Milele!

Unaweza kuishi maisha yenye kuridhisha ukisitawisha urafiki na Mungu

ABRAHAMU, mtu mashuhuri mwenye imani anayetajwa katika historia ya Biblia, aliacha maisha mazuri katika jiji tajiri la Uru. Baada ya kuishi Harani kwa muda fulani, aliishi maisha yaliyobaki katika mahema naye alihamahama bila kuwa na makao maalumu. (Mwanzo 12:1-3; Matendo 7:2-7; Waebrania 11:8-10) Lakini, imeandikwa hivi kumhusu: “Abrahamu akakata pumzi na kufa baada ya kuishi maisha marefu, akiwa amezeeka na kuridhika.” (Mwanzo 25:8) Kwa nini maisha yake yaliridhisha sana? Akikaribia kufa, hakuwa tu mzee aliyeridhika kwa sababu ya mambo aliyotimiza maishani. Baadaye Abrahamu aliitwa “rafiki ya Yehova” kwa sababu alimwamini Mungu sana. (Yakobo 2:23; Isaya 41:8) Uhusiano mzuri ambao Abrahamu alisitawisha pamoja na Muumba wake ndio uliofanya awe na maisha yenye kuridhisha.

Je, maisha yako yanaweza kuwa yenye kuridhisha kuliko ya Abrahamu?

2 Ukisitawisha urafiki na Mungu kama Abrahamu alivyofanya miaka 4,000 hivi iliyopita, wewe pia unaweza kuishi maisha yenye maana na yenye kuridhisha. Huenda ukashangazwa sana na wazo la kuwa rafiki ya Muumba wa ulimwengu mzima, lakini inawezekana. Jinsi gani? Unahitaji kumjua na kumpenda. (1 Wakorintho 8:3; Wagalatia 4:9) Uhusiano kama huo na Muumba wako unaweza kuboresha maisha yako na kufanya yawe yenye kuridhisha.

3 Yehova amewapa watu wanaokubali dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo mwongozo wa kuishi maisha yenye furaha. (Isaya 48:17) Kumbuka kwamba Adamu alimwasi Mungu kwa kujiamulia mema na mabaya. Ingawa Yehova aliwakomboa wanadamu kupitia dhabihu ya fidia ya Mwana wake, na kuwaweka huru kutoka kwa utumwa wa dhambi na kifo, ni lazima kila mtu akubali fidia hiyo na aache kujiamulia mwenyewe mema na mabaya. Ni lazima tutii sheria na kanuni ambazo Mungu anawapa wale wanaokubali dhabihu ya fidia ya Yesu.

“Nifundishe njia zako”

4 Unapoendelea kujifunza Biblia na kutumia kanuni zilizotajwa humo, bila shaka utaona umuhimu wa kufuata viwango vya Mungu kuhusu mema na mabaya. (Zaburi 19:7-9) Utachochewa kumwambia hivi Mungu, kama alivyofanya Musa, nabii wa Yehova: “Tafadhali, ikiwa nimepata kibali machoni pako, nifundishe njia zako ili nikujue.” (Kutoka 33:13; Zaburi 25:4) Biblia ina kanuni zinazoweza kukuongoza unapokabiliana na matatizo ya “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Utazipenda sana kanuni hizo, na kumfahamu Yehova zaidi na hivyo kuimarisha urafiki wako pamoja naye.

5 Abrahamu alikufa akiwa “amezeeka na kuridhika,” lakini kwa kuwa bado wanadamu wanakufa, maisha ni mafupi sana. Hata tukizeeka sana, sisi sote tunatamani kuendelea kuishi. Hii ni kwa sababu “[Mungu] ameweka umilele katika moyo [wa wanadamu]; lakini bado wanadamu hawatajua kamwe kazi ambayo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.” (Mhubiri 3:11) Hata tukiishi milele, hatutaweza kamwe kujua uumbaji wote wa Yehova. Mambo tunayoweza kuona, kujifunza, na kufurahia kuhusu kazi za ajabu za Yehova hayana mwisho!—Zaburi 19:1-4; 104:24; 139:14.

6 Labda hungependa kuishi milele katika dunia iliyojaa matatizo tunayoona leo. Lakini, hupaswi kuhangaishwa na jambo hilo. Biblia inaahidi hivi: “Tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Maneno “mbingu mpya” yanamaanisha serikali mpya ya mbinguni—Ufalme wa Mungu, ambao utatawala dunia nzima. “Dunia mpya” ni jamii mpya ya wanadamu ambao wanatii utawala wa Ufalme huo. Ili kutimiza jambo hilo, hivi karibuni Yehova atawachukulia hatua wale “wanaoiharibu dunia.”—Ufunuo 11:18; 2 Petro 3:10.

7 Atachukua hatua lini? Alipotaja kuhusu “ishara . . . ya umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu Kristo alitia ndani vita kati ya mataifa, “upungufu wa chakula na matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali,” “magonjwa,” na “kuongezeka kwa uasi sheria.” (Mathayo 24:3-13; Luka 21:10, 11; 2 Timotheo 3:1-5) Kisha akatabiri hivi: “Mtakapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba Ufalme wa Mungu umekaribia.” (Luka 21:31) Kwa kweli, wakati ambapo Yehova atawaangamiza waovu unakaribia sana. *

8 Baada ya “siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” Yehova atakapoondoa kabisa uovu duniani, dunia yetu itageuzwa kuwa paradiso. (Ufunuo 16:14, 16; Isaya 51:3) Kisha, “waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.” (Zaburi 37:29) Namna gani wale ambao wamekufa? Yesu alisema: “Msishangazwe na jambo hili, kwa maana saa inakuja ambayo wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka, wale waliotenda mema kwenye ufufuo wa uzima, na wale waliozoea kutenda maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:28, 29) Yehova, ambaye anapendezwa na kila mtu, anataka kuwafufua wale ambao wamelala katika kifo. Huenda wanasayansi wakajaribu kutokeza mwanadamu kupitia kurekebisha chembe za urithi, lakini Muumba hana haja ya kufanya hivyo. Anaweza kukumbuka kila jambo kuhusu kila mwanadamu anayeweza kukombolewa na kumfufua. Naam, una tumaini la kukutana na wapendwa wako waliokufa katika dunia paradiso!

9 Maisha yatakuwaje katika Paradiso? Dunia itajaa wanaume na wanawake wenye furaha wanaomsifu Muumba kwa umoja. “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24; 54:13) Hakuna mtu atakayepatwa na matatizo ya kiafya kwa sababu ya mkazo na magonjwa ya kihisia na kiakili. Watu wote watakuwa na chakula kingi na watafurahia kazi ya maana kulingana na kusudi la Mungu. (Zaburi 72:16; Isaya 65:23) Watakuwa na amani pamoja na wanyama, amani pamoja na wanadamu wenzao na, zaidi ya yote, “amani pamoja na Mungu.”—Waroma 5:1; Zaburi 37:11; 72:7; Isaya 11:6-9.

10 Unapaswa kufanya nini ili uishi katika Paradiso hiyo na kufurahia maisha yenye kuridhisha kabisa? Yesu Kristo alisema: “Uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Basi endelea  kupata ujuzi kumhusu Yehova na Yesu Kristo, na ujifunze mambo ambayo Mungu anataka ufanye. Kisha utampendeza Yehova Mungu, na hilo litafanya maisha yako yawe yenye kuridhisha sana.

^ fu. 7 Unaweza kujifunza mengi kuhusu unabii huo katika sura ya 9 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.