Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 3

Kitabu Chenye Mwongozo Unaotegemeka

Kitabu Chenye Mwongozo Unaotegemeka

“BIBLIA ni mkusanyo wa ustaarabu wa mwanadamu na mambo yaliyompata maishani, na ni kitabu cha pekee,” ndivyo linavyosema jarida moja lililochapishwa na Chuo Kikuu cha Chung Shang kule Guangzhou, China. Immanuel Kant, mwanafalsafa mashuhuri wa karne ya 18, alisema hivi: “Faida kubwa zaidi ambayo mwanadamu amewahi kupata ni Biblia, kitabu kwa ajili ya wanadamu. Jaribio lolote la kuipuuza . . . ni uhalifu dhidi ya binadamu.” Kitabu The Encyclopedia Americana kinasema: “Biblia haiwavutii Wayahudi na Wakristo tu. . . . Bali sasa [Biblia] inaonwa kuwa hazina ya mambo ya kiadili na ya kidini na mafundisho yake tele yanatarajiwa kuwa muhimu hata zaidi ulimwengu unapotazamiwa kufanya maendeleo makubwa zaidi.”

2 Hata uwe mfuasi wa dini gani, je, hungependa kujifunza kuhusu kitabu hicho? Kufikia mwisho wa karne ya 20, Biblia ilikuwa imetafsiriwa katika lugha zaidi ya 2,200, ikiwa nzima au kwa sehemu. Watu wengi wanaweza kupata Biblia katika lugha wanayoweza kusoma na kuelewa. Tangu mashine ya kupiga chapa ivumbuliwe, inakadiriwa kwamba Biblia bilioni nne zimeenezwa ulimwenguni kote.

3 Sasa, ikiwa una Biblia tafadhali fungua ukurasa wa yaliyomo. Utaona majina ya vitabu, Mwanzo hadi Ufunuo. Kwa kweli, Biblia ni maktaba yenye vitabu 66 vilivyoandikwa na watu wapatao 40. Sehemu ya kwanza, yenye vitabu 39 ambayo wengi wanaiita Agano la Kale, inaitwa kwa usahihi Maandiko ya Kiebrania kwa sababu iliandikwa hasa katika Kiebrania. Sehemu ya pili, yenye vitabu 27 ambayo wengi wanaiita Agano Jipya, inaitwa kwa usahihi Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kwa kuwa waandishi Wakristo waliiandika katika Kigiriki. Ilichukua zaidi ya miaka 1,600 kumaliza kuandika Biblia, kuanzia mwaka wa 1513 K.W.K. hadi 98 W.K. Waandishi hao hawakuketi ili washauriane, na vitabu vingine viliandikwa kwa wakati uleule katika maeneo tofauti yaliyotenganishwa na maelfu ya kilomita. Ingawa hivyo, Biblia ina kichwa kimoja kikuu nayo inapatana na haijipingi. Basi tunaweza kujiuliza, ‘Ingewezekanaje kwa zaidi ya wanaume 40 katika kipindi cha karne 16 kutokeza kitabu ambacho kinapatana hivyo?’

“[Mungu] hulitandaza anga la kaskazini mahali pasipo na kitu, na kuining’iniza dunia mahali pasipo na kitu.”

4 Ingawa kitabu cha mwisho cha Biblia kiliandikwa zaidi ya miaka 1,900 iliyopita, bado ujumbe wa Biblia unapendwa na wanaume na wanawake wa nyakati zetu. Kwa mfano, hebu fungua Biblia yako kwenye Ayubu 26:7. Kumbuka kwamba andiko hilo liliandikwa karne ya 15 K.W.K. Linasema: “[Mungu] hulitandaza anga la kaskazini mahali pasipo na kitu, na kuining’iniza dunia mahali pasipo na kitu.Kisha, fungua Isaya 40:22, na ukumbuke kwamba kitabu cha Isaya kiliandikwa karne ya nane K.W.K. Mstari huo unasema: “Kuna Yule anayekaa juu ya duara ya dunia, na wakaaji wake ni kama panzi. Anazitandaza mbingu kama wavu laini,naye huzitandaza kama hema la kuishi.” Unapata wazo gani unaposoma maandiko hayo mawili? Kitu chenye umbo la duara ‘kinachoning’inia’ angani. Huenda umeona picha kama hiyo iliyopigwa na vyombo vya kisasa vya angani. Labda unajiuliza, ‘Inawezekanaje kwa watu walioishi zamani sana hivyo kutoa taarifa sahihi za kisayansi?’

5 Hebu tufikirie swali lingine kuhusu Biblia. Je, Biblia ni sahihi kihistoria? Wengine wanafikiri kwamba Biblia ni mkusanyo tu wa hadithi zisizoweza kuthibitishwa kihistoria. Kwa mfano, mfikirie Daudi, mfalme Mwisraeli anayejulikana sana. Hadi hivi karibuni, Biblia peke yake ndiyo iliyotaja kwamba kulikuwa na mtu aliyeitwa Daudi. Ingawa wanahistoria mashuhuri wanakubali kwamba ni mtu halisi, watu wengine wanaotilia shaka wanasema kwamba ni mtu wa kuwaziwa tu aliyebuniwa na Wayahudi waliotaka kueneza mawazo yao. Lakini ukweli wa mambo ni nini?

Maandishi yanayotaja “Nyumba ya Daudi”

6 Mwaka wa 1993, maandishi yanayotaja “Nyumba ya Daudi” yalipatikana kwenye magofu ya jiji la kale la Dani, la Waisraeli. Maandishi hayo yalikuwa sehemu ya mnara wa ukumbusho ulioharibika wa karne ya tisa K.W.K. ulioonyesha jinsi maadui walivyowashinda Waisraeli. Ghafla maandishi mengine kando na Biblia yanayomtaja Daudi yakapatikana. Je, hilo lilikuwa jambo muhimu? Israel Finkelstein, wa Chuo Kikuu cha Tel Aviv, alisema hivi kuhusu ugunduzi huo: “Wazo la kwamba maandishi ya Biblia hayana msingi likakoma ghafla baada ya maandishi hayo yanayomtaja Daudi kupatikana.” Jambo la kupendeza ni kwamba Profesa William F. Albright, mtaalamu wa mambo ya kale aliyeishi miaka mingi Palestina akichimbua vitu vya kale, alisema hivi: “Ugunduzi mmoja baada ya mwingine umethibitisha usahihi wa mambo mengi sana madogo-madogo, na kufanya Biblia itambuliwe zaidi kuwa kitabu cha kihistoria.” Tena, tunaweza kujiuliza, ‘Tofauti na hadithi na hekaya, kwa nini kitabu hiki cha kale ni sahihi sana kihistoria?’ Lakini kuna mengi zaidi.

Sarafu inayoonyesha Aleksanda Mkuu

7 Biblia ni kitabu cha unabii pia. (2 Petro 1:20, 21) Neno “unabii” huenda likafanya ufikirie kuhusu unabii wa uwongo unaotolewa na wale wanaojiita manabii. Lakini usifikirie mawazo kama hayo, fungua Danieli sura ya 8 katika Biblia. Hapo Danieli anafafanua maono ya pambano kati ya kondoo dume mwenye pembe mbili na mbuzi dume mwenye manyoya mengi na “pembe iliyoonekana waziwazi.” Mbuzi dume anashinda, lakini pembe yake kuu inavunjika. Badala yake pembe nne zinatokea. Maono hayo yanamaanisha nini? Masimulizi ya Danieli yanaendelea kusema: “Yule kondoo dume mwenye pembe mbili uliyemwona anafananisha wafalme wa Umedi na Uajemi. Yule mbuzi dume mwenye manyoya anafananisha mfalme wa Ugiriki; na ile pembe kubwa iliyokuwa kati ya macho yake, inafananisha mfalme wa kwanza. Kuhusu ile pembe iliyovunjika, kisha pembe nne zikatokea badala yake, kuna falme nne kutoka katika taifa lake zitakazosimama, lakini hazitakuwa na nguvu kama zake.”—Danieli 8:3-22.

“Ugunduzi mmoja baada ya mwingine umethibitisha usahihi wa mambo mengi sana madogo-madogo, na kufanya Biblia itambuliwe zaidi kuwa kitabu cha kihistoria.”—Profesa William F. Albright

8 Je, unabii huu ulitimizwa? Kitabu cha Danieli kilikamilika kuandikwa mwaka wa 536 K.W.K. hivi. Mfalme wa Makedonia, Aleksanda Mkuu, aliyezaliwa miaka 180 baadaye, mnamo 356 K.W.K., alishinda Milki ya Uajemi. Yeye ndiye aliyekuwa ile “pembe kubwa” kati ya macho ya “mbuzi dume mwenye manyoya mengi.” Kulingana na Yosefo, mwanahistoria wa Kiyahudi, Aleksanda alionyeshwa kitabu cha Danieli alipoingia Yerusalemu kabla ya kuishinda Uajemi. Akafikia uamuzi kwamba unabii wa Danieli alioonyeshwa ulihusu vita yake dhidi ya Uajemi. Isitoshe, unaweza kusoma katika vitabu vya historia ya ulimwengu kilichoipata milki ya Aleksanda baada ya kifo chake mwaka wa 323 K.W.K. Hatimaye majenerali wanne wakatawala milki yake, na kufikia mwaka wa 301 K.W.K., zile “pembe nne” ambazo ziliinuka mahali pa “ile pembe kubwa” ziligawanya milki hiyo katika sehemu nne. Kwa mara nyingine tena, tuna sababu nzuri ya kujiuliza, ‘Kitabu kingewezaje kutabiri kwa njia sahihi na iliyo wazi mambo ambayo yangetokea miaka 200 baadaye?’

9 Biblia yenyewe inajibu maswali hayo: “Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.” (2 Timotheo 3:16) Neno la Kigiriki lililotafsiriwa ‘ongozwa na roho ya Mungu’ hasa linamaanisha “-enye pumzi ya Mungu.” Mungu ‘aliweka pumzi’ katika akili za waandishi wapatao 40 nao wakaandika habari tunazopata sasa katika vitabu vya Biblia. Mifano michache ambayo tumezungumzia—kuhusu sayansi, historia, na unabii—inathibitisha jambo moja. Kitabu hiki cha pekee, Biblia, hakitokani na hekima ya wanadamu bali kimetokana na Mungu. Hata hivyo, watu wengi leo wanatilia shaka kama kweli Mtungaji wake—Mungu—yuko. Wewe unaonaje?