Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 5

Kumjua Mungu

Kumjua Mungu

UNAPOTAFUTA ushauri, je, huendi kwa mtu anayeaminika? Ukipata ushauri kutoka kwa mtu unayemwamini inaelekea utaufuata iwe utafaidika papo hapo au la. Ili ufaidike na ushauri wenye hekima ulio katika Biblia ni lazima umfahamu Mtungaji wake. Hata unaweza kuwa “rafiki” yake!—Isaya 41:8.

Jina la Mungu linalopatikana katika maandishi ya Kiebrania ya kitabu cha Isaya

2 Ukitaka kuwa rafiki ya mtu, bila shaka utataka kujua jina lake. Je, Biblia inataja jina la Mungu? Yeye alitangaza hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ndilo jina langu; simpi yeyote utukufu wangu, wala kuzipa sanamu za kuchongwa sifa yangu.” (Isaya 42:8) Jina lake ni “Yehova,” ambalo linaandikwa יהוה (likisomwa kutoka kulia kwenda kushoto) katika Kiebrania. Jina hilo linapatikana mara 7,000 hivi katika Maandiko ya Kiebrania ya Biblia. Inaeleweka kwamba jina la Mungu linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa,” likidokeza kwamba Yehova anaweza kuwa chochote kile anachotaka ili atimize makusudi yake, au kuhusiana na uumbaji wake anaweza kusababisha chochote kinachohitajika ili kutimiza kusudi lake. Katika Kiebrania jina lake ni kitenzi kinachoonyesha kitendo kinachoendelea. Jambo hilo linaonyesha nini? Linatuambia kwamba Yehova amesababisha na bado anasababisha makusudi yake yatimizwe. Yeye ni Mungu aliye hai, si nguvu tu isiyo na utu!

3 Yehova akawa Muumba. (Mwanzo 1:1) Yeye ni “Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.” (Matendo 14:15) Yehova aliumba kila kitu, kutia ndani wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa. Kwa hiyo, Mungu ndiye “chanzo cha uhai.” (Zaburi 36:9) Akawa pia Mtegemezaji wa uhai. Kwa hiyo, “hakujiacha bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira ya mavuno, akiwashibisha kwa chakula na kuijaza mioyo yenu furaha.” (Matendo 14:17) Barani Afrika na Asia, wengi huabudu mababu zao kwa sababu uhai wao ulitokana nao. Je, hawapaswi kumwabudu Muumba na Mtegemezaji wa uhai, Yule aliyewaumba wanadamu wawili wa kwanza na kuwapa uwezo wa kuzaa? Ukitafakari jambo hilo, unaweza kusema hivi: “Unastahili, Ee Yehova Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilitokea navyo vikaumbwa.”—Ufunuo 4:11.

4 Kupitia Biblia, unaweza kumjua Muumba wako, Yehova, na kujifunza yeye ni Mungu wa aina gani. Biblia inafunua kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:16; Kutoka 34:6, 7) Unaposoma Biblia kuanzia Mwanzo hadi Ufunuo, utapata masimulizi mengi yanayoonyesha kwamba kwa kweli yeye ni Mungu mwenye upendo. Mbona usiwe na mazoea ya kusoma Neno la Mungu kila siku ili umjue Muumba wako? Jifunze Biblia kwa makini ukisaidiwa na wale wanaoifahamu. (Matendo 8:26-35) Ukifanya hivyo, utaona kwamba yeye ni Mungu wa haki, ambaye hataruhusu uovu uendelee milele. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Si rahisi kwa mwanadamu kuonyesha upendo na haki kwa usawaziko, lakini kwa kuwa Yehova ana hekima anasawazisha sifa hizo kikamili. (Waroma 11:33; 16:27) Kwa kuwa yeye ni Mungu Mweza Yote, ana uwezo wa kufanya chochote anachotaka ili atimize makusudi yake. (Mwanzo 17:1) Jitahidi kutumia ushauri wenye hekima ulio katika Biblia, nawe utamfahamu Muumba wako vizuri zaidi, na utatambua kwamba nyakati zote ushauri wake hutufaidi.

Mbona usisali kwa Yehova?

5 Bado kuna njia nyingine ya kuwasiliana na Mungu. Ni kupitia sala. Yehova ni “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Anaweza “kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri.” (Waefeso 3:20) Lakini, ungemwonaje “rafiki” anayekuja kwako wakati tu anapotaka umsaidie? Labda hungemwona kuwa rafiki wa kweli. Vivyo hivyo, bila shaka ungependa kutumia pendeleo la sala kumwomba Mungu mahitaji yako na vilevile kumshukuru na kumsifu.—Wafilipi 4:6, 7; 1 Wathesalonike 5:17, 18.