Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 6

Kwa Nini Yehova Alituumba?

Kwa Nini Yehova Alituumba?

Mfalme Sulemani alichunguza swali lililohusu kusudi la uhai

UTAFAIDIKAJE kwa kumjua Yehova? Miongoni mwa mambo mengine, utapata jibu la swali ambalo limewatatiza mabilioni ya watu: ‘Kwa nini niko hai?’ Huenda umewahi kujiuliza swali hilo. Mfalme mmoja mwenye hekima ambaye pia alikuwa tajiri “kuliko wafalme wengine wote duniani” katika siku zake, alichunguza swali hilo kuhusu kusudi la uhai. (2 Mambo ya Nyakati 9:22; Mhubiri 2:1-13) Mfalme huyo, Sulemani, alikuwa na mamlaka kubwa sana, mali nyingi sana, na hekima isiyo na kifani. Uchunguzi wake ulionyesha nini? “Huu ndio umalizio, baada ya mambo yote kusikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na ushike amri zake, kwa maana huu ndio wajibu wote wa mwanadamu.” (Mhubiri 12:13) Kwa kuwa Sulemani alikuwa na hekima kuliko watu wengi, tunapaswa kuchunguza uamuzi aliofikia.—Mhubiri 2:12.

2 Sulemani alipotaja kumwogopa Mungu hakumaanisha hofu isiyofaa ya kuogopa roho isiyojulikana. Badala yake, ni woga unaofaa wa kutomkasirisha mtu unayempenda sana. Ikiwa unampenda mtu sana, utajitahidi kumfurahisha nyakati zote na kuepuka kufanya jambo lolote linaloweza kumkasirisha. Unapozidi kumpenda Yehova, utahisi hivyo kumhusu.

3 Unaposoma Biblia, utajifunza mambo ambayo Muumba wetu anapenda na mambo ambayo hapendi, na pia kusudi lake la kuumba dunia. Biblia inasema Yehova ndiye “Yule aliyeiumba dunia, Yule aliyeitengeneza,” pia Biblia inamwita yule “[aliyeifanya] imara kabisa, ambaye hakuiumba tu bila sababu, lakini aliiumba ili ikaliwe.” (Isaya 45:18) Yehova alitayarisha dunia ili ikaliwe na wanadamu, ambao wangeitunza na kuwatunza viumbe wote ndani yake. (Mwanzo 1:28) Lakini, je, hilo ndilo kusudi pekee lililomfanya Yehova awaumbe wanadamu, yaani, kuwa watunzaji?

Adamu na Hawa walikuwa na uhusiano mzuri sana pamoja na Mungu

4 Hapana, kulikuwa na kusudi kubwa hata zaidi. Mwanadamu wa kwanza, Adamu, alikuwa na uhusiano mzuri sana pamoja na Yehova. Adamu angeweza kuwasiliana moja kwa moja na Muumba. Angeweza kumsikiliza Mungu na kumwambia Yehova maoni yake. (Mwanzo 1:28-30; 3:8-13, 16-19; Matendo 17:26-28) Basi, Adamu na mkewe, Hawa, walikuwa na fursa nzuri sana ya kumjua Yehova vizuri na kuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja naye. Kumjua Yehova na kumwiga kungefanya maisha yao yawe yenye kuridhisha, kwa kuwa yeye ni “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Akiwa Mungu “ambaye hutupatia kwa wingi vitu vyote tunavyofurahia,” Yehova alimweka mwanadamu wa kwanza katika paradiso iliyoitwa bustani ya Edeni, akiwa na tumaini la kuishi milele.—1 Timotheo 6:17; Mwanzo 2:8, 9, 16, 17.

Ugunduzi wa hivi karibuni kuhusu chembe za binadamu unaonyesha nini?

5 Milele? Huenda ukafikiri wazo la kuishi milele ni upuuzi mtupu, lakini je, ni upuuzi? Wanasayansi wanaamini kwamba sasa wanafahamu jambo linalosababisha chembe zizeeke. Visehemu vya chembe za urithi vinavyoitwa telomere, vinavyopatikana kwenye miisho ya kromosomu, huwa fupi kila mara chembe inapogawanyika. Baada ya chembe kugawanyika mara 50 hadi 100, telomere huchakaa, na chembe nyingi huacha kugawanyika. Lakini ugunduzi wa hivi karibuni wa kisayansi unadokeza kwamba kwa msaada wa kimeng’enya kinachoitwa telomerase, chembe za binadamu zinaweza kuendelea kugawanyika milele. Ingawa ugunduzi huo haumaanishi kwamba Yehova anaweza kufanya tuishi milele kupitia kimeng’enya hicho, unaonyesha jambo hili: Wazo la kuishi milele si upuuzi!

6 Ndiyo, simulizi la Biblia linaloonyesha kwamba wanadamu wawili wa kwanza waliumbwa waishi milele ni la kweli. Wanadamu walipaswa kusitawisha uhusiano pamoja na Yehova milele. Walipaswa kuwa na uhusiano wa karibu sana na Baba yao wa mbinguni, wakijua kabisa kusudi lake kwa wanadamu duniani na kulitimiza. Maisha yao hayakupaswa kuwa yenye kuchosha. Adamu na Hawa walikuwa na tumaini zuri sana la kuijaza dunia wazao wakamilifu wenye furaha. Wangekuwa na kazi yenye maana na yenye kuridhisha milele. Hayo yangekuwa maisha yenye kuridhisha sana!—Mwanzo 1:28.