Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 7

Kwa Nini Ni Vigumu Kuwa na Maisha Yenye Kuridhisha?

Kwa Nini Ni Vigumu Kuwa na Maisha Yenye Kuridhisha?

KWA NINI watu wengi hujitahidi sana leo lakini hawapati kusudi maishani? “Mwanadamu anayezaliwa na mwanamke, maisha yake ni mafupi na yamejaa taabu. Huchanua kama ua na kisha hunyauka; hukimbia kama kivuli na kutoweka.” (Ayubu 14:1, 2) Jambo fulani lililowapata Adamu na Hawa katika Paradiso, liliwasababishia wanadamu matatizo.

2 Ili wanadamu wawe na furaha ya kweli, ni lazima wawe na uhusiano mzuri pamoja na Mungu—uhusiano wa hiari bila kulazimishwa. (Kumbukumbu la Torati 30:15-20; Yoshua 24:15) Yehova anataka tumtii na kumwabudu kutoka moyoni, kwa sababu tunampenda. (Kumbukumbu la Torati 6:5) Basi katika bustani ya Edeni, Yehova alimpa Adamu maagizo ambayo yalimpa fursa ya kuthibitisha uaminifu wake wa moyoni. “Unaweza kula matunda ya kila mti,” Mungu akamwambia Adamu, “lakini kuhusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya, usile matunda yake, kwa maana siku utakapokula matunda yake hakika utakufa.” (Mwanzo 2:16, 17) Ulikuwa mtihani rahisi. Yehova alimkataza Adamu asile matunda ya mti mmoja tu kati ya miti yote iliyokuwa katika bustani. Mti huo uliwakilisha haki ya Muumba mwenye hekima yote ya kuamua mema na mabaya. Adamu akamwambia amri hiyo ya Mungu mke wake, ambaye Yehova alimpa awe “msaidizi” wake. (Mwanzo 2:18) Wote wawili waliridhika na mpango huo—kuishi chini ya utawala wa Mungu—wakifanya mapenzi yake kwa unyenyekevu na hivyo kuonyesha kwamba wanampenda Muumba wao na Mpaji Uhai.

3 Kisha siku moja nyoka akaongea na Hawa, akauliza: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Hawa akasema walikatazwa kula tunda la “mti ulio katikati ya bustani,” mti wa ujuzi wa mema na mabaya, ‘wasije wakafa.’—Mwanzo 3:1-3.

4 Huyo nyoka alikuwa nani? Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinamtambulisha “nyoka wa zamani” kuwa “Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Je, Mungu alimuumba Shetani Ibilisi? La, kazi za Yehova ni kamilifu na njema. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Kiumbe huyu wa roho aligeuka mwenyewe akawa Ibilisi, yaani “Mchongezi,” na Shetani, yaani “Mpinzani.” ‘Alivutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe,’ alitamani kuwa kama Mungu, akaanza kumwasi Muumba.—Yakobo 1:14.

5 Shetani Ibilisi akaendelea kumwambia Hawa: “Hakika hamtakufa. Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunguliwa nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:4, 5) Shetani alifanya wazo la kula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya livutie. Ni kana kwamba alisema: ‘Mungu anawanyima kitu kizuri. Onja tu matunda ya mti huu, nawe utakuwa kama Mungu na utaweza kujiamulia mema na mabaya.’ Leo Shetani bado anatumia njia hiyo ya kufikiri ili kuwazuia wengi wasimtumikie Mungu. ‘Fanya upendavyo,’ anasema. ‘Mpuuze Mungu aliyekupa uhai.’—Ufunuo 4:11.

6 Ghafla matunda ya mti huo yakavutia, yakatamanika sana! Hawa akachukua tunda, akala, baadaye akampa mume wake. Ingawa Adamu alijua vizuri kabisa matokeo, alimsikiliza mke wake naye akala. Matokeo yakawaje? Yehova alimhukumu hivi mwanamke: “Nitazidisha sana uchungu wa mimba yako; utazaa watoto kwa uchungu, nawe utamtamani sana mume wako, naye atakutawala.” Namna gani mwanamume? “Ardhi imelaaniwa kwa sababu yako. Kwa maumivu utakula mazao yake sikuzote za maisha yako. Itakuzalia miiba na michongoma, nawe utakula mimea ya shambani. Kwa jasho la uso wako utakula chakula mpaka utakaporudi ardhini, kwa kuwa ulitolewa humo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” Sasa Adamu na Hawa waliachwa wajitafutie wenyewe furaha na kuridhika. Je, jitihada za wanadamu za kuishi maisha yenye kuridhisha bila kusudi la Mungu zingefanikiwa? Badala ya kufanya kazi yenye kufurahisha ya kutunza Paradiso iliyo kama bustani na kuipanua hadi miisho ya dunia, sasa walifanya kazi ya kuchosha ili tu waendelee kuishi, bila kufanya chochote cha kumtukuza Muumba.—Mwanzo 3:6-19.

7 Siku waliyokula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya, machoni pa Mungu Adamu na Hawa walikufa wakaanza kudhoofika wakielekea kufa kihalisi. Walipatwa na nini walipokufa hatimaye? Biblia inatufahamisha hali ya wafu. “Walio hai wanajua kwamba watakufa, lakini waliokufa hawajui jambo lolote kamwe, wala hawana thawabu tena, kwa sababu kumbukumbu lote kuwahusu limesahauliwa.” (Mhubiri 9:5; Zaburi 146:4) “Nafsi” haiendelei kuishi mtu anapokufa. Adhabu ya dhambi ni kifo, wala si kuteswa katika moto wa milele. Isitoshe, mtu akifa haendi mbinguni kuishi raha mustarehe. *

8 Kama vile sufuria iliyobonyea inayotumiwa kuokea mikate inavyotokeza mikate iliyobonyea, ndivyo Adamu na Hawa wasio wakamilifu wangetokeza wazao wasio wakamilifu. Biblia inafafanua hali hiyo: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, basi kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Kwa hiyo, sisi sote huzaliwa tukiwa na dhambi katika hali ya kutokamilika. Maisha ya wazao wa Adamu yakawa magumu na yenye kuchosha. Lakini, je, kuna suluhisho?

^ fu. 7 Unaweza kupata habari zenye kupendeza kuhusu hali ya wafu katika broshua Ni Nini Hutupata Tunapokufa?, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.