Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 8

Maisha Yenye Kuridhisha Yarudishwa

Maisha Yenye Kuridhisha Yarudishwa

INGAWA mwanadamu alitumbukia katika maisha mabaya kwa sababu ya kuasi utawala wa Mungu, Mungu hakuwaacha wanadamu bila tumaini. Biblia inaeleza hivi: “Uumbaji ulitiishwa chini ya ubatili, si kwa mapenzi yake wenyewe bali kupitia yule aliyeutiisha, kwa msingi wa tumaini kwamba uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:20, 21) Naam, Mungu aliwapa tumaini wazao wa Adamu na Hawa. Lilikuwa tumaini hakika kwamba wanadamu wangewekwa huru kutokana na kifo na dhambi waliyorithi. Wangeweza kurudishwa kwenye uhusiano wa karibu na Yehova Mungu. Jinsi gani?

Mungu aliwapa wanadamu tumaini ili waweze kukombolewa kutokana na utumwa wa dhambi na kifo

2 Adamu na Hawa walipotenda dhambi, waliwanyima wazao wao fursa ya kuishi maisha yenye kuridhisha duniani milele. Kwa sababu ya kutaka haki ya kujiamulia mema na mabaya, waliiuza familia yao ya wakati ujao katika utumwa wa dhambi na kifo. Kwa kuwa walizaliwa katika familia hiyo, wazao wao wanaweza kufananishwa na watumwa waliofungiwa katika kisiwa cha mbali kinachotawaliwa na wafalme wakatili. Kwa kweli, kifo kimetawala kama mfalme juu ya wanadamu walio watumwa wa mfalme mwingine—dhambi. (Waroma 5:14, 21) Inaonekana hakuna mtu atakayewaokoa. Kwa sababu babu yao ndiye aliyewauza utumwani! Lakini mfadhili fulani anamtuma mwanawe, anayeleta malipo kamili yanayohitajika ili kuwakomboa wote ambao wamefungwa.—Zaburi 51:5; 146:4; Waroma 8:2.

3 Katika mfano huo, mtu aliyewaokoa watumwa hao anawakilisha Yehova Mungu. Mwana aliyetoa malipo ili wawe huru ni Yesu Kristo. Kabla ya kuwa mwanadamu aliishi mbinguni akiwa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. (Yohana 3:16) Yeye ndiye aliyeumbwa kwanza na Yehova, na viumbe wengine wote katika ulimwengu waliumbwa kupitia yeye. (Wakolosai 1:15, 16) Yehova alihamisha kimuujiza uhai wa Mwana huyo wa roho na kuuweka katika tumbo la uzazi la bikira fulani, na hivyo kufanya iwezekane mtoto huyo azaliwe akiwa mwanadamu mkamilifu, malipo yaliyohitajika ili kutimiza matakwa ya haki ya Mungu.—Luka 1:26-31, 34, 35.

4 Yesu alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi, alibatizwa kwenye Mto Yordani. Alipobatizwa, alitiwa mafuta kwa roho takatifu, au nguvu za utendaji za Mungu. Basi, akawa Kristo, yaani “Mtiwa Mafuta.” (Luka 3:21, 22) Huduma ya Yesu duniani ilichukua miaka mitatu na nusu. Katika kipindi hicho, aliwafundisha wafuasi wake kuhusu “ufalme wa Mungu,” serikali ya mbinguni ambayo itawarudishia wanadamu uhusiano wenye amani pamoja na Yehova Mungu. (Luka 4:43; Mathayo 4:17) Yesu alijua jinsi wanadamu wanavyoweza kuishi kwa furaha, na akawapa wafuasi wake maagizo hususa kuhusu furaha. Kwa nini usisome Mathayo sura ya 5 hadi ya 7 katika Biblia yako uone baadhi ya mafundisho yake katika Mahubiri ya Mlimani?

5 Tofauti na Adamu, Yesu alimtii Mungu kabisa. “Hakufanya dhambi.” (1 Petro 2:22; Waebrania 7:26) Hata alikuwa na haki ya kuishi milele duniani, lakini “alitoa uhai wake” ili amlipe Mungu kile ambacho Adamu alipoteza. Kwenye mti wa mateso, Yesu alitoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu. (Yohana 10:17; 19:17, 18, 28-30; Waroma 5:19, 21; Wafilipi 2:8) Kwa kufanya hivyo, Yesu aliandaa fidia, au malipo yanayohitajika ili kuwakomboa wanadamu kutoka kwenye utumwa wa dhambi na kifo. (Mathayo 20:28) Wazia kwamba unafanya kazi ngumu yenye mshahara mdogo katika kiwanda fulani, ukiishi kama mtumwa. Je, hungemshukuru sana mtu anayepanga kukukomboa kutoka kwenye kifungo hicho na yule anayejitolea kuutoa uhai wake kwa ajili ya uhai wako? Kupitia mpango wa fidia, ulipata nafasi ya kurudi kwenye familia ya Mungu ya ulimwenguni pote na kuishi maisha yanayoridhisha kwelikweli, ukiwa huru kutokana na utumwa wa dhambi na kifo.—2 Wakorintho 5:14, 15.

Je, hungemshukuru sana mtu aliyekukomboa kutoka kifungoni?

6 Kujua na kuthamini fadhili hizo zisizostahiliwa za Yehova kunakupa sababu kubwa zaidi ya kutumia maishani mwako maneno ya hekima yaliyo katika Biblia. Kwa mfano, fikiria mojawapo ya kanuni zilizo ngumu zaidi kufuata—kuwasamehe wengine wanapokuudhi. Je, unakumbuka maneno ya Wakolosai sura ya 3, mstari wa 12 hadi wa 14, ambayo tulizungumzia katika Somo la 2? Mistari hiyo ilikutia moyo uwasamehe wengine hata kama una sababu nzuri ya kulalamika juu yao. Muktadha unaonyesha ni kwa nini tunapaswa kufanya hivyo, unasema: “Kama vile Yehova alivyowasamehe kwa hiari, nanyi lazima mfanye vivyo hivyo.” Ukielewa vizuri mambo ambayo Yehova na Yesu Kristo wamewafanyia wanadamu, utachochewa kuwasamehe wengine makosa yoyote ambayo huenda wamefanya, hasa wanapotubu na kuomba msamaha.