Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 2

Madokezo ya Kuishi Maisha Yenye Kuridhisha

Madokezo ya Kuishi Maisha Yenye Kuridhisha

UNAPOPATA tatizo, unatafuta ushauri wapi? Huenda ukazungumza na rafiki unayemwamini au mshauri mwenye ujuzi. Unaweza kupata msaada kwa kuchunguza habari kama vile kwenye maktaba. Ama unaweza kutafuta “hekima ya Nyanya (Bibi),” kama wanavyosema watu kutoka nchi za Mashariki, ujifunze kutokana na ujuzi wake wa miaka mingi. Iwe unapendelea njia gani, ni vizuri kufikiria ushauri hususa wenye hekima ambao hutoa madokezo yanayosaidia kusuluhisha tatizo hilo. Yafuatayo ni madokezo mazuri ambayo yatakusaidia.

“Mzoeze mvulana njia anayopaswa kuifuata”

2 Maisha ya Familia: Wazazi wengi wana wasiwasi kuhusu kuwalea watoto katika ulimwengu wenye uvutano mbaya. Unaweza kupata msaada ukifuata ushauri huu: “Mzoeze mvulana njia anayopaswa kuifuata; hata atakapozeeka hataiacha.” 1 Watoto wanapoendelea kukua, wanahitaji “njia,” yaani kanuni wanazopaswa kufuata. Wataalamu wengi wametambua umuhimu wa kuwawekea watoto sheria zinazofaa. Kanuni zenye hekima za wazazi huwafanya watoto wajihisi wako salama. Isitoshe: “Fimbo na karipio hufunza hekima, lakini mtoto aliyeachiliwa humwaibisha mama yake.” 2 “Fimbo” inamaanisha mamlaka ya mzazi ambayo inapaswa kutumiwa kwa upendo ili watoto wasipotoke. Kutumia mamlaka hiyo hakumaanishi kwamba unapaswa kumtendea mtoto vibaya. Wazazi wanashauriwa hivi: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.” 3

“Kila mtu kati yenu anapaswa kumpenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe”

3 Uhusiano mzuri kati ya mume na mke ndio msingi wa familia yenye furaha. Ni nini kinachohitajika ili kuwe na uhusiano kama huo? “Kila mtu kati yenu anapaswa kumpenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” 4 Upendo na staha huboresha maisha ya familia. Ili ushauri huu utumike, ni muhimu kuwa na mawasiliano kwa sababu “mipango huvunjika watu wasiposhauriana.” 5 Ili kuwa na mawasiliano ya waziwazi, tunapaswa kujitahidi kufahamu hisia za mwenzi wetu wa ndoa, tukimtia moyo azungumze ili tujue hisia zake. Ni jambo la hekima kukumbuka kwamba “Mawazo yaliyo moyoni mwa mtu ni kama maji yenye kina, lakini mtu mwenye utambuzi huyateka.” 6

Uwe na mtazamo unaofaa, na ujitahidi kuwa na uhusiano mzuri na wengine

4 Watu wengi ambao wamezeeka huwa wapweke katika miaka yao ya baadaye kwa sababu ya kuachwa na watoto wao, hata katika nchi ambazo watoto walikuwa na desturi ya kuwaheshimu wazazi. Lakini, inafaa watoto wao wafikirie maneno haya yenye hekima: Mheshimu baba yako na mama yako.” 7 “Usimdharau mama yako kwa sababu tu amezeeka.” 8 “Yule anayemtendea vibaya baba yake na kumfukuza mama yake ni mwana anayeleta aibu na fedheha.” 9 Kwa upande mwingine, wazazi ambao wamezeeka wanahitaji kuwa na maoni mazuri na kujaribu kuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine. “Anayejitenga na wengine anafuatia tamaa zake mwenyewe za kichoyo; hukataa hekima yote inayotumika.” 10

5 Kunywa Pombe: Ni kweli kwamba “divai hufanya maisha yafurahishe,” 11 na kunywa pombe kunaweza kumfanya mtu ‘ausahau umaskini wake.’ 12 Lakini kumbuka: “Divai ni mdhihaki, kileo ni vurugu; yeyote anayepotoshwa navyo hana hekima.” 13 Hebu fikiria madhara ya kunywa kupita kiasi: “Mwishowe huuma kama nyoka, nayo hutoa sumu kama nyoka kipiri. Macho yako yataona mambo ya ajabu, na moyo wako utasema mambo yaliyopotoka. . . Nitaamka lini? Nahitaji kinywaji kingine.” 14 Kunywa pombe kwa kiasi kunaweza kunufaisha, lakini sikuzote tunapaswa kuepuka kunywa kupita kiasi.

6 Matumizi ya Pesa: Katika hali fulani, tunaweza kuepuka matatizo ya pesa kwa kuzitumia vizuri. Hebu sikiliza ushauri huu: “Usiwe miongoni mwa watu wanaokunywa divai nyingi mno, miongoni mwa wale wanaokula nyama kwa pupa, kwa maana mlevi na mlafi watakuwa maskini, na kusinzia kutamvika mtu matambara.” 15 Kwa kuepuka pombe na dawa za kulevya na vilevile mazoea kama kucheza kamari, tunaweza kutumia pesa zetu kuiandalia familia yetu ifaavyo. Lakini, wengine hushindwa kuishi kulingana na mapato yao na mwishowe hulazimika kufanya kazi kwa bidii ili walipe madeni. Wengine hata huchukua mkopo ili walipe riba ya mkopo mwingine. Kukumbuka maneno haya ya hekima kutatusaidia: “Anayefuatia vitu visivyo na thamani atakuwa na umaskini wa kutosha.” 16 Tunaweza kujiuliza: ‘Je, kweli ninahitaji vitu ambavyo ninataka kununua? Ni vitu vingapi ambavyo hukaa tu nyumbani baada ya kuvitumia mara chache?’ Mwandishi mmoja alisema hivi: “Mambo ambayo mwanadamu anahitaji ni machache lakini yale anayotaka hayana mwisho.” Hebu sikiliza maneno haya ya hekima: “Hatukuleta chochote ulimwenguni, wala hatuwezi kuondoka na chochote. Basi, tukiwa na chakula na mavazi, tutaridhika na vitu hivyo. . . . Kupenda pesa ndicho chanzo cha mambo mabaya ya kila aina, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo, wengine . . . [wamejichoma] kila mahali kwa maumivu mengi.” 17

7 Bidii husaidia sana kusuluhisha matatizo ya kifedha. “Mwendee chungu, ewe mvivu; zichunguze njia zake uwe na hekima. . . . Lala kidogo, sinzia kidogo,kunja mikono kidogo ili upumzike, na umaskini wako utakuja kama jambazi,na uhitaji wako kama mwanamume mwenye silaha.” 18 Kupanga mambo kwa uangalifu na kutumia pesa vizuri kunaweza kusaidia pia: “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?” 19

“Je, umemwona mtu aliye stadi katika kazi yake??”

8 Lakini namna gani ikiwa tunalazimika kuwa maskini kwa sababu ya hali? Kwa mfano, kwa sababu ya matatizo makubwa ya kiuchumi, huenda tukakosa kazi hata ingawa tuko tayari kufanya kazi kwa bidii. Au huenda tunaishi katika nchi ambayo watu wengi ni maskini. Tufanyeje? “Hekima ni ulinzi kama pesa zilivyo ulinzi, lakini hii ndiyo faida ya ujuzi: Hekima humhifadhi hai yule aliye nayo.” 20 Isitoshe fikiria ushauri huu: “Je, umemwona mtu aliye stadi katika kazi yake? Atasimama mbele ya wafalme.” 21 Je, tunaweza kujifunza ufundi fulani ambao unaweza kutusaidia kupata kazi?

“Muwe na mazoea ya kuwapa watu, nanyi mtapewa”

9 Ushauri ufuatao huenda ukaonekana kuwa unajipinga, lakini ni ushauri bora: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, nanyi mtapewa. . . . Kwa maana kwa kipimo mnachowapimia watu, ndicho watakachowapimia.” 22 Hii haimaanishi kuwapa watu vitu ukitarajia kupewa vitu pia. Badala yake, tunashauriwa kuwa na roho ya ukarimu: “Mtu mkarimu atapata ufanisi, na yule anayewaburudisha wengine yeye mwenyewe ataburudishwa.” 23 Tunapowasaidia wengine wanapokuwa na uhitaji, tunaendeleza roho ya kutoa ambayo hatimaye inaweza kutufaidi.

10 Uhusiano wa wanadamu: Mfalme mmoja mwenye hekima alisema: “Nami nimeona jinsi ambavyo ushindani kati ya watu unavyowafanya wajitahidi sana na kufanya kazi kwa ustadi; hili pia ni ubatili, kukimbiza upepo.” 24 Ushindani umewafanya wengi watende kwa njia isiyo ya hekima. Mtu anaona jirani yake amenunua televisheni ya inchi 32, naye anaenda kununua televisheni ya inchi 36, hata ingawa ile televisheni yake ya inchi 27 inafanya kazi vizuri. Kwa kweli ushindani kama huo ni ubatili, ni kama kufuata upepo tu—kukimbia huku na huku bila kutimiza chochote. Je, sivyo?

Tunawezaje kudhibiti hasira kali?

11 Huenda tukakasirishwa na mambo ambayo wengine wametuambia. Lakini hebu fikiria ushauri huu: “Usikasirike haraka, kwa maana hasira hukaa katika kifua cha wajinga.” 25 Ni kweli kwamba kuna pindi ambazo una haki ya kukasirika. “Iweni na hasira,” mwandishi mmoja wa kale anasema, “lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa bado mmekasirika.” 26 Lakini tunawezaje kudhibiti hasira kali? “Ufahamu wa mtu hakika hutuliza hasira yake, na ni fahari kwake kuachilia kosa.” 27 Tunahitaji ufahamu. Tunaweza kujiuliza: ‘Kwa nini alifanya hivyo? Je, kuna mambo yaliyosababisha afanye hivyo?’ Zaidi ya kuwa na ufahamu, kuna sifa ambazo tunaweza kukuza ili kudhibiti hasira. “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu, upole, na subira. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari hata ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. . . Lakini zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” 28 Ndiyo, upendo husuluhisha matatizo mengi yanayohusu uhusiano wa wanadamu.

12 Lakini, kuna “kiungo kidogo” ambacho kinaharibu amani kati ya watu—ulimi. Maneno yafuatayo ni ya kweli kabisa: “Lakini hakuna mwanadamu anayeweza kuufuga ulimi. Ulimi ni kitu kitundu chenye kudhuru, kilichojaa sumu yenye kuua.” 29 Na kwa kweli ushauri huu unafaa: “Kila mtu lazima awe mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa hasira.” 30 Na tunapotumia ulimi, tuwe waangalifu tusiseme mambo ambayo ni kweli nusu ili kudumisha amani ya kijuujuu. “Acheni ‘Ndiyo’ yenu imaanishe ndiyo, na ‘Siyo’ yenu, siyo, kwa maana linalozidi hayo linatoka kwa yule mwovu.” 31

13 Tunawezaje kudumisha uhusiano mzuri pamoja na wengine? Ona kanuni ifuatayo: “Mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.” 32 Kwa kufanya hivyo tutaishi kulingana na ile ambayo imeitwa na wengi Kanuni Bora: “Basi, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima ninyi pia mwatendee vivyo hivyo.” 33

14 Mkazo: Tunaweza kudumishaje usawaziko wa kihisia katika ulimwengu huu uliojaa mikazo? “Moyo wenye shangwe hufanya uso uchangamke, lakini maumivu ya moyo huiponda roho.” 34 Tunaweza kupoteza kwa urahisi “moyo wenye shangwe” tunapoona wengine wakipuuza mambo tunayoona kuwa sawa. Lakini ni vizuri tukumbuke maneno haya: “Usiwe mwadilifu kupita kiasi, wala kujifanya mwenye hekima kupita kiasi. Kwa nini ujiangamize?” 35 Kwa upande mwingine, huenda sikuzote tukawa na mahangaiko ya maisha. Tufanye nini? Tukumbuke maneno haya: “Mahangaiko yaliyo moyoni mwa mtu huulemea moyo, lakini neno jema huuchangamsha.” 36 Tunaweza kutafakari “neno jema,” neno lenye fadhili ambalo linatutia moyo. Kuwa na mtazamo unaofaa hata tunapokabili hali ngumu kunaweza kuchangia afya bora: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.” 37 Tukishuka moyo kwa sababu inaonekana wengine hawatujali, inafaa tufuate dokezo hili: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” 38 Tukiwa na mtazamo unaofaa, tunaweza kukabiliana na mikazo ya kila siku.

15 Je, unafikiri kwamba maneno hayo ya hekima yaliyotajwa yanaweza kukusaidia leo katika karne ya 21? Maneno hayo yanapatikana katika kitabu fulani cha kale—Biblia. Lakini, kwa nini uchunguze Biblia badala ya vyanzo vingine vya hekima? Kwa kuwa, miongoni mwa sababu nyingine, kanuni zinazopatikana katika Biblia zimethibitika kuwa zenye faida nyakati zote. Kwa mfano, fikiria Yasuhiro na Kayoko, waliokuwa wanaharakati wa kutetea haki za wanawake. Walifunga ndoa kwa sababu tu Kayoko alishika mimba ya Yasuhiro. Lakini kwa sababu ya matatizo ya kifedha na kuona kwamba hawafaani, wakaamua kutalikiana. Baadaye, bila yeyote kati yao kujua, wote wawili walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kila mmoja wao aliona mabadiliko makubwa katika maisha ya mwenzake. Yasuhiro na Kayoko wakaamua kufunga ndoa tena. Ingawa bado wanakabili matatizo, sasa wanaishi kwa kufuata kanuni za Biblia, na wote wawili wanakubaliana kusuluhisha matatizo. Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, utaona matokeo mazuri ya kutumia kanuni za Biblia maishani. Mbona usihudhurie mojawapo ya mikutano yao ili uwafahamu watu ambao wanajitahidi kuishi kulingana na Biblia?

16 Mashauri yaliyonukuliwa hapo juu ni sehemu tu ya hekima chungu nzima yenye faida unayoweza kupata katika hazina hii kubwa ya elimu, yaani Biblia. Kuna sababu zinazofanya Mashahidi wa Yehova watumie kanuni za Biblia kwa hiari maishani mwao. Kwa nini usijitahidi kujua sababu zinazofanya watumie kanuni hizo na ujifunze mambo ya msingi kuhusu Biblia?