Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 20

“Yeye Ni Mwenye Hekima Moyoni”—Lakini Mnyenyekevu

“Yeye Ni Mwenye Hekima Moyoni”—Lakini Mnyenyekevu

1-3. Tunajuaje kwamba Yehova ni mnyenyekevu?

BABA anataka kumfundisha mtoto wake mdogo somo muhimu. Ana hamu ya kugusa moyo wa mtoto huyo. Afanyeje hivyo? Je, asimame na kumtisha mtoto huyo? Au apaswa kuchuchumaa kufikia kimo cha mtoto huyo na kuzungumza naye kwa upole, na kwa urafiki? Bila shaka, baba mnyenyekevu na mwenye hekima humfikia mtoto wake kwa njia ya upole.

2 Yehova ni Baba wa aina gani—je, yeye ni mwenye kiburi au mnyenyekevu, mkali au mpole? Yehova anajua kila jambo, ana hekima kamili. Hata hivyo, je, umeona kwamba mara nyingi watu wenye ujuzi na akili hawawi wanyenyekevu? Ni kama Biblia inavyosema, ‘ujuzi hututumua.’ (1 Wakorintho 3:19; 8:1) Lakini Yehova, ni “mwenye hekima moyoni,” na mnyenyekevu pia. (Ayubu 9:4) Yehova hana kiburi licha ya kwamba ana cheo cha juu na fahari. Kwa nini?

3 Yehova ni mtakatifu. Kwa hiyo, hana sifa ya kiburi ambayo inamtia mtu unajisi. (Marko 7:20-22) Isitoshe, angalia maneno ambayo nabii Yeremia alimwambia Yehova: “Bila shaka nafsi yako [Yehova mwenyewe] itanikumbuka na kuniinamia.” * (Maombolezo 3:20, NW) Hebu wazia! Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu, alikuwa tayari ‘kumwinamia,’ au kujinyenyekeza kufikia kiwango cha Yeremia. Alifanya hivyo ili kumpa uangalifu unaofaa mwanadamu huyo asiyekamilika. (Zaburi 113:7) Naam, Yehova ni mnyenyekevu. Lakini Mungu anaonyeshaje unyenyekevu? Unahusianaje na hekima? Na kwa nini unyenyekevu ni muhimu kwetu?

Jinsi Yehova Alivyo Mnyenyekevu

4, 5. (a) Unyenyekevu ni nini, na unaonyeshwaje, na kwa nini unyenyekevu haupasi kuonwa kuwa udhaifu au woga? (b) Yehova alionyeshaje unyenyekevu aliposhughulika na Daudi, na unyenyekevu wa Yehova unatufaidi jinsi gani?

4 Unyenyekevu unamaanisha kujiweka katika hali ya chini, kutojivuna na kutokuwa na kiburi. Unyenyekevu ni sifa ya moyoni na huonyeshwa kwa sifa kama vile upole, subira, na kuzingatia maoni ya wengine. (Wagalatia 5:22, 23) Lakini sifa hizo za kimungu hazipasi kamwe kuonwa kuwa udhaifu au woga. Sifa hizo zinapatana na hasira ya Yehova ya uadilifu au jinsi anavyotumia nguvu zake za kuangamiza. Lakini unyenyekevu na upole wa Yehova unaonyesha kwamba ana nguvu nyingi, yaani, uwezo wa kujidhibiti kikamili. (Isaya 42:14) Unyenyekevu unahusianaje na hekima? Kichapo kimoja kinachozungumzia Biblia kinasema hivi: “Unyenyekevu unafafanuliwa kuwa . . . hali ya kutokuwa na ubinafsi na ni chanzo muhimu cha hekima yote.” Basi, hakuwezi kuwa na hekima ya kweli pasipo unyenyekevu. Unyenyekevu wa Yehova unatufaidi jinsi gani?

Baba mwenye hekima huwatendea watoto wake kwa upole na unyenyekevu

5 Mfalme Daudi alimwimbia Yehova hivi: “Umenipa ngao ya wokovu wako, mkono wako wa kuume umenitegemeza, na unyenyekevu wako umenikuza.” (Zaburi 18:35) Ni kana kwamba Yehova aliinama ili amsaidie mwanadamu huyo asiyekamilika, alimlinda na kumtunza siku kwa siku. Daudi alitambua kwamba hangeweza kamwe kuokolewa—na hata, hatimaye kuwa mfalme—endapo Yehova hangejinyenyekeza. Kwa kweli, ni nani kati yetu angeweza kuwa na tumaini lolote la kuokoka ikiwa Yehova hangekuwa mnyenyekevu, na kama hangekuwa tayari kujiweka katika hali ya chini ili kushughulika nasi akiwa Baba mpole mwenye upendo?

6, 7. (a) Kwa nini Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova ni mwenye kiasi kama wanadamu? (b) Kuna uhusiano gani kati ya upole na hekima, na ni nani aliye mfano bora kabisa wa sifa hizo?

6 Inafaa kukumbuka kwamba kuna tofauti kati ya unyenyekevu na kiasi. Kiasi ni sifa nzuri sana ambayo wanadamu waaminifu wanapaswa kukuza. Sifa hiyo, kama vile sifa ya unyenyekevu, inahusiana na hekima. Kwa mfano, Mithali 11:2, NW, yasema: “Hekima hukaa na wenye kiasi.” Hata hivyo, Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova ni mwenye kiasi kama wanadamu. Kwa nini? Kulingana na Maandiko, mtu mwenye kiasi ni mtu anayetambua mipaka yake mwenyewe. Mungu Mweza-Yote hana mipaka yoyote ila mipaka anayojiwekea mwenyewe kwa sababu ya kanuni zake adilifu. (Marko 10:27; Tito 1:2) Isitoshe, hajitiishi kwa yeyote kwa sababu yeye ni Mungu Mwenyezi. Kwa hiyo, Yehova si mwenye kiasi katika maana hiyo.

7 Hata hivyo, Yehova ni mnyenyekevu na mpole. Yeye huwafundisha watumishi wake kwamba hawawezi kuwa na hekima ya kweli wasipokuwa wapole. Neno lake hutaja “upole ulio wa hekima.” * (Yakobo 3:13) Fikiria jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hizo.

Yehova Huwakabidhi Wengine Madaraka Naye Huwasikiliza kwa Unyenyekevu

8-10. (a) Kwa nini inashangaza kwamba Yehova yu tayari kuwakabidhi wengine madaraka na kuwasikiliza? (b) Mwenyezi ameonyeshaje unyenyekevu anaposhughulika na malaika wake?

8 Utayari wa Yehova wa kusikiliza na kuwakabidhi wengine madaraka unaonyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu. Inashangaza kwamba Yehova yu tayari kufanya hivyo ingawa yeye hahitaji msaada wala shauri. (Isaya 40:13, 14; Waroma 11:34, 35) Hata hivyo, Biblia inaonyesha tena na tena kwamba Yehova hujinyenyekeza katika njia hizo.

9 Kwa mfano, fikiria kisa kimoja cha pekee kilichotukia katika maisha ya Abrahamu. Abrahamu alitembelewa na wageni watatu, alimwita mmoja wao “Bwana.” Wageni hao walikuwa malaika, lakini mmoja wao alikuja kwa jina la Yehova na alikuwa akitenda kwa jina hilo. Malaika huyo aliponena na kutenda, ni kana kwamba Yehova mwenyewe alikuwa akinena na kutenda. Kupitia malaika hao, Yehova alimwambia Abrahamu kwamba Alikuwa amesikia “kilio cha Sodoma na Gomora.” Yehova alisema hivi: “Nitashuka sasa nione kama wanayotenda ni kiasi cha kilio kilichonijia; na kama sivyo, nitajua.” (Mwanzo 18:3, 20, 21) Bila shaka, ujumbe huo wa Yehova haukumaanisha kwamba Mweza Yote ‘angeshuka’ kihalisi. Badala yake, aliwatuma malaika wamwakilishe tena. (Mwanzo 19:1) Kwa nini? Je, Yehova ambaye ana uwezo wa kuona kila jambo hangeweza ‘kujua’ hali ya eneo hilo bila msaada? Bila shaka angeweza. Lakini badala yake, kwa unyenyekevu Yehova aliwapa malaika hao kazi ya kuchunguza hali na kumtembelea Loti na familia yake Sodoma.

10 Isitoshe, Yehova husikiliza. Pindi moja aliwaomba malaika wake watoe maoni kuhusu njia mbalimbali za kumshinda Mfalme Ahabu aliyekuwa mwovu. Yehova hakuhitaji msaada huo. Lakini, alikubali maoni ya malaika mmoja, naye akamtuma atekeleze jambo hilo. (1 Wafalme 22:19-22) Tukio hilo linaonyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu, sivyo?

11, 12. Abrahamu alipataje kuelewa unyenyekevu wa Yehova?

11 Yehova yu tayari pia kuwasikiliza wanadamu wasiokamilika ambao wanataka sana kumweleza mahangaiko yao. Kwa mfano, Yehova alipomwambia Abrahamu kwamba alikusudia kuharibu Sodoma na Gomora, mwanamume huyo mwaminifu alishtuka. Abrahamu akasema, “Hasha usifanye hivyo,” kisha akaongezea hivi: “Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?” Alimwuliza Yehova kama angeacha miji hiyo iwapo ingekuwa na watu 50 wenye haki. Yehova alimhakikishia kwamba Hangeiangamiza. Lakini Abrahamu akamwuliza swali hilo tena na tena, na kupunguza idadi hiyo hadi 45, kisha 40, na kuendelea. Abrahamu aliendelea kuuliza maswali hadi idadi hiyo ilipofikia kumi licha ya Yehova kumhakikishia kwamba hangeangamiza miji hiyo. Huenda Abrahamu hakufahamu vyema rehema ya Yehova. Vyovyote iwavyo, kwa subira Yehova alimruhusu rafiki na mtumishi wake Abrahamu aeleze mahangaiko yake.—Mwanzo 18:23-33.

12 Ni wanadamu wangapi wenye akili, na wenye elimu ambao wangemsikiliza kwa subira mtu asiye na akili nyingi sana? * Mungu wetu alionyesha unyenyekevu mkubwa kwa kumsikiliza Abrahamu kwa makini sana. Wakati wa mazungumzo hayo, Abrahamu alitambua pia kwamba Yehova “si mwepesi wa hasira.” (Kutoka 34:6) Huenda Abrahamu alitambua kwamba hakuwa na haki ya kumwuliza Mungu mambo aliyokusudia kufanya, kwa hiyo alimsihi hivi mara mbili: “Bwana asiwe na hasira.” (Mwanzo 18:30, 32) Bila shaka Yehova hakukasirika. Kwa kweli, Yehova ana “upole ulio wa hekima.”

Yehova Hukubali Sababu

13. Usemi “kukubali sababu” hutumiwa katika Biblia kumaanisha nini, na kwa nini sifa hiyo inamfaa kabisa Yehova?

13 Unyenyekevu wa Yehova unadhihirishwa na sifa nyingine yenye kupendeza—kukubali sababu. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba wanadamu wengi wasiokamilika hawana sifa hiyo. Yehova yuko tayari kuwasikiliza viumbe wake wenye akili, na yuko tayari pia kukubali maoni yao maadamu hayakiuki kanuni zake za uadilifu. Usemi “kukubali sababu” hutumiwa katika Biblia kumaanisha kihalisi ‘kukubali maoni ya wengine.’ Hiyo pia ni sifa muhimu ya hekima ya Mungu. Andiko la Yakobo 3:17 lasema hivi: ‘Hekima ya kutoka juu ni yenye kukubali sababu.’ Yehova ambaye ni mwenye hekima kamilifu anakubali sababu kwa njia gani? Kwanza, yeye hujipatanisha na hali mbalimbali. Kumbuka kwamba jina lake linatufundisha kwamba Yeye hujisababisha kuwa chochote kinachohitajiwa ili kutimiza makusudi yake. (Kutoka 3:14) Je, hilo halionyeshi kwamba yeye hujipatanisha na hali na ni mwenye kukubali sababu?

14, 15. Ono la Ezekieli la gari la kimbingu la Yehova linatufunza nini kuhusu tengenezo Lake la kimbingu, na hilo linatofautianaje na mashirika ya wanadamu?

14 Kuna ono moja la Biblia linalotusaidia kuelewa kwa kadiri fulani jinsi Yehova anavyojipatanisha na hali mbalimbali. Nabii Ezekieli alipata ono la tengenezo la kimbingu la Yehova la viumbe wa roho. Aliona gari kubwa ajabu na Yehova mwenyewe ndiye anayelielekeza gari hilo daima. Lilienda kwa njia ya kustaajabisha sana. Magurudumu yake makubwa yenye pande nne, yalijaa macho hivi kwamba yaliweza kuona kila mahali na kusafiri kuelekea upande wowote ghafula bila kusimama wala kugeuka. Na gari hilo kubwa mno halikujikokota polepole kama gari lililotengenezwa na wanadamu. Liliweza kwenda kwa mwendo wa umeme, na hata kugeuka ghafula! (Ezekieli 1:1, 14-28) Naam, tengenezo la Yehova linaweza kujipatanisha kabisa na hali mbalimbali na kushughulikia mahitaji yanayotokea kama anavyofanya Mungu Mwenye Enzi Kuu na mweza-yote ambaye analiongoza.

15 Wanadamu hawawezi kamwe kujipatanisha kikamili na hali kwa njia hiyo. Mara nyingi wanadamu na mashirika yao hushikilia mno maoni yao bila kubadilika, na hawakubali sababu. Kwa mfano: Meli ya mafuta au garimoshi la kubeba mizigo laweza kuwa kubwa sana na lenye nguvu nyingi sana. Lakini je, garimoshi au meli inaweza kugeuka mara moja hali zikibadilika? Garimoshi la mizigo haliwezi kuepuka kitu fulani kinachoanguka kwenye reli yake. Haliwezi kusimama ghafula. Baada ya breki kufungwa, garimoshi lenye mizigo mizito laweza kwenda umbali wa kilometa mbili hivi kabla ya kusimama! Vivyo hivyo, huenda meli kubwa ya mafuta ikasafiri umbali wa kilometa nane baada ya injini kuzimwa. Hata injini zikiendeshwa kinyumenyume, bado meli hiyo inaweza kusonga mbele umbali wa kilometa tatu! Ndivyo ilivyo na mashirika ya wanadamu ambayo mara nyingi hushikilia sana sera zake na kutokubali mawazo mapya. Mara nyingi watu hukataa kubadilika kulingana na mahitaji na hali mpya kwa sababu ya kiburi. Mashirika mengi yamevunjika na hata serikali nyingi kupinduliwa kwa sababu ya kutobadilika kulingana na hali. (Mithali 16:18) Twaweza kushukuru kama nini kwamba Yehova na tengenezo lake ni tofauti sana na mashirika hayo ya wanadamu!

Jinsi Yehova Anavyokubali Sababu

16. Yehova alionyeshaje sifa ya kukubali sababu aliposhughulika na Loti kabla ya kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora?

16 Fikiria tena kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora. Malaika wa Yehova alimpa Loti na familia yake maagizo yaliyo wazi kabisa: “Ujiponye mlimani.” Lakini maagizo hayo hayakumpendeza Loti. “Sivyo, bwana wangu!” akasihi. Akiamini kwamba angekufa kama angekimbilia milimani, Loti aliomba kwamba yeye na familia yake waruhusiwe kukimbilia mji wa karibu ulioitwa Soari. Kumbuka kwamba Yehova alikuwa amekusudia kuuangamiza mji huo. Isitoshe, Loti hakuwa na sababu nzuri ya kuogopa. Bila shaka Yehova angeweza kumlinda Loti huko milimani! Hata hivyo, Yehova alikubali ombi la Loti, hakuuangamiza mji wa Soari. Malaika akamwambia hivi Loti, “Tazama, nimekukubali hata kwa neno hili.” (Mwanzo 19:17-22) Je, jambo hilo halionyeshi kwamba Yehova ni mwenye kukubali sababu?

17, 18. Yehova alionyeshaje sifa ya kukubali sababu kuhusiana na Waninawi?

17 Yehova hukubali pia toba ya kutoka moyoni. Sikuzote yeye huonyesha rehema na kutenda yaliyo sawa. Fikiria jambo lililotukia nabii Yona alipotumwa mji wa Ninawi wenye uovu na jeuri. Yona alitangaza ujumbe rahisi sana wa Mungu kotekote katika Ninawi: Mji huo mashuhuri ungeangamizwa baada ya siku 40. Lakini, mambo yalibadilika ghafula. Waninawi walitubu!—Yona, sura ya 3.

18 Tunajifunza jambo fulani tunapolinganisha jinsi Yehova alivyohisi na jinsi Yona alivyohisi hali ilipobadilika. Yehova alijipatanisha na hali hiyo mara moja, akawa Mwenye Kusamehe dhambi badala ya kuwa “mtu wa vita.” * (Kutoka 15:3) Lakini Yona hakuwa tayari kubadilika wala hakuonyesha rehema kama Yehova alivyofanya. Badala ya kukubali sababu kama Yehova, alikuwa kama garimoshi la mizigo au meli kubwa ya mafuta tuliyotaja awali. Alitaka mji huo uangamizwe tu kama alivyokuwa ametangaza. Hata hivyo, kwa subira Yehova alimfundisha nabii wake asiye na subira somo lisilosahaulika kuhusu kukubali sababu na kuonyesha rehema.—Yona, sura ya 4.

Yehova ni mwenye kukubali sababu na anajua udhaifu wetu

19. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ni mwenye kukubali sababu kuhusiana na mambo anayotarajia tufanye? (b) Mithali 19:17 inaonyeshaje kwamba Yehova ni Bwana ‘mwema na mwenye kukubali sababu,’ na kwamba unyenyekevu wake hauna kifani?

19 Mwishowe, Yehova ni mwenye kukubali sababu kuhusiana na mambo anayotarajia tufanye. Mfalme Daudi alisema: “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:14) Yehova anajua udhaifu wetu na kasoro zetu kuliko tunavyojijua. Hatarajii kamwe tufanye mambo yanayozidi uwezo wetu. Biblia inasema kwamba mabwana fulani ni ‘wema na wenye kukubali sababu’ na wengine ni “wagumu kupendeza.” (1 Petro 2:18) Je, Yehova ni Bwana wa aina gani? Mithali 19:17 inasema: “Amhurumiaye maskini humkopesha BWANA.” Ni wazi kwamba bwana aliye mwema na mwenye kukubali sababu ndiye tu anayezingatia kila tendo la fadhili ambalo maskini wanafanyiwa. Isitoshe, andiko hilo pia linadokeza kwamba Muumba wa ulimwengu anajiona kuwa na deni kwa wanadamu duni wanaofanya matendo hayo ya rehema! Huo ni unyenyekevu usio na kifani.

20. Tuna uhakika gani kwamba Yehova husikiliza na kujibu sala zetu?

20 Hata leo Yehova ni mpole na mwenye kukubali sababu anaposhughulika na watumishi wake. Yeye husikiliza sala zetu za imani. Hatupaswi kukata kauli kwamba hajibu sala zetu kwa sababu hawatumi malaika waongee nasi. Kumbuka kwamba mtume Paulo alipowaomba waamini wenzake ‘waendeleze sala’ ili aweze kuachiliwa kutoka gerezani, aliongeza hivi: “Ili nipate kurudishwa kwenu karibuni zaidi.” (Waebrania 13:18, 19) Kwa hiyo, sala zetu zinaweza kwa kweli kumfanya Yehova atende jambo ambalo huenda hangetenda!—Yakobo 5:16.

21. Hatupaswi kuwa na maoni gani kuhusu unyenyekevu wa Yehova, lakini tunapaswa kumthamini kwa sababu gani?

21 Bila shaka, sifa zinazoonyesha unyenyekevu wa Yehova, yaani, upole, utayari wa kutusikiliza, subira, na kukubali sababu, hazimaanishi kwamba Yehova hulegeza kanuni zake adilifu. Huenda makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wakadhani kwamba wanakubali sababu wanapotekenya masikio ya wafuasi wao kwa kulegeza kanuni za Yehova za maadili. (2 Timotheo 4:3) Lakini mwelekeo wa wanadamu wa kuridhiana ili wapendwe haupatani kabisa na sifa ya Mungu ya kukubali sababu. Yehova ni mtakatifu; hawezi kamwe kupotosha kanuni zake adilifu. (Mambo ya Walawi 11:44) Basi, na tupende sifa ya Yehova ya kukubali sababu kwa kuwa inathibitisha unyenyekevu wake. Je, hufurahi sana kujua kwamba Yehova Mungu ni mnyenyekevu sana licha ya kwamba ana hekima isiyo na kifani katika ulimwengu wote? Inapendeza kama nini kumkaribia Mungu huyu mtukufu ambaye ni mpole, mwenye subira, na mwenye kukubali sababu!

^ fu. 3 Waandishi wa kale, au Wasoferi, walibadili mstari huu kusema kwamba ni Yeremia anayeinama wala si Yehova. Inaonekana kwamba walidhani haifai kusema kwamba Mungu alitenda kitendo hicho cha unyenyekevu. Ndiyo sababu tafsiri nyingi zinakosa maana ya mstari huu wenye kupendeza. Hata hivyo, The New English Bible inasema kwa usahihi kwamba Yeremia alimwambia Mungu hivi: “Kumbuka, Ee kumbuka, na uniinamie.”

^ fu. 7 Tafsiri nyingine husema “unyenyekevu unaotokana na hekima” na “upole ambao ni wonyesho muhimu wa hekima.”

^ fu. 12 Biblia inaonyesha kwamba subira ni kinyume cha kiburi. (Mhubiri 7:8) Subira ya Yehova inathibitisha hata zaidi kwamba yeye ni mnyenyekevu.—2 Petro 3:9.

^ fu. 18 Zaburi 86:5 inasema kwamba Yehova ni ‘mwema na yuko tayari kusamehe.’ Zaburi hiyo ilipotafsiriwa katika Kigiriki, usemi “tayari kusamehe” ulitafsiriwa e·pi·ei·kesʹ, au “mwenye kukubali sababu.”