Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 3

“Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Ni Bwana”

“Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Ni Bwana”

1, 2. Isaya alipokea ono gani, na linatufundisha nini juu ya Yehova?

ISAYA alitiwa kicho na mandhari aliyoona—ono kutoka kwa Mungu. Ni kana kwamba lilikuwa halisi! Baadaye Isaya aliandika kwamba kwa kweli ‘alimwona Bwana’ ameketi katika kiti Chake cha enzi kilicho juu sana. Na pindo la vazi la Yehova lilijaza hekalu kubwa la Yerusalemu.—Isaya 6:1, 2.

2 Isaya alitiwa kicho pia na sauti aliyosikia—wimbo wenye nguvu sana hivi kwamba ulitikisa hekalu na misingi yake. Wimbo huo uliimbwa na maserafi, viumbe wa roho wenye cheo cha juu. Wimbo huo mtamu ulioimbwa kwa sauti ya juu na upatano ulivumisha maneno sahili ya fahari ya kifalme: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu, ni BWANA wa majeshi; dunia yote imejaa utukufu wake.” (Isaya 6:3, 4) Kuimba neno “mtakatifu” mara tatu kulikazia neno hilo kwa njia ya pekee sana. Jambo hilo lafaa kwa sababu utakatifu wa Yehova ni wa hali ya juu sana. (Ufunuo 4:8) Utakatifu wa Yehova unakaziwa katika Biblia nzima. Kuna mamia ya mistari ya Biblia inayotaja jina lake pamoja na maneno “takatifu” na “utakatifu.”

3. Kwa nini maoni yenye kosa kuhusu utakatifu wa Yehova yanawafanya watu wengi wakatae kumkaribia Mungu?

3 Hivyo basi, ni wazi kwamba mojawapo ya mambo muhimu ambayo Yehova anataka tujue kumhusu ni kuwa yeye ni mtakatifu. Lakini watu wengi leo huchukizwa na wazo hilo. Baadhi yao hudhani kimakosa kwamba kuwa mtakatifu kunamaanisha kujiona kuwa mwadilifu au kujidai kuwa mchaji-Mungu. Watu wanaojiona kuwa hawafai huenda wakahofu badala ya kuvutiwa na wazo la kuwa Mungu ni mtakatifu. Huenda wakahofu kwamba hawawezi kustahili kamwe kumkaribia Mungu huyo mtakatifu. Kwa hiyo, watu wengi hawataki kumkaribia Mungu kwa sababu ya utakatifu wake. Inasikitisha sana kwa sababu utakatifu wa Mungu kwa kweli ni kichocheo cha kumkaribia. Kwa nini? Kabla ya kujibu swali hilo, hebu tuzungumzie maana halisi ya utakatifu.

Utakatifu Ni Nini?

4, 5. (a) Neno “utakatifu” linamaanisha nini, nalo halimaanishi nini? (b) Yehova “amejitenga” katika njia zipi mbili muhimu?

4 Ingawa Mungu ni mtakatifu haimaanishi kwamba yeye anajivuna, ni mwenye kiburi, au anawadharau wengine. Badala yake, anachukia sifa hizo. (Mithali 16:5; Yakobo 4:6) Basi neno “-takatifu” linamaanisha nini? Katika Kiebrania cha Biblia, neno lililotafsiriwa “-takatifu” linatokana na neno linalomaanisha “kutenga.” Katika ibada, kitu “kitakatifu” ni kile kilichotengwa kwa ajili ya matumizi maalumu. Utakatifu pia hutoa wazo la usafi na utakato. Neno hilo hutumiwaje kuhusiana na Yehova? Je, yamaanisha kwamba yeye ‘hujitenga’ mbali na wanadamu wasiokamilika, au kwamba yuko mbali nasi?

5 La hasha. Akiwa “Mtakatifu wa Israeli,” Yehova alisema kuwa anakaa “katikati” ya watu wake, licha ya kwamba walikuwa wenye dhambi. (Isaya 12:6; Hosea 11:9) Kwa hiyo, hajitengi na watu kwa sababu yeye ni mtakatifu. Basi yeye “hujitengaje”? Yeye hujitenga katika njia mbili muhimu. Kwanza, yeye amejitenga na viumbe wote katika maana ya kwamba yeye peke yake ndiye Aliye Juu Sana. Usafi wake, na utakato wake, ni kamili kabisa na unadumu milele. (Zaburi 40:5; 83:18) Pili, Yehova amejitenga kabisa na dhambi, na hilo linatufariji. Kwa nini?

6. Kwa nini ni faraja kujua kwamba Yehova hana dhambi kabisa?

6 Tunaishi katika ulimwengu ambamo utakatifu wa kweli ni haba. Kila jambo linalofanywa na wanadamu waliojitenga na Mungu limepotoka kwa njia fulani, limechafuliwa na dhambi na kutokamilika. Sote tunapambana na dhambi iliyo mwilini mwetu. Sote tunakabili hatari ya kushindwa na dhambi tusipojihadhari. (Waroma 7:15-25; 1 Wakorintho 10:12) Yehova hakabili hatari hiyo. Yeye hana dhambi kabisa, hatachafuliwa kamwe na dhambi yoyote. Hilo latuthibitishia kwamba Yehova ndiye Baba bora, kwa sababu yeye ni mwenye kutegemeka kabisa. Tofauti na akina baba wengi wenye dhambi, Yehova hawezi kupotoka kamwe, wala kuwa na utovu wa maadili, au kuwadhuru kamwe watoto wake. Hawezi kutenda kamwe mambo hayo kwa sababu yeye ni mtakatifu. Yehova hata ameapa kwa utakatifu wake pindi fulani-fulani, na hilo linafanya viapo vyake viwe vyenye kutumainika kabisa. (Amosi 4:2) Je, hilo halitufariji?

7. Kwa nini tunaweza kusema kwamba utakatifu ni sehemu ya utu wa Yehova?

7 Utakatifu ni sehemu ya utu wa Yehova. Hilo lamaanisha nini? Kwa mfano: Fikiria maneno “mwanadamu” na “kutokamilika.” Huwezi kueleza hali ya wanadamu bila kufikiria hali ya kutokamilika. Hali ya kutokamilika inaathiri kila jambo tunalofanya. Sasa fikiria maneno mawili tofauti kabisa—“Yehova” na “utakatifu.” Yehova ana utakatifu kamili. Kila jambo kumhusu ni safi, limetakata, na ni adilifu. Hatuwezi kumjua Yehova kikweli bila kufikiria kwa uzito na kufahamu neno hili muhimu—“-takatifu.”

“Utakatifu Ni wa Yehova”

8, 9. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova huwasaidia wanadamu wasiokamilika kuwa watakatifu kwa kadiri fulani?

8 Kwa kuwa utakatifu ni sehemu ya utu wa Yehova, tunaweza kusema kwa kufaa kwamba yeye ndiye chanzo cha utakatifu wote. Yeye hajiwekei kwa ubinafsi sifa hii yenye thamani; yeye huwapa wengine, naye huwapa kwa ukarimu. Mungu aliponena na Musa kwa kutumia malaika kwenye kichaka kilichokuwa kikiwaka moto, ardhi yote iliyokuwa karibu ikawa takatifu kwa sababu Yehova alikuwa akitumia sehemu hiyo!—Kutoka 3:5.

9 Je, wanadamu wasiokamilika wanaweza kuwa watakatifu kwa msaada wa Yehova? Ndiyo, kwa kadiri fulani. Mungu aliwapa watu wake Israeli fursa ya kuwa “taifa takatifu.” (Kutoka 19:6) Alibariki taifa hilo kwa kuliandalia ibada iliyokuwa takatifu na safi. Kwa hiyo, Sheria ya Kimusa inakazia utakatifu tena na tena. Kwa kweli, kuhani mkuu alivaa bamba la dhahabu upande wa mbele wa kilemba chake, na watu wote waliweza kuliona likimetameta kwenye nuru. Maneno haya yalichongwa juu yake: “Utakatifu ni wa Yehova.” (Kutoka 28:36, NW) Kwa hiyo, kiwango cha juu cha usafi na utakato kingefanya ibada yao na hata njia yao ya maisha iwe ya pekee. Yehova aliwaambia hivi: “Mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi BWANA, Mungu wenu ni mtakatifu.” (Mambo ya Walawi 19:2) Waisraeli walikuwa watakatifu kwa kadiri fulani maadamu waliishi kupatana na maagizo ya Mungu kwa kadiri ya uwezo wa wanadamu wasiokamilika.

10. Israeli la kale lilitofautianaje na mataifa yaliyolizunguka kwa habari ya utakatifu?

10 Utakatifu huo ulikaziwa sana katika Israeli, tofauti sana na ibada ya mataifa yaliyolizunguka. Mataifa hayo ya kipagani yaliabudu miungu bandia ambayo haikuishi kamwe, miungu ambayo ilisifiwa kuwa yenye jeuri, yenye pupa, na yenye maadili mapotovu. Haikuwa mitakatifu kwa njia yoyote. Kuabudu miungu hiyo kuliwafanya watu wasiwe watakatifu. Kwa hiyo, Yehova aliwaonya watumishi wake wajitenge na waabudu hao wapagani na kuepuka mazoea yao machafu ya kidini.—Mambo ya Walawi 18:24-28; 1 Wafalme 11:1, 2.

11. Utakatifu wa tengenezo la Yehova la kimbingu unadhihirishwaje na (a) malaika? (b) maserafi? (c) Yesu?

11 Hata lilipokuwa katika hali bora zaidi, taifa la Israeli la kale lililochaguliwa na Yehova lilidhihirisha kwa kiwango kidogo sana utakatifu wa tengenezo la Mungu la kimbingu. Mamilioni ya viumbe wa roho wanaomtumikia Mungu kwa uaminifu wanaitwa “elfu kumi za watakatifu.” (Kumbukumbu la Torati 33:2, Zaire Swahili Bible; Yuda 14) Wanadhihirisha kikamilifu uangavu, na uzuri wa utakatifu wa Mungu. Kumbuka maserafi ambao Isaya aliona katika ono. Maneno ya wimbo wao yanadokeza kwamba viumbe hao wa roho wenye nguvu wanatimiza fungu muhimu sana katika kutangaza utakatifu wa Yehova kotekote ulimwenguni. Hata hivyo, kuna kiumbe mmoja wa roho aliye juu ya wote—Mwana mzaliwa pekee wa Mungu. Yesu anadhihirisha utakatifu wa Yehova kwa kiwango cha juu zaidi. Anaitwa kwa kufaa, “Mtakatifu wa Mungu.”—Yohana 6:68, 69.

Jina Takatifu, Roho Takatifu

12, 13. (a) Kwa nini jina la Mungu linaelezwa kwa kufaa kuwa takatifu? (b) Kwa nini ni lazima jina la Mungu litakaswe?

12 Vipi jina la Mungu? Kama tulivyoona kwenye Sura ya Kwanza, hilo si jina la cheo tu au kitambulisho. Linamwakilisha Yehova Mungu na sifa zake zote. Ndiyo sababu Biblia inatuambia kuwa “jina lake ni takatifu.” (Isaya 57:15, NW) Kulingana na Sheria ya Musa, mtu yeyote aliyelikufuru jina la Mungu aliuawa. (Mambo ya Walawi 24:16) Hebu ona jambo ambalo Yesu alitaja kwanza katika sala: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Kutakasa kitu kwamaanisha kukitenga kuwa kitakatifu na kukistahi. Lakini kwa nini jina la Mungu ambalo ni takatifu kabisa linahitaji kutakaswa?

13 Jina takatifu la Mungu limechambuliwa na kuchafuliwa kwa uwongo na uchongezi. Katika Edeni, Shetani alisema uwongo kumhusu Yehova na akadokeza kwamba Yeye ni Mtawala asiye na haki. (Mwanzo 3:1-5) Tangu hapo, Shetani—mtawala wa ulimwengu huu usio mtakatifu—amehakikisha kwamba uwongo kumhusu Mungu umesambazwa kote. (Yohana 8:44; 12:31; Ufunuo 12:9) Dini zimefundisha kwamba Mungu ni mdhalimu, hana hisia, au ni mkatili. Wamedai kwamba Mungu anaunga mkono vita vyao vya kikatili. Mara nyingi wamesema kwamba uumbaji wa Mungu wa kustaajabisha ulijitokeza wenyewe, au viumbe viligeuka-geuka. Naam, jina la Mungu limechafuliwa vibaya sana. Ni lazima litakaswe; na kurudishiwa tena utukufu unaostahili. Tuna hamu ya kuona jina lake likitakaswa na enzi yake kuu ikitetewa, nasi tunafurahi kushiriki kutimiza kusudi hilo tukufu.

14. Kwa nini roho ya Mungu inaitwa takatifu, na kwa nini kukufuru roho takatifu ni dhambi nzito?

14 Kuna kitu kingine ambacho kinahusiana sana na Yehova ambacho daima kinaitwa kitakatifu—roho yake, au kani yake ya utendaji. (Mwanzo 1:2) Yehova hutumia kani yake isiyoweza kushindwa kutimiza makusudi yake. Matendo yote ya Mungu ni Matakatifu na safi, kwa hiyo kani yake ya utendaji inaitwa kwa kufaa roho takatifu, au roho ya utakatifu. (Luka 11:13; Waroma 1:4) Kukufuru roho takatifu, yaani kupinga makusudi ya Yehova kwa kudhamiria, ni dhambi isiyoweza kusamehewa.—Marko 3:29.

Kwa Nini Utakatifu wa Mungu Unatufanya Tumkaribie?

15. Kwa nini inafaa kumhofu Yehova kwa sababu ya utakatifu wake, na hofu hiyo yahusisha nini?

15 Basi si vigumu kuelewa kwa nini Biblia inahusianisha utakatifu wa Mungu na hali ya mwanadamu ya kumhofu. Kwa mfano, Zaburi 99:3 husema hivi: “Na walishukuru jina lake kuu la kuhofiwa; ndiye mtakatifu.” Lakini hofu hiyo si woga wa kupatwa na mabaya. Badala yake, ni kuwa na kicho na heshima sana, staha ya hali ya juu sana. Inafaa kuhisi hivyo, kwa sababu hatuwezi kamwe kufikia utakatifu wa Mungu. Umetakata sana na ni wenye utukufu. Hata hivyo, haupaswi kutuzuia kumkaribia. Kinyume chake, tukiwa na maoni yanayofaa kuhusu utakatifu wa Mungu tutaweza kumkaribia zaidi. Kwa nini?

Utakatifu unapaswa kutuvutia kama uzuri unavyotuvutia

16. (a) Utakatifu unahusianaje na uzuri? Toa mfano. (b) Maono kumhusu Yehova yanakaziaje usafi, utakato na nuru?

16 Kwanza, Biblia huhusianisha utakatifu na uzuri. Kwenye Isaya 63:15, NW, mbingu inasemwa kuwa ‘makao matukufu ya Mungu ya utakatifu na uzuri.’ Uzuri hutuvutia. Kwa mfano, tazama picha iliyo kwenye ukurasa wa 33. Je, mandhari hiyo haikuvutii? Kwa nini inavutia? Hebu tazama jinsi maji yalivyo safi. Bila shaka, hewa pia ni safi, kwa kuwa anga lina rangi ya buluu na ni kana kwamba nuru inang’aa. Endapo mandhari hiyo ingebadilishwa—kijito kijazwe takataka, miti na miamba ichafuliwe kwa maandishi, hewa ijae moshi—haingetuvutia tena; ingetuchukiza. Kwa kawaida sisi huhusianisha uzuri na usafi, utakato, na nuru. Maneno hayohayo yanaweza kutumiwa kufafanua utakatifu wa Yehova. Si ajabu kwamba maono kumhusu Yehova yanatusisimua! Uzuri wa Mungu wetu mtakatifu ni kama nuru inayong’aa, unametameta kama vito, unawaka kama moto au madini safi yenye thamani ambayo yanang’aa.—Ezekieli 1:25-28; Ufunuo 4:2, 3.

17, 18. (a) Mwanzoni Isaya aliathiriwaje na ono alilopata? (b) Yehova alimtumiaje serafi ili kumfariji Isaya, na jambo alilotenda serafi huyo lilikuwa na maana gani?

17 Lakini je, tunapaswa kujihisi kuwa duni kwa sababu ya utakatifu wa Mungu? Bila shaka, jibu ni ndiyo. Vyovyote iwavyo, sisi ni duni tunapojilinganisha na Yehova—sisi ni duni sana isivyoelezeka. Je, kujua hivyo kwapasa kutufanya tujitenge naye? Fikiria itikio la Isaya aliposikia maserafi wakitangaza utakatifu wa Yehova. “Ndipo niliposema, Ole wangu! kwa maana nimepotea; kwa sababu mimi ni mtu mwenye midomo michafu, nami ninakaa kati ya watu wenye midomo michafu; na macho yangu yamemwona Mfalme, BWANA wa majeshi.” (Isaya 6:5) Ndiyo, utakatifu wa Yehova usio na kikomo ulimkumbusha Isaya kwamba yeye ni mwenye dhambi na mtu asiyekamilika. Mwanzoni, mwanamume huyo mwaminifu alifadhaika sana. Lakini Yehova hakumwacha akiwa katika hali hiyo.

18 Serafi alimfariji nabii huyo mara moja. Jinsi gani? Kiumbe huyo wa roho mwenye nguvu alipaa kwenye madhabahu, akatwaa kaa la moto, akagusa kinywa cha Isaya kwa kaa hilo. Huenda hilo likaonekana kuwa jambo lenye kuumiza sana badala ya kufariji. Hata hivyo, kumbuka kwamba hilo lilikuwa ono lenye maana nyingi ya mfano. Isaya, Myahudi mwaminifu, alijua vyema kwamba dhabihu zilitolewa kila siku kwenye madhabahu ya hekalu ili kulipia dhambi. Na kwa upendo, serafi huyo alimkumbusha nabii huyo kwamba ijapokuwa alikuwa “mtu mwenye midomo michafu” asiyekamilika, bado angeweza kuwa mwadilifu machoni pa Mungu. * Yehova alikuwa tayari kumwona mwanadamu asiyekamilika, na mwenye dhambi kuwa mtakatifu—angalau kwa kadiri fulani.—Isaya 6:6, 7.

19. Tunawezaje kuwa watakatifu kwa kadiri fulani, ijapokuwa hatujakamilika?

19 Ndivyo ilivyo leo. Dhabihu zote zilizotolewa kwenye madhabahu huko Yerusalemu zilikuwa kivuli tu cha kitu fulani kikubwa zaidi—dhabihu pekee iliyokuwa kamilifu, iliyotolewa na Yesu Kristo mwaka wa 33.W.K. (Waebrania 9:11-14) Tukitubu dhambi zetu kikweli, na kurekebisha mwenendo wetu mbaya, na kudhihirisha imani katika dhabihu hiyo, tunapata msamaha. (1 Yohana 2:2) Sisi pia tunaweza kuwa waadilifu machoni pa Mungu. Kwa hiyo, mtume Petro anatukumbusha hivi: “Imeandikwa: ‘Lazima mwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” (1 Petro 1:16) Ona kwamba Yehova hakusema lazima tuwe watakatifu kwa kadiri ambayo yeye ni mtakatifu. Yeye hatarajii kamwe tutimize mambo tusiyoweza. (Zaburi 103:13, 14) Badala yake, Yehova anatuambia tuwe watakatifu kwa sababu yeye ni mtakatifu. ‘Tukiwa watoto wapendwa,’ tunajitahidi kumwiga kadiri tuwezavyo tukiwa wanadamu wasiokamilika. (Waefeso 5:1) Kwa hiyo, kuwa watakatifu ni jitihada inayoendelea. Kadiri tunavyokua kiroho, tunajitahidi ‘kukamilisha utakatifu’ siku baada ya siku.—2 Wakorintho 7:1.

20. (a) Kwa nini ni muhimu kufahamu kwamba tunaweza kuwa safi machoni pa Mungu wetu mtakatifu? (b) Isaya alihisije alipojua kwamba dhambi zake zilikuwa zimefunikwa?

20 Yehova, anapenda mambo ya uadilifu na yaliyo safi. Anachukia dhambi. (Habakuki 1:13) Lakini yeye hatuchukii. Maadamu tuna maoni kama yake juu ya dhambi—tukichukia lililo baya, na kupenda lililo jema—na tunajitahidi kufuata hatua kamilifu za Kristo Yesu, Yehova husamehe dhambi zetu. (Amosi 5:15; 1 Petro 2:21) Tunapofahamu kwamba tunaweza kuwa safi machoni pa Mungu wetu mtakatifu, matokeo yanaweza kuwa mazuri ajabu. Kumbuka kwamba, mwanzoni utakatifu wa Yehova ulimkumbusha Isaya kwamba hakuwa safi. Alipaaza kilio: “Ole wangu!” Lakini mara tu alipojua kwamba dhambi zake zilikuwa zimefunikwa, mtazamo wake ulibadilika. Yehova alipokuwa akitafuta mtu ambaye angejitolea kutimiza kazi fulani, Isaya aliitikia mara moja, japo hakujua kazi hiyo ilihusisha nini. Alisema hivi kwa shauku: “Mimi hapa, nitume mimi.”—Isaya 6:5-8.

21. Tuna uhakika gani kwamba tunaweza kusitawisha sifa ya utakatifu?

21 Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu wetu mtakatifu, tumepewa sifa za adili na uwezo wa kuelewa mambo ya kiroho. (Mwanzo 1:26) Tunaweza sote kuwa watakatifu. Yehova anafurahi kutusaidia kuendelea kuusitawisha utakatifu. Tufanyapo hivyo, tutamkaribia zaidi Mungu wetu mtakatifu. Zaidi ya hayo, tunapozungumzia sifa za Yehova katika sura zinazofuata, tutaona kwamba kuna sababu nyingi nzuri za kumkaribia!

^ fu. 18 Maneno “mwenye midomo michafu” yanafaa, kwa kuwa midomo mara nyingi hutumiwa kitamathali katika Biblia kurejezea usemi au lugha. Sehemu kubwa ya dhambi za wanadamu wote wasiokamilika, yamkini zinahusiana na jinsi tunavyotumia uwezo wetu wa kusema.—Mithali 10:19; Yakobo 3:2, 6.