Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 4

“Mwenyezi-Mungu . . . Amejaa Nguvu”

“Mwenyezi-Mungu . . . Amejaa Nguvu”

1, 2. Eliya alikuwa ameona mambo gani ya ajabu maishani mwake, lakini aliona matukio gani ya kustaajabisha alipokuwa katika pango kwenye Mlima Horebu?

ELIYA alikuwa ameona mambo ya ajabu hapo awali. Alikuwa ameona kunguru wakimletea chakula mara mbili kwa siku alipokuwa mafichoni. Alikuwa ameona unga na mafuta yaliyokuwa katika vyombo viwili yakitumiwa kwa muda mrefu sana wakati wa njaa kali. Hata alikuwa ameona moto ukishuka kutoka mbinguni baada ya kutoa sala. (1 Wafalme, sura ya 17, 18) Na bado, Eliya hakupata kuona tukio lolote la kustaajabisha kama matukio yafuatayo.

2 Eliya aliyejikunyata kwenye mwingilio wa pango kwenye Mlima Horebu aliona mfululizo wa matukio yenye kustaajabisha. Kwanza upepo ulivuma. Haikosi ulivuma kwa nguvu sana, na kwa sauti kubwa sana kwa kuwa uliipasua milima na kuvunja-vunja miamba. Kisha kukawa na tetemeko la nchi, nishati kubwa sana iliibuka na kutikisa dunia kwa nguvu sana. Halafu kukawa na moto. Yaelekea Eliya alipigwa na joto kali sana moto huo uliposambaa kwenye eneo hilo.—1 Wafalme 19:8-12.

“Na tazama, BWANA akapita”

3. Eliya aliona uthibitisho wa sifa ipi ya Mungu, nasi tuna uthibitisho gani wa sifa hiyo?

3 Matukio hayo mbalimbali ambayo Eliya aliona yalikazia jambo moja tu—yalidhihirisha nguvu nyingi za Yehova Mungu. Bila shaka, si lazima tuone muujiza ili tufahamu kwamba Mungu ana sifa hii. Sifa hii yaonekana waziwazi. Biblia yatuambia kwamba uumbaji unathibitisha ‘nguvu za Yehova za milele na Uungu’ wake. (Waroma 1:20) Hebu fikiria nuru yenye kupofusha na ngurumo za dhoruba ya radi, poromoko kubwa maridadi la maji, na anga pana kupindukia lililotapakaa nyota! Je, unaona nguvu za Mungu katika vitu hivyo? Lakini ni watu wachache tu ulimwenguni wanaotambua kikweli nguvu za Mungu. Na ni watu wachache hata zaidi walio na maoni yanayofaa kuhusu nguvu hizo. Hata hivyo, kufahamu sifa hii ya Mungu kunatupa sababu nyingi za kumkaribia Yehova zaidi. Katika sehemu hii, tutajifunza kwa undani kuhusu nguvu za Yehova zisizo na kifani.

Sifa Muhimu ya Yehova

4, 5. (a) Kuna uhusiano gani kati ya jina la Yehova na uwezo wake, au nguvu zake? (b) Kwa nini inafaa kwamba Yehova alitumia fahali kuwakilisha nguvu zake?

4 Nguvu za Yehova hazina kifani. Andiko la Yeremia 10:6 lasema hivi: “Hapana hata mmoja aliye kama wewe, Ee BWANA; wewe ndiwe uliye mkuu, na jina lako ni kuu katika uweza.” Ona kwamba uweza, au nguvu, zinahusianishwa na jina la Yehova. Ni wazi kwamba jina hilo linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwe.” Ni nini kinachomwezesha Yehova aumbe kitu chochote anachotaka na awe chochote anachotaka? Sababu moja ni nguvu zake. Naam, uwezo wa Yehova wa kutenda, na wa kutimiza mapenzi yake hauna mipaka. Nguvu hizo ni mojawapo ya sifa zake muhimu.

5 Hatuwezi kamwe kufahamu nguvu kamili za Yehova, kwa hivyo yeye hutumia mifano ili kutusaidia. Kama tulivyoona, yeye hutumia fahali kuwakilisha nguvu zake. (Ezekieli 1:4-10) Mfano huo unafaa, kwa sababu hata fahali wa kufugwa ni kiumbe mkubwa na mwenye nguvu. Katika nyakati za Biblia, ilikuwa vigumu sana kwa wakazi wa Palestina kukutana na mnyama yeyote mwenye nguvu kuliko fahali. Lakini walimjua fahali mwingine mwenye kutisha zaidi—fahali-mwitu, au auroch, ambaye ametoweka kabisa sasa. (Ayubu 39:9-12) Maliki Mroma Yulio Kaisari alisema wakati mmoja kwamba fahali hao walikuwa na ukubwa unaokaribia wa ndovu. “Wana nguvu nyingi sana, na wanakimbia kasi sana,” akaandika. Hebu wazia jinsi ungehisi dhaifu na mdogo mno kama ungesimama karibu na kiumbe huyo!

6. Kwa nini ni Yehova peke yake anayeitwa “Mweza-Yote”?

6 Vivyo hivyo, mwanadamu ni duni na dhaifu sana anapolinganishwa na Mungu mwenye nguvu, Yehova. Yehova huona mataifa yenye nguvu kama mavumbi membamba katika mizani. (Isaya 40:15) Yehova ana nguvu zisizo na mipaka, yeye si kama viumbe, kwa kuwa yeye peke yake ndiye anayeitwa “Mweza-Yote.” * (Ufunuo 15:3) Yehova ni “hodari kwa nguvu zake.” (Isaya 40:26) Yeye ni chanzo cha kudumu cha nguvu maridhawa. Hategemei nishati kutoka kwa chanzo kingine chochote, kwa kuwa “nguvu ni mali ya Mungu.” (Zaburi 62:11, NW) Lakini Yehova hutumiaje nguvu zake?

Jinsi Yehova Anavyotumia Nguvu Zake

7. Roho takatifu ya Yehova ni nini, na maneno ya lugha ya awali yanayotumiwa katika Biblia yanadokeza nini?

7 Roho takatifu humiminika kutoka kwa Yehova kwa wingi sana, ni nguvu yake inayotenda kazi. Kwa kweli, kwenye Mwanzo 1:2, (NW) Biblia hurejezea roho hiyo kuwa “nguvu ya Mungu ya utendaji.” Maneno ya awali ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa “roho” huenda nyakati nyingine, yakatafsiriwa “upepo,” “pumzi,” na “mkumbo wa hewa.” Watungaji wa kamusi wanasema kwamba maneno ya lugha ya awali yanadokeza nguvu isiyoonekana inayotenda kazi. Hatuwezi kuona roho ya Mungu kama tusivyoweza kuona upepo, lakini tunaweza kuona na kutambua matokeo yake.

8. Biblia hufananisha roho ya Mungu na nini, na kwa nini ufananisho huo mbalimbali unafaa?

8 Roho takatifu ya Mungu inaweza kutimiza mambo mengi sana. Yehova anaweza kuitumia kutimiza kusudi lolote alilo nalo. Ndiyo sababu Biblia hufananisha roho ya Mungu na viungo kama vile “kidole,” ‘mkono wenye nguvu,’ au ‘mkono ulionyoshwa.’ (Luka 11:20; Kumbukumbu la Torati 5:15; Zaburi 8:3) Kama vile tu mwanadamu anavyoweza kutumia mikono yake kufanya kazi mbalimbali zinazohitaji nguvu au uwezo mbalimbali, ndivyo Mungu anavyoweza kutumia roho yake kutimiza kusudi lolote lile—kama vile kuumba atomu ndogo sana au kugawanya Bahari Nyekundu au kuwawezesha Wakristo wa karne ya kwanza kuongea kwa lugha za kigeni.

9. Nguvu za Yehova za kutawala ni nyingi kadiri gani?

9 Yehova pia hudhihirisha nguvu zake kupitia mamlaka yake akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Je, waweza kuwazia ukiwa na mamilioni ya mamilioni ya viumbe wenye akili na uwezo, walio tayari kutekeleza amri yako? Yehova ana nguvu hizo za utawala. Ana wanadamu wanaomtumikia, ambao mara nyingi Maandiko huwafananisha na jeshi. (Zaburi 68:11; 110:3) Hata hivyo, mwanadamu ni kiumbe dhaifu sana anapolinganishwa na malaika. Kwani, wakati jeshi la Ashuri liliposhambulia watu wa Mungu, malaika mmoja tu aliua wanajeshi 185,000 wa Ashuri katika usiku mmoja! (2 Wafalme 19:35) Malaika wa Mungu wana “uwezo kwa nguvu.”—Zaburi 103:19, 20, ZSB.

10. (a) Kwa nini Mweza-Yote anaitwa Yehova wa majeshi? (b) Ni kiumbe yupi aliye na uwezo zaidi ya viumbe wote wa Yehova?

10 Kuna malaika wangapi? Nabii Danieli alipata ono la mbinguni ambapo aliona viumbe wa roho zaidi ya milioni 100 wakiwa mbele ya kiti cha enzi cha Yehova, lakini hakuna uthibitisho wa kwamba aliona malaika wote ambao Yehova alikuwa ameumba. (Danieli 7:10) Kwa hivyo, huenda kukawa na mamia ya mamilioni ya malaika. Ndiyo sababu Mungu anaitwa Yehova wa majeshi. Cheo hicho kinaonyesha wadhifa wake mkubwa akiwa Amiri wa kikosi kikubwa kilichopangwa cha malaika wenye nguvu. Amemweka Mwanaye mpendwa, “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote,” kusimamia viumbe hao wote wa roho. (Wakolosai 1:15) Akiwa malaika-mkuu—mkuu wa malaika, maserafi, na makerubi wote—Yesu ndiye kiumbe mwenye uwezo zaidi ya viumbe wote wa Yehova.

11, 12. (a) Neno la Mungu hukaziaje nguvu? (b) Yesu alisema nini kuhusu nguvu za Yehova?

11 Yehova hudhihirisha nguvu zake kwa njia nyingine pia. Andiko la Waebrania 4:12 lasema: “Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu.” Je, umeona nguvu za ajabu za neno la Mungu, au za ujumbe uliopuliziwa na roho, ambao sasa umehifadhiwa katika Biblia? Unaweza kutuimarisha, kujenga imani yetu, na kutusaidia kufanya mabadiliko makubwa maishani mwetu. Mtume Paulo aliwaonya waamini wenzake wajiepushe na watu walioishi maisha mapotovu. Halafu akasema: “Hata hivyo baadhi yenu ndivyo mlivyokuwa.” (1 Wakorintho 6:9-11) Naam, “neno la Mungu” lilikuwa na nguvu maishani mwao na liliwasaidia kubadilika.

12 Yehova ana nguvu nyingi sana naye huzitumia kwa matokeo hivi kwamba hakuna kitu kinachoweza kumzuia. Yesu alisema hivi: “Kwa Mungu mambo yote yawezekana.” (Mathayo 19:26) Yehova hutumia nguvu zake kutimiza makusudi yapi?

Anatumia Nguvu Zake Kupatana na Makusudi Yake

13, 14. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova si chanzo cha nguvu kisicho na utu? (b) Yehova anatumia nguvu zake kwa njia zipi?

13 Roho ya Yehova ni bora kuliko kani yoyote ile; na Yehova si kani tu isiyo na utu, chanzo tu cha nguvu. Yeye ni Mungu mwenye utu ambaye anadhibiti nguvu zake kikamili. Lakini ni nini kinachomchochea azitumie?

14 Kama tutakavyoona, Mungu hutumia nguvu zake kuumba, kuharibu, kulinda, au kuhuisha—kwa ufupi, yeye huzitumia kufanya jambo lolote linalofaa makusudi yake makamilifu. (Isaya 46:10) Pindi fulani-fulani, Yehova hutumia nguvu zake kufunua sifa na sheria zake muhimu. Na zaidi ya yote, anatumia nguvu zake kutimiza mapenzi yake—kutetea enzi yake kuu na kutakasa jina lake takatifu kupitia Ufalme wa Kimesiya. Hakuna kitu chochote kinachoweza kuzuia kusudi hilo.

15. Yehova hutumia nguvu zake kwa kusudi gani kuhusiana na watumishi wake, na hali iliyompata Eliya inathibitishaje jambo hilo?

15 Yehova hutumia pia nguvu zake kutusaidia tukiwa mtu mmoja-mmoja. Hebu angalia andiko la 2 Mambo ya Nyakati 16:9 linavyosema: “Kwa maana macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.” Kisa cha Eliya kilichotajwa mwanzoni ni mfano unaofaa. Kwa nini Yehova alimwonyesha tukio hilo la kustaajabisha la nguvu Zake? Malkia mwovu Yezebeli alikuwa ameapa kumwua Eliya. Nabii huyo alitoroka ili asiuawe. Alihisi upweke, aliogopa, na alikuwa amevunjika moyo—kana kwamba kazi yake yote ilikuwa ya bure. Yehova alimfariji Eliya aliyekuwa taabani kwa kumkumbusha waziwazi kuhusu nguvu Zake. Upepo, tetemeko la nchi, na moto vilionyesha kwamba Mungu mwenye nguvu zaidi katika ulimwengu wote alikuwa pamoja na Eliya. Kwa nini amhofu Yezebeli huku Yehova akiwa upande wake?—1 Wafalme 19:1-12. *

16. Kwa nini tunaweza kupata faraja kwa kutafakari juu ya nguvu nyingi za Yehova?

16 Ijapokuwa huu si wakati wa Yehova wa kufanya miujiza, yeye hajabadilika tangu siku za Eliya. (1 Wakorintho 13:8) Yeye angali na hamu ileile ya kutumia nguvu zake kwa niaba ya wale wanaompenda. Ni kweli kwamba anaishi katika makao matukufu ya roho, lakini hayuko mbali nasi. Nguvu zake hazina mipaka, kwa hiyo umbali si kizuizi. Badala yake, “BWANA yu karibu na wote wamwitao.” (Zaburi 145:18) Pindi moja wakati nabii Danieli alipomwomba Yehova msaada, malaika alifika alipokuwa angali anasali! (Danieli 9:20-23) Hakuna kitu kinachoweza kumzuia Yehova kuwasaidia na kuwaimarisha wale anaowapenda.—Zaburi 118:6.

Je, Nguvu za Mungu Hutuzuia Tusimkaribie?

17. Nguvu za Yehova hututiaje woga, lakini huo si woga wa aina gani?

17 Je, tunapaswa kumwogopa Mungu kwa sababu ya nguvu zake? Ni lazima tujibu ndiyo na la. Ndiyo, kwa sababu sifa hii hutupatia sababu nzuri ya kumwogopa Mungu, kuwa na kicho na staha ya hali ya juu ambayo tulizungumzia kwa ufupi katika sura iliyotangulia. Biblia inatuambia kwamba woga huo ni “mwanzo wa hekima.” (Zaburi 111:10) Hata hivyo, twajibu la kwa sababu nguvu za Mungu hazifanyi tuwe na woga usiofaa au tuhofu kumkaribia.

18. (a) Kwa nini watu wengi hukosa kuwatumaini wenye mamlaka? (b) Twajuaje kwamba Yehova hawezi kufisidiwa na mamlaka yake?

18 “Mamlaka hufisidi; na mamlaka kamili hufisidi kikamili.” Ndivyo alivyoandika mwanahistoria Mwingereza Bwana Acton mnamo mwaka wa 1887. Maneno yake yamerudiwa mara nyingi, na huenda ni kwa sababu watu wengi huyaona kuwa ya kweli kabisa. Mara nyingi, wanadamu wasiokamilika hutumia vibaya mamlaka waliyo nayo, jambo hilo limethibitishwa na historia tena na tena. (Mhubiri 4:1; 8:9) Ndiyo sababu watu wengi hukosa kuwatumaini na huwaepuka wenye mamlaka. Yehova ana mamlaka kamili. Je, mamlaka hayo yamemfisidi kwa njia yoyote? Bila shaka la! Kama tulivyoona, yeye ni mtakatifu, hawezi kamwe kufisidiwa. Yehova si kama wanaume na wanawake wasiokamilika wenye mamlaka katika ulimwengu huu wenye ufisadi. Hajawahi kutumia vibaya mamlaka yake na hatafanya hivyo kamwe.

19, 20. (a) Sikuzote Yehova hutumia nguvu zake kwa kupatana na sifa gani nyingine, na kwa nini hilo linafariji? (b) Simulia mfano ambao unaonyesha jinsi Yehova anavyojidhibiti, na kwa nini hilo linakuvutia?

19 Kumbuka kwamba Yehova ana sifa nyingine mbali na nguvu. Baadaye tutajifunza kuhusu haki yake, hekima yake, na upendo wake. Lakini hatupaswi kudhani kwamba Yehova hudhihirisha sifa zake bila hisia wala ufikirio, kana kwamba anadhihirisha sifa moja tu kwa wakati mmoja. Kinyume chake, tutaona katika sura zijazo kwamba sikuzote Yehova hutumia nguvu zake kwa kupatana na haki yake, hekima yake, na upendo wake. Fikiria sifa nyingine ya Mungu, sifa ambayo watawala wengi leo ulimwenguni hawana—kujidhibiti.

20 Wazia kama ungekutana na mtu mkubwa mno mwenye nguvu nyingi, anayetisha. Lakini baada ya muda, unagundua kwamba yeye ni mpole. Yuko tayari kila wakati kutumia nguvu zake kuwasaidia na kuwalinda watu, hasa wale walio dhaifu na wanyonge. Hatumii vibaya kamwe nguvu zake. Waona akichongewa bila sababu, lakini yeye ni thabiti na mtulivu, ana staha na hata ni mwenye fadhili. Washangaa iwapo ungebaki mpole na kujidhibiti endapo ungekuwa na nguvu kama mwanamume huyo! Kadiri unavyomjua mwanamume huyo, je, hungetaka kuwa karibu naye? Tuna sababu nzuri sana za kumkaribia Yehova aliye mweza-yote. Hebu angalia mstari ambao ni msingi wa kichwa kikuu cha sura hii: “Mwenyezi-Mungu hakasiriki upesi, lakini amejaa nguvu.” (Nahumu 1:3, BHN) Yehova hatumii nguvu zake haraka-haraka kuwaadhibu watu, hata watu waovu. Yeye ni mpole na mwenye fadhili. Amethibitika kuwa ‘asiyekasirika upesi’ ajapochukizwa mara nyingi.—Zaburi 78:37-41.

21. Kwa nini Yehova hawalazimishi watu kufanya mapenzi yake, na hilo latufundisha nini kumhusu?

21 Fikiria kujidhibiti kwa Yehova kwa njia nyingine. Kama ungekuwa na nguvu zisizo na mipaka, je, wafikiri kwamba nyakati nyingine, ungekuwa na mwelekeo wa kuwalazimisha watu wafanye mambo jinsi unavyotaka? Licha ya nguvu nyingi alizo nazo, Yehova hawalazimishi kamwe watu wamtumikie. Hata ingawa kumtumikia Mungu ndiyo njia pekee ya kupata uhai udumuo milele, Yehova hatulazimishi kumtumikia. Badala yake, kwa fadhili yeye humstahi kila mtu kwa kumpa uhuru wa kuchagua. Anaonya kuhusu matokeo ya kufanya uchaguzi usiofaa na kutuambia faida za kufanya uchaguzi mzuri. Lakini anaturuhusu kufanya uchaguzi wetu binafsi. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Yehova hataki kamwe watu wamtumikie kwa kulazimishwa au kwa sababu wanahofu isivyofaa nguvu zake za kutisha. Anatafuta watu watakaomtumikia kwa hiari, kwa sababu wanampenda.—2 Wakorintho 9:7.

22, 23. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova hufurahia kuwapa wengine mamlaka? (b) Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?

22 Na tuchunguze sababu ya mwisho inayotufanya tusiwe na woga usiofaa kumwelekea Mungu Mweza-Yote. Wanadamu wenye uwezo huogopa kuwapa wengine mamlaka. Lakini Yehova hufurahia kuwapa waabudu wake waaminifu mamlaka. Yeye huwapa wengine mamlaka kubwa, kama vile Mwanaye. (Mathayo 28:18) Yehova pia huwapa watumishi wake uwezo kwa njia nyingine. Biblia yaeleza: “Ee BWANA, ukuu ni wako, na uweza, na utukufu, na kushinda, na enzi; maana vitu vyote vilivyo mbinguni na duniani ni vyako. . . . Mkononi mwako mna uweza na nguvu; tena mkononi mwako mna kuwatukuza na kuwawezesha wote.”—1 Mambo ya Nyakati 29:11, 12.

23 Ndiyo, Yehova atafurahi kukuimarisha. Yeye hata huwapa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” wale wanaotaka kumtumikia. (2 Wakorintho 4:7) Je, huvutiwi kumkaribia Mungu huyo mwenye nguvu sana, ambaye anatumia nguvu zake kwa fadhili na kupatana na kanuni za juu za maadili? Katika sura inayofuata, tutazungumzia jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake za kuumba.

^ fu. 6 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “Mweza-Yote” humaanisha kihalisi “Mtawala Juu ya Wote; Yule Aliye na Nguvu Zote.”

^ fu. 15 Biblia inasema kwamba “BWANA hakuwamo katika upepo ule . . . , tetemeko la nchi . . . , moto ule.” Tofauti na wale wanaoabudu miungu ya kihekaya ya nguvu za asili, watumishi wa Yehova hawamtafuti katika nguvu za maumbile. Yeye ni mkuu sana hivi kwamba hawezi kuishi katika kitu chochote alichoumba.—1 Wafalme 8:27.