Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 10

“Iweni Waigaji wa Mungu” Mnapotumia Uwezo

“Iweni Waigaji wa Mungu” Mnapotumia Uwezo

1. Wanadamu wasiokamilika hutumbukia kwa urahisi katika mtego gani?

“PALIPO na uwezo hapakosi mtego.” Maneno hayo yaliyosemwa na mtungaji-mashairi wa karne ya 19 yanaonyesha hatari ya kutumia uwezo vibaya. Inasikitisha kwamba wanadamu wasiokamilika hutumbukia kwa urahisi katika mtego huo. Kwa kweli, katika muda wote wa historia ya mwanadamu, ‘mtu mmoja amekuwa na mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9) Wanadamu wameteseka sana kwa sababu ya kutawaliwa na watawala wasio na upendo.

2, 3. (a) Ni nini kinachostaajabisha kuhusu jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake? (b) Twaweza kuwa na uwezo gani, nasi twapaswa kutumiaje uwezo huo wote?

2 Hata hivyo, je, haistaajabishi kwamba Yehova Mungu hatumii kamwe vibaya nguvu zake zisizo na mipaka? Kama tulivyoona kwenye sura zilizotangulia, sikuzote yeye hutumia nguvu zake kupatana na makusudi yake ya upendo, iwe ni nguvu za uumbaji, za kuharibu, kulinda, au za kufanya hali upya. Tunapotafakari jinsi anavyotumia nguvu zake, tunachochewa kumkaribia. Na hilo linatutia moyo ‘tumwige Mungu’ tunapotumia uwezo tulio nao. (Waefeso 5:1) Lakini sisi wanadamu duni tuna uwezo gani?

3 Kumbuka kwamba mwanadamu aliumbwa kwa sura na “mfano wa Mungu.” (Mwanzo 1:26, 27) Hivyo basi, hata sisi tuna uwezo, angalau kwa kadiri fulani. Twaweza kutimiza mambo kwa kufanya kazi; kuwa na mamlaka juu ya wengine; kuwa na uvutano juu ya wengine, hasa wale wanaotupenda; pia tunaweza kuwa na nguvu ya kimwili; au uwezo wa kifedha. Mtunga-zaburi alisema hivi kumhusu Yehova: “Wewe ndiwe asili ya uhai.” (Zaburi 36:9, BHN) Kwa hiyo, kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja, Mungu ndiye chanzo cha uwezo wowote ufaao ambao huenda tukawa nao. Kwa hiyo, tunataka kutumia uwezo wetu katika njia zinazompendeza. Tutafanyaje hivyo?

Upendo Ni Muhimu

4, 5. (a) Tunahitaji sifa gani muhimu ili kutumia uwezo kwa njia ifaayo, na kielelezo cha Mungu kinaonyeshaje hivyo? (b) Upendo utatusaidiaje kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo?

4 Upendo ni muhimu ili kutumia uwezo kwa njia ifaayo. Je, kielelezo cha Mungu hakionyeshi hivyo? Kumbuka Sura ya 1 iliyozungumzia sifa nne kuu za Mungu, yaani, nguvu, haki, hekima na upendo. Kati ya sifa hizo nne ni ipi iliyo kuu zaidi? Upendo. Andiko la 1 Yohana 4:8 lasema kwamba “Mungu ni upendo.” Naam, upendo ni utu wa Yehova; unamwongoza katika kila jambo analotenda. Kwa hiyo, kila jambo analotenda kwa nguvu zake linachochewa na upendo na mwishowe huwafaidi wale wanaompenda.

5 Upendo utatusaidia pia kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo. Kwani, Biblia hutuambia kwamba upendo ni “wenye fadhili” na “hautafuti masilahi yao wenyewe.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Kwa hiyo, tukiwa na upendo hatutakuwa wakali au wakatili kwa wale walio chini ya mamlaka yetu. Badala yake, tutawatendea wengine kwa staha na kutanguliza mahitaji na hisia zao wala si zetu.—Wafilipi 2:3, 4.

6, 7. (a) Kumhofu Mungu kwamaanisha nini, na sifa hiyo itatusaidiaje kuepuka kutumia uwezo vibaya? (b) Simulia mfano ambao unaonyesha uhusiano uliopo kati ya kumpenda Mungu na hofu ya kutompendeza.

6 Upendo unahusiana na sifa nyingine ambayo inaweza kutusaidia kuepuka kutumia uwezo wetu vibaya: kumhofu Mungu. Sifa hii ni muhimu jinsi gani? Andiko la Mithali 16:6 lasema: “Kwa kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA watu hujiepusha na maovu.” Bila shaka kutumia uwezo vibaya ni miongoni mwa mambo maovu ambayo tunapaswa kuepuka. Kumhofu Mungu kutatuzuia kuwakandamiza wale walio chini ya mamlaka yetu. Kwa nini? Kwanza, tunajua kwamba tunawajibika kwa Mungu kwa sababu ya jinsi tunavyowatendea wengine. (Nehemia 5:1-7, 15) Lakini kumhofu Mungu kwatia ndani mambo mengi zaidi. Maneno ya lugha ya awali yaliyotafsiriwa “hofu” mara nyingi humaanisha staha nyingi sana na kicho kwa Mungu. Basi, Biblia inaonyesha kwamba hofu inahusiana na kumpenda Mungu. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13) Staha hiyo yenye kicho inatia ndani hofu inayofaa ya kutompendeza Mungu—si kwa sababu tu tunahofu kuadhibiwa bali kwa sababu tunampenda kikweli.

7 Kwa mfano: Fikiria uhusiano mzuri uliopo kati ya mvulana mdogo na baba yake. Mvulana huyo anajua kwamba baba yake anampenda sana naye humtendea kwa fadhili. Lakini anajua pia mambo ambayo baba yake anamtarajia afanye, na anajua kwamba atatiwa nidhamu akikosa adabu. Mvulana huyo hana hofu isiyofaa kumwelekea baba yake. Badala yake, anampenda sana baba yake. Anapenda kufanya mambo ambayo yatamfurahisha baba yake. Ndivyo ilivyo na kumhofu Mungu. Kwa sababu tunampenda Yehova, Baba yetu wa mbinguni, tunaogopa kutenda jambo lolote ambalo ‘litamhuzunisha moyo.’ (Mwanzo 6:6) Badala yake, tunataka sana kuufurahisha moyo wake. (Mithali 27:11) Ndiyo sababu tunataka kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo. Na tuchunguze jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

Katika Familia

8. (a) Waume wana mamlaka gani katika familia, na wanapaswa kuitumiaje? (b) Mume anawezaje kuonyesha kwamba anamheshimu mkewe?

8 Fikiria kwanza familia. Andiko la Waefeso 5:23 lasema kwamba “mume ni kichwa cha mke wake.” Mume anapaswa kutumiaje mamlaka aliyopewa na Mungu? Biblia inawaambia waume wakae na wake zao ‘kulingana na ujuzi, wakiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi.’ (1 Petro 3:7) Nomino ya Kigiriki inayotafsiriwa “heshima” yamaanisha “thamani, ubora, . . . staha.” Neno hilo hutafsiriwa pia “zawadi” na “-enye bei.” (Matendo 28:10; 1 Petro 2:7) Mume anayemheshimu mkewe hawezi kamwe kumpiga; wala hawezi kumwaibisha au kumtukana, na kumfanya ajihisi hafai. Badala yake, anatambua kwamba yeye ni mwenye thamani sana na anamtendea kwa heshima. Anaonyesha kwa maneno na matendo kwamba anamthamini sana mkewe iwe faraghani au mbele ya watu. (Mithali 31:28) Mume kama huyo hupendwa na kuheshimiwa na mkewe, na la muhimu hata zaidi ni kwamba anapata kibali cha Mungu.

Waume na wake wanatumia uwezo wao kwa njia inayofaa kwa kuonyeshana upendo na heshima

9. (a) Wake wana uwezo gani katika familia? (b) Ni nini kinachoweza kumsaidia mke atumie vipawa vyake kumwunga mkono mumewe, na matokeo yatakuwa nini?

9 Wake pia wana uwezo fulani katika familia. Biblia hutaja wanawake fulani waliomhofu Mungu ambao walichukua hatua ya kuwasaidia waume zao kufanya maamuzi yanayofaa, au kuwasaidia kuepuka kufanya maamuzi yasiyofaa bila kudharau ukichwa wao. (Mwanzo 21:9-12; 27:46–28:2) Mke anaweza kuwa na akili nyingi kumshinda mumewe, au anaweza kuwa na vipawa vingine ambavyo mumewe hana. Hata hivyo, anahitaji “kuwa na staha yenye kina kirefu” kwa mume wake na ‘kujitiisha’ kwake “kama kwa Bwana.” (Waefeso 5:22, 33) Mke aliye na lengo la kumpendeza Mungu atatumia vipawa vyake kumwunga mkono mumewe, badala ya kumdharau au kujaribu kumtawala. “Mwanamke mwenye hekima ” kama huyo hushirikiana kabisa na mumewe kujenga familia. Kwa kufanya hivyo anakuwa na amani pamoja na Mungu.—Mithali 14:1, BHN.

10. (a) Mungu amewapa wazazi mamlaka gani? (b) Neno “nidhamu” linamaanisha nini, na inapasa kutolewaje? (Ona pia kielezi-chini.)

10 Wazazi pia wamepewa mamlaka na Mungu. Biblia inashauri hivi: “Akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Katika Biblia, neno “nidhamu” linaweza kumaanisha “malezi, mazoezi, mafundisho.” Watoto wanahitaji nidhamu; wanafurahi na kufanikiwa wanapopewa maagizo yaliyo wazi, na wanapowekewa mipaka na vizuizi. Kulingana na Biblia, nidhamu au mafundisho huhusisha upendo. (Mithali 13:24) Kwa hiyo, “fimbo ya adhabu” haipaswi kamwe kuwaumiza watoto kihisia-moyo au kimwili. * (Mithali 22:15; 29:15) Mzazi anayetoa nidhamu kwa ukali bila upendo anatumia vibaya mamlaka yake. Kufanya hivyo kunaweza kumvunja moyo mtoto. (Wakolosai 3:21) Kwa upande mwingine, kutoa nidhamu kwa usawaziko na kwa njia ifaayo kunawathibitishia watoto kwamba wazazi wanawapenda na wanapendezwa na utu wanaositawisha.

11. Watoto wanawezaje kutumia nguvu zao ifaavyo?

11 Vipi watoto? Wanawezaje kutumia ifaavyo nguvu zao? Mithali 20:29 yasema kwamba “fahari ya vijana ni nguvu zao.” Kwa kweli, hakuna njia nyingine bora zaidi ya vijana kutumia nguvu na nishati yao isipokuwa kumtumikia ‘Muumba wetu Mtukufu.’ (Mhubiri 12:1, NW) Vijana wanapaswa kukumbuka kwamba matendo yao yanaweza kuathiri hisia za wazazi wao. (Mithali 23:24, 25) Watoto wanapotii na kufuata mwenendo unaofaa, wanafurahisha mioyo ya wazazi wao wanaomhofu Mungu. (Waefeso 6:1) Mwenendo huo ‘unapendeza vema katika Bwana.’—Wakolosai 3:20.

Kutanikoni

12, 13. (a) Wazee wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mamlaka yao kutanikoni? (b) Toa mfano ambao unaonyesha umuhimu wa wazee kuwatendea kondoo kwa fadhili.

12 Yehova ameweka waangalizi wa kuongoza kutaniko la Kikristo. (Waebrania 13:17) Wanaume hao wenye sifa za kustahili wanapaswa kutumia mamlaka waliyopewa na Mungu kutoa msaada unaohitajiwa na kulisaidia kutaniko likue kiroho. Je, wazee wana haki ya kupiga ubwana juu ya waamini wenzao kwa sababu ya wadhifa wao? La hasha! Wazee wanahitaji kuwa na usawaziko na unyenyekevu wanapotimiza daraka lao kutanikoni. (1 Petro 5:2, 3) Biblia inawaambia hivi waangalizi: ‘Lichungeni kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.’ (Matendo 20:28) Kwa sababu hiyo, wazee wanapaswa kumtendea kila mshiriki wa kutaniko kwa fadhili.

13 Mfano ufuatao unaonyesha jambo hilo: Rafiki yako mpendwa anakuomba umtunzie mali fulani yenye thamani kubwa. Wajua kwamba mali hiyo ilimgharimu pesa nyingi sana. Je, hutaitunza kwa tahadhari na uangalifu mkubwa mno ili isiharibike? Vivyo hivyo, Mungu amewakabidhi wazee wajibu wa kutunza mali yenye thamani kubwa sana: kutaniko, ambalo washiriki wake wanalinganishwa na kondoo. (Yohana 21:16, 17) Yehova anapenda sana kondoo wake—anawapenda kiasi cha kwamba aliwanunua kwa damu yenye thamani ya Mwana wake mzaliwa-pekee, Yesu Kristo. Yehova aliwanunua kondoo wake kwa bei ya juu sana. Wazee wanyenyekevu hukumbuka jambo hilo na kuwatendea kondoo wa Yehova kwa njia inayofaa.

“Uwezo wa Ulimi”

14. Ulimi una uwezo gani?

14 Biblia inasema kwamba “mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi.” (Mithali 18:21) Kwa kweli, ulimi unaweza kusababisha madhara makubwa sana. Ni nani kati yetu hajapata kuumizwa moyoni na maneno ya madharau au yaliyonenwa bila kufikiri? Lakini ulimi unaweza pia kujenga. Mithali 12:18 yasema kwamba “ulimi wa mwenye haki ni afya.” Naam, maneno yenye kutia moyo na yenye kujenga yanaweza kufariji na kutuliza moyo kama dawa. Angalia mifano kadhaa.

15, 16. Tunawezaje kutumia ulimi wetu kuwatia moyo wengine?

15 Andiko la 1 Wathesalonike 5:14 linasihi hivi: “Semeni kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo.” Naam, hata watumishi waaminifu wa Yehova wanaweza kushuka moyo nyakati nyingine. Tunawezaje kuwasaidia watu hao? Toa pongezi hususa na ya kutoka moyoni ili watambue kwamba wanathaminiwa sana na Yehova. Wasomee maandiko ya Biblia yenye kuimarisha sana yanayoonyesha kwamba Yehova anawapenda na anawajali kikweli wale “waliovunjika moyo” na “waliopondeka roho.” (Zaburi 34:18) Tunapotumia uwezo wa ulimi kuwafariji wengine, tunaonyesha kwamba tunamwiga Mungu wetu mwenye rehema, “ambaye hufariji walioshuka moyo.”—2 Wakorintho 7:6, New American Standard Bible.

16 Tunaweza pia kutumia uwezo wetu wa ulimi kuwatia moyo wengine wanaohitaji sana kitia-moyo. Je, mwamini mwenzetu amefiwa na mpendwa wake? Tunaweza kumfariji aliyefiwa kwa kuzungumza naye kwa huruma na kumwonyesha kwamba tunamjali na tunamhangaikia. Je, kuna ndugu au dada mzee kwa umri ambaye anahisi kwamba hafai? Tunaweza kuwahakikishia wale walio wazee kwa umri kwamba wanathaminiwa sana kwa kuwaambia maneno yenye kujenga. Je, kuna mtu anayepambana na ugonjwa wa kudumu? Tunaweza kumtia moyo mgonjwa huyo kwa kuzungumza naye kwa fadhili tunapomtembelea au kumpigia simu. Muumba wetu hufurahi kama nini kuona tukitumia uwezo wa ulimi kusema mambo ‘yaliyo mema kwa ajili ya kujenga’!—Waefeso 4:29.

Kuhubiri habari njema​—ni njia bora ya kutumia uwezo wetu

17. Tunaweza kutumia ulimi wetu kuwafaidi wengine kwa njia gani bora zaidi, na kwa nini tufanye hivyo?

17 Njia bora zaidi ya kutumia uwezo wa ulimi ni kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Mithali 3:27 yasema hivi: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.” Tuna wajibu wa kuwaeleza wengine habari njema zinazookoa uhai. Ni kosa kuwanyima wengine ujumbe huo muhimu sana ambao Yehova ametupatia kwa ukarimu. (1 Wakorintho 9:16, 22) Lakini Yehova anataka tushiriki kwa kadiri gani katika kazi hiyo?

Kumtumikia Yehova kwa ‘Nguvu Zetu Zote’

18. Yehova anataka tufanye nini?

18 Upendo wetu kwa Yehova hutuchochea kushiriki kikamili zaidi katika huduma ya Kikristo. Yehova anataka tushiriki kwa kadiri gani katika huduma hiyo? Anataka tufanye yote tuwezayo haidhuru hali yetu maishani: “Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kwa wanadamu.” (Wakolosai 3:23) Yesu alisema kwamba amri kuu kupita zote ni hii: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Ndiyo, Yehova anataka kila mmoja wetu ampende na kumtumikia kwa nafsi yote.

19, 20. (a) Kwa kuwa nafsi inatia ndani moyo, akili, na nguvu, kwa nini sehemu hizo zinatajwa kwenye Marko 12:30? (b) Yamaanisha nini kumtumikia Yehova kwa nafsi yote?

19 Yamaanisha nini kumtumikia Mungu kwa nafsi yote? Nafsi ni mtu mwenyewe, akiwa na uwezo wake wote wa kimwili na kiakili. Kwa kuwa nafsi inatia ndani moyo, akili, na nguvu, kwa nini sehemu hizo zinatajwa kwenye Marko 12:30? Fikiria mfano mmoja. Katika nyakati za Biblia, mtu angeweza kujiuza (nafsi yake) na kuwa mtumwa. Lakini, huenda mtumwa asimtumikie bwana wake kwa moyo wake wote; huenda asitumie nguvu zake zote au uwezo wake wote wa akili kutunza masilahi ya bwana wake. (Wakolosai 3:22) Kwa hiyo, ni wazi kwamba Yesu alitaja moyo, akili, na nguvu ili kukazia kwamba tunapaswa kumtumikia Mungu kwa uwezo wetu wote. Kumtumikia Mungu kwa nafsi yote kwamaanisha kujitoa wenyewe, kutumia nguvu na nishati yetu yote katika utumishi wake.

20 Je, kutumikia kwa nafsi yote kwamaanisha kwamba ni lazima sote tutumie kiasi kilekile cha wakati na nishati katika huduma? Hilo haliwezekani, kwa kuwa sote tuna hali na uwezo mbalimbali. Kwa mfano, kijana mwenye nguvu na afya njema anaweza kuhubiri kwa saa nyingi zaidi kuliko mzee aliye dhaifu. Mseja asiye na wajibu wa familia anaweza kutimiza mengi zaidi kuliko mtu mwenye familia. Tunapaswa kushukuru sana ikiwa hali na nguvu zetu zinaturuhusu kufanya mengi katika huduma. Bila shaka, hatutaki kamwe kuwachambua-chambua wengine, wala kulinganisha utumishi wetu na wao. (Waroma 14:10-12) Badala yake, tunataka kutumia uwezo wetu kuwatia moyo wengine.

21. Ni njia ipi iliyo bora kabisa na muhimu zaidi ya kutumia uwezo wetu?

21 Yehova ametuwekea kielelezo bora kabisa cha kutumia uwezo kwa njia ifaayo. Tunataka kumwiga yeye kadiri tuwezavyo tukiwa wanadamu wasiokamilika. Tunaweza kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo kwa kuwatendea kwa heshima wale walio chini ya mamlaka yetu. Zaidi ya hayo, tunataka kutimiza kwa nafsi yote kazi ya kuhubiri inayookoa uhai ambayo Yehova ametukabidhi. (Waroma 10:13, 14) Kumbuka kwamba Yehova anafurahi unapomtolea yaliyo bora kabisa kulingana na uwezo wako. Je, huchochewi na moyo kutaka kumtumikia Mungu huyo mwenye kujali na mwenye upendo kulingana na uwezo wako? Hiyo ndiyo njia bora kabisa au muhimu zaidi ya kutumia uwezo wetu.

^ fu. 10 Katika nyakati za Biblia, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fimbo” lilimaanisha kijiti au gongo kama lile lililotumiwa na mchungaji kuwaongoza kondoo. (Zaburi 23:4) Vivyo hivyo, “fimbo” ya mamlaka ya wazazi inaonyesha mwongozo wa upendo, wala si adhabu kali au ya kikatili.