Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 28

“Wewe Peke Yako Ni Mwaminifu-Mshikamanifu”

“Wewe Peke Yako Ni Mwaminifu-Mshikamanifu”

1, 2. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mfalme Daudi alijua matokeo mabaya ya kukosa uaminifu-mshikamanifu?

MFALME DAUDI alijua matokeo mabaya ya kukosa uaminifu-mshikamanifu. Pindi moja utawala wake wenye misukosuko ulikabili matatizo wakati watu wa taifa lake walipopanga njama ya kumwondoa mamlakani. Isitoshe, Daudi alisalitiwa na baadhi ya watu ambao tungetarajia wawe marafiki wake wa karibu. Fikiria Mikali, mke wa kwanza wa Daudi. Mwanzoni, “alimpenda Daudi” na hapana shaka kwamba alimuunga mkono katika madaraka yake ya kifalme. Hata hivyo, baadaye ‘alimdharau moyoni mwake,’ hata akamwona Daudi kama ‘mmojawapo wa watu baradhuli.’—1 Samweli 18:20; 2 Samweli 6:16, 20.

2 Mwingine alikuwa Ahithofeli, aliyekuwa mshauri wa Daudi. Shauri lake lilithaminiwa sana kana kwamba lilikuwa neno la Yehova mwenyewe. (2 Samweli 16:23) Lakini, mwishowe, mshauri huyo mwenye kutumainiwa alimsaliti Daudi na kujiunga na waasi. Ni nani aliyepanga njama hiyo? Absalomu, mwana wa Daudi! Mhaini huyo mwenye kujitafutia makuu ‘aliwadanganya watu wa Israeli,’ akajitawaza mwenyewe kuwa mfalme mpinzani. Uasi wa Absalomu ulipamba moto sana hivi kwamba Mfalme Daudi alilazimika kukimbia ili kujiokoa.—2 Samweli 15:1-6, 12-17.

3. Daudi alikuwa na uhakika gani?

3 Je, hakukuwa mtu yeyote aliyebaki mwaminifu-mshikamanifu kwa Daudi? Katika shida zake zote, Daudi alikuwa na uhakika kwamba kulikuwa na mmoja aliyekuwa mwaminifu-mshikamanifu kwake. Nani? Yehova Mungu mwenyewe. Daudi alisema hivi kumhusu: “Wewe ni mwaminifu kwa walio waaminifu.” (2 Samweli 22:26, BHN) Uaminifu-mshikamanifu ni nini, na Yehova anaonyeshaje sifa hii kwa njia bora zaidi?

Uaminifu-Mshikamanifu Ni Nini?

4, 5. (a) “Uaminifu-mshikamanifu” ni nini? (b) Uaminifu-mshikamanifu unatofautianaje na uaminifu?

4 Kulingana na Maandiko ya Kiebrania, “uaminifu-mshikamanifu” ni fadhili ambayo inashikamana kabisa kwa upendo na kitu fulani hadi kusudi lake kuhusiana na kitu hicho linapotimia. Uaminifu-mshikamanifu unahusisha mambo mengi mbali na uaminifu. Mtu anaweza kuwa mwaminifu kwa sababu tu ya wajibu. Kinyume chake, uaminifu-mshikamanifu unategemea upendo. Isitoshe, neno “-aminifu” linaweza kutumiwa kuhusiana na vitu visivyo hai. Kwa mfano, mtunga-zaburi alisema kwamba mwezi ni “shahidi aliye mbinguni mwaminifu” kwa sababu unaangaza kwa ukawaida wakati wa usiku. (Zaburi 89:37) Lakini hatuwezi kusema kwamba mwezi ni mwaminifu-mshikamanifu. Kwa nini? Kwa sababu uaminifu-mshikamanifu unategemea upendo. Na vitu visivyo hai haviwezi kuonyesha sifa hiyo.

Mwezi unaitwa shahidi mwaminifu, lakini ni viumbe wenye akili tu wanaoweza kuiga uaminifu-mshikamanifu wa Yehova

5 Maandiko yanaonyesha kwamba uaminifu-mshikamanifu hudhihirisha upendo. Ni wazi kwamba kuna uhusiano fulani kati ya mtu anayeonyeshwa sifa hiyo na yule anayeionyesha. Uaminifu-mshikamanifu hauna kigeugeu. Si kama mawimbi ya bahari yanayopeperushwa huku na huku. Kinyume chake, sifa ya uaminifu-mshikamanifu, au upendo-mwaminifu inaweza kushinda hali ngumu sana.

6. (a) Uaminifu-mshikamanifu ni haba kadiri gani miongoni mwa wanadamu, na Biblia inathibitishaje jambo hilo? (b) Njia bora ya kujifunza kuhusu uaminifu-mshikamanifu ni ipi, na kwa nini?

6 Ni kweli kwamba uaminifu-mshikamanifu ni haba sana leo. Mara nyingi, marafiki wa karibu ‘huangamizana.’ Tunasikia visa vingi sana vya watu wanaowaacha wenzi wao wa ndoa. (Mithali 18:24; Malaki 2:14-16) Matendo ya hiana ni mengi sana hivi kwamba tunaweza kurudia maneno ya nabii Mika: “Mtu mwaminifu-mshikamanifu ametoweka duniani.” (Mika 7:2, NW) Mara nyingi wanadamu hushindwa kuonyesha uaminifu-mshikamanifu, lakini Yehova huonyesha sifa hiyo kwa njia ya pekee sana. Njia bora ya kujifunza kuhusu uaminifu-mshikamanifu ni kwa kuchunguza jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hii kuu ya upendo wake.

Uaminifu-Mshikamanifu wa Yehova Usio na Kifani

7, 8. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba ni Yehova peke yake aliye mwaminifu-mshikamanifu?

7 Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Wewe peke yako ni mwaminifu-mshikamanifu.” (Ufunuo 15:4) Kwa nini Biblia inasema hivyo, hali wanadamu na malaika wameonyesha uaminifu-mshikamanifu wa pekee pindi kwa pindi? (Ayubu 1:1; Ufunuo 4:8) Vipi Yesu Kristo? Yeye ndiye mtu “mwaminifu-mshikamanifu” zaidi mbele za Mungu. (Zaburi 16:10, NW) Basi, kwa nini inaweza kusemwa kwamba ni Yehova peke yake aliye mwaminifu-mshikamanifu?

8 Kwanza, kumbuka kwamba uaminifu-mshikamanifu ni sifa ya upendo. Hakuna mtu awaye yote anayeweza kuwa mwaminifu-mshikamanifu kikamili zaidi kuliko Yehova, kwa sababu “Mungu ni upendo,” yaani, yeye ni wonyesho halisi wa upendo. (1 Yohana 4:8) Kwa kweli, malaika na wanadamu wanaweza kuiga tu sifa za Mungu, lakini hawawezi kuwa na uaminifu-mshikamanifu wa hali ya juu sana kama yeye. Amekuwa akionyesha uaminifu-mshikamanifu kwa muda mrefu kuliko kiumbe yeyote duniani au mbinguni, kwa sababu Yeye ni “mzee wa siku.” (Danieli 7:9) Kwa hiyo, Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa kadiri kubwa sana. Yehova anaonyesha sifa hiyo kwa njia isiyo na kifani. Fikiria mifano kadhaa.

9. Yehova ni “mwaminifu-mshikamanifu juu ya kazi zake zote” kwa njia gani?

9 Yehova ni “mwenye fadhili [“mwaminifu-mshikamanifu,” NW] juu ya kazi zake zote.” (Zaburi 145:17) Jinsi gani? Zaburi 136 inajibu swali hilo. Andiko hilo linataja matendo kadhaa ya Yehova ya kuokoa, kutia ndani alipowaokoa Waisraeli kwa njia ya kustaajabisha katika Bahari Nyekundu. Jambo la kutokeza ni kwamba kila mstari wa zaburi hiyo unakaziwa na usemi: “Kwa maana fadhili [au, uaminifu-mshikamanifu] zake ni za milele.” Zaburi hiyo imetajwa katika Maswali ya Kutafakari kwenye ukurasa wa 289. Unaposoma mistari hiyo, utavutiwa sana kuona jinsi Yehova alivyoonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa watu wake kwa njia mbalimbali. Naam, Yehova huwa mwaminifu-mshikamanifu kwa watumishi wake waaminifu kwa kusikia vilio vyao vya kuomba msaada na kwa kuchukua hatua kwa wakati wake. (Zaburi 34:6) Yehova huendelea kuwaonyesha watumishi wake upendo-mshikamanifu maadamu wanaendelea kuwa waaminifu kwake.

10. Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kuhusiana na kanuni zake jinsi gani?

10 Zaidi ya hayo, Yehova huwaonyesha watumishi wake uaminifu-mshikamanifu kwa kushikilia kabisa kanuni zake. Yehova si kama wanadamu wasiotegemeka au wasio na msimamo ambao wanafuata tu hisia zao, maoni yake kuhusu mema na mabaya hayabadiliki. Miaka nenda miaka rudi, Yehova hajabadili kamwe maoni yake kuhusu uwasiliani-roho, ibada ya sanamu, na kuua. Alisema hivi kupitia nabii wake Isaya, “Mimi ni yuleyule hata katika uzee wenu.” (Isaya 46:4, BHN) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba tutafaidika tukifuata mwongozo wa kiadili unaoelezwa waziwazi katika Neno la Mungu.—Isaya 48:17-19.

11. Taja mifano inayoonyesha kwamba Yehova hutimiza ahadi zake kwa uaminifu-mshikamanifu.

11 Yehova huonyesha pia uaminifu-mshikamanifu kwa kutimiza ahadi zake. Kila jambo analotabiri linatimia. Yehova alisema hivi: “Neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” (Isaya 55:11) Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa watu wake kwa kutimiza ahadi zake. Yeye hawaahidi mambo ambayo hatatimiza. Yehova amethibitisha kabisa kwamba anatimiza ahadi zake hivi kwamba mtumishi wake Yoshua aliweza kusema: “Halikuanguka neno lo lote katika jambo lo lote lililokuwa ni jema ambalo BWANA alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.” (Yoshua 21:45) Hivyo basi, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hatatukatisha tamaa kwa kukosa kutimiza ahadi zake.—Isaya 49:23; Waroma 5:5.

12, 13. Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova “ni wa milele” katika maana gani?

12 Kama tulivyoona hapo awali, Biblia inatuambia kwamba uaminifu-mshikamanifu wa Yehova “ni wa milele.” (Zaburi 136:1, NW) Jinsi gani? Kwanza, Yehova husamehe kabisa dhambi. Kama Sura ya 26 ilivyoonyesha, Yehova hakumbuki na kumhukumu mtu kwa sababu ya dhambi ambazo tayari amesamehewa. Kila mmoja wetu anapaswa kushukuru kwamba uaminifu-mshikamanifu wa Yehova ni wa milele kwa sababu ‘sote tumefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.’—Waroma 3:23.

13 Lakini uaminifu-mshikamanifu wa Yehova ni wa milele katika maana nyingine pia. Neno lake linasema kwamba mtu mwadilifu “atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa.” (Zaburi 1:3) Hebu wazia mti mkubwa sana ambao majani yake hayanyauki! Vivyo hivyo, tukipendezwa kikweli na Neno la Mungu, tutaishi muda mrefu, tutakuwa na amani, na kufanikiwa. Yehova awaahidi watumishi wake waaminifu baraka za milele. Kwa kweli, katika ulimwengu mpya wenye uadilifu ambao Yehova ataleta, wanadamu watiifu watafurahia uaminifu-mshikamanifu wake milele.—Ufunuo 21:3, 4.

Yehova ‘Hatawaacha Waaminifu Wake’

14. Yehova anaonyeshaje kwamba anathamini uaminifu wa watumishi wake?

14 Yehova ameonyesha uaminifu-mshikamanifu tena na tena. Kwa sababu Yehova hana kigeugeu kamwe, yeye huwaonyesha watumishi wake uaminifu-mshikamanifu wa kudumu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Nilikuwa kijana na sasa ni mzee; kamwe sijaona mwadilifu ameachwa na Mungu, au: watoto wake wakiombaomba chakula. Maana Mwenyezi-Mungu hupenda uadilifu, wala hawaachi waaminifu wake.” (Zaburi 37:25, 28, BHN) Ni kweli kwamba Yehova anastahili ibada yetu kwa sababu yeye ni Muumba. (Ufunuo 4:11) Hata hivyo, Yehova anathamini sana uaminifu wetu kwa sababu yeye ni mwaminifu-mshikamanifu.—Malaki 3:16, 17.

15. Eleza jinsi Yehova alivyoonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Israeli.

15 Kwa uaminifu-mshikamanifu, sikuzote Yehova huwasaidia watu wake wanapokumbwa na matatizo. Mtunga-zaburi anatuambia hivi: “Huwalinda nafsi zao watauwa wake, na kuwaokoa na mkono wa wasio haki.” (Zaburi 97:10) Fikiria jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli. Baada ya kuokolewa kimuujiza katika Bahari Nyekundu, Waisraeli walitangaza hivi katika wimbo waliomwimbia Yehova: “Wewe kwa fadhili-upendo zako [au, “upendo-mshikamanifu,” kielezi-chini] umewaongoza watu uliowakomboa.” (Kutoka 15:13, NW) Hapana shaka kwamba Yehova alionyesha upendo-mshikamanifu alipowaokoa katika Bahari Nyekundu. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “BWANA hakuwapenda ninyi, wala hakuwachagua ninyi, kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, maana mlikuwa wachache kuliko watu wote; bali kwa sababu BWANA anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu, ndiyo sababu BWANA akawatoa kwa mkono wa nguvu, akawakomboa katika nyumba ya utumwa, katika mkono wa Farao, mfalme wa Misri.”—Kumbukumbu la Torati 7:7, 8.

16, 17. (a) Waisraeli walikosa kabisa kuthamini nini, lakini Yehova aliwaonyeshaje rehema? (b) Waisraeli wengi walionyeshaje kwamba ‘hawangeweza kuponywa,’ na hilo linatupatia onyo gani?

16 Bila shaka, taifa la Israeli halikuthamini uaminifu-mshikamanifu wa Yehova. Baada ya kukombolewa, ‘walizidi kumtenda dhambi [Yehova], walipomwasi Aliye Juu.’ (Zaburi 78:17) Kadiri miaka ilivyopita, waliasi tena na tena, walimwacha Yehova na kugeukia miungu ya uwongo na mazoea ya kipagani ambayo yaliwatia unajisi. Hata hivyo, Yehova hakuvunja agano lake. Badala yake, Yehova aliwasihi hivi watu wake kupitia nabii Yeremia: “Rudi, Ee Israeli mwenye kuasi . . . Sitakutazama kwa hasira; maana mimi ni mwenye rehema [“mwaminifu-mshikamanifu,” NW].” (Yeremia 3:12) Lakini, kama Sura ya 25 ilivyoonyesha, Waisraeli wengi walikataa kubadilika. Hata, “waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake.” Matokeo yalikuwa nini? Mwishowe, ‘ghadhabu ya BWANA ilizidi juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponywa.’—2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16.

17 Twajifunza nini kutokana na mambo hayo? Twajifunza kwamba uaminifu-mshikamanifu wa Yehova haudanganyiki wala si wa kijinga. Ni kweli kwamba Yehova ni ‘mwingi wa rehema’ naye hupenda kuonyesha rehema kunapokuwa na msingi wa kufanya hivyo. Lakini Yehova huchukua hatua gani mtu mwovu anapokuwa sugu? Inapokuwa hivyo, Yehova hushikamana na kanuni zake adilifu naye humhukumu mtu mwovu. Musa aliambiwa kwamba Yehova “si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.”—Kutoka 34:6, 7.

18, 19. (a) Yehova anaonyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa kuwaadhibu waovu? (b) Yehova ataonyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa watumishi wake ambao wameteswa na kuuawa?

18 Mungu huonyesha pia uaminifu-mshikamanifu kwa kuwaadhibu waovu. Vipi? Amri ambazo Yehova anawapa wale malaika saba katika kitabu cha Ufunuo zaonyesha jambo hilo: “Nendeni mkamwage mabakuli saba ya hasira ya Mungu ndani ya dunia.” Malaika wa tatu anapomwaga bakuli lake “ndani ya mito na mabubujiko ya maji,” yanakuwa damu. Kisha malaika huyo anamwambia Yehova hivi: “Wewe, Uliyeko na uliyekuwako, Mwaminifu-Mshikamanifu, ni mwadilifu, kwa sababu umetoa maamuzi haya, kwa sababu walimwaga damu ya watakatifu na ya manabii, nawe umewapa damu wanywe. Wao wastahili hilo.”—Ufunuo 16:1-6.

Yehova atawakumbuka na kuwafufua kwa uaminifu wale ambao wamedumu wakiwa waaminifu-washikamanifu hadi kifo

19 Ona kwamba malaika huyo anapotangaza ujumbe huo wa hukumu anasema kwamba Yehova ni “Mwaminifu-Mshikamanifu.” Kwa nini? Kwa sababu anapowaangamiza waovu, Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa watumishi wake ambao wameteswa na kuuawa. Kwa uaminifu-mshikamanifu, Yehova anawakumbuka vizuri watumishi hao. Anatamani kuwaona tena waaminifu hao waliokufa, na Biblia inaonyesha waziwazi kwamba anakusudia kuwathawabisha kwa kuwafufua. (Ayubu 14:14, 15) Yehova hawasahau watumishi wake waaminifu eti kwa sababu wamekufa. Badala yake, “kwake, wao wote wako hai.” (Luka 20:37, 38) Kusudi la Yehova la kuwafufua wale walio katika kumbukumbu lake linathibitisha kabisa kwamba yeye ni mwaminifu-mshikamanifu.

Wanazi walimuua Bernard Luimes (kushoto) na Wolfgang Kusserow (katikati)

Kikundi cha kisiasa kilimuua Moses Nyamussua kwa kumchoma mkuki

Upendo-Mshikamanifu wa Yehova Huandaa Njia ya Wokovu

20. “Vyombo vya rehema” ni nani? na Yehova anawaonyeshaje uaminifu-mshikamanifu?

20 Katika historia yote, Yehova ameonyesha uaminifu-mshikamanifu wa pekee kwa wanadamu. Kwa maelfu ya miaka, Yehova ‘amevumilia kwa ustahimilivu mwingi vyombo vya hasira ya kisasi vilivyofanywa kufaa kwa ajili ya uharibifu.’ Kwa nini? “Ili apate kujulisha utajiri wa utukufu wake juu ya vyombo vya rehema, alivyotayarisha kimbele kwa ajili ya utukufu.” (Waroma 9:22, 23) “Vyombo vya rehema” ni wale walio na mtazamo ufaao ambao wametiwa mafuta kwa roho takatifu ili wawe warithi pamoja na Kristo katika Ufalme wake. (Mathayo 19:28) Kwa kuandaa njia ya wokovu kwa ajili ya vyombo hivyo vya rehema, Yehova alionyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Abrahamu, kwa sababu alikuwa amemwahidi hivi alipofanya agano naye: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”—Mwanzo 22:18.

Watumishi wote waaminifu wa Yehova wana tumaini hakika la wakati ujao kwa sababu yeye ni mwaminifu-mshikamanifu

21. (a) Yehova anaonyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa “umati mkubwa” ambao unatumaini kuokoka “dhiki kubwa”? (b) Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova unakuchochea kufanya nini?

21 Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu pia kwa “umati mkubwa” ambao unatumaini kuokoka “dhiki kubwa” na kuishi milele katika paradiso duniani. (Ufunuo 7:9, 10, 14) Kwa uaminifu-mshikamanifu, Yehova anawapa watumishi wake fursa ya kuishi milele katika paradiso duniani ingawa wao si wakamilifu. Jinsi gani? Anawapa fursa hiyo kupitia fidia—wonyesho mkuu zaidi wa uaminifu-mshikamanifu wa Yehova. (Yohana 3:16; Waroma 5:8) Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova unawavuta wale ambao wana njaa ya uadilifu mioyoni mwao. (Yeremia 31:3) Je, huhisi ukiwa karibu zaidi na Yehova kwa sababu ya uaminifu-mshikamanifu wa dhati ambao amekuonyesha na atakuonyesha? Kwa sababu tunatamani kumkaribia Mungu, na tuthamini upendo wake kwa kuimarisha azimio letu la kumtumikia kwa uaminifu-mshikamanifu.