Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 1

“Aliyepotea Nitamtafuta”

“Aliyepotea Nitamtafuta”

Kondoo amechanganyikiwa. Aliachwa na kondoo wengine alipokuwa akila majani malishoni. Sasa, hawezi kuwaona kondoo wenzake wala mchungaji. Giza linaingia. Amepotea katika bonde lenye wanyama hatari na kondoo huyo hana ulinzi. Mwishowe, anasikia sauti anayoifahamu, sauti ya mchungaji, ambaye anakimbia kumwelekea kondoo huyo. Anamchukua na kumfunika kwenye mikunjo ya vazi lake na kumbeba hadi nyumbani.

MARA nyingi Yehova hujilinganisha na mchungaji kama huyo. Katika Neno lake, anatuhakikishia hivi: “Mimi mwenyewe, nami nitawatafuta kondoo zangu na kuwatunza.”—Ezekieli 34:11, 12.

“Kondoo wa Malisho Yangu”

Kondoo wa Yehova ni nani? Kwa ufupi, kondoo wa Yehova ni watu wanaompenda na kumwabudu. Biblia inasema: “Tuabudu na kuinama; Na tupige magoti mbele za Yehova Mtengenezaji wetu. Kwa maana yeye ni Mungu wetu, na sisi ni watu wa malisho yake na kondoo wa mkono wake.” (Zaburi 95:6, 7) Kama tu kondoo halisi wanavyomfuata mchungaji, waabudu wa Yehova wako tayari kumfuata Mchungaji wao. Je, ni wakamilifu? Hapana. Nyakati nyingine, watu wa Mungu wamekuwa ‘kondoo waliotawanyika,’ “kondoo waliopotea,” na “kondoo wanaopotea njia.” (Ezekieli 34:12; Mathayo 15:24; 1 Petro 2:25) Hata hivyo, mtu anapopeperuka, sikuzote Yehova anatumaini kwamba atarudi.

Je, bado unahisi kwamba Yehova ni Mchungaji wako? Ni kwa njia gani Yehova ni Mchungaji leo? Fikiria njia hizi tatu:

Anatulisha kiroho. Yehova anasema hivi: “Katika malisho mazuri nitawalisha wao, . . . Huko watalala katika makao mazuri, na kwenye malisho manono watajilisha.” (Ezekieli 34:14) Sikuzote Yehova hutupatia kila aina ya chakula kizuri cha kiroho kinachoburudisha na kwa wakati ufaao. Je, unaweza kukumbuka makala, hotuba, au video iliyojibu sala yako ya kuomba msaada? Je, jambo hilo halikukuthibitishia kwamba Yehova anakujali wewe kibinafsi?

Anatulinda na kututegemeza. Yehova anaahidi hivi: “Aliyefukuzwa nitamrudisha, na aliyevunjika nitamfunga na anayeugua nitamtia nguvu.” (Ezekieli 34:16) Yehova huwatia nguvu walio dhaifu au waliolemewa na mahangaiko. Anawafunga kondoo wake, akiwasaidia wapone ikiwa wameumizwa, labda hata na kondoo wenzao. Pia, anawarudisha kundini wale waliopeperuka ambao huenda wanapambana na hisia zisizofaa.

Anahisi ana wajibu wa kututunza. Yehova anasema hivi: “Nitawakomboa kutoka mahali pote ambapo wametawanyika. Aliyepotea nitamtafuta.” (Ezekieli 34:12, 16) Yehova hamwachi kondoo aliyepotea bila tumaini. Kondoo akipotea, Yehova hujua, humtafuta, na kushangilia anapompata. (Mathayo 18:12-14) Zaidi ya yote, anasema hivi kuhusu waabudu wake wa kweli: Ninyi ni “kondoo zangu, kondoo wa malisho yangu.” (Ezekieli 34:31) Wewe ni mmoja wa kondoo hao.

Yehova hamwachi kondoo aliyepotea bila tumaini. Yehova hushangilia anapompata kondoo huyo

“Utuletee Siku Zilizo Mpya Kama Katika Zamani za Kale”

Kwa nini Yehova anakutafuta na kukusihi umrudie? Ni kwa sababu anataka uwe na furaha. Anaahidi kwamba ‘atamimina baraka zake’ juu ya kondoo zake. (Isaya 44:3) Ahadi hiyo ni hakika. Tayari umejionea jambo hilo.

Kumbuka ulipoanza kujifunza na kumjua Yehova. Kwa mfano, ulihisije mara ya kwanza ulipojifunza kweli zenye kusisimua kuhusu jina la Mungu na kusudi lake kwa wanadamu? Je, unakumbuka jinsi ilivyoburudisha kushirikiana na Wakristo wenzako kwenye makusanyiko? Zamani uliposhiriki habari njema na mtu aliyependezwa, je, hukurudi nyumbani ukiwa na furaha na mwenye kuridhika sana?

Unaweza kupata tena shangwe hiyo. Watumishi wa Mungu wa kale walisali hivi: “Uturudishe kwako, Ee Yehova, nasi tutarudi bila kukawia. Utuletee siku zilizo mpya kama katika zamani za kale.” (Maombolezo 5:21) Yehova alijibu sala hiyo, na watu wake walirudi na kuanza kumtumikia wakiwa na shangwe tena. (Nehemia 8:17) Yehova atafanya vivyohivyo kwako.

Hata hivyo, kumrudia Yehova si rahisi. Fikiria baadhi ya changamoto unazoweza kukabili unapotaka kumrudia Yehova na jinsi unavyoweza kuzishinda.