Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 2

Mahangaiko​—‘Kukazwa Katika Kila Njia’

Mahangaiko​—‘Kukazwa Katika Kila Njia’

“Baada ya miaka 25 ya ndoa, tulitalikiana na mume wangu. Watoto wangu waliacha kweli. Nilipatwa na matatizo makubwa ya kiafya. Kisha nikashuka moyo. Niliishiwa na nguvu kabisa na nikashindwa kuhimili. Niliacha kuhudhuria mikutano, na nikawa asiyetenda.”—June.

MAHANGAIKO huwapata watu wote, hata watu wa Mungu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: ‘Fikira zangu zinazofadhaisha zilikuwa nyingi ndani yangu.’ (Zaburi 94:19) Hata Yesu alisema kwamba katika siku za mwisho, “mahangaiko ya maisha” yangefanya iwe vigumu sana kumtumikia Yehova. (Luka 21:34) Namna gani wewe? Je, unalemewa na matatizo ya kiuchumi, ya familia, au ya kiafya? Yehova anawezaje kukusaidia?

“Nguvu Zinazopita Zile za Kawaida”

Hatuna uwezo wa kukabiliana na mahangaiko kwa nguvu zetu wenyewe. Mtume Paulo aliandika hivi: “Tunakazwa katika kila njia. Tunafadhaishwa . . . ; tunaangushwa chini.” Hata hivyo, alisema pia kwamba “hatubanwi kupita kiasi cha kuweza kusonga,” “si bila njia ya kutokea kabisa” na “hatuangamizwi.” Ni nini hutusaidia kuvumilia? Ni “nguvu zinazopita zile za kawaida,” yaani, nguvu kutoka kwa Mungu wetu mweza yote, Yehova.—2 Wakorintho 4:7-9.

Fikiria jinsi ulivyopata “nguvu zinazopita zile za kawaida” wakati uliopita. Je, unakumbuka jinsi hotuba fulani yenye kutia moyo ilivyokuchochea kuthamini zaidi upendo mshikamanifu wa Yehova? Je, imani yako katika ahadi za Yehova iliongezeka ulipowafundisha wengine kuhusu tumaini la Paradiso? Tunapohudhuria mikutano ya Kikristo na kuwaeleza wengine kuhusu imani yetu, tunapata nguvu za kuvumilia mahangaiko maishani na kuwa na amani ya akili ili tuweze kumtumikia Yehova kwa shangwe.

“Onjeni Mwone ya Kuwa Yehova Ni Mwema”

Kihalisi, huenda wakati fulani ukahisi umebanwa katika kila njia. Kwa mfano, Yehova anataka tutafute kwanza Ufalme na kudumisha ratiba nzuri ya utendaji wa kiroho. (Mathayo 6:33; Luka 13:24) Hata hivyo, namna gani ikiwa ugonjwa, upinzani, au matatizo ya familia yanakuzuia kufanya mengi? Namna gani ikiwa kazi ya kimwili inamaliza wakati na nguvu ambazo ungetumia pamoja na kutaniko? Unapokuwa na mambo mengi ya kufanya na huna wakati na nguvu za kutosha, huenda ukahisi umelemewa. Huenda hata wakati fulani umefikiria kwamba Yehova anatazamia mengi mno kutoka kwako.

Yehova anaelewa hali zetu. Hatazamii tufanye mambo tusiyoweza. Na anatambua kwamba ili tupone kimwili na kihisia, tunahitaji muda.—Zaburi 103:13, 14.

Kwa mfano, fikiria jinsi Yehova alivyomjali nabii Eliya. Alipovunjika moyo na kuogopa hivi kwamba akakimbilia nyikani, je, Yehova alimkemea na kumwamuru arudi kwenye mgawo wake? La. Yehova alimtuma malaika wake mara mbili ili amwamshe Eliya kwa wororo na kumpa chakula. Hata hivyo, siku 40 baadaye, bado Eliya alikuwa na wasiwasi na woga. Yehova alifanya nini kingine ili kumsaidia? Kwanza, Yehova alimthibitishia kwamba angemlinda. Pili, Yehova alimfariji kwa “sauti tulivu, ya chini.” Mwishowe, Yehova alimfunulia kwamba kulikuwa na maelfu wengine ambao walimwabudu Mungu kwa uaminifu. Muda si muda, Eliya akawa tena nabii mwenye bidii. (1 Wafalme 19:1-19) Tunajifunza nini? Eliya alipolemewa na mahangaiko, Yehova alimtendea kwa huruma na subira. Yehova hajabadilika. Anatujali kwa njia hiyohiyo.

Uwe na usawaziko unapofikiria kile ambacho unaweza kumpa Yehova. Usilinganishe yale uliyotimiza zamani na unayoweza kutimiza sasa. Kwa mfano: Mkimbiaji ambaye hajafanya mazoezi kwa miezi au miaka kadhaa hawezi kuanza kukimbia kwa kasi mara moja. Badala yake, anaanza na miradi midogo ambayo itamwezesha kupata nguvu na uvumilivu. Wakristo ni kama wakimbiaji. Wao hufanya mazoezi wakiwa na lengo hususa. (1 Wakorintho 9:24-27) Kwa nini usifuatie mradi mmoja wa kiroho ambao unaweza kuufikia kwa sasa? Kwa mfano, unaweza kujiwekea mradi wa kuhudhuria mkutano wa kutaniko. Mwombe Yehova akusaidie ili uufikie. Unapoendelea kupata tena nguvu za kiroho, ‘utaonja na kuona ya kuwa Yehova ni mwema.’ (Zaburi 34:8) Kumbuka kwamba jambo lolote ambalo unafanya ili kuonyesha kwamba unampenda Yehova, hata kama ni dogo sana, lina thamani kwake.—Luka 21:1-4.

Yehova hatazamii tufanye mambo yanayopita uwezo wetu

“Kichocheo Nilichokuwa Nikisubiri”

Yehova alimtiaje nguvu June ili amrudie? June anasema hivi: “Niliendelea kumwomba Yehova anisaidie. Kisha, binti-mkwe wangu alinieleza kuhusu kusanyiko ambalo lingefanywa katika mji wetu. Niliamua kuhudhuria siku moja ya kusanyiko hilo. Nilifurahi sana kuwa miongoni mwa watu wa Yehova tena! Kusanyiko hilo lilikuwa kichocheo nilichokuwa nikisubiri. Sasa, ninamtumikia tena Yehova kwa shangwe. Maisha yangu yana kusudi. Nimetambua kwamba ninahitaji msaada wa ndugu na dada kuliko wakati mwingine wowote na siwezi kujitegemea. Ninashukuru kwamba nilikuwa na nafasi ya kumrudia Yehova.”