Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 5

Mrudieni “Mchungaji na Mwangalizi wa Nafsi Zenu”

Mrudieni “Mchungaji na Mwangalizi wa Nafsi Zenu”

Je, umekabili mojawapo ya changamoto zilizozungumziwa katika broshua hii? Ikiwa ndivyo, huko peke yako. Watumishi wengi waaminifu wa Mungu katika nyakati za Biblia na leo pia wamekabili changamoto kama hizo. Kama tu Yehova alivyowasaidia kukabiliana na changamoto hizo, ndivyo atakavyokusaidia pia.

Yehova atakutegemeza unapojitahidi kumrudia

UWE na hakika kwamba Yehova atakutegemeza unapojitahidi kumrudia. Atakusaidia kukabiliana na mahangaiko, kuondoa maumivu ya kihisia, na kupata amani ya akili na moyo kwa sababu ya kuwa na dhamiri safi. Kisha unaweza kuchochewa kumtumikia tena Yehova pamoja na waabudu wenzako. Hali yako itafanana na ya baadhi ya Wakristo wa karne ya kwanza, ambao mtume Petro aliwaandikia hivi: “Mlikuwa kama kondoo, wanaopotea njia; lakini sasa mmerudi kwa mchungaji na mwangalizi wa nafsi zenu.”—1 Petro 2:25.

Jambo bora zaidi unaloweza kufanya ni kumrudia Yehova. Kwa nini? Kwa sababu utafanya moyo wa Yehova ushangilie. (Methali 27:11) Kama ujuavyo, matendo yetu yanaweza kumkasirisha Yehova au kumfurahisha. Bila shaka, Yehova hatulazimishi tumpende au tumtumikie. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Kuhusiana na hilo, msomi mmoja wa Biblia alisema hivi: “Moyo wa mwanadamu ni kama mlango ambao hauna komeo. Mtu mwingine hawezi kuufungua, lazima mtu mwenyewe aufungue.” Tunachagua kufungua mlango huo kwa kumwabudu Yehova kwa sababu tunampenda sana kutoka moyoni. Tukifanya hivyo, tunampa zawadi yenye thamani kubwa, yaani, utimilifu wetu, na hivyo kuufanya moyo wake ushangilie sana. Kwa kweli, tunapomtolea Yehova ibada anayostahili, tunapata furaha isiyoweza kulinganishwa na kitu kingine chochote.—Matendo 20:35; Ufunuo 4:11.

Isitoshe, ukirudia ibada ya Kikristo, utatosheleza uhitaji wako wa kiroho. (Mathayo 5:3) Kwa njia gani? Watu wengi ulimwenguni pote hujiuliza hivi: ‘Tulitoka wapi?’ Wana kiu ya kupata majibu ya maswali kuhusu kusudi la maisha. Wanadamu wameumbwa na Yehova wakiwa na uhitaji huo. Alituumba tupate shangwe kwa kumtumikia. Tunapata uradhi mkubwa tunapojua kwamba tunamwabudu Yehova kwa sababu tunampenda.—Zaburi 63:1-5.

Tafadhali usisahau kwamba Yehova anataka umrudie. Unawezaje kuwa na uhakika huo? Fikiria hili: Kwa sala nyingi, broshua hii iliandaliwa kwa makini. Huenda mzee Mkristo au mwamini mwenzako mwingine alikuletea broshua hii. Kisha ukachochewa kuisoma na kukubali ujumbe wake. Hayo yote yanathibitisha kwamba Yehova hajakusahau. Badala yake, anakuvuta kwake kwa wororo.—Yohana 6:44.

Tunaweza kupata faraja kwa kujua kwamba Yehova hawasahau kamwe watumishi wake waliopotea. Dada anayeitwa Donna alikuja kuthamini jambo hilo. Alisema hivi: “Nilipeperuka polepole kutoka katika kweli, hata hivyo mara nyingi nilitafakari andiko la Zaburi 139:23, 24, linalosema: ‘Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Unichunguze, na uzijue fikira zangu zinazofadhaisha, Na uone kama ndani yangu mna njia yoyote yenye kuumiza, Na uniongoze katika njia ya mpaka wakati usio na kipimo.’ Nilijua kwamba mimi si sehemu ya ulimwengu, yaani, sikustahili kuwa ulimwenguni, na nilijua kwamba nilipaswa kuwa katika tengenezo la Yehova. Nilianza kutambua kwamba Yehova kamwe hajaniacha; nilichopaswa kufanya ni kumrudia. Ninafurahi sana kwamba nimerudi!”

“Nilianza kutambua kwamba Yehova kamwe hajaniacha; nilichopaswa kufanya ni kumrudia”

Tunasali kwa dhati kwamba wewe pia utafurahia tena “shangwe ya Yehova.” (Nehemia 8:10) Ukimrudia Yehova, hutajuta kamwe.