Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 4

Hisia za Kuwa na Hatia​—‘Nitakase Kutokana na Dhambi Yangu’

Hisia za Kuwa na Hatia​—‘Nitakase Kutokana na Dhambi Yangu’

“Kazi yangu mpya iliboresha hali ya uchumi ya familia yetu, lakini pia ilifanya nijihusishe na mambo yasiyofaa ya kila namna. Nilianza kusherehekea sikukuu, kujihusisha na siasa, na hata kwenda kanisani. Nilikuwa Shahidi wa Yehova asiyetenda kwa miaka 40. Kadiri miaka ilivyopita, ndivyo nilivyohisi kwamba Yehova hawezi kunisamehe. Nilijilaumu sikuzote. Zaidi ya yote, nilijua ukweli kabla sijapotea.”—Martha.

HISIA za kuwa na hatia zinaweza kuwa mzigo unaolemea sana. Mfalme Daudi aliandika hivi: “Makosa yangu yamepita juu ya kichwa changu; Kama mzigo mzito, ni mazito sana kwangu.” (Zaburi 38:4) Baadhi ya Wakristo wamelemewa sana na huzuni kupita kiasi, na hivyo kuamini kwamba Yehova hawezi kamwe kuwasamehe. (2 Wakorintho 2:7) Je, ni sawa kufikiri hivyo? Hata ikiwa umefanya dhambi nzito, je, uko mbali sana na Yehova hivi kwamba hawezi kamwe kukusamehe? Hapana!

‘Natunyooshe Mambo Kati Yetu’

Yehova hawawekei kinyongo watenda dhambi wanaotubu. Badala yake, anawasihi wamrudie. Katika mfano wa mwana mpotevu, Yesu alimfananisha Yehova na baba mwenye upendo ambaye mwana wake aliondoka nyumbani na kwenda kuishi maisha ya upotovu. Baadaye, mwana huyo aliamua kurudi nyumbani. “[Mwana huyo] alipokuwa angali mbali, baba yake akamwona, akamsikitikia, akakimbia, akamwangukia shingoni na kumbusu kwa wororo.” (Luka 15:11-20) Je, unataka kumkaribia zaidi Yehova lakini unahisi ‘ungali mbali’ naye? Kama baba katika mfano huo wa Yesu, Yehova anakupenda kwa wororo. Anatazamia kwa hamu kukukaribisha tena.

Hata hivyo, namna gani ikiwa unahisi kwamba dhambi zako ni nzito au nyingi sana hivi kwamba Yehova hawezi kukusamehe? Tafadhali fikiria mwaliko wa Yehova kwenye Isaya 1:18: “‘Sasa, njooni, nasi tunyooshe mambo kati yetu,’ asema Yehova. ‘Hata dhambi zenu zikiwa nyekundu, zitafanywa kuwa nyeupe kama theluji; hata zikiwa nyekundu kama kitambaa chekundu; zitakuwa kama sufu.’” Naam, Yehova anaweza kusamehe hata dhambi zinazoonekana kama rangi nyekundu sana kwenye vazi jeupe.

Yehova hataki uendelee kuteseka kwa sababu ya dhamiri yenye hatia. Hivyo basi, unawezaje kupata faraja inayotokana na msamaha wa Mungu na kuwa na dhamiri safi? Fikiria hatua mbili ambazo Mfalme Daudi alichukua. Kwanza, alisema hivi: “Nitaungama makosa yangu kwa Yehova.” (Zaburi 32:5) Kumbuka kwamba Yehova tayari amekualika umwendee katika sala ili ‘unyooshe mambo’ pamoja naye. Kubali mwaliko huo. Ungama dhambi zako kwa Yehova, na umweleze hisia zako. Daudi alisali hivi kutokana na mambo aliyojionea: ‘Nitakase kutokana na dhambi yangu. . . . Moyo uliovunjika na kupondwa, Ee Mungu, hutaudharau.’—Zaburi 51:2, 17.

Pili, Daudi alisaidiwa na mwakilishi aliyechaguliwa na Mungu, nabii Nathani. (2 Samweli 12:13) Leo, Yehova ametupatia wazee wa kutaniko ambao wamezoezwa kuwasaidia watenda dhambi wanaotubu kurudisha urafiki wao pamoja na Yehova. Ukiwafikia wazee, watatumia Maandiko na kusali kutoka moyoni ili kuutuliza moyo wako, na hivyo kupunguza au kuondoa kabisa hisia zako zisizofaa na kukusaidia kupona kiroho.—Yakobo 5:14-16.

Yehova anataka uwe na dhamiri safi

“Mwenye Furaha Ni Mtu Ambaye Amesamehewa Maasi Yake”

Huenda isiwe rahisi kuungama dhambi zako kwa Yehova Mungu na kuwafikia wazee. Bila shaka hata Daudi alihisi vivyohivyo. Kwa kipindi fulani, ‘alikaa kimya’ kuhusu dhambi zake. (Zaburi 32:3) Hata hivyo, baadaye alithamini faida ya kuungama dhambi zake na kurekebisha mwenendo wake.

Faida kubwa ambayo Daudi alipata ni kupata tena shangwe yake. Aliandika hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye amesamehewa maasi yake, ambaye dhambi yake imefunikwa.” (Zaburi 32:1) Pia, alisali hivi: “Ee Yehova, na uifungue hii midomo yangu, Ili kinywa changu mwenyewe kipate kutangaza sifa yako.” (Zaburi 51:15) Alipoondolewa hisia za hatia, Daudi alithamini msamaha wa Mungu, na akachochewa kuwaeleza wengine kumhusu Yehova.

Yehova anataka upate kitulizo kwa sababu ya kuwa na dhamiri safi. Na anataka uwaambie wengine kumhusu yeye na makusudi yake kwa unyoofu na shangwe nyingi, bali si kwa hisia za hatia. (Zaburi 65:1-4) Kumbuka kwamba anataka urudi ili ‘dhambi zako zipate kufutwa, ili majira ya kuburudisha yapate kuja kutoka kwa uso wa Yehova.’—Matendo 3:19.

Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Martha. Anasema hivi: “Mwanangu aliendelea kunitumia magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Pole kwa pole, nikaanza kumkaribia tena Yehova. Nilipotaka kumrudia Yehova, jambo gumu zaidi lilikuwa kuomba msamaha wa dhambi zote nilizokuwa nimefanya. Hata hivyo, mwishowe nilisali kwa Mungu na kumwomba msamaha. Sikuamini kwamba miaka 40 ilikuwa imepita tangu nilipomwacha Yehova. Mambo niliyojionea yanathibitisha kwamba hata baada ya miaka mingi kupita, mtu anaweza tena kumtumikia Mungu na kurudi katika upendo wake.”