Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barua Kutoka Baraza Linaloongoza

Barua Kutoka Baraza Linaloongoza

Mwamini mwenzetu mpendwa:

Kama ujuavyo, Biblia ni kitabu kinachohusu watu kwa ujumla. Wengi wao ni wanaume na wanawake waaminifu waliokabili changamoto sawa na zetu. Walikuwa na “hisia kama zetu.” (Yakobo 5:17) Baadhi yao walilemewa na mahangaiko na mfadhaiko. Wengine waliumizwa kihisia na watu wa familia au waabudu wenzao. Na wengine walijilaumu kwa sababu ya makosa waliyofanya.

Hali hizo zilifanya baadhi yao kupeperuka mbali na Yehova. Hata hivyo, je, walikuwa wamemuacha kabisa Yehova? Hapana. Wengi wao walikuwa kama mtunga zaburi aliyesali hivi: “Nimetanga-tanga kama kondoo aliyepotea. Umtafute mtumishi wako, kwa maana sijazisahau amri zako.” (Zaburi 119:176) Je, umewahi kuhisi hivyo?

Yehova hawasahau kamwe waabudu wake wanaotanga-tanga nje ya zizi. Badala yake, anawasihi wamrudie, na mara nyingi anafanya hivyo kupitia waamini wenzao. Kwa mfano, fikiria jinsi Yehova alivyomsaidia mtumishi wake Ayubu, aliyepatwa na misiba kadhaa, iliyotia ndani kupoteza mali, wapendwa wake, na kupatwa na ugonjwa mbaya sana. Pia, Ayubu alidhihakiwa na watu ambao walipaswa kumfariji. Hata ingawa kwa muda fulani mawazo yake yalipotoka, hakumwacha Yehova. (Ayubu 1:22; 2:10) Yehova alimsaidia Ayubu jinsi gani ili apate tena usawaziko?

Njia moja ambayo Yehova alimsaidia Ayubu ni kupitia mwamini mwenzake aliyeitwa Elihu. Ayubu alipoeleza mahangaiko yake, Elihu alimsikiliza, naye alichochewa kusema. Angesema nini? Je, angemshutumu Ayubu au kujaribu kumchochea kubadili mtazamo wake kwa kumfanya ajihisi kuwa na hatia au kumwaibisha? Je, Elihu alijiona kuwa bora kuliko Ayubu? La hasha! Akichochewa na roho ya Mungu, Elihu alisema hivi: “Mimi ni kama wewe tu mbele za Mungu wa kweli; Mimi pia niliumbwa kutoka kwenye udongo.” Kisha akamhakikishia hivi Ayubu: “Hofu yoyote kutoka kwangu haitakutisha, wala mkazo kutoka kwangu hautakuwa mzito juu yako.” (Ayubu 33:6, 7) Badala ya kumtwika Ayubu mizigo mingine, Elihu alimshauri na kumtia moyo kwa njia ya upendo.

Tafadhali kumbuka kwamba tumeandaa broshua hii tukiwa na nia hiyohiyo. Kwanza tulisikiliza, kisha tukatafakari kwa makini hali na hisia za baadhi ya wale waliopeperuka. (Methali 18:13) Halafu tukachunguza Maandiko, na kwa sala tukachunguza masimulizi ya jinsi Yehova alivyowasaidia watumishi wake zamani walipokabili hali kama hizo. Hatimaye, tukajumlisha masimulizi hayo ya Kimaandiko na hali za kisasa ili tuandae broshua hii. Tunakualika kwa uchangamfu uchunguze habari hii. Uwe na hakika kwamba tunakupenda kwa dhati.

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova