Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dai la Uwongo la Mashetani Kwamba Wafu Wako Hai

Dai la Uwongo la Mashetani Kwamba Wafu Wako Hai

Biblia inasema kwamba Shetani ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9) Shetani na roho wake waovu hawataki tuamini Neno la Mungu, Biblia. Wanajaribu kuwafanya watu waamini kwamba wafu wako hai mahali fulani katika makao ya roho. Acheni tuone jinsi wanavyofanya hivyo.

Dini za Uwongo

Wanadamu, wanyama, samaki, na ndege​—wote ni nafsi

Dini nyingi hufundisha kwamba mwanadamu ana nafsi ambayo huenda kuishi katika makao ya roho baada ya mwili kufa. Zinafundisha kwamba mwili hufa lakini nafsi haifi. Isitoshe, zinasisitiza kwamba nafsi haiwezi kufa, kwamba ni kitu kisichoweza kufa.

Lakini Neno la Mungu halifundishi hivyo. Biblia inafundisha kwamba nafsi ni mtu, bali si kitu fulani kilicho ndani ya mtu. Kwa mfano, ikizungumzia kuumbwa kwa Adamu, Biblia inasema: “Yehova Mungu akamuumba mtu kutokana na mavumbi ya ardhi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, na mtu huyo akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7, maelezo ya chini) Hivyo basi, Adamu hakupewa nafsi; yeye mwenyewe alikuwa nafsi.

Wanyama wanaitwa nafsi pia.—Mwanzo 1:20, 21, 24, 30, maelezo ya chini.

Kwa kuwa katika Biblia neno “nafsi” linamaanisha mtu mwenyewe, haishangazi kujua kwamba nafsi zaweza kufa nazo hufa. Maandiko husema:

  • “Nafsi inayotenda dhambi ndiyo itakayokufa.”—Ezekieli 18:4.

  • “Kisha Samsoni akasema hivi kwa sauti kubwa: ‘Acha nafsi yangu ife pamoja na Wafilisti!’”—Waamuzi 16:30, maelezo ya chini.

  • “Je, ni halali kufanya mema au kufanya mabaya siku ya Sabato, kuokoa nafsi au kuua?”Marko 3:4, maelezo ya chini.

Biblia inafundisha kwamba nafsi yaweza kufa

Maandiko mengine yanaonyesha kwamba nafsi inaweza kuangamizwa (Zaburi 63:9, maelezo ya chini), kuuawa kwa upanga (Zaburi 22:20, maelezo ya chini), na kuzama au kufa maji (Yona 2:5, maelezo ya chini). Kwa hiyo, nafsi hufa.

Ukisoma Biblia kuanzia mwanzo mpaka mwisho, hutaona kamwe maneno “nafsi isiyoweza kufa.” Nafsi ya mwanadamu si roho. Fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa si fundisho la Biblia. Ni fundisho la Shetani na roho wake waovu. Yehova anachukia uwongo wote wa dini.—Methali 6:16-19; 1 Timotheo 4:1, 2.

Watu Wanaosiliana na Roho

Mashetani hujifanya kuwa roho za wafu

Njia nyingine anayotumia Shetani kupotosha watu ni kupitia watu wanaowasiliana na roho. Mtu anayewasiliana na roho ni mtu anayeweza kupokea jumbe moja kwa moja kutoka katika ulimwengu wa roho. Watu wengi sana, kutia ndani wale wanaowasiliana na roho, huamini kwamba jumbe hizo zinatoka kwa roho za wafu. Lakini kama vile ambavyo tumeona katika Biblia, hilo haliwezekani.—Mhubiri 9:5, 6, 10.

Hivyo basi, jumbe hizo hutoka kwa nani? Kwa mashetani wenyewe! Mashetani wanaweza kumchunguza mtu akiwa hai; wanajua jinsi alivyokuwa akiongea, alikuwa na sura gani, alifanya mambo gani, na alijua nini. Kwa hiyo si vigumu kwao kuwaiga watu waliokufa.—1 Samweli 28:3-19.

Hadithi za Uwongo

Njia nyingine ambayo Shetani hutumia kuendeleza uwongo kuhusu wafu ni kupitia hadithi za uwongo. Mara nyingi hadithi hizo huondoa fikira za watu kutoka kwa kweli ya Biblia.—2 Timotheo 4:4.

Watu fulani hufikiri wamewaona watu ambao wamerudi kutoka kwa wafu

Barani Afrika, kuna hadithi nyingi kuhusu watu ambao walionekana wakiwa hai baada ya kufa. Mara nyingi, watu kama hao huonekana mbali sana na mahali walipokuwa wakiishi. Lakini jiulize: ‘Je, ni jambo linalopatana na akili kwamba ikiwa mtu angekuwa na uwezo wa kurudi kutoka kwa wafu, angerudi mahali palipo mbali sana na familia na rafiki zake?’

Pia, je, haiwezekani kwamba mtu aliyeonwa anafanana tu na mtu aliyekufa? Kwa mfano, wahubiri wawili Wakristo waliokuwa wakihubiri katika eneo moja la vijijini walimwona mzee aliyewafuata kwa saa kadhaa. Walipomuuliza maswali, walipata kujua kwamba mtu huyo alifikiri kwamba mmoja wa wahubiri hao ni ndugu yake aliyekuwa amekufa miaka kadhaa iliyopita. Ni wazi kwamba alikuwa amekosea, hata hivyo, hakukubali kuamini kwamba alikuwa amekosea. Wazia hadithi ambayo baadaye mzee huyo aliwasimulia rafiki na jirani zake!

Maono, Ndoto, na Sauti

Mashetani hupotosha watu kupitia ndoto, maono, na sauti

Labda umesikia habari za mambo ya ajabu ambayo watu wameona, wamesikia, au wameota. Mambo hayo ya ajabu yanayopita uwezo wa kibinadamu mara nyingi huwaogopesha wale wanaoyaona. Marein, aliyekuwa akiishi Afrika ya Magharibi, alisikia kwa ukawaida sauti ya nyanya (bibi) yake aliyekufa ikimwita usiku. Akiwa na woga mwingi, Marein alikuwa akipiga mayowe, na kuamsha watu wote wa familia yake. Hatimaye, akawa kichaa.

Sasa, ikiwa kweli wafu wako hai, je, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba wangewaogopesha wapendwa wao? Bila shaka sivyo. Chanzo cha jumbe hizo zenye kuumiza ni mashetani.

Lakini namna gani jumbe ambazo huonekana kuwa zenye kusaidia na kufariji? Kwa mfano, Gbassay, wa Sierra Leone, alikuwa mgonjwa. Katika ndoto, alimwona baba yake aliyekuwa amekufa. Alimwagiza aende kwenye mti fulani, atwae jani, alichanganye na maji, na kunywa. Hakupaswa kuongea na mtu yeyote kabla ya kufanya hivyo. Alifanya hivyo naye akapona.

Mwanamke mwingine alisema kwamba mume wake alimtokea usiku mmoja baada ya kufa kwake. Alisema kwamba mume wake alionekana akiwa mzuri sana, akiwa amevaa mavazi mazuri sana

Maono na jumbe kama hizo huonekana kuwa nzuri na zenye kusaidia. Je, zinatoka kwa Mungu? Hapana, hazitoki kwake. Yehova ni “Mungu wa ukweli.” (Zaburi 31:5) Hawezi kamwe kukubali kutufanyia hila au kutudanganya. Mashetani tu ndio hufanya hivyo.

Basi je, kuna mashetani wema? Hapana. Hata ingawa huenda wakaonekana kuwa wenye kusaidia nyakati nyingine, wote ni wabaya. Ibilisi alipozungumza na Hawa, alionekana kuwa mwenye urafiki. (Mwanzo 3:1) Lakini Hawa alipatwa na matokeo gani baada ya kumsikiliza na kufanya alivyosema? Alikufa.

Shetani alisema Hawa hangekufa. Hawa alimwamini, lakini hatimaye alikufa

Si ajabu kwa mtu mbaya kuwaonyesha urafiki wale anaotaka kudanganya au kupunja. “Meno meupe, moyo mweusi,” yasema Methali ya Kiafrika. Na Neno la Mungu linasema: “Shetani mwenyewe huendelea kujifanya kuwa malaika wa nuru.”—2 Wakorintho 11:14.

Leo, Mungu hawasiliani tena na watu duniani kwa njia ya ndoto, maono, au sauti kutoka katika ulimwengu wa roho. Anawaongoza na kuwapa maagizo kupitia Biblia, ambayo inaweza kumfanya mtu awe “na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:17.

Kwa hiyo, Yehova anapotuonya kuhusu hila za Ibilisi, anafanya hivyo kwa sababu anatupenda. Anajua mashetani ni maadui hatari.