Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mashetani Hutia Moyo Kumwasi Mungu

Mashetani Hutia Moyo Kumwasi Mungu

Desturi fulani hutegemea uwongo wa kwamba wafu waweza kutuona

Lakini kwa nini Shetani na roho wake waovu hujitahidi sana kuwadanganya watu? Kwa sababu wanataka tujiunge nao katika uasi wao. Wanataka tuwaabudu. Wanataka tuamini uwongo wao na kufanya mambo ambayo Yehova hapendi. Mengi ya mambo hayo yanatia ndani desturi zinazohusu wafu.

Kifo cha mtu tuliyempenda ni jambo lenye kuumiza sana. Ni kawaida na inafaa kuonyesha huzuni. Baada ya kifo cha rafiki yake Lazaro, Yesu ‘alitokwa na machozi.’—Yohana 11:35.

Kuna desturi nyingi sana zinazoshirikishwa na kifo, nazo hutofautiana sana ulimwenguni kote. Nyingi hazivunji kanuni za Biblia. Hata hivyo, mazoea fulani, hutegemea wazo la kwamba wafu wako hai na wanaweza kuwaona walio hai. Makesha, maombolezo yanayopita kiasi, na mazishi yenye mapambo mengi, hufanywa kwa kuwa watu wanahofia kuzichukiza roho za wafu. Lakini kwa kuwa wafu “hawajui neno lolote kamwe,” wale wanaofanya mambo hayo wanaendeleza uwongo wa Shetani.—Mhubiri 9:5.

Desturi nyingine hutegemea uwongo wa kwamba wafu wanahitaji msaada wetu

Desturi au sherehe nyingine hutokana na imani ya kwamba wafu wahitaji msaada kutoka kwa walio hai na kwamba wanaweza kuwaumiza walio hai wasipotulizwa. Katika nchi fulani, sherehe hufanywa na dhabihu kutolewa siku 40 au mwaka mmoja baada ya kifo cha mtu. Inaaminika kwamba kufanya hiyo kutamsaidia aliyekufa ‘kuvuka’ na kuingia katika makao ya roho. Zoea lingine ambalo limeenea sana ni kuwaandalia wafu chakula na kinywaji.

Mambo hayo hayafai kwa sababu yanaendeleza uwongo wa Shetani kuhusu hali ya wafu. Je, Yehova angekubali tujihusishe hata kidogo katika desturi zinazotegemea mafundisho ya mashetani? La! Hasha—2 Wakorintho 6:14-18.

Watumishi wa Mungu wa kweli hawashiriki hata kidogo katika mazoea ambayo huunga mkono uwongo wa Shetani. Badala yake, wanachochewa na upendo kuwasaidia na kuwafariji walio hai. Wanajua kwamba mtu akiisha kufa, Yehova tu ndiye anayeweza kumsaidia.—Ayubu 14:14, 15.

Mungu Anashutumu Mazoea ya Kuwasiliana na Roho

Watu fulani huwasiliana na mashetani moja kwa moja au kupitia mjumbe wa kibinadamu. Ulozi, uchawi, mizungu, kubashiri, na kutafuta habari kuhusu wafu, zote hizo ni namna mbalimbali za kuwasiliana na roho.

Mungu anapinga mambo hayo mabaya. Yeye anataka watu wamwabudu yeye peke yake.—Kutoka 20:5

Biblia inashutumu mambo hayo, ikisema: “Asipatikane miongoni mwenu mtu yeyote . . . anayefanya uaguzi, mtu yeyote anayefanya uchawi, mtu yeyote anayetafuta ishara za ubashiri, mlozi, mtu yeyote anayewafunga wenzake kwa uchawi, mtu yeyote anayetafuta ushauri kutoka kwa watu wanaowasiliana na roho, mpiga ramli, au mtu yeyote anayetafuta habari kuhusu wafu. Kwa maana mtu yeyote anayefanya mambo haya ni chukizo kwa Yehova.”—Kumbukumbu 18:10-12.

Kwa nini Yehova anatuonya kwa uthabiti sana hivyo dhidi ya mazoea hayo?

Yehova anatuonya dhidi ya namna zote za kuwasiliano na roho kwa faida yetu wenyewe. Anawapenda na kuwajali watu, naye anajua kwamba wale wanaojihusisha na mashetani wataumia.

Nchini Brazili, Nilda alikuwa na mazoea ya kuwasiliana na roho. Mashetani walimtesa sana. Mwanamke huyo anasimulia hivi: “Roho hao . . . walinipagaa, wakiniamrisha huku na huku. Nilipoteza fahamu mara kwa mara nami nikalazwa hospitalini nikiwa na matatizo ya akili. Mashetani hao walinitesa sana hivi kwamba mishipa yangu ya fahamu iliathirika. Nilitumia dawa za kunituliza, nami nikawa mraibu wa pombe na sigara. Hali hiyo iliendelea kwa miaka mingi.”

Mara nyingi wale walio na mazoea ya kuwasiliana na roho huumia. Wanaweza kupoteza makao yao, uhuru wao, hata uhai wao.

Baada ya muda, kwa msaada wa Yehova na Mashahidi wake, Nilda akawa huru kutokana na uvutano wa mashetani na sasa anaishi maisha mazuri yenye kusudi. Anasema hivi: “Nawahimiza wote, wasijihusishe kamwe, hata kidogo, na roho [waovu].”