Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Roho Si Viumbe Walioishi Duniani Kisha Wakafa

Roho Si Viumbe Walioishi Duniani Kisha Wakafa

Roho wako! Katika makao ya roho yasiyoonekana, kuna roho wema na wabaya pia. Je, roho hao ni watu walioishi duniani na baadaye wakafa?

La, sivyo. Mtu anapokufa, haendi kuishi katika ulimwengu wa roho, kama watu wengi wanavyofikiri. Tunajuaje? Biblia inasema hivyo. Biblia ni kitabu cha kweli kinachotoka kwa Mungu wa pekee wa kweli, ambaye jina lake ni Yehova. Yehova aliumba wanadamu; anajua vema linalowapata wanapokufa.—Zaburi 83:18; 2 Timotheo 3:16.

Adamu alitoka mavumbini, naye alirudi mavumbini

Biblia inasema kwamba Mungu alimfanya mtu wa kwanza, Adamu, “kutokana na mavumbi ya ardhi.” (Mwanzo 2:7) Mungu alimweka katika bustani ya Edeni iliyokuwa Paradiso. Kama Adamu angetii sheria ya Yehova, asingekufa; bado angekuwa hai duniani leo. Lakini Adamu alipovunja sheria ya Mungu kimakusudi, Mungu alimwambia: ‘utarudi ardhini, kwa kuwa ulitolewa humo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.’—Mwanzo 3:19.

Hilo linamaanisha nini? Adamu alikuwa wapi kabla Yehova hajamuumba kutokana na mavumbi? Hakuwa popote. Hakuwa kiumbe wa roho huko mbinguni, ambaye baadaye angezaliwa akiwa mwanadamu. Hakuwa popote. Hivyo basi, Yehova aliposema kwamba Adamu ‘atarudi ardhini,’ alimaanisha kwamba Adamu atakufa. Hakuenda kuishi katika makao ya roho. Alipokufa, Adamu alipoteza uhai, hakuwako tena. Kifo ni kinyume cha uhai.

Lakini namna gani wengine ambao wamekufa? Je, ina maana kwamba wao pia hawapo popote? Biblia inasema:

  • “Wote [wanadamu na wanyama] wanaenda mahali palepale. Wote wanatoka mavumbini, na wote wanarudi mavumbini.”—Mhubiri 3:20.

  • “Waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.”—Mhubiri 9:5.

  • “Upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari umetoweka.”—Mhubiri 9:6.

  • “Hakuna kazi wala mipango wala ujuzi wala hekima Kaburini, mahali unapokwenda.”—Mhubiri 9:10.

  • “[Mtu] hurudi ardhini; Siku hiyohiyo mawazo yake hupotea.”—Zaburi 146:4.

Walio hai ndio tu wanaoweza kufanya mambo haya

Je, unaona vigumu kukubali maandiko hayo yanavyosema? Ikiwa ndivyo, fikiria hili: Katika familia nyingi, mwanamume hufanya kazi ili apate pesa za kuruzuku familia yake. Mwanamume huyo anapokufa, kwa kawaida familia yake hupatwa na hali ngumu. Nyakati fulani mke wake na watoto wake hukosa hata pesa za kununua chakula. Huenda hata adui za mwanamume huyo wakawatendea vibaya. Sasa jiulize: ‘Ikiwa mwanamume huyo yuko hai katika ulimwengu wa roho, kwa nini haendelei kuiandalia familia yake? Kwa nini halindi familia yake dhidi ya watu wabaya?’ Ni kwa sababu maandiko hayo yanasema kweli. Mwanamume huyo hayuko hai, hawezi kufanya lolote.—Zaburi 115:17.

Wafu hawawezi kuwasaidia wenye njaa au kuwalinda wanaotendewa vibaya

Je, inamaanisha kwamba wafu hawatakuwa hai tena kamwe? La, sivyo. Baadaye tutazungumzia ufufuo. Lakini inamaanisha kwamba wafu hawajui unalofanya. Hawawezi kukuona, kukusikia, au kuongea nawe. Huna haja ya kuwaogopa. Hawawezi kukusaidia, na hawawezi kukuumiza.—Mhubiri 9:4; Isaya 26:14.