Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Yako ni Jambo la Kuhangaikiwa?

Imani Yako ni Jambo la Kuhangaikiwa?

Unafikiri maisha yana kusudi? Mwana-mageuzi William B. Provine anasema: “Mambo ambayo tumejifunza kuhusu mageuzi yamekuwa na matokeo makubwa kwetu, yanaathiri maoni yetu kuhusu kusudi la maisha.” Alikata kauli gani? “Sioni kusudi lolote la mwanadamu wala ulimwengu.”32

Fikiria uzito wa maneno hayo. Ikiwa maisha hayana kusudi lolote, basi kuwa kwako hai hakuna kusudi lolote isipokuwa labda tu kufanya mema kidogo na ikiwezekana kuachia vizazi vijavyo sifa na tabia zako. Kisha ukifa, umetoweka milele. Ubongo wako, pamoja na uwezo wake wa kufikiri na kutafakari kusudi la maisha, ungekuwa tu tokeo la matukio yasiyo na mpangilio wowote.

Isitoshe, watu wengi wanaoamini mageuzi hudai kwamba hakuna Mungu au kwamba hataingilia mambo ya wanadamu. Vyovyote vile, wakati wetu ujao ungetegemea viongozi wa kisiasa, kielimu, na kidini. Tukizingatia jinsi ambavyo wamekuwa wakijiendesha, basi hakungekuwa na mwisho wa machafuko, mapigano, na ufisadi ambao umeikumba jamii ya wanadamu. Ikiwa kwa kweli fundisho la mageuzi ni la kweli, basi kungekuwa na sababu za kuishi kulingana na kauli-mbiu hii hatari: “Tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.”—1 Wakorintho 15:32.

Tofauti na hilo, Biblia inafundisha kwamba kwa Mungu “iko chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Maneno hayo yanastahili kufikiriwa kwa uzito.

Ikiwa yale ambayo Biblia inasema ni kweli, basi maisha yana kusudi. Muumba wetu ana kusudi lenye upendo kwa ajili ya wale wanaochagua kuishi kulingana na mapenzi yake. (Mhubiri 12:13) Kusudi hilo linatia ndani ahadi ya kuishi katika ulimwengu mpya usio na machafuko, mapigano, ufisadi, wala kifo.—Zaburi 37:10, 11; Isaya 25:6-8.

Wakiwa na sababu nzuri, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanaamini kwamba kujifunza kumhusu Mungu na kumtii huwapa kusudi halisi maishani! (Yohana 17:3) Imani hiyo si ndoto. Kuna uthibitisho mwingi wa kwamba uhai uliumbwa.