Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaamini Nini?

Unaamini Nini?

Watu fulani wanaodai kwamba wanaamini masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji husema kwamba dunia na vyote vilivyomo viliumbwa katika siku sita za saa 24, miaka elfu kumi hivi iliyopita. Wengine hudai kwamba hakuna Mungu, Biblia ni kitabu cha hekaya, na viumbe vyote vyenye uhai vilitokea kiholela.

Watu wengi huunga mkono mojawapo ya dhana hizo, au wana imani iliyo tofauti kidogo. Huenda kuisoma kwako broshua hii kunaonyesha kwamba wewe pia unapendezwa na suala la chanzo cha uhai. Huenda unaamini kwamba kuna Mungu, na unaiheshimu Biblia. Wakati uleule, unaheshimu pia maoni ya wanasayansi waliobobea katika taaluma zao, ambao wanaamini kwamba uhai ulijitokeza wenyewe. Ikiwa wewe ni mzazi, huenda usijue jinsi ya kuwajibu watoto wako wanapokuuliza kuhusu mageuzi au uumbaji.

Kusudi la Broshua Hii

Habari zilizo katika broshua hii hazikusudiwi kudhihaki wenye maoni tofauti kuhusu uumbaji au wale wasioamini kuwapo kwa Mungu. Badala yake, tunatumaini kwamba broshua hii itakuchochea kufikiria kwa uzito ni kwa nini unaamini mambo unayoamini. Itachanganua masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji, masimulizi ambayo huenda hujawahi kuyafikiria kwa njia hiyo. Pia, itakazia kwa nini ni vizuri kuzingatia msingi wa mambo unayoamini kuhusu chanzo cha uhai.

Je, utaamini madai ya wale wanaosema kwamba hakuna Muumba mwenye akili na kwamba Biblia haitegemeki? Au utachunguza yale hasa ambayo Biblia inasema? Ni mafundisho gani unayoweza kutegemea na kuamini: ya Biblia au ya wanamageuzi? (Waebrania 11:1) Tunakutia moyo uchunguze ukweli wa mambo.