Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 17

Yesu Afundisha Kuhusu Ufalme wa Mungu

Yesu Afundisha Kuhusu Ufalme wa Mungu

Yesu awafundisha wanafunzi wake mambo mengi, hata hivyo akazia jambo moja kuu—Ufalme wa Mungu

KWA nini Yesu alikuja duniani? Yeye mwenyewe alisema: “Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu . . . kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Fikiria mambo manne ambayo Yesu alifundisha kuhusu Ufalme, jambo kuu katika mahubiri yake.

1. Yesu aliteuliwa kuwa Mfalme. Yesu alisema waziwazi kwamba yeye ndiye Masihi aliyeahidiwa. (Yohana 4:25, 26) Pia, alionyesha kwamba ndiye Mfalme ambaye nabii Danieli aliona katika maono. Yesu aliwaambia mitume wake kwamba siku moja ataketi juu ya ‘kiti cha ufalme chenye utukufu’ na kwamba wao pia wataketi juu ya viti vya ufalme. (Mathayo 19:28) Alikiita kikundi hicho cha watawala “kundi dogo,” naye alisema kwamba ana “kondoo wengine,” ambao si sehemu ya kikundi hicho.—Luka 12:32; Yohana 10:16.

2. Ufalme wa Mungu utaleta haki ya kweli. Yesu alionyesha kwamba Ufalme utaondolea mbali ukosefu mkubwa zaidi wa haki kwa kulitakasa, au kulifanya kuwa takatifu, jina la Yehova Mungu na kuliondolea masuto yote ambayo Shetani amelimbikiza juu ya jina hilo tangu uasi wa Edeni. (Mathayo 6:9, 10) Pia, Yesu alionyesha kila siku kwamba hana ubaguzi, kwa kuwahubiria wanaume kwa wanawake, matajiri kwa maskini. Ijapokuwa alipaswa kuwafundisha Waisraeli hasa, alikuwa tayari kuwasaidia Wasamaria na Watu wa Mataifa au wasio Wayahudi. Tofauti na viongozi wa dini wa siku zake, hakuonyesha upendeleo hata kidogo.

3. Ufalme wa Mungu si sehemu ya ulimwengu huu. Yesu aliishi wakati ambapo kulikuwa na misukosuko mingi. Nchi ya kwao ilikuwa ikitawaliwa na serikali ya nchi nyingine. Hata hivyo, watu walipojaribu kumhusisha katika masuala ya kisiasa ya siku zake, alijiondoa. (Yohana 6:14, 15) Alimwambia mwanasiasa mmoja: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Nao wafuasi wake, aliwaambia: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Hakuwaruhusu kutumia silaha za vita, hata kwa kusudi la kumlinda yeye mwenyewe.—Mathayo 26:51, 52.

“Akaanza kusafiri . . . kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.”—Luka 8:1

4. Kristo atatawala kwa upendo. Yesu aliahidi kwamba atawaburudisha watu, na kuwapumzisha mizigo yao. (Mathayo 11:28-30) Ndivyo alivyofanya. Alitoa mashauri yenye upendo na yenye kutumika kuhusu kukabiliana na mahangaiko ya maisha, kuboresha mahusiano, kuepuka kufuatia vitu vya kimwili, na kupata furaha. (Mathayo, sura ya 5-7) Kwa sababu alionyesha upendo watu wa tabaka zote walipenda kuwa pamoja naye. Hata watu wa hali ya chini walimiminika kwake, wakiwa na hakika kwamba atawatendea kwa fadhili na heshima. Kwa kweli Yesu atakuwa Mtawala asiye na kifani!

Kuna njia nyingine yenye matokeo sana ambayo Yesu alitumia kuwafundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu. Alifanya miujiza mingi. Kwa nini? Tutaona.

—Inatoka kwenye Kitabu cha Mathayo, Marko, Luka, na Yohana.