Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 19

Yesu Atabiri Matukio ya Wakati Ujao Yatakayoikumba Dunia Nzima

Yesu Atabiri Matukio ya Wakati Ujao Yatakayoikumba Dunia Nzima

Yesu ataja mambo yatakayotia alama kuwapo kwake katika mamlaka ya kifalme na ya umalizio wa mfumo wa mambo

KATIKA Mlima wa Mizeituni, ambapo jiji la Yerusalemu na hekalu lake lilikuwa likionekana vizuri, mitume wanne wa Yesu walimuuliza faraghani kuhusu mambo fulani aliyokuwa amezungumzia. Yesu alikuwa ametoka kusema kwamba hekalu lililo Yerusalemu litaharibiwa. Na mapema, alikuwa amewaambia kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 13:40, 49) Sasa mitume wakamuuliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”—Mathayo 24:3.

Akiwajibu, Yesu aliwaambia mambo ambayo yangetokea kabla ya Yerusalemu kuharibiwa. Lakini maneno yake yalikuwa na utimizo zaidi. Unabii wake ungetimizwa kwa kiwango kikubwa zaidi ulimwenguni pote. Yesu alitabiri matukio na hali za ulimwengu ambazo zingekuwa ishara. Ishara hiyo ingewaonyesha walio duniani kwamba kuwapo kwa Yesu akiwa Mfalme mbinguni kumeanza. Yaani, ishara hiyo ingeonyesha kwamba Yehova Mungu amemfanya Yesu kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi ulioahidiwa zamani za kale. Ishara hiyo ingemaanisha kwamba karibuni Ufalme huo utaondolea mbali uovu na kuwaletea wanadamu amani. Mambo ambayo Yesu alitabiri yangetia alama siku za mwisho za mfumo huu wa kale wa mambo—mifumo ya dini, siasa, na kijamii iliyopo leo—na kuashiria mwanzo wa mfumo mpya.

Akieleza mambo ambayo yangetokea duniani wakati wa kuwapo kwake akiwa Mfalme mbinguni, Yesu alisema kwamba kungekuwa na vita kati ya mataifa, upungufu wa chakula, matetemeko makuu ya ardhi, na magonjwa yenye kuenea. Uvunjaji wa sheria ungeongezeka. Wanafunzi wa kweli wa Yesu wangehubiri habari njema za Ufalme wa Mungu katika dunia yote. Yote hayo yangeishia katika “dhiki kuu” ambayo haijapata kutokea tena.—Mathayo 24:21.

Wafuasi wa Yesu wangejua jinsi gani kwamba dhiki hiyo iko karibu? Yesu aliwaambia: “Jifunzeni jambo hili kutokana na mtini.” (Mathayo 24:32) Majani ya mtini yanapotokea kwenye matawi ni ishara ya kwamba msimu wa kiangazi unakaribia. Vivyo hivyo, kutokea kwa ishara zote hizo alizotabiri Yesu katika kipindi kimoja cha wakati kungekuwa ishara ya kwamba mwisho uko karibu. Hakuna yeyote ila Baba aliyejua siku na saa barabara ambayo dhiki kuu ingeanza. Kwa hiyo, Yesu aliwahimiza hivi wanafunzi wake: “Endeleeni kukesha, kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni gani.”—Marko 13:33.

—Inatoka kwenye Mathayo, sura ya 24 na 25; Marko, sura ya 13; Luka, sura ya 21.

^ fu. 14 Unaweza kupata habari zaidi kuhusu unabii wa Yesu katika Sura ya 9 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.