Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ulimwengu Usio na Vita Utakuwako Wakati Wowote?

Je, Ulimwengu Usio na Vita Utakuwako Wakati Wowote?

1, 2. Ni maswali gani huzuka kuhusu wakati ujao wa ulimwengu?

TANGU lianzishwe likiwa taifa la kisasa katika 1948, Israeli limekuwa tayari kujilinda dhidi ya majirani wake. Kabiliano hili, bishano hili lenye kuendelea, limeacha pande zote mbili zikiwa na akina mama wengi, wanawake, watoto, na wengine waliofiwa na wenye kuomboleza. Hata hivyo, mojayapo tamaa za asili za ainabinadamu, hasa katika kiwango cha familia, ni kuweza kuishi kwa amani.

2 Hata hivyo, vita na ugomvi si matatizo ya Mashariki ya Kati tu. Hali zenye wasiwasi zikingojea tu uchochezi kidogo ndipo zilipuke zaonekana kotekote ulimwenguni. Hivyo swali ni, Je! amani, si katika Mashariki ya Kati tu bali amani ya ulimwengu, itapatikana wakati wowote? Ikiwa ndivyo, itatimizwaje? Je! itakuwa kwa njia ya nia njema ya ainabinadamu ya kisiasa, kidini, na kikabila? Je! hiyo inaelekea kutukia? Au je, Mungu, ambaye ndiye Mwenye dunia na ndiye Aliyeiumba, atalazimika kuingilia mambo?

3-5. (a) Ni ahadi gani kuhusu amani inayotolewa katika Biblia? (b) Ni maswali gani yanayohitaji uchunguzi zaidi?

3 Maandiko ya Kiebrania hutupa sisi unabii mbalimbali wenye kutia moyo juu ya wakati ambao mataifa “yatafua panga zao ziwe majembe ya plau na mikuki yao iwe miundu ya kupogolea: taifa halitainua upanga dhidi ya taifa; hayatajua vita tena kamwe.”—Isaya 2:4.

4 Si Isaya pekee aliyenena juu ya amani hiyo ya ulimwenguni pote. (Zaburi 46:9-11 [46:8-10, UV]) Kwa kweli, wakati wa amani kamili na upatani miongoni mwa watu ndicho kichwa kikuu katika Biblia. Kama vile mkuu mmoja wa serikali Mwisraeli ambaye pia ni mtunga-vitabu Abba Eban alivyosema, Maandiko ya Kiebrania yaliwapa Waisraeli wa kale maoni na tumaini la wakati ujao la pekee sana, kwani ni “Israeli pekee lililotazama mbele kwenye pindi ya furaha na ufanisi katika wakati ujao.”1 Naam, wakati ujao mzuri ajabu u karibu sana kwa ajili ya ainabinadamu yote, mwisho wa vita, na mambo mengi zaidi. Isaya alitoa unabii pia juu ya hali za Paradiso duniani pote—mwisho wa umaskini, magonjwa, na hata kifo.—Isaya 11:9; 25:8; 33:24; 35:5, 6; 65:21.

5 Huenda wengine wakajibu, ‘Unabii huo mbalimbali uliandikwa maelfu ya miaka iliyopita, hata hivyo vita vingali viko. Biblia inaweza kufikiriwaje kuwa chanzo chenye kutegemeka cha tumaini? Kuna uthibitisho gani imara kwamba kweli kweli Biblia ni Neno la Mungu?’