Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumjua Mungu wa Kweli​—Kwamaanisha Nini?

Kumjua Mungu wa Kweli​—Kwamaanisha Nini?

1, 2. Kulingana na Isaya 2:3, ni mwaliko gani unaotolewa katika siku za mwisho, na kwa nani?

UNABII wa Isaya wenye kuchochea mawazo kuhusu siku za mwisho una mwaliko upaswao kupendeza watu wa kila taifa. Mwaliko huo ni wa kupata kumjua Mungu wa kweli kibinafsi: “Na watu wa vikundi vingi watakwenda na kusema: ‘Njoni, acheni sisi tupande kwenye Mlima wa BWANA, kwenye Nyumba ya Mungu wa Yakobo; ili Yeye aweze kutufunza sisi katika njia Zake, na ili sisi tuweze kutembea katika vijia Vyake.’” *Isaya 2:3.

2 Unabii huo huonyesha kwamba katika siku za mwisho, mataifa mengi ulimwenguni pote yangeongozwa kwenye chanzo kimoja cha mafunzo ili kuyasaidia yapate kumjua yule Mungu wa kweli. Ni kweli zipi ambazo mataifa hayo yatajifunza zinazotumika katika kuyaunganisha katika vifungo vya amani ya kweli?

3. Sehemu yenye maana ya Biblia ilikaribiaje sana kupotezwa kama tokeo la pokeo?

3 Sehemu yenye kutokeza ya Biblia, iliyokaribia sana kupotea kwa sababu ya pokeo, ni ile ya kuanzisha uhusiano na Mungu, Baba na Muumba wetu wa kimbingu, kwa msingi wa kibinafsi sana, kwa kumwita kwa jina lake. Ni mtu yupi aliye na rafiki mpendwa na mwenye kuthaminiwa sana ambaye jina lake akataa kutumia au hata kulitamka aulizwapo juu yalo? Kwa kawaida ni adui tu ambaye hudharauliwa sana hivi kwamba mtu hupenda kutomheshimu hata kwa kutamka jina lake. Ule uhusiano wa pekee uliokuwako kati ya Israeli wa kale na Mungu wao—ambapo walimjua kwa jina lake—unaonyeshwa vizuri sana na mtunga zaburi wa kale: “Kwa sababu amejitoa Kwangu Mimi nitamwokoa; Mimi nitamhifadhi salama, kwa maana yeye ajua jina Langu.”—Zaburi 91:14.

Je! Yatupasa Kutumia Jina la Mungu?

4, 5. Ni nini maana ya jina la Mungu?

4 Kwa maoni ya Biblia, hakujapata kamwe kuwa na shaka yoyote juu ya jina la Mungu wa kweli. Wakati Mungu aliposema na Musa, akimweleza kwamba Yeye angemtumia kuongoza taifa la Israeli kutoka utumwa wa Misri, Musa aliuliza swali la akili: “Nijapo kwa Waisraeli na kusema kwao ‘Yule Mungu wa baba zenu amenituma kwenu,’ nao waniulize, ‘Jina Lake ni nani?’ nitasema nini kwao?” Mungu akajibu: “Utasema hivi kwa Waisraeli: BWANA [Kiebrania יהוה=YHWH= Yahweh, au tangu karne ya 13 W.K., Yehova], yule Mungu wa baba zenu, yule Mungu wa Abrahamu, yule Mungu wa Isaka, na yule Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu: Hilo ndilo jina Langu milele, hilo [ndilo ukumbusho, JP] Wangu kwa umilele wote.”Kutoka 3:13, 15, italiki ni zetu.

5 Jina hilo linajaa maana kwa mtu asemaye lugha ya Kiebrania. Latokana na shina la msingi la Kiebrania הוה, h·w·h, kumaanisha “kupata kuwa.” Hata hivyo, jina hilo liko katika fani sababishi, Hiph·ʽilʹ, kulingana na sarufi ya Kiebrania. Kwa hiyo maana yake ya msingi haihusiani na kuwako kwa milele kwa Mungu bali inahusiana na kusababisha kwake vitu vipate kuwa au vitokee. Hiyo ni kweli hasa kwa njia ya pekee kuhusiana na makusudi yake. Kwa kuwa alikusudia kuweka huru taifa lake chaguliwa kutoka utumwa wa Misri, hivyo yeye alisababisha iwe hivyo. Hapana nguvu ambayo ingeweza kuzuia mapenzi yake yaliyosemwa. Yehova ndiye Mungu ambaye husababisha makusudi yake yatimie. Hivyo yeye hujisababisha mwenyewe apate kuwa Mtimizaji wa ahadi zake. Ilikuwa hivyo pia kuhusu kusudi lake la kukomboa taifa lake katika utekwa wa Kibabuloni. Na ndivyo ilivyo kuhusiana na kusudi lake la kuleta hali za kiparadiso kwenye dunia hii. Jina lake lenyewe latoa maana na uhakikisho kwa ahadi hizo.—Isaya 41:21-24; 43:10-13; 46:9, 10.

6-9. (a) Sisi twajuaje kwamba Mungu hakatazi utumizi wa jina lake? (b) Ni namna gani na wakati gani katazo la utumizi wa jina la Mungu lilipopata kuwa sehemu ya Dini ya Kiyahudi?

6 Lakini je, zile Amri Kumi hazikatazi kutajwa kwa jina la Mungu? Sivyo kabisa! Ijapokuwa wengi wamefasiri ile amri ya tatu kwa njia hiyo, angalia jambo ambalo Encyclopaedia Judaica hueleza: “Kule kuepuka kutamka jina YHWH . . . kulisababishwa na kueleweka kimakosa kwa ile Amri ya Tatu (Kut. 20:7; Kum. 5:11) kuwa kukimaanisha ‘Wewe hutachukua jina la YHWH Mungu wako bure,’ hali kwa kweli humaanisha ‘Wewe hutaapa kibandia kwa jina la YHWH Mungu wako.’”5 Angalia kwamba andiko hilo halikatazi ‘kuchukua’ au kutamka jina la Mungu. Hata hivyo, hata kama ilimaanisha kulichukua jina la Mungu “bure,” angalia jinsi kamusi ya Kiebrania ya Koehler na Baumgartner hutaarifu kuhusu usemi wa Kiebrania uliotafsiriwa “bure” (Kiebrania, lash·shawʹʼ): “tamka jina bila sababu . . . tumia jina vibaya.”6 Kwa hiyo, amri hiyo haikatazi kutumia jina la Mungu, bali kulitumia vibaya.

7 Lakini namna gani ile hoja ya kwamba jina la Mungu ni “takatifu mno kuweza kutamkwa?” Basi, je, haielekei kuwa jambo la akili kwamba kama Mungu aliona jina lake kuwa takatifu mno kwa wanadamu kuweza kulitamka, hangalilifunua kabisa? Uhakika wa kwamba katika maandishi ya awali ya Maandiko ya Kiebrania, jina la Mungu la kibinafsi huonekana mara zaidi ya 6,800, huonyesha kwamba yeye hutaka watu wamjue na kutumia jina lake. Tofauti sana na kuwekea mipaka utumizi wa jina lake ili kuzuia lisitendewe kwa njia isiyo ya staha, Mungu hutia moyo kwa kurudia-rudia na hata huwaamuru watu wake watumie jina lake na kulijulisha. Kufanya hivyo kulikuwa uthibitisho wa uhusiano wao wa karibu pamoja naye na pia upendo wao kwake. (Zaburi 91:14) Nabii Isaya, alionyesha waziwazi ni nini yaliyo mapenzi ya Mungu kuhusu jambo hilo wakati alipotaarifu hivi: “Sifuni BWANA [Kiebrania, יהזה=YHWH=Yehova], pigeni mbiu ya jina Lake. Fanyeni matendo yake yajulikane miongoni mwa vikundi vya watu; julisheni kwamba jina Lake limetukuka.”—Isaya 12:4. Ona pia Mika 4:5; Malaki 3:16; Zaburi 79:6; 105:1; Mithali 18:10.

8 Ikiwa Yehova hakutaka watu watamke jina lake, angalikataza jambo hilo waziwazi. Hata hivyo, hapana mahali popote ambapo Biblia hukataza utumizi mzuri au kutamka jina lake. Wanaume waaminifu wa nyakati za Biblia walitumia sana jina lake. (Mwanzo 12:8; Ruthu 2:4; 4:11, 14) Kwa kweli, Mungu alishutumu kwa kurudia-rudia wale ambao wangesababisha watu wake wasahau jina lake takatifu.—Yeremia 23:26, 27; Zaburi 44:21, 22 (44:20, 21, UV).

9 Lakini katazo hilo lilipataje kuwa sehemu ya kuwaza kwa Wayahudi, kwa kuwa ni wazi sana halikuwa sehemu ya Biblia? Maelezo ya Dakt. A. Cohen, aliye rabi na mtungaji wa kitabu Everyman’s Talmud, huonyesha kwamba pokeo hilo lilipata kuimarishwa hatua kwa hatua kwa kipindi cha karne nyingi. Dakt. Cohen aandika hivi: “Katika kipindi cha Biblia yaelekea hakukuwa na kusita-sita kulitumia katika maongezi ya kila siku. Kuongezwa kwa Yah au Yahu kwenye majina ya kibinafsi, ambako kuliendelea miongoni mwa Wayahudi hata baada ya uhamisho wa Babuloni, ni kidokezi cha kwamba hakukuwa na katazo dhidi ya utumizi wa lile Jina lenye herufi nne. Lakini mapema katika kipindi cha kirabi kutamkwa kwa Jina hilo kuliruhusiwa [wakati tu wa] ibada katika Hekalu.” Kuhusu maendeleo mengine wakati wa kipindi hicho, asema hivi: “Badala ya YHWH Jina hilo lilitamkwa Adonai (Bwana wangu) katika ibada ya Sinagogi; lakini kuna pokeo la kwamba tamko la awali lilipitishwa na Wasomi kwa wanafunzi wao pindi kwa pindi—mara moja au mbili kila miaka saba (Kiddushin 71a). Hata zoea hilo lilikoma baada ya wakati, na njia ya kutamka Jina hilo haijulikani tena kwa uhakika.”7 Hayo ndiyo yaliyokuwa matokeo ya “amri za wanadamu.”—Isaya 29:13; Kumbukumbu la Torati 4:2; ona Sehemu ya “Biblia—Je! Imepuliziwa na Mungu?,” mafungu 15-16.

Matakwa kwa Wale Wachukuao Jina Hilo

10-14. (a) Mungu hutaka nini kwa wale ambao huchukua jina lake? (b) Ni namna zipi za usafi hutakwa kwa wale watakao kumpendeza Mungu? (c) Ni uvutano gani wa kigeni wa kipagani ulioacha alama yenye kina juu ya Dini ya Kiyahudi?

10 Kwa wazi, kujua tu au hata kutumia jina la Mungu hakutoshi ili mtu ampendeze Mungu. Kuchukua jina la Mungu mtu akiwa mmoja wa waabudu wake wa kweli ni pendeleo la pekee sana, kama vile nabii Yeremia alivyopiga mbiu: “Neno lako liliniletea upendezi mwingi na shangwe ya kujua kwamba jina Lako limeshikamanishwa na mimi.” (Yeremia 15:16) Lakini pendeleo hili tukufu huleta daraka zito. Yehova aliwaambia kwa mkazo wafalme wa mataifa Wasio Wayahudi hivi: “Mimi naleta adhabu kwanza juu ya jiji ambalo huchukua jina Langu.” (Yeremia 25:29) Wakati Yehova alipoachilia taifa la Israeli kutoka utekwa wa miaka 70 katika Babuloni, alikuwa tayari amewaonya watu wake kupitia nabii Isaya: “Geukeni, geukeni mbali, msiguse chochote kilicho kichafu mwondokapo kutoka huko; jiwekeni safi, mtokapo huko, nyinyi mchukuao vyombo vya BWANA [יהזה]!” (Isaya 52:11) Ni nini lingehusika leo katika kujiweka safi wakiwa waabudu wa kweli, wakiwa wachukuaji wa jina la Mungu mtakatifu zaidi, Yehova?

11 Hakika mtu atamaniye kumpendeza Mungu katika ibada yake angalipaswa kuendelea kuwa safi katika mwenendo, hasa kwa habari ya viwango vya adili ambavyo Mungu mwenyewe huweka. Tofauti na viwango vyenye kuendekeza vya jamii ya leo, Maandiko hayaachi shaka au kutoa nafasi ya kufasiri yanapoonyesha kwamba Mungu hulaani kusema uwongo, wivi, uasherati, uzinzi, ugoni-jinsia-moja, uuaji-kimakusudi, na kila namna ya udanganyifu. (Kutoka 20:12, 13 [20:12-16, UV]; 23:1, 2; Mambo ya Walawi 5:1; 19:35, 36; 20:13) Maandiko hulaani si tendo baya lenyewe tu bali pia kule kufikiri kubaya ambako huongoza kwenye mwenendo mbaya.​—Kutoka 20:14 (20:17, UV); Mambo ya Walawi 19:17; Zaburi 14:1-5; Ayubu 31:1, 9-11.

12 Kuongezea usafi wa kiadili, hakika usafi wa kidini ungetakwa kwa wale wachukuao jina la Yehova. Yehova alionya taifa la Israeli la kale kwa kurudia-rudia lisivutwe na kufikiri, mazoea, na desturi za kidini za mataifa jirani, walioabudu miungu mingine. Kwa kweli, ni kwa sharti hilo pekee—kwamba hawangeiga ibada bandia ya mataifa—kwamba wangeendelea kukaa katika Nchi ya Ahadi. (Mambo ya Walawi 18:24-30; Kumbukumbu la Torati 12:29-31) Si ibada ya sanamu pekee iliyokatazwa waziwazi bali pia namna zote za mazoea na imani za kishirikina, kama vile unajimu, uwasiliano na roho, ubashiri wa matukio, mizungu, na kuomba au kuulizia habari za wafu.—Kutoka 20:3-5; 22:17 (22:18, UV); Mambo ya Walawi 20:27; Kumbukumbu la Torati 18:9-13; Isaya 8:19, 20; 47:13; Yeremia 10:2.

13 Unaohusiana sana na usafi wa kidini ni lile jambo la usafi wa kimafundisho. Lile onyo la kutoiga adili na ibada ya mataifa yaliyowazunguka lilitumika zaidi ya wakati tu taifa la Israeli lilipotwaa nchi kutoka kwa Wakanaani. Yehova alikuwa amefunulia watu wake kweli za kidini. Ni wao tu walioabudu yule Mungu wa kweli, Yehova. (Kutoka 19:5, 6; Kumbukumbu la Torati 4:32-37; Zaburi 147:19, 20) Ni wao tu waliomjua Mungu huyo kibinafsi na, wakiwa mashahidi wake, walikuwa katika hali ya kuweza kuwafundisha wengine juu yake. (Isaya 43:9-12; Zaburi 105:1) Kwa kutofautisha, desturi na mazoea ya kidini ya mataifa mengine yalionyesha ukosefu wa msingi wa ujuzi wa Mungu.—Isaya 60:2.

Sakafu hii ya Sinagogi la kale katika Tiberio, Israeli, ni mfano mmoja tu wa kadiri ambayo wazo na utamaduni wa Kigiriki vilitia uvutano juu ya Dini ya Kiyahudi. Angalia ishara za zodiaki (nyota) majina yayo yakiwa yameandikwa kwa Kiebrania. Umbo lililo katikati ni kijimungu-jua Heliosi

14 Ujapokuwa mwanzo walo mzuri, taifa la Israeli lilivutwa kwa kurudia-rudia na mawazo ya kidini ya kigeni. (Waamuzi 2:11-13; 1 Wafalme 18:21; Yeremia 2:11-13; Ezekieli 8:14-18) Ingawa Wakanaani na Wababuloni waliacha alama yao ya utamaduni yenye kudumu, ushindani mkubwa zaidi sana uliopata kukabili Dini ya Kiyahudi ulikuja wakati wa kipindi cha uvutano wa utamaduni wa Kigiriki wa Milki ya Kigiriki. * Akitoa muhtasari wa kipindi hicho kirefu cha uvutano wa utamaduni wa Kigiriki, kilichoanzia karne ya nne K.W.K. hadi kuingia ndani sana katika karne za mapema za Wakati wa Kawaida, mtungaji-vitabu Myahudi Max Dimont alisema hivi: “Wakiongezewa fikira ya Kiplato, hoja ya Aristoteli, na sayansi ya Euklidia, wasomi Wayahudi walijifunza Torati wakiwa na vyombo vipya. . . . Walianza kuongeza kusababu kwa Kigiriki kwenye ufunuo wa Kiyahudi.”

Je! Binadamu Ana Nafsi Isiyoweza Kufa?

15-17. (a) Biblia hufundisha nini juu ya kifo na nafsi? (Ona kisanduku, “ Kifo Na Nafsi—Ni Nini?”) (b) Biblia hutoa tumaini gani kwa wale ambao wamekufa?

15 Je! mafundisho na imani za kidini za Kiyahudi viliathiriwa wakati wa kipindi hicho? Encyclopaedia Judaica hukubali waziwazi hivi: “Labda ilikuwa chini ya uvutano wa Kigiriki kwamba fundisho la kutokufa kwa nafsi liliingia katika Dini ya Kiyahudi.”8 Maandiko ya Kiebrania hufundisha kwa urahisi na kwa wazi kwamba hapo awali Mungu aliwakusudia watu waishi milele katika afya kamilifu juu ya dunia hii. (Ona kurasa 11-12, mafungu 2 hadi 4.) Kwenye Mwanzo 2:7 twasoma hivi: “BWANA Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai; naye mtu akawa nafsi hai.” (JP) Angalia kwamba andiko hilo halitaarifu kwamba mtu alipewa nafsi, bali, kwamba akawa nafsi. Kwa sababu ya kumwasi Mungu kwa kutokutii, mwanadamu wa kwanza, Adamu, alihukumiwa kifo. Kwa hiyo, Adamu, akiwa nafsi ya kibinadamu, akafa. Hakuna sehemu yake iliyoendelea kuishi katika makao mengine. Hivyo, wazo la nafsi isiyoweza kufa si fundisho la Biblia. * Biblia husema waziwazi hivi: “Ile nafsi itendayo dhambi, itakufa.”—Ezekieli 18:4JP.

16 Yale ambayo Maandiko hufunua juu ya hali ya wafu hupatana na fundisho la Biblia kwamba nafsi hufa. Kwenye Mhubiri sura ya 9, mistari 5 na 10, twasoma hivi: “Walio hai wanajua watakufa. Lakini wafu hawajui lolote . . . Maana hamna tendo, hamna kufikiri, hamna kujifunza, hamna hekima katika Sheoli [kaburi la kawaida la ainabinadamu], ambamo waenda.” (Linganisha Zaburi 146:3, 4.) Kifo kilitolewa na Mungu kikiwa adhabu. (Mwanzo 2:17) Hicho ni kinyume cha uhai, si namna nyingine ya uhai. Kwa kuwa hiyo ni kweli, hatupaswi kushangaa kugundua kwamba hapana mahali ambapo Maandiko husema juu ya adhabu yenye kuwaka ya moto wa helo (geh hin·nomʹ). Hilo pia ni wazo lililokubaliwa kutoka kwenye falsafa ya Kigiriki na fundisho la kipagani. Kuhusu imani ya kifumbo ya Kiyahudi juu ya kuzaliwa tena katika umbo jingine, The New Standard Jewish Encyclopedia hutaarifu hivi: “Wazo hilo huonekana lilitoka India. . . . Katika Kabbalah [vitabu vya kifumbo vya Dini ya Kiyahudi] huibuka kwanza katika kitabu Bahir, kisha, kutoka Zohar na kuendelea, likakubaliwa na wanamafumbo, likiwa na sehemu ya maana katika imani na fasihi ya Kihasidi.”9

17 Kwa kuwa kifo ni kinyume cha uhai na nafsi haiendelei kuishi katika makao mengine, kuna tumaini gani kwa wale ambao wamekufa? Neno la Mungu hufundisha waziwazi kwamba baada ya ainabinadamu kurudishiwa hali za kiparadiso duniani wakati Mfalme wa Kimesiya aliyewekwa rasmi na Mungu aingiliapo mambo ya kibinadamu, walio wengi miongoni mwa wafu watarudishwa kwenye uhai. Fundisho hilo la Biblia hurejezewa mara nyingi kuwa ‘ufufuo wa wafu.’ Watakaofufuliwa si wale tu waliomtumikia Mungu kwa uaminifu, bali pia mamilioni mengi, hata mabilioni, ambao hawakupokea fursa kamili ya kujifunza juu yake, na kumtumikia katika kweli.—Danieli 12:2, 12 (13, UV, JP); Isaya 26:19; Ayubu 14:14, 15.

18, 19. Kwa nini mtu apaswa apate kumjua Mungu wa kweli, naye anawezaje kufanya hivyo?

18 Je! tumaini hilo la Biblia la ufufuo kwenye uhai mkamilifu duniani si msukumo wenye nguvu kwa watu wa mataifa yote wamtafute na kuja kumjua Mungu wa kweli? Lakini ki wapi chanzo cha kweli cha mafunzo kutoka kwa Yehova kwa ajili ya hizi siku za mwisho, kama ilivyotajwa kwenye Isaya 2:2, 3? Ni nani awezaye kuwafunza watu katika njia za Yehova, ili ‘waweze kutembea katika vijia Vyake’? Je! Dini ya Kiyahudi au Jumuiya ya Wakristo yaweza kuandaa mafunzo kama hayo, kwa kufikiria habari ya Biblia iliyozungumzwa kufikia hatua hii?

19 Kulingana na unabii kungekuwako kikundi cha watu chenye kuchukua jina la Yehova kwa usafi, ambao wangetumika kikweli wakiwa Mashahidi wake na wakiwa chanzo cha nuru ya kiroho kwa mataifa.—Isaya 60:2, 3.

^ fu. 1 Usomaji wa juujuu wa unabii huo ungeweza kutoa wazo kwamba katika siku za mwisho, kungekuwako kuongolewa kwa wengi sana wa mataifa kuingia katika Dini ya Kiyahudi. Hata hivyo, muktadha, pamoja na matukio ya kisasa, huonyesha kwamba hayo siyo maoni sahihi. Mazungumzo katika sehemu hii na ile inayofuata yatakuwa msaada pia katika kuelewa kwa nini sisi twafikia mkataa huo.

^ fu. 14 Tokea wakati wa utawala wa Aleksanda Mkuu (336-323 K.W.K.), Wagiriki walitia jitihada kubwa kueneza falsafa, utamaduni, na lugha yao kwenye nchi zote zilizotiwa ndani ya Milki ya Ugiriki. Wale waliokubali utamaduni na kufikiri kwa Kigiriki walionwa kuwa wamegeuzwa kuwa Wagiriki. Jitihada hiyo ya kushinda tamaduni nyinginezo na kuziingiza katika ule wa Ugiriki uliendelezwa chini ya Milki ya Roma, ambayo, ijapokuwa ilikuwa imeshinda Ugiriki, ilipata utamaduni na falsafa zake kuwa zenye kuvutia. Hata miongoni mwa wengi kati ya wale waliopinga kwa bidii yenye kuendelea wimbi hilo kubwa la uvutano wa Kigiriki, twapata uthibitisho ulio wazi kwamba walikubali mawazo, hoja, na mafundisho ya kifalsafa ya Kigiriki.

^ fu. 15 Katika Kiebrania cha Biblia neno linalotafsiriwa “nafsi” ni neʹphesh. Hata hivyo, katika Dini ya Kiyahudi ya leo, neno la Kiebrania nesha·mahʹ mara nyingi hufikiriwa kuwa sehemu ya mwanadamu ambayo huendelea kuishi baada ya kifo. Lakini funzo la uangalifu la Maandiko hufunua kwamba neno nesha·mahʹ halikuwasilisha kamwe maana kama hiyo; hilo hurejezea tu ile njia ya kupumua au kiumbe chenye kupumua, binadamu au mnyama.—Mwanzo 7:22; Kumbukumbu la Torati 20:16; Yoshua 10:39, 40; 11:11; Isaya 2:22.