Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kusudi la Mungu kwa Ainabinadamu?

Ni Nini Kusudi la Mungu kwa Ainabinadamu?

1-4. (a) Ni nini lililokuwa kusudi la Mungu la awali kwa ainabinadamu? (b) Ni kwa nini mwanadamu alithibitika kuwa asiyetii? (Ona kisanduku,  Shetani Ni Nani?”)

ILE ahadi ya ulimwengu usio na vita kama ifunuliwavyo kwenye Isaya 2:2-4 na Mika 4:1-4 haituandalii tu tumaini lenye msingi mzuri kwa wakati ujao ulio karibu bali pia hutuambia jambo la maana sana juu ya Muumba. Yeye ni Mungu wa kusudi. Unabii kwenye Isaya sura ya 2 kwa kweli ni sehemu ya mfululizo mrefu wa unabii mwingi ambao hupatikana kuanzia kurasa za kwanza za Biblia hadi ukurasa wa mwisho, kutujulisha waziwazi jinsi Mungu atakavyotimiza kusudi lake la awali.

2 Mungu alipoumba wanadamu wawili wa kwanza, aliwaambia waziwazi ni nini lililokuwa kusudi lake kwao. Kwenye Mwanzo sura ya 1, mstari wa 28, twasoma hivi: “Mungu akawabariki naye Mungu akawaambia, ‘Zaeni sana na kuongezeka, jazeni dunia na kuiweza; na kutawala samaki wa baharini, na ndege wa angani, na vitu vyote vilivyo hai vitambaavyo juu ya dunia.’” Tuhusianishapo amri hiyo na jambo lisemwalo katika sura inayofuata ya Mwanzo—“BWANA Mungu akatwaa mtu huyo akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza”—inakuwa wazi kwamba Mungu alikusudia kwamba watu wawili wa kwanza, pamoja na wazao wao, waeneze Paradiso kupita mipaka ya bustani ya Edeni, hatimaye itie ndani tufe lote la kidunia. *Mwanzo 2:15.

3 Wangefurahia makao yao ya kiparadiso kwa muda mrefu kadiri gani? Maandiko hudokeza kwamba binadamu aliumbwa aishi milele duniani. Kifo cha ainabinadamu kingekuja tu ikiwa wangekosa kutii Muumba wao, kama itaarifiwavyo kwenye Mwanzo sura ya 2, mistari 16 na 17: “BWANA Mungu akamwamuru mtu huyo, akisema, ‘Ya kila mti wa bustani una uhuru wa kula; lakini kwa habari ya mti wa maarifa ya mema na mabaya, ni lazima wewe usile ya huo; maana mara tu ulapo ya huo, utakufa.’” Kwa hiyo, kupatana na akili, utii wenye kuendelea ungalitokeza uhai wenye kuendelea, uhai wa milele, katika hali hizo za kiparadiso.—Zaburi 37:29; Mithali 2:21, 22.

4 Hata hivyo, malaika mmoja, ambaye baadaye hurejezewa kuwa Shetani (kumaanisha “Hasimu”), alivuta watu hao wawili wa kwanza watumie vibaya hiari yao kwa kuchagua kumwasi Mungu. (Ayubu 1:6-12; linganisha Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.) Akitokeza wazo lenye kosa kwamba ni nyoka aliyekuwa akisema, malaika huyo mwasi alimwambia Hawa na, kupitia Hawa, Adamu, kwamba wangekuwa wenye hekima zaidi na maisha zao zingekuwa kamili zaidi kwa kutojitiisha kwa Mungu akiwa Mamlaka Kuu Zaidi. * (Mwanzo 3:1-19) Kwa sababu ya uasi wao ulio wazi, walihukumiwa kifo. Je! hiyo ilimaanisha kwamba kusudi la Mungu kwa ainabinadamu lilikatizwa au kufutwa? Hapana, badala ya hivyo, ilimaanisha kwamba njia nyingine ingehitajiwa ili kutimiza kusudi la awali la Mungu la dunia-paradiso yenye kujaa wanadamu watiifu wakifurahia uhai wa milele. Hilo lingetimizwaje?

Mbegu Iliyoahidiwa

5, 6. (a) Mungu aliahidi nini ukiwa utatuzi wa matatizo yaliyosababishwa duniani na uasi wa Shetani? (b) Mungu alimwahidi Abrahamu nini?

5 Katika kutamka hukumu juu ya hao waliohusika katika uasi dhidi ya mamlaka yake, Yehova Mungu alijulisha kwamba angeinua “mbegu,” au “mzao,” ambaye angeondoa dhara lililosababishwa na mchochezi wa uasi huo. Katika semi za ufananisho, Mungu alisema juu ya huyo nyoka, akiwakilisha Shetani, kuwa akipigwa, au kupondwa, katika kichwa na Mbegu huyo, hivyo kukomesha kuwako kwa Shetani na uasi. Katika muda wa miaka iliyopita mstari huo katika Mwanzo umefasiriwa katika njia mbalimbali na zenye kupingana. Lakini kwa kuwa neno “mbegu” hutumiwa katika unabii mwingi, ahadi nyingine zinazohusiana hufunua unavyomaanisha.—Mwanzo 3:15.

6 Neno “mbegu” huhusiana mara nyingi na kutimizwa kwa kusudi la Mungu kwa ainabinadamu kwa ujumla. Kama ilivyorekodiwa kwenye Mwanzo 22:18, yule Mwebrania mwaminifu Abrahamu alipewa ahadi hii na Mungu: “Mataifa yote ya dunia yatajibariki yenyewe kwa wazao [mbegu, JP] wako, kwa sababu wewe umetii amri Yangu.” (Italiki ni zetu.) Mungu alionyesha kupendezwa kipekee na Abrahamu akiwa binadamu aliyemtafuta Yeye kikweli. Hata hivyo, ijapokuwa Mungu alithawabisha Abrahamu moja kwa moja, andiko hilo huonyesha waziwazi kwamba kupendezwa kwa Mungu hakukuwa katika Abrahamu peke yake, wala katika wazao wake wa kimwili peke yao. Mungu alikuwa akikumbuka sana kusudi lake la awali la dunia-paradiso kwa ajili ya ainabinadamu yote, “mataifa yote.” Alikuwa akifunulia Abrahamu sasa kwamba kama tokeo la uaminifu wake, yeye angekuwa na pendeleo la kutokeza “mbegu” ambaye kwake mataifa yote yangejibariki yenyewe.

7, 8. Mbegu huyo aliyeahidiwa alikuja kufungamanishwaje na mawazo ya umaliki na yule Mesiya?

7 Abrahamu alikuwa baba ya mataifa mengi makubwa. (Mwanzo 17:4, 5) Lakini Yehova Mungu alifunua waziwazi ni kupitia nasaba ipi katika hizo yule Mbegu aliyeahidiwa angekuja, akiiletea ainabinadamu yote baraka. (Mwanzo 17:17, 21) Wote wawili Isaka mwana wa Abrahamu na Yakobo mjukuu wake walitajwa kuwa walikuwa wa nasaba ambayo ingetokeza “mbegu” huyo. Mojapo mataifa yaliyotokana na Abrahamu lilikuwa taifa la Israeli, lenye makabila 12 yaliyotokana na wana wa Yakobo, mjukuu wa Abrahamu. Ni katika taifa hilo kwamba yule “mbegu” aliyeahidiwa angetokea hatimaye.—Mwanzo 26:1, 4; 28:10, 13-15, JP.

8 Unabii ulifunua baadaye kwamba mbegu wa pekee, au mtawala, angekuja hasa kupitia kabila la Yuda. Mwanzo 49:10 hutaarifu hivi: “Fimbo haitaondoka Yuda, wala mpaji-sheria kutoka katikati ya miguu yake, mpaka Shilo aje; na uwe wake utii wa watu.”3 Mwelezaji wa Biblia Rashi hutaarifu kwamba hicho kifungu cha maneno “mpaka Shilo aje” humaanisha “mpaka yule Mfalme Mesiya atakapokuja, ambaye ufalme utakuwa wake.”4 Kama vile Rashi, waelezaji wengi wa Biblia wameelewa unabii huo kuwa na maana ya Kimesiya.

9. (a) Mungu alimwahidi Mfalme Daudi nini kuhusu yule Mbegu? (b) Ahadi katika Mwanzo 49:10 inahusianaje na ile iliyo kwenye Zaburi 72:7, 8?

9 Mtawala wa kwanza katika nasaba ya Yuda, Mfalme Daudi, aliahidiwa hivi na Mungu: “Nyumba yako na . . . kiti cha ufalme chako vitaimarishwa milele.” (2 Samweli 7:16) Mungu aliahidi zaidi hivi: “Nitasimamisha mbegu yako baada yako, . . . nami nitaimarisha ufalme wake. Yeye atajengea Mimi nyumba, nami nitaimarisha kiti cha ufalme chake milele.” (1 Mambo ya Nyakati 17:11, 12, JP) Mwana na mwandamizi wa Daudi, Mfalme Sulemani, kwa kweli alijenga nyumba au hekalu la Yehova, lakini kwa wazi yeye hakutawala milele. Hata hivyo, mmoja kati ya mbegu za Daudi angekuwa “Shilo,” au Mesiya yuleyule, aliyetolewa unabii kwenye Mwanzo 49:10. (JP) Akisema kiunabii juu ya huyo, Mfalme Daudi aliandika hivi: “Katika siku zake acha mwadilifu asitawi, na wingi wa amani, hata mwezi usiwepo tena. Na awe na enzi pia toka bahari hata bahari, na toka ule Mto hadi miisho ya dunia.”—Zaburi 72:7, 8JP.

10. Ni nini lingetimizwa na Mbegu aliyeahidiwa katika Mwanzo 3:15, na hilo hupatanaje na ahadi aliyopewa Abrahamu?

10 Tukifuata ufunuo wa hatua kwa hatua kupitia unabii, twaja kuelewa kwamba baraka alizoahidiwa Abrahamu—“katika mbegu yako mataifa yote ya dunia yatabarikiwa” —kwa kweli zitatimizwa kupitia Mtawala uyo huyo wa nasaba ya Daudi. (Mwanzo 22:18, JP) Kwa njia hiyo unabii mwingi juu ya Mbegu waungana na tumaini la taifa la Kiyahudi katika Mesiya, ambaye wakati wa utawala wake dunia itakuwa na amani kamili. Kwa kweli, yeye ndiye “mbegu” iliyotajwa kwenye Mwanzo 3:15 ambaye angekomesha uasi wa awali dhidi ya enzi kuu ya Mungu na kuondoa madhara ambayo yametokea. (Zaburi 2:5, 8, 9) Maswali mengine na habari juu ya Mesiya aliyeahidiwa yanashughulikiwa katika “Ni Nani Ataongoza Mataifa Kwenye Amani?”. Lakini acheni sasa tufikirie shughuli zaidi za Mungu na wazao wa Abrahamu.

Kusudi la Agano la Sheria

11-13. Agano la Sheria lilinufaishaje taifa hilo, na je, lilikusudiwa lidumu milele?

11 Waisraeli walipata kuwa taifa mamia machache ya miaka baada ya wakati wa Abrahamu. Mungu aliweka huru wazao hao kutoka utekwa katika Misri, na chini ya uongozi wa Musa, mwanamume mwingine wa imani ambaye Yeye alikuwa amechagua, Mungu alifanya agano la pekee, au mapatano, pamoja nao. (Kutoka 19:5, 6; Kumbukumbu la Torati 5:2, 3) Hilo Agano la Sheria lililipa taifa hilo mwelekezo ulio wazi kuhusu jinsi Mungu alivyotaka aabudiwe. Liliwapanga kitengenezo wakiwa taifa kwa ajili ya ibada hiyo.

12 Tuangalie kwamba tangu mwanzoni agano hilo lilikuwa lenye masharti. Kabla ya kufunulia taifa la Israeli zile Amri Kumi na agano lote ambalo hizo zilikuwa sehemu yalo, Mungu aliwaarifu hivi: “Sasa basi, ikiwa nyinyi mtanitii Mimi kwa uaminifu na kushika agano Langu, nyinyi mtakuwa milki Yangu yenye thamani miongoni mwa vikundi vyote vya watu. Kweli kweli, dunia yote ni Yangu, lakini nyinyi mtakuwa Kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.” (Kutoka 19:5, 6) Ili waendelee kutumiwa na Mungu wakiwa milki yenye thamani, wangalipaswa kumtii kwa uaminifu. Hayo ndiyo yaliyokuwa masharti ya agano hilo.

13 Thawabu iliyoahidiwa kwa uaminifu wao—kwamba wangetumika wakiwa ufalme wa makuhani—hufunua kwamba agano la Sheria lenyewe halikuwa ndilo mwisho wa mambo bali, hatua ya mpisho kuelekea kustahilisha ukuhani ambao ungesaidia mataifa mengine yapate kumjua yule Mungu wa kweli. Tangu mwanzo kusudi la Mungu lilikuwa kwamba ainabinadamu yote, na wala si watu wa taifa moja tu, ingejibarikia yenyewe.Mwanzo 22:18.

14. Ni manufaa gani nyingine zilizotokana na agano la Sheria?

14 Kwa kuwa agano la Sheria lenyewe halikuwa mwisho wa mambo, kusudi lalo lilikuwa nini? Lilifunua na kushutumu pasipo shaka yoyote mawazo bandia yote ya kidini ambayo binadamu alikuwa ameanza kusitawisha kwa kujitegemea tangu wakati wa uasi katika bustani ya Edeni. (Kumbukumbu la Torati 18:9-13) Pia lililinda taifa la Israeli na mazoea yenye kuchukiza na ibada ya mataifa yaliyolizunguka kwa kupunguza uhusiano wote na mataifa hayo. (Kumbukumbu la Torati 7:1-6) Maadamu Israeli walishika Sheria hiyo, wangehifadhiwa katika hali safi kidini, ambamo hatimaye wangeweza kutambua na kukaribisha yule Mbegu, au Mesiya aliyeahidiwa.

Kwa nini Mungu aliagiza kutoa dhabihu kuwe sehemu ya agano la Sheria?

15, 16. Ni masomo gani ya kiroho ya maana yaliyotiwa ndani ya agano la Sheria ambayo pia huelekeza kwenye asili yalo isiyo ya kudumu?

15 Agano la Sheria lilikazia pia uhitaji wa upatanisho, likitia ndani mfumo ulioelezwa vizuri wa dhabihu zilizokuwa sehemu isiyotenganika ya ibada ya Kiyahudi. (Mambo ya Walawi 1:1-17; 3:1-17; 16:1-34; Hesabu 15:22-29) Tangu wakati wa uasi wa Adamu na Hawa, ainabinadamu ilipoteza ukamilifu ambao ungaliiwezesha kuishi milele katika afya kamilifu. (Mwanzo 2:17) Kama tokeo la dhambi hiyo ya kwanza, wazao wa Adamu na Hawa (wote wakizaliwa baada ya uasi) walirithi kutokamilika na mwelekeo waliozaliwa nao wa kutenda dhambi. (Mwanzo 8:21; Zaburi 51:7 [51:5, UV]; Mhubiri 7:20) Kutokamilika kuliongoza kwenye magonjwa, kuzeeka, na kifo, pamoja na kufanyiza kizuizi kati ya binadamu na Mungu. (1 Wafalme 8:46; linganisha Maombolezo 3:44.) Msingi fulani ulihitajiwa wa kuondoa madhara hayo pamoja na kushinda na kuleta upatanisho kwa ajili ya hali ya binadamu ya kutokamilika. Sikuzote wanaume wenye imani walijua sana uhitaji huo.—Ayubu 1:4, 5; Zaburi 32:1-5.

16 Agano la Sheria lilikazia kwamba Mungu ana viwango vya kisheria ambavyo lazima vitimizwe. Pia liliandaa msingi wa kuelewa jinsi viwango vya Mungu vya haki vingetoshelezwa kabisa. * Maandalizi ya dhabihu katika agano la Sheria yasingeweza kamwe kurudisha kusudi la awali la Mungu kwa ajili ya ainabinadamu, kwa kuwa matokeo yazo yalikuwa ya kitambo tu, yakikazia hali yenye dhambi lakini yasiweze kuiondoa au kuizuia. Kwa hiyo, Sheria ilikuwa hatua ya mpisho ili kusaidia taifa hilo la waabudu lililopangwa kitengenezo lielewe katika wakati ufaao jinsi ya kutambua yule Mbegu na jinsi Mbegu huyo angeondoa madhara yaliyosababishwa na dhambi ya Adamu. Ni wapi ambapo Torati ilionyesha jambo hilo?

Ahadi ya Nabii Aliye Kama Musa

17, 18. Ni jambo gani lililomaanishwa na ahadi ya Mungu kwenye Kumbukumbu la Torati 18:15, 18, 19 ya kuinua nabii?

17 Kwenye Kumbukumbu la Torati sura ya 18, mstari 15, Musa aliambia taifa la Israeli hivi: “BWANA Mungu wenu atainua kwa ajili yenu nabii kutoka miongoni mwa watu wenu wenyewe, kama mimi mwenyewe; huyo mtamsikiliza.” Katika sura iyo hiyo, kwenye mistari 18 na 19, Yehova alinena na Musa, yeye ambaye alikuwa amemweka rasmi awe mpatanishi kati yake mwenyewe na watu Wake, akisema: “Mimi nitainua nabii kwa ajili yao kutoka miongoni mwa watu wao wenyewe, kama wewe: Mimi nitaweka maneno Yangu katika kinywa chake naye atanena kwao yote ambayo Mimi nitamwamuru yeye; na ikiwa mtu yeyote ashindwa kutii maneno asemayo katika jina Langu, Mimi mwenyewe nitataka hesabu kwake.” Unabii huo wapasa kuelewekaje?

18 Nabii anayetajwa hapa kwa wazi ni mtu mmoja hususa na aliye wa pekee. Maneno yanayotangulia na kufuata yaonyesha wazi kwamba hiyo si kanuni ya ujumla tu kuhusu kusudi la Mungu la kuendelea kuinua manabii kwa ajili ya taifa, kama vile baadhi ya watu wamedhania. Neno la Kiebrania la nabii (na·viʼʹ) liko katika umoja, likimlinganisha na Musa, aliyekuwa wa pekee katika historia ya taifa hilo. Kwa kuongezea, maneno ya kumalizia katika kitabu hichohicho cha Kumbukumbu la Torati hutaarifu hivi: “Hapakuinuka tena kamwe katika Israeli nabii kama Musa—ambaye BWANA aliteua, uso kwa uso.” (Kumbukumbu la Torati 34:10-12) Yule aliyerekodi maneno hayo yaelekea sana alikuwa Yoshua, mwana wa Nuni, ambaye mwenyewe alikuwa kiongozi na nabii mkuu aliyewekwa rasmi na Mungu. Lakini kutokana na maneno yake mwenyewe, hakuna shaka kwamba hakujiona mwenyewe kuwa utimizo wa maneno ya Musa kuhusu nabii kama Musa. Hivyo, Mungu alimaanisha nini wakati alipoahidi kuinua nabii kama Musa? Musa alikuwa nabii wa namna gani?

Agano Jipya Latolewa Unabii

19. (a) Musa alikuwaje wa pekee? (b) Nabii kama Musa angalipaswa kutumika akiwa nini pia?

19 Musa alikuwa kiongozi mkuu; alikuwa mpaji-sheria, nabii, mfanya-miujiza, mwalimu, na hakimu. Pia alikuwa mpatanishi, nabii pekee aliyepata kupatanisha agano kati ya Mungu na binadamu (katika habari hii, taifa la Israeli). Nabii aliye kama yeye kweli kweli angepaswa kufanya jambo kama hilo. Je! hiyo yamaanisha kwamba Mungu alikusudia kwamba nafasi ya agano la Sheria ingechukuliwa na agano jingine? Ndivyo. Kupitia nabii Yeremia, Mungu alitaarifu waziwazi kusudio lake la kufanya agano jipya. Agano jipya lingetaka mpatanishi mpya. Ni mtu fulani aliye kama Musa tu ambaye angeweza kufaa kutimiza matakwa ya mgawo kama huo. Tukichunguza yanayohusika katika agano hilo jipya, tunaweza kuelewa vizuri zaidi fungu la mpatanishi huyo.

20, 21. (a) Ni nini kinachoahidiwa kwenye Yeremia 31:31-34? (b) Kusudi lililotaarifiwa la agano jipya lilikuwa nini? (c) Likiwa tokeo, kungetukia nini kwa agano la Sheria?

20 Ilikuwa yapata miaka 900 baada ya Musa kwamba Yeremia aliwasilisha kwa taifa la Israeli maneno ya Mungu: “Ona, wakati waja—ajulisha BWANA—ambapo mimi nitafanya agano jipya na Nyumba ya Israeli na Nyumba ya Yuda. Halitakuwa kama lile agano ambalo nilifanya pamoja na baba zao, wakati mimi nilipowachukua kwa mkono kuwaongoza kutoka nchi ya Misri, agano ambalo walivunja, . . .—ajulisha BWANA. Bali ndivyo lilivyo agano nitakalofanya pamoja na Nyumba ya Israeli baada ya siku hizi . . . Mimi nitasamehe maovu yao, na nisikumbuke dhambi zao tena.” *Yeremia 31:31-34.

21 Ikiwa nabii kama Musa atumika akiwa mpatanishi mpya wa agano jipya, basi inakuwa wazi pia kwamba yale mambo mengi madogomadogo hususa ya ibada yaliyotakwa chini ya Sheria ya Musa yasingetumika daima ila tu mpaka lile agano jipya lisimamishwe. Hakika, wakati Mungu angeandaa msingi wa ‘kusamehe maovu yao na asikumbuke dhambi zao tena,’ kusingekuwa tena na uhitaji wa mfumo mzima wa dhabihu ulioandaliwa na mpango wa hekalu, ulioleta msamaha wa kitambo tu. Kwa kuanzishwa kwa agano jipya, pande za kisherehe za agano la Sheria, kama vile kushika Sabato na sikukuu mbalimbali, pia kusingekuwa na maana ileile. Kwa wakati wake, hakika Mungu angefunua ni nini lingetakwa kwa wale walio katika mpango huo wa agano jipya lililoahidiwa.—Amosi 3:7.

Baraka kwa Mataifa Yote

22, 23. (a) Ni nini lililokuwa kusudi la agano jipya kuhusu mataifa? (b) Unabii mwingineo huonyeshaje ni nini lililokuwa kusudi la Mungu kwa mataifa yote?

22 Kuelewa kwamba nabii kama Musa na Mbegu ya Abrahamu ni yuleyule mmoja hutusaida kuona upande mwingine wa maana sana wa agano jipya; lingekuwa ndilo njia ya kisheria ambayo kwayo watu wa mataifa yote wangeweza kumwabudu Mungu wa kweli. Kwa kuwa Mwanzo 22:18 husema ni kwa njia ya “mbegu” (JP) kwamba “mataifa yote ya dunia yatajibarikia yenyewe,” ni wazi kwamba katika hatua fulani katika historia ya kibinadamu, Mungu asingeshughulika tena kipekee na taifa moja tu, wale wazao wa Abrahamu. Baada ya taifa la Israeli kuwa limetumikia katika fungu hilo muhimu la kuandaa Mbegu aliyeahidiwa na baada ya kuanzishwa kwa agano jipya, ibada ya Mungu wa kweli ingefunguliwa kwa watu wa mataifa na jamii zote.

23 Hakika hapana yeyote ambaye angeweza kwa kufaa kubishia uhaki wa Mungu katika kuruhusu watu wenye mioyo myeupe wa kila taifa na jamii wamwabudu. Hilo lilikuwa kusudi la Mungu tangu mwanzo, na kuna unabii mwingi katika Biblia kuthibitisha uhakika wa kwamba watu wa mataifa yote wangejibariki wenyewe kwa njia ya mbegu ya Abrahamu. (Zekaria 8:20-23) Mfano mmoja waweza kupatikana kwenye Sefania sura ya 3, mstari wa 9, ambapo Mungu hujulisha hivi: “Maana ndipo Mimi nitafanyia watu usemi safi, ili kwamba wao wamwite BWANA kwa jina na wamtumikie Yeye kwa umoja.” Unabii uleule wa Isaya sura ya 2 uliotajwa mwanzoni mwa broshua hii hukazia upande huu wenye kuunganisha wa ibada ya Mungu, watu wa mataifa mengi wakigeuka wamtumikie katika kweli, wakijifunza njia za amani; hukazia pia wakati ambapo jambo hilo lingetukia: “Itakuwa katika mwisho wa siku.” (Isaya 2:2, JP) Ni nini linalomaanishwa na usemi huo “mwisho wa siku”?

24. (a) Ni nini linalomaanishwa na usemi “mwisho wa siku”? (b) Ni jambo gani linaloelezwa katika Ezekieli sura ya 38 na 39?

24 Maandiko husema tena na tena juu ya siku ambayo Mungu ataleta mataifa yote kwenye hukumu. (Isaya 34:2, 8; Yeremia 25:31-35; Yoeli 4:2 [3:2, UV]; Habakuki 3:12; Sefania 1:18; 3:8) Tangu kukataliwa kwa enzi kuu ya Mungu katika bustani ya Edeni, kushindwa kwa ainabinadamu kujitawala yenyewe kwa mafanikio kumezidi kuwa wazi. Serikali za mwanadamu zimeshindwa kabisa, zikisababisha kuteseka kwingi. Zikiruhusiwa ziendelee kuwako katika kizazi hiki cha silaha za nyukilia na uchafuzi wa mazingira wa ulimwenguni pote, watu wangeweza kujiangamiza wenyewe na makao yao ya kidunia. Kwa hiyo, Mungu, akitumia Mesiya aliyewekwa rasmi, yule Mbegu, ataingilia mambo. (Zaburi 2:1-11; 110:1-6) Nabii Ezekieli alitangulia kuona lile pigano la mwisho la Mungu dhidi ya serikali za mwanadamu. Katika sura za 38 na 39 za kitabu chake, yeye aeleza vita ya Mungu dhidi ya “Gogu wa nchi ya Magogu.” (Ezekieli 38:2) Huu umetambuliwa na wengi kuwa unabii wa siku za mwisho. Uchunguzi wa uangalifu wa Maandiko hufunua kwamba hapa “Gogu” ni jina la ufananisho la yuleyule roho mwasi, Shetani, aliyeongoza Adamu na Hawa katika mwendo wa kutomtii Mungu. Kushindwa kwa roho huyo pamoja na majeshi yake, ambao wamekuwa maadui wa Mungu wa muda mrefu, kwa kweli ni sehemu ya kwanza ya utimizo wa ahadi ya awali kwamba “mbegu” angemchubua kichwani, yule “nyoka,” Shetani, kusema kwa ufananisho, kwa njia yenye kuleta kifo.—Mwanzo 3:15JP.

25. Ni nini lililotabiriwa kutukia baada ya kuharibiwa kwa majeshi ya Shetani?

25 Kufuata uharibifu huo wa majeshi ya Shetani, zile hali za awali za paradiso ya Kiedeni zitarudishwa. Lakini wakati huu, chini ya ule mpango wa agano jipya, ainabinadamu itakuwa tiifu kwa Mungu. (Isaya 11:1-9; 35:1-10) Si kwamba tu dhambi zitasamehewa bali pia ainabinadamu itarudishwa kabisa kwenye ukamilifu. (Isaya 26:9) Kama tokeo watapewa uhai wa milele. (Zaburi 37:29; Isaya 25:8) Wakati huo hata wafu, wale waliokufa wakiwa waaminifu kwa Mungu na pia mabilioni ambao hawakuwa kamwe na fursa kamili ya kujifunza juu yake katika kweli, watarudishwa kwenye uhai—watafufuliwa! (Danieli 12:2, 12 [12:2, 13, UV, JP]; Isaya 26:19) Je! tumaini hilo la ajabu halituvuti karibu zaidi na Mungu aliyebuni mambo kama hayo?

26. Kuja kwa nabii kama Musa kwataka nini kwetu?

26 Hizo ni baadhi tu ya baraka kwa watu wa mataifa yote ambao huja kutambua na kusikiliza sauti ya yule nabii kama Musa, yule Mbegu atakayetawala katika kiti cha ufalme cha Daudi “hata mwezi usiwepo tena,” kumaanisha milele. (Zaburi 72:7) Kuhusu nabii huyo kama Musa, Kumbukumbu la Torati 18:19 husema pia hivi: “Ikiwa mtu yeyote ashindwa kutii maneno asemayo katika jina Langu, Mimi mwenyewe nitataka hesabu kwake.” Je! wewe utachukua wakati, utafanya jitihada inayohitajiwa, utambue Nabii huyo aliye kama Musa, Mesiya huyo, hivyo ujifunze yote ambayo Mungu ataka? Je! wewe binafsi utakuja kumjua yule Mungu wa kweli?

^ fu. 2 Simulizi katika kitabu cha Mwanzo lielezalo bustani ya Edeni si fumbo la maneno, bali Edeni palikuwa mahali hasa palipokuwa pakubwa. Andiko hilo huelekeza kwenye mahali kaskazini mwa nyanda za Mesopotamia, chanzo cha mito Frati na Tigri. (Mwanzo 2:7-14) Ilipaswa kutumika kuwa kiolezo, ambacho kulingana nacho mtu angefananisha na kulima sehemu nyingine ya dunia.

^ fu. 4 Kupata uelewevu mwingi zaidi wa yaliyomaanishwa na uasi huo, ona kisanduku, “ Kwa Nini Mungu Huruhusu Uovu?

^ fu. 16 Kigezo cha kisheria kilichotiwa na Musa katika fungu la sheria kwa kurejezea namna ya malipo kwa ajili ya uhalifu mbalimbali wa Sheria—“uhai kwa uhai, jicho kwa jicho, jino kwa jino”—huonyesha kanuni yenye kuongoza iliyotumiwa na Mungu mwenyewe katika kutatua suala la wokovu wa binadamu. (Kumbukumbu la Torati 19:21) Mwanadamu mkamilifu, Adamu, alikuwa amekuwa mwenye kulaumika kwa ajili ya hukumu ya laana ya jamii ya kibinadamu, hivyo mwanamume mwingine mkamilifu alihitajiwa ili kulipia dhambi ya Adamu na matokeo yayo kwa ainabinadamu. Ni kuja tu kwa “mbegu” aliyeahidiwa, ambaye uhai wake ungetolewa kuwa fidia ya kisheria, ndiye angeweza kutimiza kufunguliwa huko. (Mwanzo 3:15, JP) Kwa mazungumzo kamili zaidi ya upande huo wa Mbegu katika kusudi la Mungu, ona sehemu “Ni Nani Ataongoza Mataifa Kwenye Amani?,” mafungu 17 hadi 20.

^ fu. 20 Ufafanuzi uliokubaliwa wa Dini ya Kiyahudi ya ki-siku-hizi ni kwamba Yeremia alikuwa akitabiri tu kufanywa upya na kuthibitishwa upya kwa agano la Sheria pamoja na Israeli, kama ilivyotukia baada ya kurudi kwao kutoka uhamisho katika Babuloni katika 537 K.W.K. (Ezra 10:1-14) Lakini kwa mara nyingine tena unabii wenyewe hukanusha ufafanuzi kama huo. Mungu alitaarifu waziwazi kwamba hilo litakuwa “agano jipya,” si agano lililofanywa upya tu. Zaidi ya hilo, yeye akazia kwamba si kama lile agano lililofanywa wakati alipowaongoza kutoka katika utumwa wa Misri. Baadhi yao wamesema kwamba lilikuwa “jipya” katika maana ya kwamba sasa wangelishika kwa uaminifu agano lilo hilo, lakini historia huonyesha tofauti. Kwa kweli, ukosefu wao wa uaminifu uliongoza kwenye uharibifu wa lile hekalu la pili.—Kumbukumbu la Torati 18:19; 28:45-48.