Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia​—Je, Imepuliziwa na Mungu?

Biblia​—Je, Imepuliziwa na Mungu?

1, 2. Kwa nini wengi huistahi Biblia, na waandikaji wayo hutoa dai gani?

THE New Encyclopædia Britannica huita Biblia “labda [ndiyo] mkusanyo wa vitabu wenye uvutano zaidi katika historia ya kibinadamu.” Biblia inaheshimiwa sana na wengi kwa sababu ya kuwa ya kale sana—sehemu zayo zikiwa ziliandikwa miaka 3,500 iliyopita. Hata hivyo, shauri layo lenye kutumika, lenye kupatana na hali za kisasa ni sababu moja kwamba zaidi ya nakala bilioni tatu zimegawanywa na kwamba imetafsiriwa, ikiwa kamili au kwa sehemu, katika karibu lugha elfu mbili, hiyo ikiifanya kuwa kitabu chenye kuuzwa zaidi ulimwenguni kwa wakati wote.

2 Kando na mambo hayo ya hakika, yote ambayo hufanya Biblia istahiwe, bado kuna jambo jingine ambalo limeifanya kuwa yenye uvutano na yenye kuvutia muda wote wa enzi zilizopita—dai layo la kuwa ufunuo uliopuliziwa na Mungu Mweza Yote. Musa, aliyekusanya pamoja ile Torati (vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia) ‘aliandika’ yote ambayo Mungu alimwambia aandike, yaliyotia ndani masimulizi ya uumbaji, maandishi ya Furiko la siku ya Noa, na historia ya Abrahamu na shughuli za Musa mwenyewe pamoja na Mungu. (Kutoka 24:3, 4) Mfalme Daudi alisema: “Roho ya BWANA imenena kupitia mimi, ujumbe wake u juu ya ulimi wangu.” (2 Samweli 23:2) Waandikaji wengine wa Biblia walitoa dai ilo hilo la kuwa na mwongozo wa kimungu. Maandishi hayo yote pamoja hufanyiza maelezo ya Mungu mwenyewe ya historia—maana yayo ya kweli, ufasiri wayo, na tokeo layo la mwisho. Wale waandikaji wengi mbalimbali wa Maandiko—wafalme, vibarua wa kuajiriwa, makuhani, na wengine—wote walikuwa wakitenda wakiwa waandishi katika kuandika mawazo ya Mungu, yule Mtungaji wa Biblia na Mhakikishaji wa ahadi zayo.

3. Ni jambo gani huonyesha kwamba imani katika Mungu na imani katika sayansi hupatana?

3 Kwa kuwa Biblia hudai kuwa na mtungaji wa kimungu, labda swali la kwanza kabisa kwa wengi huhusiana na kuwako kwenyewe kwa Mtungaji wayo. Wengi hukataa kabisa kuwako kwa Mungu. Wengine, wakidhani kuwa watu wote wenye akili wamekataa wazo la kuwako kwa Mungu na imani katika Biblia, huuliza: “Kwa nini wanasayansi hawaamini katika Mungu?” Je! kweli wazo hilo ni la kweli? Makala moja katika gazeti New Scientist ilisema kwamba “maoni ambayo kwa kawaida hutarajia wanasayansi kuwa si waamini . . . ni maoni yenye kosa kabisa.”2 Makala iyo hiyo iliripoti kwamba chunguzi za vivi hivi katika vyuo vikuu, taasisi za utafiti, na maabara za viwanda huonyesha kwamba “wengi kama wanane kwa kila wanasayansi 10 hufuata imani ya kidini au hukubali kanuni ‘zisizo za kisayansi.’” Hivyo si sahihi kusema kwamba imani haipatani na sayansi au wanasayansi. ( Mageuzi—Je! ni Uhakika?”))

Je! Kuna Uthibitisho wa Kupuliziwa?

4. Ni kweli zipi za kisayansi zilizotajwa maelfu ya miaka iliyopita katika Biblia?

4 Mtu afikiapo mkataa kwamba kuna uthibitisho wenye kusadikisha wa kuwako kwa Muumba, bado swali labaki kama amewapulizia watu waandike mawazo na makusudi yake katika Biblia. Kuna sababu nyingi kwa nini sisi twaweza kuwa na hakika kwamba ndivyo ilivyo, mojawapo ikiwa usahihi wayo wa kisayansi. (Ona kisanduku, “ ‘Katika Mwanzo Mungu Aliumba’ . . .” ukurasa 6.) Kwa mfano, zaidi ya miaka 3,000 iliyopita, Ayubu alisema kwamba Mungu “huining’iniza dunia pasipo kitu.” (Ayubu 26:7, JP) Miaka 2,700 hivi iliyopita, nabii Isaya alitaarifu kwamba Mungu “hukaa juu ya duara ya dunia.” (Isaya 40:22, JP) Sasa, Ayubu au Isaya wangeweza kujuaje kweli hizo za msingi za kisayansi kwamba dunia imeangikwa katika anga na ni duara? Zaweza kuwa zinajulikana vema leo, lakini taarifa hizo zilitolewa wakati ambapo mawazo kama hayo yalikuwa hayajasikika. Je! ufunuo wa kimungu silo elezo lenye kupatana na akili zaidi?

5, 6. Ni utimizo gani mbalimbali wa unabii ambao hutoa uthibitisho kwamba waandikaji wa Biblia walipuliziwa na Mungu?

5 Unabii, kwa kweli historia iliyoandikwa kabla haijatukia, labda ndio sehemu kuu ya Biblia ambayo hutegemeza dai layo la kupuliziwa kimungu. Kwa mfano, nabii Isaya alitabiri si kwamba tu Yerusalemu lingeangamizwa na Babuloni na kwamba taifa zima la Kiyahudi lingechukuliwa mateka bali pia kwamba baada ya wakati fulani jenerali Mwajemi Koreshi angeshinda Babuloni na kukomboa Wayahudi kutoka utekwa. (Isaya 13:17-19; 44:27–45:1) Je! wewe waweza kufikiria njia yoyote, isipokuwa kupuliziwa kimungu, ambayo kwayo, Isaya angeweza kutabiri kwa mafanikio uzaliwa wa Koreshi, jina lake, na yale ambayo angefanya hasa miaka 200 mbeleni? (Ona kisanduku,  Mungu—‘Mfunua Mafumbo’ Kupitia Unabii.”))

6 Baadhi ya unabii mbalimbali wenye kutokeza sana umerekodiwa na Danieli, nabii aliyeishi katika karne ya sita K.W.K. Si kwamba tu alitabiri kuangushwa kwa Babuloni na Wamedi na Waajemi bali pia alitabiri matukio ambayo yangetukia baada ya wakati wake, katika wakati ujao uliokuwa mbali sana. Kwa mfano, unabii wa Danieli ulitabiri kuinuka kwa Ugiriki ikiwa milki ya ulimwengu chini ya Aleksanda Mkuu (336-323 K.W.K.), kugawanywa kwa milki ya Aleksanda miongoni mwa majenerali wake wanne baada ya kifo chake kisichotazamiwa, na kuinuka kwa Milki ya Roma, pamoja na nguvu zake za kijeshi zenye kutisha (karne ya kwanza K.W.K.). (Danieli 7:6; 8:21, 22) Matukio hayo yote sasa ni mambo ya hakika yasiyokanushika ya historia.

7, 8. (a) Baadhi ya watu wametoa shtaka gani dhidi ya unabii mbalimbali wa Biblia? (b) Ni nini huthibitisha kwamba shtaka la udanganyifu halina msingi mzuri?

7 Kwa sababu unabii mbalimbali wa Biblia umetimizwa kwa usahihi sana, wachambuzi wameuita kwa dharau madanganyo, yaani, historia iliyoandikwa baada ya kutukia na kufanywa kwa ubandia kuwa unabii. Lakini mtu angewezaje kwa njia yenye akili kushikilia kwamba makuhani wa Kiyahudi wangejasiria kubuni unabii? Na kwa nini wabuni unabii mbalimbali wenye kuwachambua vibaya sana iwazikavyo? (Isaya 56:10, 11; Yeremia 8:10; Sefania 3:4) Kwa kuongezea, taifa zima lenye kujua kusoma na kuandika, lililozoezwa na kuelimishwa kwa kutumia Biblia ikiwa maandishi yalo matakatifu, lingewezaje kudanganywa kwa danganyo kama hilo?—Kumbukumbu la Torati 6:4-9.

8 Kungewezaje kuwa na udanganyifu wowote kuhusiana na kutoweka kwa staarabu nzima-nzima, kama vile Edomu na Babuloni, hali matukio hayo yalitukia karne nyingi baada ya kukamilishwa kwa Maandiko ya Kiebrania? (Isaya 13:20-22; Yeremia 49:17, 18) Hata kama mtu ashikilia kwamba unabii huo mbalimbali uliandikwa baada ya pindi ya wakati wa manabii wenyewe, bado ulirekodiwa kabla ya karne ya tatu K.W.K., kwa kuwa kufikia wakati huo ulikuwa tayari ukitafsiriwa katika Kigiriki katika Septuagint. Pia, Hati-kunjo za Bahari ya Chumvi (ambazo hutia ndani sehemu za vitabu vyote vya kiunabii) ni zenye tarehe ya karne ya pili na ya kwanza K.W.K. Kama ilivyoonyeshwa, unabii mwingi mbalimbali ulitimizwa baada tu ya tarehe hizo.

Je! Biblia Imejaa Mambo Yenye Kupingana?

9-12. (a) Kwa nini baadhi ya watu husema kwamba Biblia hujipinga yenyewe? (b) Baadhi ya “mambo yenye kujipinga” hutatuliwaje?

9 Lakini baadhi ya watu hupinga: ‘Biblia imejaa mambo yenye kupingana na yenye kuhitilafiana.’ Mara nyingi sana, wale ambao hushikilia hayo hawajajichunguzia wao wenyewe jambo hilo bali wamesikia tu kutoka kwa wengine mfano mmoja au miwili inayodaiwa kuwamo. Kwa kweli yale yanayodhaniwa mara nyingi kuwa mambo yenye kuhitilafiana yanatatuliwa kwa urahisi ikikumbukwa kwamba waandikaji wa Biblia mara nyingi walisema habari yao kwa maneno machache. Mfano wa jambo hilo unapatikana katika masimulizi ya uumbaji. Katika kulinganisha Mwanzo 1:1, 3 na Mwanzo 1:14-16, wengi wameuliza jinsi inavyoweza kuwa kwamba Mungu ‘alifanya’ vile vimulikaji katika siku ya nne ya uumbaji hali nuru—kwa wazi kutoka kwa vimulikaji vivyo hivyo—ilikuwa ikifikia dunia katika siku ya kwanza ya uumbaji. Katika kisa hiki mwandikaji Mwebrania aliondoa uhitaji wa maelezo marefu kwa uteuzi wa uangalifu wa maneno. Angalia kwamba mistari 14-16 husema juu ya “kufanya” tofauti na “kuumba” katika Mwanzo 1:1, na “mianga [vimulikaji]” tofauti na “nuru” katika Mwanzo 1:3. Hiyo yaonyesha kwamba katika siku ya nne ya uumbaji ndipo jua na mwezi, ambazo tayari zilikuwako, zilipopata kuonekana waziwazi kupitia anga zito la dunia. *

10 Orodha za nasaba pia zimetokeza mvurugo. Kwa mfano, Ezra huorodhesha majina 23 katika nasaba yake ya kikuhani kwenye 1 Mambo ya Nyakati 5:29-40 (6:3-14, UV) lakini yeye huorodhesha majina 16 tu kwa kipindi icho hicho wakati wa kutoa nasaba yake mwenyewe kwenye Ezra 7:1-5. Hiyo, si hitilafu, bali ni kufupiza tu. Kuongezea, kulingana na kusudi la mwandikaji katika kurekodi tukio, yeye alikazia, akapunguza, akaongezea, au akaacha mambo mengi ambayo mwandikaji mwingine wa Biblia aliyasema kwa njia tofauti katika kurekodi tukio lile lile. Hayo si mambo yenye kupingana, bali ni masimulizi tofauti tu yakionyesha njia ya mwandikaji ya kuona mambo na watu waliokusudiwa. *

11 Mara nyingi, kule kunakoonekana kuwa kutopatana kwaweza kutatuliwa kwa kuchunguza habari muktadha. Kwa mfano, “Kaini alipata wapi mke wake?” ni swali ambalo husikiwa mara nyingi, kukazia imani kwamba hiyo hufunua hitilafu katika masimulizi ya Biblia. Dhana ni kwamba Adamu na Hawa walikuwa na wana wawili tu, Kaini na Abeli. Gumu hilo linatatuliwa kwa urahisi ikiwa mtu anaendelea kusoma. Mwanzo 5:4 husema: “Baada ya kuzaliwa kwa Sethi, Adamu aliishi miaka 800 na kuzaa wana na mabinti.” Hivyo Kaini alioa mmoja wa dada zake au labda mpwa wake wa kike, jambo ambalo lingalipatana kabisa na kusudi la Mungu la awali la kuzidisha jamii ya kibinadamu.—Mwanzo 1:28.

12 Kwa wazi kuna mambo mengi ya historia ya kibinadamu yasiyoandikwa kuwa Rekodi ya Kimungu. Lakini kila jambo lililohitajiwa, kwa wale walioisoma kwanza na kwetu sisi leo pia, limetiwa ndani bila kuifanya iwe nyingi mno na isiyoweza kusomeka.

Ieleweke na Wasomi Tu?

13-15. (a) Ni kwa nini baadhi ya watu huamini kwamba Biblia ni ngumu mno kwetu kuweza kuielewa? (b) Sisi twajuaje kwamba Mungu alikusudia Neno lake lieleweke?

13 Je! umepata kuuliza: “Kwa nini kuna fasiri nyingi sana za Biblia zenye kuhitilafiana?” Baada ya kusikiliza wajuzi wa kidini wakipingana, baadhi ya watu wenye mioyo myeupe huvurugika na kuvunjika moyo. Mkataa ambao wengi hufikia ni kwamba Biblia haieleweki nayo hujipinga. Kama tokeo, wengi huikataa Biblia kabisa, wakiamini kwamba ni ngumu sana kuweza kusomeka na kueleweka. Wengine, wakabiliwapo na fasiri hizo nyingi sana tofauti-tofauti za kidini, hawataki kuchunguza Maandiko kwa uzito. Baadhi yao husema: “Watu wenye elimu wamejifunza kwa miaka mingi katika seminari za kidini. Ningewezaje kuwa na msingi wa kutilia shaka yale wanayofundisha?” Lakini je, hivyo ndivyo Mungu huona mambo?

 14 Wakati Mungu alipolipa taifa la Israeli Sheria, yeye hakuonyesha kwamba alikuwa akiwapa mfumo wa ibada ambao hawangeweza kuelewa, ambao ingekuwa lazima kuuacha mikononi mwa wajuzi au “wasomi” wa kitheolojia. Kupitia Musa, kwenye Kumbukumbu la Torati 30:11, 14, Mungu alijulisha hivi: “Hakika, Agizo hili ambalo nakuagiza leo hii si lenye kutatiza mno kwako, wala si lisiloweza kufikilika. Sivyo, jambo hilo li karibu sana nawe, katika kinywa chako na katika moyo wako, ili kulishika.” Taifa lote, si viongozi tu, liliambiwa: “Zingatia moyoni maagizo hayo ambayo ninakuamuru leo hii. Yakaze ndani ya watoto wako. Yakariri ukaapo nyumbani na uendapo njiani, ulalapo na uamkapo.” (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Amri za Mungu, zote zikiwa zimeandikwa, zilikuwa wazi vya kutosha kwa taifa zima kuweza kufuata, wazazi na watoto pia. *

15 Kurudi huko nyuma sana katika siku za Isaya, viongozi wa kidini walijiletea shutumu la Mungu kwa kujitwalia wenyewe daraka la kuongeza na kufasiri sheria ya Mungu. Nabii Isaya aliandika: “Watu hao wamekaribia Mimi kwa kinywa chao na kuheshimu Mimi kwa midomo yao, bali wameweka mioyo yao mbali na Mimi, na ibada yao kwangu Mimi imekuwa amri ya wanadamu, waliyojifunza kwa kukariri.” (Isaya 29:13) Ibada yao ilikuwa imekuwa amri ya wanadamu, si ya Mungu. (Kumbukumbu la Torati 4:2) ‘Amri hizo za wanadamu,’ fasiri na maelezo yao wenyewe, ndizo zilizokuwa zenye kupingana. Maneno ya Mungu hayakupingana. Ndivyo ilivyo leo.

Je! Kuna Msingi Wowote wa Kibiblia kwa Torati ya Mdomo?

16, 17. (a) Baadhi ya watu huamini nini kuhusu sheria ya mdomo? (b) Biblia huonyesha nini kuhusu sheria ya mdomo?

16 Baadhi ya watu huamini kwamba Musa alipokea “Torati ya Mdomo” kuongezea ile “Torati Iliyoandikwa.” Kulingana na imani hiyo, Mungu aliagiza kwamba amri fulani zisiandikwe bali zipitishwe kwa neno la mdomo toka kizazi hadi kizazi, zikihifadhiwa hivyo kwa pokeo la mdomo. (Ona kisanduku, “ Je! Torati Ina “Nyuso Sabini”?”) Hata hivyo, masimulizi ya Biblia huonyesha waziwazi kwamba Musa hakuamriwa kamwe kupitisha sheria ya mdomo. Kutoka 24:3, 4 hutuambia hivi: “Musa akaenda na kuwaambia watu kwa kuzirudia amri zote za BWANA na kanuni zote; nao watu wote wakajibu kwa sauti moja, wakisema, ‘Mambo yote ambayo BWANA ameamuru tutafanya!’” Ndipo Musa “akaandika amri zote za BWANA.” Mbele kidogo, katika Kutoka 34:27 twaambiwa hivi: “Naye BWANA akasema kwa Musa: Andika amri hizi, kwa kuwa kwa kulingana na amri hizi mimi nafanya agano pamoja na wewe na pamoja na Israeli.” Sheria ya mdomo isiyoandikwa haikuwa na fungu lolote katika agano ambalo Mungu alifanya pamoja na Israeli. (Ona kisanduku, “ Sheria ya Mdomo Ilikuwa Wapi . . .”.) Biblia haina mtajo wowote katika mahali popote kuhusu kuwako kwa sheria ya mdomo. * La maana zaidi, mafundisho yayo hupingana na Maandiko, yakiongeza lile wazo lenye kosa la kwamba Biblia hujipinga. (Ona kisanduku, “Kifo Na Nafsi—Ni Nini?”) Lakini mwanadamu, wala si Mungu, ndiye wa kulaumiwa kwa mvurugo huo.—Isaya 29:13. (Ona visanduku, “Showing Honor to the Divine Name.”))

17 Tofauti na fasiri zenye kupingana za wanadamu, Biblia yenyewe ni wazi na yenye kutumainika. Mungu ametuandalia uthibitisho wa kutosha ndani ya Neno lake kwamba ule ulimwengu wenye amani ulioonwa katika njozi kwenye Isaya 2:2-4 si ndoto tu bali ni uhakika utakaotimizwa karibuni. Si mwingine ila Mungu mwenyewe, Mungu wa unabii, Mungu wa Biblia, ndiye atautimiza.

^ fu. 9 Yapasa iangaliwe kwamba zile “siku” sita za uumbaji hazitii ndani ile taarifa kwenye Mwanzo 1:1, ambayo hurejezea uumbaji wa yale maumbo ya kimbingu. Zaidi ya hilo, neno la Kiebrania litafsiriwalo “siku” huruhusu kuwe na wazo la kwamba matukio yaelezwayo kwenye Mwanzo 1:3-31 yalitukia kwa ‘vipindi vya wakati’ sita ambavyo vingeweza kuwa na urefu wa maelfu mengi ya miaka.—Linganisha Mwanzo 2:4.

^ fu. 10 Ili kuona mifano, ona kitabu “Je! Biblia Hujipinga Yenyewe?

^ fu. 14 Maswali magumu ya kesi za hukumu yalishughulikiwa na mpango wa hukumu ulioonyeshwa waziwazi. (Kumbukumbu la Torati 17:8-11) Katika mambo mengine yoyote ya maana yaliyoonekana kutokuwa wazi, ili kupokea jibu la Mungu, taifa lilielekezwa, si kwa sheria ya mdomo, bali kwa Urimu na Thumimu mikononi mwa makuhani.—Kutoka 28:30; Mambo ya Walawi 8:8; Hesabu 27:18-21; Kumbukumbu la Torati 33:8-10.

^ fu. 16 Baadhi ya watu wamejaribu kufasiri maneno kwenye Kumbukumbu la Torati 17:8-11 kuwa yakidokezea pokeo la mdomo lililopuliziwa. Hata hivyo, kama ilivyotajwa katika kielezi cha chini kwenye  fungu la 14, maneno hayo hushughulikia tu utaratibu wa hukumu katika kesi za hukumu. Angalia kwamba suala halikuwa kama desturi tofauti-tofauti au mapokeo yalipitishwa kupitia karne nyingi au la. Bila shaka kulikuwako mapokeo fulani yaliyopitishwa kwa habari ya jinsi ya kutimiza kihususa sehemu fulani za Sheria. Lakini uhakika wa kwamba pokeo limedumu muda mrefu hauthibitishi kwamba lilipuliziwa. Kwa mfano, angalia pokeo lililositawi kuhusu ile nyoka ya shaba.—Hesabu 21:8, 9; 2 Wafalme 18:4.