Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Ataongoza Mataifa Kwenye Amani?

Ni Nani Ataongoza Mataifa Kwenye Amani?

1, 2. Unabii kwenye Isaya 2:2-4 unatimizwaje katika siku yetu?

ISAYA sura ya 2 si unabii tu juu ya kurudi Yerusalemu kwa Wayahudi baada ya miaka 70 ya utekwa wa Kibabuloni, ni zaidi. Kweli kweli, unabii huo hurejezea hasa kurudishwa kwa vikundi vya watu wa mataifa yote kwenye ibada safi ya yule Mungu pekee wa kweli, Yehova. Hudokeza kufanyizwa kwa udugu wa kimataifa wenye kutoa utumishi mtakatifu wenye kukubalika kwa Mungu.

2 Mgeuzo mkubwa kadiri hiyo, wenye kutia ndani watu wa kila sehemu ya ulimwengu, usingekuwa wenye kutokeza tu bali pia wenye kuonekana, kana kwamba unatukia juu ya mlima ukionekana na kila mtu. Hilo ndilo hasa linalotukia miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Mamilioni kutoka dini za Jumuiya ya Wakristo wamejifunza kwamba Mungu ni mmoja na wameacha kuabudu Utatu. Katika India, Wahindu wameacha mkusanyo wa miungu mingi na makumi ya maelfu ya sanamu kwa ajili ya yule Mungu mmoja wa kweli. Na ndivyo ilivyo pia kwa habari ya watu katika Afrika, kwenye visiwa vya mbali, na katika Mashariki ya Kati. Wale ambao wamepanda kwenda kwenye mlima mtakatifu wa Yehova, ibada yake safi, wameondolea mbali chuki zote za kijamii, kikabila, na kisiasa; kihalisi wao ‘hawajifunzi vita tena.’—Isaya 2:2-4.

Utambulisho wa Mesiya—Chanzo cha Ubishi

3. Kulingana na Isaya 11:10, Mesiya angekuwa na matokeo gani juu ya mataifa?

3 Udugu huo wa kimataifa unahusiana pia na utimizo wa kusudi la Mungu kwa ainabinadamu yote: kwamba watu wa mataifa yote wangejibariki wenyewe kwa njia ya “mbegu” aliyeahidiwa, mzao wa Abrahamu, na hivyo wamwabudu Mungu katika kweli na umoja. (Mwanzo 3:15; 22:18, JP) Unabii mwingi wa baadaye ulionyesha kwamba “mbegu” huyo angekuwa pia ndiye ‘nabii aliye kama Musa,’ ambaye angepatanisha agano jipya ambalo lingetumika kuwa msingi wa kisheria ili watu wenye mioyo myeupe wa mataifa yote wamwabudu Mungu katika umoja. (Kumbukumbu la Torati 18:15, 18, 19; Yeremia 31:31-34) Kwa kuongeza, uyo huyo angekuwa ndiye Mesiya, mtawala kutoka nasaba ya Daudi, ambaye kiti cha ufalme chake Mungu angesimamisha milele. (1 Mambo ya Nyakati 17:11, 12) Kulingana na nabii Isaya, Mesiya angekuwa ndiye mtu wa kuendewa ambaye angeunganisha watu kutoka kwa mataifa (Kiebrania, Goh·yimʹ) yote. Isaya 11:10 husema hivi: “Itakuwa katika siku hiyo, kwamba lile shina la Yese, lisimamalo kuwa bendera [“kama kionyo,” NW] ya vikundi vya watu, mataifa yatamtafuta; na mahali pake pa kupumzikia patakuwa patukufu.”—JP.

4. Rabi mmoja alitaarifu nini kuhusu matokeo ya Yesu juu ya jamii ya kibinadamu?

4 Utambulisho wa Mesiya umejadiliwa kwa karne nyingi. Kulingana na Isaya 11:10 na maandiko mengine, angekuwa Myahudi, mzao wa Daudi (mwana wa Yese), na watu wa mataifa yote wangemkubali kuwa Mesiya halali aliyetumwa na Mungu. Mwalimu Myahudi wa karne ya kwanza, Rabi H. G. Enelow aliandika hivi, akirejezea Yesu: “Hakuna Myahudi mwenye akili awezaye kupuuza uhakika wa kwamba Myahudi angalipaswa kuwa na sehemu kubwa sana hivyo katika elimu na mwelekezo wa kidini kwa jamii ya kibinadamu.”10 Ni Myahudi mwingine yupi ambaye Wasio-Wayahudi wengi hivyo wamemkubali kuwa Mesiya? Je! Myahudi mwingine angekubaliwa zaidi? Hata hivyo, kuna wale ambao huliona hilo kuwa lenye kufadhaisha sana, yaani, kwamba yaelekea Yesu ndiye Mesiya. Sababu zao zastahili kuchunguzwa.

Uasi-Imani wa Jumuiya ya Wakristo

5-7. Kwa nini wengi huona majina yenyewe ya Yesu na Ukristo kuwa yenye kuchukiza?

5 Kwa walio wengi sana miongoni mwa wasio Wakristo, ni Jumuiya ya Wakristo, ambayo waamini wayo hudhaniwa kuwa wafuata mafundisho ya Kristo, ndiyo imesababisha wachukizwe na jina hasa la Yesu. Katika jina la Yesu, mataifa mengi yameteseka mikononi mwa Jumuiya ya Wakristo, lakini bila shaka Wayahudi wameteseka zaidi ya lolote la hayo.

6 Katika wakati wetu wenyewe, upinzani wa Jumuiya ya Wakristo dhidi ya Wayahudi ulifikia upeo katika yale Machinjo Makuu ya Nazi. Ingawa sababu nyingi zilihusika, uadui wa kidini hauwezi kupuuzwa kuwa moja ya zile kubwa. Na ikiwa katika Jumuiya ya Wakristo baadhi yao wangekana jambo hilo, uhakika wa kwamba “Wakristo,” Wakatoliki na Waprotestanti pia, walikuwa miongoni mwa wale waliofanya mauaji hayo au wakayaachilia, ni jambo lisiloweza kukanwa. Elie Wiesel hutoa muhtasari wa maoni ya Wayahudi katika kitabu chake A Jew Today: “Mtu ataelezaje ni kwa nini kanisa halikutenga na ushirika ama Hitler ama Himmler? Kwa nini Pius 12 hakufikiria kwamba kushutumu [kambi za mateso za] Auschwitz na Treblinka kulihitajiwa kabisa, licha ya kuwa jambo la lazima? Kwa nini miongoni mwa wale S.S. [kikosi maalum cha askari wa Hitler], sehemu yao kubwa walikuwa waamini walioendelea kuwa waaminifu kwa mafungamano yao ya Kikristo mpaka mwisho? Kwa nini walikuwako wauaji waliokwenda kuungama katikati ya machinjo? Kwa nini wote walikuwa watu wa kutoka familia za Kikristo na walikuwa wamepokea elimu ya Kikristo?”11 Kwa hiyo, ni imani ya kadiri gani ambayo Wayahudi wangetarajiwa kuonyesha katika mtu fulani ambaye jina lake lilihusianishwa kwa karne nyingi na kila mtwezo na pigo walilopokea?

7 Kando na mnyanyaso wa moja kwa moja, nchi za “Kikristo” zimetolea sehemu nyingine ya ulimwengu kielelezo cha kiadili cha aina gani? Hakuna, isipokuwa vita, Krusedi, na Mabaraza “matakatifu” ya Kuhukumia Wazushi. Hata Vita ya Ulimwengu 1 na Vita ya Ulimwengu 2 vilianza katika nchi za “Kikristo.” Je! ingeweza kusemwa kwamba adili za “Kikristo” zimekuwa kielelezo kizuri? UKIMWI kama kielelezo, umeenea sana katika nchi ambako idadi iliyo kubwa hudai kufuata Ukristo. Kashifa miongoni mwa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo ni zenye sifa mbaya sana. Waevanjeli wa TV wenye ukosefu wa adili, ambao hujipatia mamilioni ya dola na kuishi kama wafalme pamoja na makasisi wagoni-jinsia-moja, ambao baadhi yao wameshtakiwa kwa kuwatenda vibaya kingono vijana wachanga wa kiume, ni mambo machache tu kati ya yale ambayo wasio Wakristo huhisi kwamba huonyesha Ukristo ulivyo—tunda ambalo huchafua jina la Yesu, ambaye “Wakristo” hudai kumfuata.

8-10. (a) Kwa nini Jumuiya ya Wakristo haiwezi kudai kwa haki kumwakilisha Yesu na Ukristo wa kweli? (b) Maandiko yalitoa onyo gani juu ya uasi-imani dhidi ya mafundisho ya kweli ya Yesu?

8 Kwa kuongezea, Dini ya Kiyahudi na Uislamu pia zina haki ya kuchukizwa na ibada ya sanamu ieneayo katika Jumuiya ya Wakristo. Mafundisho mengi yasiyo ya Kimaandiko ya Jumuiya ya Wakristo, kama vile kuabudu Maria kuwa “Mama ya Mungu,” pia huchukiza dini hizo. Lile fundisho la Utatu hasa huonwa na Wayahudi kwa dharau kuwa unapingana waziwazi na kiini chenyewe cha Dini ya Kiyahudi—lile wazo la imani katika Mungu mmoja lililotiwa katika maneno “SIKIA E ISRAELI: BWANA MUNGU WETU, BWANA NI MMOJA.”—Kumbukumbu la Torati 6:4, JP.

9 Minyanyaso iliyotendwa na Jumuiya ya Wakristo, vita vyayo, ukosefu wa adili, unafiki, na mafundisho yenye kukufuru havisameheki si machoni pa wasio-Wakristo tu bali pia machoni pa Mungu Mweza Yote. Kwa sababu hiyo, ingawa Mashahidi wa Yehova, ni wafuasi wa Yesu Kristo, wao si sehemu ya Jumuiya ya Wakristo. Jumuiya ya Wakristo, kwa upande mwingine, si sehemu ya Ukristo wa kweli. Kwa kweli ufanani pekee kati ya Jumuiya ya Wakristo na Wakristo wa kwanza ni utumizi wa jina Yesu. Lakini ikiwa mafundisho ya Yesu yalikuwa mema na yenye kutumika kwa kutokeza sana hivyo, uasi-imani kama huo ulitukiaje?

10 Kwa kweli, jambo la kwamba Wakristo bandia wangeinuka na kwamba kungekuwako uasi-imani dhidi ya mafundisho ya kweli ya Yesu kulitabiriwa na Yesu mwenyewe pamoja na waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambayo hurejezewa kimakosa kuwa Agano Jipya. (Matendo 20:29, 30; 2 Wathesalonike 2:1-12; 1 Timotheo 4:1-3; 2 Petro 2:1, 2) Kulingana na Mathayo 7:21-23, Mesiya mwenyewe angehukumu waasi-imani hao kwa vile walivyo naye angewaambia, “Mimi sikuwajua kamwe! Ondokeni kwangu, nyinyi wafanyaji wa uasi-sheria.”—NW; linganisha Mathayo 13:24-30, 37-43.

Kwa Nini Maandiko Zaidi Yalihitajiwa?

11, 12. (a) Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ni nini? (b) Ni nani walioandika Maandiko hayo? (c) Kwa nini kupuliziwa na Mungu kulihitajiwa kwa ajili ya maandishi hayo?

11 Mwanzoni, wafuasi wote wa Yesu walikuwa Wayahudi. Kwa kweli, maelfu ya Wayahudi katika karne ya kwanza, kutia “jamii kubwa ya makuhani,” walimkubali Yesu kuwa ndiye ‘nabii aliye kama Musa,’ ndiye Mesiya hasa. (Matendo 2:5, 37, 41; 4:4; 6:7; Kumbukumbu la Torati 18:18) Wayahudi haohao wakawa msingi wa kikundi kipya cha kimataifa cha waabudu wa Yehova Mungu, kilichoanzishwa kisheria juu ya msingi wa “agano jipya,” alilopatanisha nabii huyo aliye mfano wa Musa.—Yeremia 31:31-34.

12 Agano jipya lilikuja na uhitaji wa maandishi zaidi yaliyopuliziwa ambayo yangeandaa habari zaidi iliyohitajiwa kwa ajili ya wale ambao wangemtumikia Mungu chini ya huu mpango wa agano jipya. Maandishi hayo, yale Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, yote yaliandikwa na Wayahudi. Hayo huripoti juu ya maisha na mafundisho ya Yesu, hujazia mambo mengi madogomadogo kuhusu unabii mwingi ulioandikwa katika Maandiko ya Kiebrania, na kueleza waziwazi mambo kuhusu Mesiya na fungu lake katika kusudi la kimungu. Kwa kuongezea, yanatia ndani barua ambazo hutumika kuwa shauri na kitia-moyo kwa kikundi hicho kipya cha kimataifa cha waabudu. *

Je! Yesu Alikuwa Ndiye Mesiya Aliyeahidiwa?

13-16. Ni nini kilichosadikisha Wayahudi wengi wa karne ya kwanza kwamba Yesu alikuwa ndiye yule Mesiya?

13 Lakini je, Yesu hakukataliwa na viongozi wa kidini wa siku zake? Ndiyo, na hao nao walitumia uvutano wao juu ya umati. Lakini je, Yeremia na manabii wengine hawakukataliwa na viongozi wa kidini wa siku zao? (Yeremia 7:25, 26; 20:1-6; 2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16) Wale wa kizazi cha Yesu walioamini katika yeye, waliokuwa na fursa wao wenyewe ya kuchunguza mafundisho na kazi zake pamoja na unabii mwingi kumhusu, hawakukengeushwa na upinzani wa viongozi wa kidini, walioona umiliki wao wa mambo ya kidini ukitishwa. Yale ambayo Wayahudi hao wenye mioyo myeupe walikuwa wameshuhudia yaliwasadikisha kwamba ule unabii mwingi wa Kimesiya ulikuwa umetimizwa katika Yesu. Ni nini uliokuwa uthibitisho mwingi wenye nguvu uliowafanya Wayahudi hao wa karne ya kwanza wawe na nia ya kuhatirisha kila kitu, hata kifo, kwa kujulisha imani katika Yesu kuwa ndiye yule Mesiya aliyeahidiwa?—Yohana 9:22; 16:2.

14 Jambo la kwanza kabisa, wakati ulikuwa sahihi. Unabii kwenye Danieli sura ya 9, kuhusu Mesiya, ulionyesha kwamba angetokea kabla ya uharibifu wa hekalu la pili. *Danieli 9:24-27.

15 Pili, huyo mtu mwenyewe alikuwa na sifa za ustahili. Alikuwa wa kutoka kabila la Yuda na mzao wa Mfalme Daudi. (Mwanzo 49:10; 1 Mambo ya Nyakati 17:11-14; linganisha Mathayo 1:1-16; Luka 3:23-31.) Pia, alizaliwa katika Bethlehemu, ulioeleweka kwa ujumla miongoni mwa Wayahudi wa karne ya kwanza kuwa ndipo mahali pa uzaliwa wa Mesiya. * (Mika 5:1 [5:2, UV]; linganisha Mathayo 2:4-6; Luka 2:1-7; Yohana 7:42.) Zote hizi zilikuwa sifa za ustahili za maana ambazo Wayahudi wa siku za Yesu walitarajia Mesiya awe nazo zikiwa njia ya utambulisho.

16 Kisha, mafundisho ya huyo mtu hayana makosa. Hayakuwa ya kisiasa au ya kushikilia sana sheria bali ya kiroho na yenye kanuni za kiadili. * Alifikia kiini cha mambo kwa njia isiyotatanisha. Zaidi ya hayo, alithubutu kutegemea kabisa Maandiko kuwa mamlaka yake ya mwisho, si maneno ya viongozi wa kidini wa wakati uliopita, kama ilivyokuwa desturi. Jambo hilo lilishangaza umati, maana “alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi wao.” (Mathayo 7:29, UV) Masimulizi ya maisha ya Yesu hufunua utu wenye nguvu sana, na mafundisho yaliyo wazi sana, hivi kwamba wanahistoria hutaja hiyo kuwa mojawapo ya sababu za kushikilia kwamba yeye hakuwa mtu wa kihadithi tu. *

17-20. (a) Ni unabii upi mbalimbali katika Maandiko ya Kiebrania uliosema juu ya wakati wa kuja kwa Mesiya na wa kifo chake cha dhabihu? (b) Kwa nini Mesiya alihitajiwa kufa?

17 Unabii mbalimbali wa Maandiko ya Kiebrania, uliokubaliwa kwa muda mrefu kuwa wa Kimesiya, ulitimizwa kupitia kuteseka na kifo cha Yesu. Unabii huo hufungamanisha kifo cha Mesiya na msamaha wa dhambi. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ufuniko huo ulioandaliwa na kifo cha Mesiya unarejezewa kuwa ‘dhabihu ya fidia.’ (Mathayo 20:28; Warumi 3:24) Baadhi ya unabii huo ulikuwa nini?

18 Angalia maneno ya unabii kwenye Danieli 9:24, 25 (JP): “Majuma sabini yameamriwa juu ya watu wako na juu ya jiji lako takatifu, ili kumaliza ukiukaji sheria, na kufanyiza mwisho wa dhambi, na kusamehe makosa, na kuleta ndani uadilifu wa milele . . . mpaka kwa yule mpakwa-mafuta [“Mesiya,” Kiebrania, Ma·shiʹach], mkuu.” Mtu hawezi kuepuka kuona ufungamano uliowekwa katika andiko hilo kati ya “Mesiya” (Mpakwa-Mafuta) na ‘kumalizwa kwa ukiukaji sheria na kufanyiza mwisho wa dhambi.’ Mstari wa 26 huendelea kutaarifu kwamba “baada ya majuma sitini na mawili mpakwa-mafuta [“Mesiya,” Kiebrania Ma·shiʹach] atakatiliwa mbali,” yaani, auawe. (Ona kisanduku,  Mpakwa-Mafuta’ Alikuwa Nani? Angekuja Wakati Gani?”)

19 Andiko jingine ambalo linahusiana na ‘kukatiliwa mbali,’ au kuuawa kwa Mesiya akiwa dhabihu yenye kufunika, lapatikana kwenye Isaya 52:13 hadi 53:12. (Ona kisanduku, “ ‘Mtumishi Wangu”—Yeye Ni Nani?”) Marabi katika karne ya kwanza walitumia andiko hilo juu ya Mesiya, kama vile Rambam na wengine walivyofanya katika Enzi za Katikati. Andiko hilo huonyesha waziwazi kwamba msamaha unafungamanishwa na Mesiya na kifo chake.

20 Kwa sababu hizo zilizo juu, fundisho la kwamba kifo cha Mesiya kingewezesha msamaha kamili wa dhambi machoni pa Mungu lilieleweka kwa urahisi na Wayahudi wengi wa karne ya kwanza. Walijua kwamba Maandiko yalisema juu ya kutokamilika kwa mwanadamu kulikorithiwa. (Mhubiri 7:20) Uhitaji wa dhabihu ili kufunika dhambi ulikuwa somo lililotambuliwa kila siku; ulidokezwa waziwazi katika mpango na namna yenyewe ya agano la Sheria. Matukio yaliyoelezwa katika masimulizi ya maisha ya Yesu humwonyesha akiwa mwanadamu mkamilifu ambaye kifo chake kingeweza kuleta ufuniko wa dhambi ya ainabinadamu. * (Mathayo 20:28; Luka 1:26-38) Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalipokazia kwamba dhabihu mbalimbali chini ya Sheria zilifananisha dhabihu hiyo moja kamilifu na ya mwisho, maana kamili zaidi ilitolewa kwa mpango mzima wa Sheria, pamoja na sehemu nyingine za Maandiko. *Waebrania 10:1-10.

Kama Musa​—Nabii Mwenye Kutegemeka

21, 22. (a) Matukio ya kihistoria kuhusu uharibifu wa Yerusalemu huthibitishaje kwamba Yesu alikuwa nabii wa kweli? (b) Matukio ya kihistoria kuhusu siku yetu huthibitishaje pia jambo hilo?

21 Zaidi ya kuelezea kifo cha Yesu akiwa dhabihu ya fidia, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hukazia pia fungu lake akiwa ‘nabii aliye kama Musa.’ (Kumbukumbu la Torati 18:18; ona sehemu ya “Ni Nini Kusudi la Mungu kwa Ainabinadamu?,” mafungu 17 hadi 19.) Akiwa hivyo, alitoa unabii wa kuharibiwa kwa Yerusalemu naye akawaagiza wanafunzi wake walikimbie jiji wakati ambapo wangeona limezingirwa na majeshi. (Mathayo 23:37–24:2; Luka 21:20, 21) Lakini mtu aweza kukimbiaje jiji wakati limezingirwa na majeshi? Mwanahistoria Myahudi Yoseph ben Mattatiyahu (Yosefu), mwenyewe akiwa shahidi aliyejionea kwa macho matukio hayo, arekodi jibu: “Sestio [kamanda wa jeshi la Kiroma, 66 W.K.] . . . akaamuru watu wake waondoke, akakata tumaini ijapokuwa hakuwa ameshindwa, na bila sababu yoyote akaondoka katika Jiji hilo.”13 Hiyo ndiyo nafasi ambayo Wakristo walihitaji ili kulikimbia hilo jiji. Miaka minne baadaye, katika 70 W.K., vikosi vya Roma, sasa chini ya Jenerali Tito, vilirudi na kulizingira hilo jiji tena. Yesu alikuwa ametoa unabii kuhusu hilo jiji kwamba adui angejenga ‘mazingiwa kwa miti yenye kuchongoka na angezunguka jiji na kulibana kila upande.’ (Luka 19:43, NW) Yosefu huthibitisha kwamba Tito alijenga mazingiwa kama hayo kwa miti yenye kuchongoka, kwa umbali wa karibu kilometa 8, akimaliza miti ya mashambani kwa umbali wa kilometa 16 hivi kuzunguka jiji. Unabii wa Yesu ulitoa maagizo sahihi kabisa juu ya jinsi ya kuepuka uharibifu mikononi mwa Waroma, na usahihi wayo wathibitishwa na uhakika wa kwamba maisha za wale wote walioyatii ziliokolewa.—Luka 21:20-24.

22 Yesu alitoa unabii pia juu ya uharibifu wa wakati ujao utakaoletwa na Mungu dhidi ya uovu wote na wale ambao huusababisha. Kwenye Luka 21:24 (NW), alirejezea “zile nyakati zilizowekwa za mataifa,” kuonyesha kwamba Mungu alikuwa na mpaka kuhusu urefu wa muda ambao angevumilia utawala wa kibinadamu. * Yesu alitabiri pia kwamba siku za mwisho za utawala wa mwanadamu zingeonyeshwa na vita, njaa, matetemeko ya dunia, magonjwa ya kipuku, uhalifu, na jeuri, na kwamba kabla ya mwisho wa utawala wa mwanadamu, kazi ya elimu ya ulimwenguni pote ingefanywa ili kuarifu watu wa mataifa yote kwamba serikali ya Mungu ingekuwa ikitawala kutoka mbinguni. (Ona Mathayo 24:3-14; Luka 21:10, 11.) Mashahidi wa Yehova huamini kwamba ishara hiyo kubwa yenye sehemu nyingi imekuwa ikionekana tangu 1914, wakati “zile nyakati zilizowekwa za mataifa” zilipofikia mwisho wazo. Muda mrefu kabla ya wakati huo walikuwa wakitangaza kwamba 1914 ungekuwa tarehe iliyotiwa alama katika historia ya kibinadamu. Wakati vita ya ulimwengu ya kwanza ilipoanza katika Agosti wa mwaka huo, matarajio yao juu ya jambo hilo yalithibitishwa. Kwa kweli, hapana yeyote kati ya Mashahidi aliyekuwa amepokea njozi za kimungu; funzo lao la bidii yenye kuendelea la Maandiko Matakatifu ndilo lililoongoza kwenye mkataa huo.

Mataifa Yaelimishwa Katika Njia za Amani

23. Yesu angewezaje kuwa ndiye Mfalme wa Ufalme wa Mungu aliyewekwa rasmi?

23 Hata hivyo, fungu la Mesiya katika kuandaa dhabihu ya fidia na katika kuwa nabii aliye kama Musa lingekuwa na thamani ndogo tu ikiwa upande wa mwisho wa fungu lake katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu haukutimizwa—kuwa kwake ndiye Mfalme wa Ufalme wa Mungu aliyewekwa rasmi. (Isaya 9:5, 6 [9:6, 7, UV]) Lakini Yesu angeweza kushikaje cheo hicho akifa? Kwa kupatana na unabii kuhusu Mesiya, Mungu alifufua Yesu katika siku ya tatu ya kifo chake. (Zaburi 16:8-11; Isaya 53:10, 12; linganisha Mathayo 28:1-7; Luka 24:44-46; Matendo 2:24-32; 1 Wakorintho 15:3-8.) Mungu alimrudisha kwenye uhai, si akiwa binadamu, kwani alikuwa amekwisha kutoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu katika dhabihu, bali akiwa kiumbe-roho mwenye nguvu, akingojea kwenye mkono wa kulia wa Mungu ili kupata maagizo zaidi.—Zaburi 110:1; Matendo 2:33-35; Waebrania 10:12, 13.

24-26. Mashahidi wa Yehova wanashirikije katika utimizo wa unabii wa Isaya?

24 Mfalme Daudi aliandika kwamba wakati ambapo huyo Mesiya angeanza kutawala, ‘watu wa Mungu wangejitolea kwa moyo wa kupenda.’ (Zaburi 110:3, NW) Ijapokuwa hali za ulimwengu zimezidi kuwa mbaya tangu mwaka huo uliotiwa alama wa 1914, kumekuwako pia utimizo wa upande mzuri wa unabii huo; watu wa Mungu wamejitolea kwa moyo wa kupenda wakati wao ili kuhubiri hizi ‘habari njema za ufalme katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya ushahidi kwa mataifa yote.’ (Mathayo 24:14, NW) Kwa mfano, kila mwaka Mashahidi hutumia mamia ya mamilioni ya saa wakiongea na watu juu ya Ufalme wa Mungu na kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani bila malipo pamoja na wale wenye kupendezwa katika kuchunguza mambo ya hakika.

25 Wakati huo wote hutolewa bila malipo. Wale wenye kufanya kazi hiyo watoka katika kila namna ya maisha, wa umri wote, na kutoka karibu kila namna ya kazi iwazikayo. Hao ndio waelezwao kwenye Isaya 2:3 kwa maneno haya: “Na watu wa vikundi vingi watakwenda na kusema: ‘Njoni, acheni sisi tupande kwenye Mlima wa BWANA, [Kiebrania, יהזה, Yehova].’” Hiyo si kampeni tu ya “kupata nafsi.” Ni programu ya elimu ya ulimwenguni pote yenye malengo mawili: (1) Kuarifu watu wa kila taifa kwamba Ufalme wa Mungu unatawala na kuwaambia jambo hususa ambalo utafanya hivi karibuni, na (2) kuelimisha, bila malipo, wale wote wanaotaka kuchunguza mambo ya hakika na kumtumikia Mungu aliye hai kulingana na matakwa yake. Fanikio la kazi hii na utimizo wa unabii vimehakikishwa. Kwa nini? Kwa sababu Yehova Mungu mwenyewe anaiunga mkono.—Zekaria 4:6.

26 Je! si jambo la akili kuona kazi ya Mashahidi wa Yehova kuwa utimizo wa unabii kwenye Isaya 2:3? Je! wewe wajua mtu mwingine yeyote anayefanya kazi hii? Au wafikiri ni tukio la nasibu tu kwamba mamilioni ya watu hutafuta wakati katika maisha zao ili kuongea juu ya ujumbe uliotolewa unabii miaka elfu mbili hivi iliyopita, ujumbe ambao ungetangazwa katika pindi ya wakati wa msukosuko usio na kifani? Ndiyo, katika siku hizi za mwisho, Mashahidi wa Yehova ndio wamekuwa ‘nuru kwa mataifa.’ (Isaya 42:6; 49:6) Wao ndio udugu wa kimataifa pekee utumikiao Yehova Mungu kwa umoja na kwa amani chini ya mwelekezo wa Mesiya, lile “shina la Yese,” ambaye wanamtangaza kuwa ‘kionyo’ kwa mataifa.—Isaya 11:10, NW, JP.

Mashahidi wa Yehova, waonekanao hapa kando ya Bahari ya Galilaya, Israeli, wanatenda pia ulimwenguni pote, wakiwaalika watu wa mataifa yote wajifunze zaidi juu ya makusudi na matakwa ya Mungu

^ fu. 12 Baadhi ya watu hudai kwamba maandishi hayo hujipinga yenyewe au kwamba hupinga Maandiko ya Kiebrania. Hata hivyo, uchunguzi wa hayo yanayodhaniwa kuwa mapingano huthibitisha kwamba sivyo ilivyo. Kwa kweli, kanuni ile ile iliyotumika kwa yanayodhaniwa kuwa mapingano ndani ya Maandiko ya Kiebrania yenyewe yatumika hapa. (Ona sehemu ya “Biblia—Je! Imepuliziwa na Mungu?,” mafungu 9 hadi 12.) Kwa kuwa Wakristo wote wa kwanza, kutia na wale walioandika vitabu vilivyojumuika kuwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, walikuwa Wayahudi, hawakuchochea upinzani dhidi ya Wayahudi kama wasivyofanya wale manabii Wayahudi kabla yao ambao walishutumu viongozi wa kidini wa siku zao.

^ fu. 14 Miongoni mwa Wayahudi wa karne ya kwanza, mlikuwamo uelewevu wa ujumla kwamba unabii huo ungetimia katika wakati wao wenyewe. (Luka 3:15) Katika kitabu chake De Termino Vitae (Kuhusu Mwisho wa Maisha), rabi mmoja wa karne ya 17, Menasseh ben Israel, aliandika hivi: “Wengine wangekubali hayo majuma 70 kuwa yamaanisha kwamba baada ya mwisho wayo Mesiya angekuja ambaye angewafanya kuwa watawala wa ulimwengu wote. Kweli kweli, wote waliochukua silaha dhidi ya Waroma wakati ule walikuwa na maoni hayo.”

^ fu. 15 Lile fasilio la kale katika Kiaramu la Kiyahudi, au Targumu, la Mika 5:1 hutaarifu hivi: “Kutoka kwako [Bethlehemu] Mesiya atatoka kwenda mbele zangu.”

^ fu. 16 Mwanahistoria Myahudi Joseph Klausner aliandika hivi: “Mtu kama Yesu, ambaye kwake kanuni bora ya adili ilikuwa ya maana sana, alikuwa kitu kisichopata kusikiwa katika Dini ya Kiyahudi ya wakati huo. . . . Hivyo, mafundisho yake ya kiadili, kwa wazi hupita yale ya Pirkē Aboth na ya fasihi nyingineyo ya Talmud na ya Midrash. Hayapotelei katikati ya kiasi kikubwa mno cha maagizo ya kisheria-sheria na mambo ya habari ya kilimwengu.”12

^ fu. 16 Kwa masimulizi kamili zaidi ya maisha na huduma ya Yesu, ona kitabu Yesu—Njia, Kweli, na Uzima.

^ fu. 20 Mtume Paulo alirejezea Yesu kuwa ‘Adamu wa pili,’ ambaye kifo chake kilileta kufunikwa kwa dhambi iliyorithiwa kutoka Adamu. (1 Wakorintho 15:45-47; Warumi 5:12, 15-19) Kwa habari zaidi juu ya kwa nini mpango kama huo ulihitajiwa, ona sehemu ya “Ni Nini Kusudi la Mungu kwa Ainabinadamu?,” mafungu , na na kielezi-chini.

^ fu. 20 Kwa msaada wa habari hiyo hadithi yote ya Abrahamu huchukua maana mpya. Mungu hakuwa akimwomba Abrahamu amwue mwana wake ili kujaribu tu imani yake bali pia afanye drama ya mfano ili watu waweze kuelewa kwamba Mungu mwenyewe angeandaa dhabihu, mtu fulani ampendaye sana, kwa manufaa za milele za ainabinadamu. Yule aliyetolewa angekuwa Mbegu hasa ya Abrahamu, ambaye kupitia yeye Mungu alikuwa ameahidi kwamba “mataifa yote ya dunia yangejibarikia yenyewe.” (Mwanzo 22:10-12; 16-18; linganisha Yohana 3:16.) Ufanani na wazo ni wazi na hususa mno kuwa tukio la nasibu au ubuni wa werevu tu wa wanaume fulani.

^ fu. 22 Katika kutaja “zile nyakati zilizowekwa za mataifa,” kwa wazi Yesu alikuwa akirejezea ule unabii kwenye Danieli 4:10-34 (4:10-37, UV). Kwa maelezo kamili ya unabii huo, ona nyongeza “Jinsi Unabii wa Danieli Ulivyotabiri Kutokea kwa Masihil” katika kitabu Biblia Inatufundisha Nini Hasa?