Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 1

“Kumpenda Mungu Humaanisha Hivi”

“Kumpenda Mungu Humaanisha Hivi”

“Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”—1 YOHANA 5:3.

1, 2. Ni nini ambacho kinakuchochea kumpenda Yehova Mungu?

JE, UNAMPENDA Mungu? Ikiwa umejiweka wakfu kwa Yehova Mungu, basi jibu lako litakuwa: “Bila shaka!” Na ndivyo inavyopaswa kuwa! Kwa kweli, tuna tamaa ya kiasili ya kumpenda Yehova. Tunachochewa kumpenda Mungu kwa kuwa anatupenda. Biblia inasema: “Kwa habari yetu, sisi tunaonyesha upendo, kwa sababu [Yehova] alitupenda sisi kwanza.”—1 Yohana 4:19.

2 Yehova ndiye wa kwanza kutuonyesha upendo. Ametupa makao mazuri duniani. Anatuandalia mahitaji yetu ya kimwili. (Mathayo 5:43-48) Mbali na hayo, anatutimizia mahitaji yaliyo ya maana zaidi, mahitaji ya kiroho. Anatupa Neno lake, Biblia. Tena, anatutia moyo tusali kwake tukiwa na uhakika wa kwamba atatusikia na kutupa roho yake takatifu itusaidie. (Zaburi 65:2; Luka 11:13) Zaidi ya yote, alimtuma Mwana wake wa pekee awe Fidia ili tukombolewe kutoka katika dhambi na kifo. Yehova ametuonyesha upendo mkubwa kama nini!—Yohana 3:16; Waroma 5:8.

3. (a) Tunahitaji kufanya nini ili kukaa katika upendo wa Mungu? (b) Ni jambo gani la maana ambalo tunapaswa kujiuliza, na jibu linapatikana wapi?

3 Yehova anataka tufaidike kutokana na upendo wake milele. Hata hivyo, maamuzi tunayofanya yataamua ikiwa tutafaidika au hatutafaidika. Neno la Mungu linatutia moyo hivi: “Jitunzeni katika upendo wa Mungu,” mkitazamia uzima wa milele. (Yuda 21) Neno “jitunzeni” linaonyesha kwamba ili kukaa katika upendo wa Mungu, tunahitaji kuchukua hatua fulani. Hatuwezi kuonyesha upendo wetu kwa maneno tu. Basi, jambo la maana ambalo tunapaswa kujiuliza ni: ‘Ninaweza kuonyesha jinsi gani kwamba ninampenda Mungu?’ Jibu linapatikana katika maneno haya ya mtume Yohana yaliyoongozwa na roho: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Tunapaswa kuchunguza kwa uangalifu maana ya maneno hayo, kwa kuwa tunataka kumwonyesha Mungu wetu jinsi tunavyompenda.

“KUMPENDA MUNGU HUMAANISHA HIVI”

4, 5. Eleza jinsi upendo wako kwa Yehova ulivyoanza kukua moyoni mwako.

4 “Kumpenda Mungu.” Mtume Yohana alikuwa akifikiria nini alipoandika maneno hayo? Alikuwa akizungumzia jinsi kila mmoja wetu anavyohisi kumwelekea Mungu. Je, unakumbuka wakati ambapo upendo wako kwa Mungu ulianza kukua moyoni mwako?

Kujiweka wakfu na kubatizwa ni mwanzo wa maisha ya kumtii Yehova kwa upendo

5 Fikiria mara ya kwanza ulipojifunza kweli kumhusu Yehova na makusudi yake na kuanza kuwa na imani. Ulipata kuelewa kwamba ingawa ulizaliwa katika dhambi na kutenganishwa na Mungu, Yehova kupitia Kristo alifungua njia ili ufikie ukamilifu ambao Adamu alipoteza na pia kukuwezesha kupata uzima wa milele. (Mathayo 20:28; Waroma 5:12, 18) Ulianza kuelewa jinsi Yehova alivyojidhabihu sana kwa kumtuma Mwana wake wa pekee ili afe kwa ajili yako. Ulichochewa, na kuanza kumpenda Mungu ambaye amekuonyesha upendo huo mwingi.—1 Yohana 4:9, 10.

6. Upendo wa kweli unaonyeshwa jinsi gani, na kumpenda Mungu kulikuchochea ufanye nini?

6 Hata hivyo, huo ulikuwa mwanzo tu wa kukuza upendo wa kweli kumwelekea Yehova. Upendo si hisia tu; wala hauonyeshwi kwa maneno matupu. Kumpenda Mungu kikweli kunahusisha mengi zaidi ya kusema tu “Ninampenda Yehova.” Kama imani, upendo wa kweli unaonekana kupitia matendo. (Yakobo 2:26) Kwa ufupi, upendo unaonekana kupitia matendo yanayompendeza yule tunayempenda. Hivyo, upendo kwa Yehova ulipotia mizizi moyoni mwako, ulichochewa kutaka kuishi kwa njia inayompendeza Baba yako wa mbinguni. Je, wewe ni Shahidi aliyebatizwa? Ikiwa ndivyo, upendo huo mwingi na ushikamanifu ulikuchochea kufanya uamuzi wa maana zaidi maishani mwako. Ulijiweka wakfu kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake, nawe ukaonyesha wakfu wako kwa kubatizwa. (Waroma 14:7, 8) Kutimiza wakfu wetu kwa Yehova kunahusisha jambo ambalo mtume Yohana anafuatia kutaja.

“TUZISHIKE AMRI ZAKE”

7. Taja amri fulani za Mungu na yale yanayohusika katika kuzishika.

7 Yohana anaeleza kwamba kumpenda Mungu kunamaanisha hivi: “Tuzishike amri zake.” Amri za Mungu ni nini? Kupitia Neno lake, Biblia, Yehova anatupa amri mbalimbali zilizo wazi. Kwa mfano, anakataza mazoea kama vile ulevi, uasherati, ibada ya sanamu, kuiba, na kusema uwongo. (1 Wakorintho 5:11; 6:18; 10:14; Waefeso 4:28; Wakolosai 3:9) Kuzishika amri za Mungu kunahusisha kuishi kulingana na viwango vya maadili vya Biblia vilivyo wazi.

8, 9. Ni kwa njia gani tunaweza kujua mambo yanayomfurahisha Yehova hata katika hali ambazo hakuna sheria ya moja kwa moja ya Biblia? Toa mfano.

8 Hata hivyo, ili kumpendeza Yehova tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kutii amri zake ambazo zinatajwa waziwazi. Yehova hatukandamizi kwa sheria kuhusu kila jambo katika maisha yetu ya kila siku. Hivyo, siku baada ya siku, huenda mara nyingi tukajikuta katika hali ambazo hakuna amri za Biblia zinazotajwa waziwazi. Katika hali hizo, ni kwa njia gani tunaweza kujua yale yanayompendeza Yehova? Biblia inaonyesha waziwazi maoni ya Mungu. Tunapojifunza Biblia, tunajua yale ambayo Yehova anapenda na yale anayochukia. (Zaburi 97:10; Methali 6:16-19) Tunapata kuelewa mitazamo na matendo ambayo anathamini. Kadiri tunavyojifunza utu na njia za Yehova, ndivyo maoni yake yatakavyotuongoza katika maamuzi na matendo yetu. Hivyo basi, hata katika hali ambazo hakuna sheria ya Biblia inayohusika, tunaweza kufahamu “yale yaliyo mapenzi ya Yehova.”—Waefeso 5:17.

9 Kwa mfano, Biblia haina amri ya moja kwa moja inayotukataza tusitazame sinema au vipindi vya televisheni ambavyo vinaonyesha jeuri au upotovu wa kingono. Lakini je, kwa kweli tunahitaji amri ya moja kwa moja inayotukataza tusitazame mambo hayo? Tunajua maoni ya Yehova kuhusu mambo hayo. Neno lake linatuambia hivi waziwazi: “Mtu yeyote anayependa jeuri nafsi [ya Yehova] hakika inamchukia.” (Zaburi 11:5) Pia linasema: “Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Tunapotafakari maneno hayo yaliyoongozwa na roho, tunaweza kufahamu waziwazi mapenzi ya Yehova. Kwa hiyo, tunachagua kutojiburudisha kwa kutazama picha zinazoonyesha waziwazi mazoea ambayo Mungu wetu anachukia. Tunajua kwamba tunampendeza Yehova tunapojiepusha na uchafu wa kiadili ambao ulimwengu huu unajaribu kuufanya uonekane kuwa burudani isiyo na ubaya wowote. *

10, 11. Kwa nini tunachagua kumtii Yehova, nasi tunampa utii wa aina gani?

10 Ni sababu gani ya msingi inayotuchochea kuzishika amri za Mungu? Kwa nini tunataka kuishi kila siku kulingana na maoni ya Mungu? Hatuchagui kufanya hivyo ili tusipate adhabu au ili kuepuka matokeo mabaya yanayowapata wale ambao wanapuuza mapenzi ya Mungu. (Wagalatia 6:7) Badala yake, tunaona kumtii Yehova kuwa njia ya pekee ya kumwonyesha kwamba tunampenda. Kama vile mtoto anavyotaka sana kukubaliwa na baba yake, ndivyo na sisi tunavyotaka kukubaliwa na Yehova. (Zaburi 5:12) Yeye ni Baba yetu, nasi tunampenda. Hakuna jambo linalotufurahisha na kuturidhisha zaidi kuliko kujua kwamba tunaishi katika njia inayotuwezesha ‘kupata kibali kutoka kwa Yehova.’—Methali 12:2.

11 Kwa hiyo, utii wetu si wa kulazimishwa; si wa kuchagua-chagua wala wenye masharti. * Hatuchagui sheria tutakazotii na zile tutakazopuuza, au kutii wakati ambapo kufanya hivyo ni kwa faida yetu au wakati ambapo hakuna ugumu wowote wa kufanya hivyo. Badala ya hivyo, tunatii “kutoka moyoni.” (Waroma 6:17) Maoni yetu ni kama ya mtunga-zaburi wa Biblia aliyeandika: “Nitapendezwa na amri zako ambazo nimezipenda.” (Zaburi 119:47) Ndiyo, tunapenda kumtii Yehova. Tunatambua kwamba anastahili, na anataka tumtii kikamili pasipo masharti. (Kumbukumbu la Torati 12:32) Tungependa Yehova aseme kutuhusu kama Neno lake linavyosema kumhusu Noa. Kuhusu mzee huyo mwaminifu, ambaye alionyesha kwamba anampenda Mungu kwa kutii kwa miaka mingi, Biblia inasema: “Noa akafanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Alifanya vivyo hivyo.”—Mwanzo 6:22.

12. Ni wakati gani utii wetu unapofanya moyo wa Yehova ushangilie?

12 Yehova anahisije tunapomtii kwa kupenda? Neno lake linasema kwamba tunafanya ‘moyo wake ushangilie.’ (Methali 27:11) Je, kweli utii wetu unafanya moyo wa Bwana Mwenye Enzi Kuu ushangilie? Bila shaka—na ana sababu nzuri ya kushangilia! Yehova alituumba tukiwa viumbe huru. Hiyo inamaanisha kwamba tuna uhuru wa kuchagua; tunaweza kuchagua kumtii Mungu au kutomtii. (Kumbukumbu la Torati 30:15, 16, 19, 20) Tunapochagua kumtii Yehova kutoka moyoni, na tunapofanya hivyo kwa sababu tunachochewa na upendo mwingi tulio nao kumwelekea Mungu, tunamfanya Baba yetu wa mbinguni ashangilie sana. (Methali 11:20) Pia tunachagua njia bora ya maisha.

“AMRI ZAKE SI MZIGO MZITO”

13, 14. Kwa nini tunaweza kusema kwamba amri za Mungu “si mzigo mzito”? Toa mfano.

13 Mtume Yohana anatupa uhakikisho wenye kutia moyo sana kuhusu mambo ambayo Yehova anataka tufanye: “Amri zake si mzigo mzito.” Tafsiri nyingine ya Biblia inasema hivi: “Amri zake hazitulemei.” (Neno—Agano Jipya) Mambo ambayo Yehova anataka tufanye si magumu sana wala yenye kukandamiza. * Wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kutii amri zake.

14 Mfano unaofuata unaweza kutusaidia kuelewa hali hiyo. Tuseme kwamba rafiki yako wa karibu anakuomba umsaidie kuhama. Kuna masanduku mengi yanayohitaji kubebwa. Masanduku fulani ni mepesi na mtu mmoja anaweza kuyabeba kwa urahisi, lakini mengine ni mazito na yanahitaji kubebwa na watu wawili. Rafiki yako anakuonyesha masanduku ambayo angependa ubebe. Je, anaweza kukuomba ubebe masanduku ambayo anajua huwezi hata kuyainua kwa kuwa ni mazito sana? Hapana. Hangetaka uumie kwa kujaribu kuyabeba ukiwa peke yako. Vivyo hivyo, Mungu wetu mwenye upendo na mwenye fadhili hatuambii tushike amri zilizo ngumu sana. (Kumbukumbu la Torati 30:11-14) Hawezi kamwe kutuomba tubebe mzigo mzito kama huo. Yehova anaelewa uwezo wetu, kwa maana “yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.”—Zaburi 103:14.

15. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika wa kwamba amri za Yehova zinatufaidi sana?

15 Amri za Yehova si mzigo mzito hata kidogo; badala yake zimekusudiwa kutufaidi sana. (Isaya 48:17) Hivyo, Musa angeweza kuwaambia Waisraeli wa kale hivi: ‘Yehova alituamuru tushike masharti yote haya, tumwogope Yehova Mungu wetu kwa ajili ya hali njema yetu sikuzote, ili tupate kuendelea kuwa hai kama ilivyo leo hii.’ (Kumbukumbu la Torati 6:24) Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika wa kwamba Yehova anapotupa sheria zake, ni kwa faida yetu, ndiyo, hali njema yetu ya milele. Huo ndio ukweli wa mambo! Yehova ni Mungu mwenye hekima isiyo na kifani. (Waroma 11:33) Kwa sababu hiyo anajua mambo ambayo yanatufaa zaidi. Pia Yehova ndiye mfano mzuri zaidi wa upendo. (1 Yohana 4:8) Upendo, sehemu kuu ya utu wake, unaongoza kila jambo ambalo anasema na kufanya. Ndio msingi wa amri zote anazowapa watumishi wake.

16. Ijapokuwa uvutano wa ulimwengu huu uliopotoka na hali yetu ya kutokamilika, kwa nini tunaweza kuendelea kuonyesha utii maishani?

16 Hiyo haimaanishi kwamba ni rahisi kumtii Mungu. Ni lazima tupambane na uvutano wa ulimwengu huu uliopotoka, ambao “unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Ni lazima pia tupambane na hali ya kutokamilika, ambayo inafanya tuwe na mwelekeo wa kuvunja sheria za Mungu. (Waroma 7:21-25) Lakini kumpenda Mungu kunaweza kutusaidia kushinda. Yehova anawabariki wale wanaotaka kuonyesha upendo wao kwake kwa kumtii. Anawapa roho yake takatifu “wale wanaomtii yeye akiwa mtawala.” (Matendo 5:32) Roho hiyo inatuwezesha kukuza matunda yenye kupendeza—sifa zenye thamani zinazoweza kutusaidia kuendelea kuonyesha utii maishani.—Wagalatia 5:22, 23.

17, 18. (a) Tutachunguza nini katika kitabu hiki, na tunapofanya hivyo, tunapaswa kukumbuka nini? (b) Sura inayofuata itazungumzia nini?

17 Katika kitabu hiki, tutachunguza kanuni na viwango vya maadili vya Yehova na mambo mengine mengi yanayoweza kutusaidia kujua mapenzi yake. Tunapofanya hivyo, tunahitaji kukumbuka mambo fulani ya maana. Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova hatulazimishi tutii sheria na kanuni zake; anataka tutii kwa kupenda na kutoka moyoni. Tusisahau kwamba Yehova anataka tuishi kwa njia ambayo itatufaidi sana sasa na kutuwezesha kupata uzima wa milele wakati ujao. Na tuuone utii wetu wa moyo wote kuwa nafasi ya pekee ya kumwonyesha Yehova kwamba tunampenda sana.

18 Kwa upendo, Yehova ametupa dhamiri itusaidie kutofautisha yaliyo sawa na yasiyo sawa. Hata hivyo, ili ituongoze vizuri, dhamiri yetu inahitaji kuzoezwa, kama tutakavyoona katika sura inayofuata.

^ fu. 9 Unaweza kupata habari zaidi katika Sura ya 6 ya kitabu hiki kuhusu jinsi ya kuchagua burudani inayofaa.

^ fu. 11 Hata roho waovu wanaweza kutii kwa kulazimishwa. Pindi fulani, Yesu alipowaamuru roho waovu wawatoke watu, roho hao waovu walilazimika kukubali mamlaka ya Yesu na kumtii, hata ingawa hawakutaka kufanya hivyo.—Marko 1:27; 5:7-13.

^ fu. 13 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mzigo mzito” kwenye 1 Yohana 5:3 linatafsiriwa ‘-enye kukandamiza’ kwenye Matendo 20:29, 30 na linazungumzia waasi-imani wenye kukandamiza ambao ‘wangesema mambo yaliyopotoka’ ili kuwapotosha watu.