Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 7

Je, Wakati Fulani Unajihisi Mpweke na Kuogopa?

Je, Wakati Fulani Unajihisi Mpweke na Kuogopa?

Hebu mwangalie mvulana huyu mdogo kwenye picha hii. Anaonekana ni mpweke na anaogopa, sivyo? Je, umewahi kuhisi hivyo?— Kila mtu huhisi hivyo nyakati fulani. Biblia inazungumza kuhusu marafiki wa Yehova ambao walihisi upweke na kuogopa. Mmoja wao ni Eliya. Acha tujifunze kumhusu.

Yezebeli alitaka kumuua Eliya

Eliya aliishi Israeli miaka mingi iliyopita, kabla Yesu hajazaliwa. Mfalme wa Israeli, Ahabu, hakuwa akimwabudu Mungu wa kweli, Yehova. Ahabu na mke wake, Yezebeli, walikuwa wakimwabudu mungu wa uwongo Baali. Hivyo, watu wengi nchini Israeli wakaanza kumwabudu Baali. Malkia Yezebeli alikuwa mkatili sana na alitaka kuwaua watu wote waliokuwa wakimwabudu Yehova, kutia ndani Eliya! Je, unajua Eliya alifanya nini?—

Eliya alikimbia! Alienda mbali jangwani na kujificha ndani ya pango. Unafikiri kwa nini alifanya hivyo?— Naam, aliogopa. Lakini Eliya hakupaswa kuogopa. Kwa nini? Kwa sababu alijua kwamba Yehova angeweza kumsaidia. Kabla ya tukio hilo, Yehova alikuwa amemwonyesha Eliya nguvu zake. Wakati fulani, Yehova alijibu sala ya Eliya kwa kutuma moto kutoka mbinguni. Kwa hiyo, Yehova angeweza kumsaidia Eliya wakati huu pia!

Yehova alimsaidiaje Eliya?

Eliya alipokuwa ndani ya pango, Yehova alizungumza naye na kumuuliza: ‘Unafanya nini hapa?’ Eliya akajibu: ‘Mimi tu ndiye niliyebaki ninayeendelea kukuabudu. Nimebaki peke yangu, na ninaogopa kwamba nitauawa.’ Eliya alifikiri kwamba waabudu wengine wote wa Yehova wameuawa. Lakini Yehova akamwambia Eliya: ‘Hapana, si kweli. Bado kuna watu wengine elfu saba ambao wananiabudu. Uwe jasiri. Bado una kazi nyingi ya kufanya!’ Je, unafikiri Eliya alifurahi kusikia hivyo?—

Unaweza kujifunza nini kutokana na yale yaliyompata Eliya?— Hupaswi kujihisi mpweke na kuogopa. Una marafiki ambao wanampenda Yehova na wanakupenda pia. Jambo lingine ni kwamba, Yehova ana nguvu nyingi sana, na nyakati zote atakusaidia! Je, umefurahi kujua kwamba kwa kweli wewe si mpweke?—