Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 8

Yosia Alikuwa na Marafiki Wazuri

Yosia Alikuwa na Marafiki Wazuri

Je, unafikiri ni vigumu kufanya mambo mazuri?— Watu wengi wanafikiri kwamba ni vigumu. Biblia inatuambia kuhusu mvulana aliyeitwa Yosia, inasema kwamba ilikuwa vigumu sana kwake kufanya mambo mazuri. Lakini, alikuwa na marafiki wazuri ambao walimsaidia kufanya mambo mazuri. Sasa, ngoja tujifunze mambo fulani yanayomhusu Yosia na rafiki zake.

Baba yake Yosia aliitwa Amoni, alikuwa mfalme wa Yuda. Amoni alikuwa mtu mbaya sana, na aliabudu sanamu. Baada ya baba ya Yosia kufa, Yosia akawa mfalme wa Yuda. Lakini alikuwa na miaka nane tu! Je, unafikiri alikuwa mbaya kama baba yake?— Hapana, Yosia alikuwa mtu mzuri!

Sefania aliwaonya watu wasiabudu sanamu

Hata alipokuwa mvulana mdogo sana, bado Yosia alitaka kumtii Yehova. Kwa hiyo, akachagua kuwa na marafiki waliompenda Yehova tu. Na kwa kweli, rafiki hao walimsaidia Yosia afanye mambo mazuri. Je, unawajua baadhi ya marafiki wa Yosia?

Sefania alikuwa mmoja wa marafiki hao. Sefania alikuwa nabii. Nabii huyo aliwaonya watu wa Yuda kwamba wangepatwa na mambo mabaya ikiwa wangeabudu sanamu. Yosia alimsikiliza Sefania, kwa hiyo alimwabudu Yehova, na wala hakuabudu sanamu.

Rafiki mwingine wa Yosia alikuwa Yeremia. Walikuwa wanakaribiana kwa umri, na tangu utotoni waliishi katika maeneo yaliyokaribiana. Walikuwa marafiki wakubwa sana, hivi kwamba Yosia alipokufa, Yeremia aliandika wimbo wa pekee, ili kuonyesha jinsi alivyomkumbuka sana Yosia. Yeremia na Yosia walisaidiana ili wafanye mambo mazuri na kumtii Yehova.

Yosia na Yeremia walisaidiana ili wafanye mambo mazuri

Unajifunza jambo gani katika mfano wa Yosia?— Hata alipokuwa mvulana mdogo sana, bado Yosia alitaka kufanya mambo mazuri. Alijua kwamba rafiki zake wanapaswa kuwa watu wanaompenda Yehova. Basi hakikisha kwamba unachagua marafiki wanaompenda Yehova na ambao wanaweza kukusaidia ufanye mambo mazuri!