Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 33

Atimiza Unabii wa Isaya

Atimiza Unabii wa Isaya

MATHAYO 12:15-21 MARKO 3:7-12

  • UMATI WAMSONGA YESU

  • ATIMIZA UNABII WA ISAYA

Anapogundua kwamba Mafarisayo na wafuasi wa chama cha Herode wanapanga kumuua, Yesu na wanafunzi wake wanaondoka na kwenda kwenye Bahari ya Galilaya. Umati mkubwa unamjia kutoka sehemu mbalimbali—Galilaya, majiji ya Tiro na Sidoni yaliyo pwani, eneo lililo upande wa mashariki wa Mto Yordani, Yerusalemu, na Idumea iliyo mbali upande wa kusini. Yesu anawaponya watu wengi. Kwa hiyo, wale walio wagonjwa sana wanajitahidi kuja mbele. Hawasubiri awaguse, bali wanajitahidi sana kumgusa.—Marko 3:9, 10.

Umati ni mkubwa sana hivi kwamba Yesu anawaambia wanafunzi wake wamtayarishie mashua ndogo ili asonge mbali na ufuo na hivyo kuzuia umati kumsonga. Pia, anaweza kuwafundisha akiwa kwenye mashua au hata kwenda sehemu nyingine kwenye ufuo ili awasaidie watu wengi zaidi.

Mwanafunzi Mathayo anataja kwamba matendo ya Yesu yanatimiza ‘maneno yaliyosemwa kupitia nabii Isaya.’ (Mathayo 12:17) Yesu anatimiza unabii gani?

“Tazama! Mtumishi wangu niliyemchagua, mpendwa wangu, ambaye nimemkubali! Nitaweka roho yangu juu yake, naye atayatangazia mataifa haki. Hatagombana wala kupiga kelele, wala yeyote hatasikia sauti yake kwenye barabara kuu. Hataponda tete lililovunjika, wala hatazima utambi unaofifia, hadi atakapofanikiwa kuleta haki. Kwa kweli, mataifa yatalitumainia jina lake.”​—Mathayo 12:18-21; Isaya 42:1-4.

Bila shaka, Yesu ndiye mtumishi mpendwa ambaye Mungu anamkubali. Yesu anafafanua wazi maana ya haki ya kweli, ambayo inafichwa na desturi za uwongo za kidini. Kwa kuwa wanafafanua Sheria ya Mungu kwa maoni yao wenyewe, Mafarisayo hata hawawezi kumsaidia mtu mgonjwa siku ya Sabato! Akionyesha wazi haki ya Mungu na kwamba roho ya Mungu iko juu yake, Yesu anawaondolea watu mzigo wa desturi zenye uonevu. Kwa sababu hiyo, viongozi wa kidini wanataka kumuua. Ni jambo la kusikitisha sana!

Inamaanisha nini kwamba “hatagombana wala kupiga kelele, wala yeyote hatasikia sauti yake kwenye barabara kuu”? Yesu anapowaponya watu, hawaruhusu watu hao—au roho waovu—‘wamtangaze.’ (Marko 3:12) Hataki watu wajifunze kumhusu kupitia matangazo ya barabarani yenye kelele au kupitia habari zisizo sahihi ambazo zinapitishwa kwa msisimko kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine.

Pia, Yesu anawatangazia ujumbe wake wenye kufariji watu ambao kwa njia ya mfano ni kama tete lililovunjika, lililoinama na kuangushwa. Wao ni kama utambi unaofifia, ambao mwanga wake wa mwisho uko karibu kwisha. Yesu hapondi tete lililovunjika wala kuzima utambi unaofifia na kutoa moshi. Badala yake kwa wororo na upendo anawainua wapole kwa ustadi. Kwa kweli, Yesu ndiye ambaye mataifa yanaweza kumtumainia!