Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 59

Mwana wa Binadamu Ni Nani?

Mwana wa Binadamu Ni Nani?

MATHAYO 16:13-27 MARKO 8:22-38 LUKA 9:18-26

  • YESU AMPONYA MWANAMUME KIPOFU

  • PETRO ATAPOKEA FUNGUO ZA UFALME

  • YESU ATABIRI KUHUSU KIFO NA UFUFUO WAKE

Yesu na wanafunzi wake wanawasili Bethsaida. Watu wanamletea mtu aliye kipofu na kumwomba Yesu amguse ili apone.

Yesu anamshika mtu huyo mkono na kumpeleka nje ya kijiji. Baada ya kutema mate kwenye macho ya mtu huyo, Yesu anamuuliza: “Je, unaona kitu chochote?” Mtu huyo anajibu: “Ninaona watu, lakini wanaonekana kama miti inayotembea.” (Marko 8:23, 24) Yesu anaweka mikono kwenye macho ya mtu huyo, na kumwezesha kuona. Kisha anamwambia mtu huyo ambaye sasa anaweza kuona vizuri aende nyumbani na anamwagiza asiingie kijijini.

Kisha Yesu na wanafunzi wake wanasafiri kuelekea kaskazini katika eneo la Kaisaria Filipi. Ni mwinuko mrefu wa kilometa 40 hivi. Kijiji hicho kiko kilometa 350 juu ya usawa wa bahari, na kaskazini mashariki kuna mlima Hermoni ulio na theluji. Huenda safari hiyo inachukua siku kadhaa.

Wanapofika mahali fulani njiani, Yesu anaenda kusali faraghani. Ni miezi tisa au kumi tu iliyobaki kabla ya kifo chake, na Yesu anawahangaikia wanafunzi wake. Hivi karibuni wengi wameacha kumfuata na wengine huenda wamechanganyikiwa au kuvunjika moyo. Huenda wanajiuliza kwa nini alipinga jitihada za watu za kumfanya awe mfalme au kwa nini hakutoa ishara ya kuthibitisha yeye ni nani hasa.

Wanafunzi wanapoenda mahali anaposali, Yesu anawauliza: “Watu wanasema Mwana wa binadamu ni nani?” Wanajibu: “Baadhi yao husema Yohana Mbatizaji, wengine Eliya, na bado wengine Yeremia au mmoja wa manabii.” Naam, watu wanafikiri kwamba huenda Yesu ni mmoja kati ya wanaume hao ambaye amefufuliwa kutoka kwa wafu. Ili kujua mawazo yao, anawauliza hivi wanafunzi wake: “Hata hivyo, ninyi mnasema mimi ni nani?” Petro anajibu hivi haraka: “Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.”—Mathayo 16:13-16.

Yesu anasema Petro anaweza kuwa na furaha kwa kuwa Mungu amemfunulia jambo hilo: “Ninakuambia: Wewe ni Petro, na juu ya mwamba huu nitajenga kutaniko langu, na malango ya Kaburi hayatalishinda.” Yesu anamaanisha kwamba yeye mwenyewe atalijenga kutaniko na kwamba hata Kaburi halitawafunga washiriki wake ikiwa wataendelea kuwa washikamanifu duniani. Anamwahidi Petro hivi: “Nitakupa funguo za Ufalme wa mbinguni.”—Mathayo 16:18, 19.

Yesu hampi Petro nafasi ya kwanza kati ya mitume wake, wala Yesu hamfanyi kuwa msingi wa kutaniko. Yesu mwenyewe ndiye Mwamba ambao kutaniko lake litajengwa juu yake. (1 Wakorintho 3:11; Waefeso 2:20) Hata hivyo, Petro atapokea funguo tatu. Atakuwa na pendeleo la kufungua kwa njia ya mfano, nafasi ya vikundi vya watu kuingia katika Ufalme wa mbinguni.

Petro angetumia ufunguo wa kwanza wakati wa Pentekoste 33 W.K., kuwaonyesha Wayahudi waliotubu na wageuzwa imani mambo wanayopaswa kufanya ili waokolewe. Angetumia ufunguo wa pili kuwafungulia nafasi ya kuingia katika Ufalme wa Mungu Wasamaria wanaoamini. Kisha mwaka wa 36 W.K., Petro angetumia ufunguo wa tatu kuwafungulia watu wa Mataifa ambao hawajatahiriwa, kama Kornelio na wengine.—Matendo 2:37, 38; 8:14-17; 10:44-48.

Katika mazungumzo hayo, mitume wa Yesu wanakuwa na wasiwasi anapotabiri kuhusu mateso na kifo ambacho atakabili hivi karibuni huko Yerusalemu. Bila kuelewa kwamba Yesu atafufuliwa na kuishi mbinguni, Petro anamwita kando na kumkemea akisema: “Bwana jihurumie; hutapatwa kamwe na mambo hayo.” Lakini Yesu anageuza mgongo wake na kujibu: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu hufikirii mawazo ya Mungu, bali ya wanadamu.”—Mathayo 16:22, 23.

Sasa Yesu anawaita watu wengine pamoja na mitume na kuwaeleza kwamba haitakuwa rahisi kuwa wafuasi wake. Anasema: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso na aendelee kunifuata. Kwa kuwa yeyote anayetaka kuokoa uhai wake ataupoteza, lakini yeyote anayeupoteza uhai wake kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema atauokoa.”—Marko 8:34, 35.

Naam, ili wastahili kupata kibali cha Yesu, lazima wafuasi wake wawe jasiri na wajidhabihu. Yesu anasema: “Yeyote atakayenionea aibu mimi na maneno yangu katika kizazi hiki chenye uzinzi na chenye dhambi, Mwana wa binadamu atamwonea aibu pia atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu.” (Marko 8:38) Naam, Yesu atakapokuja, “atamlipa kila mtu kulingana na mwenendo wake.”—Mathayo 16:27.