Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 74

Masomo Kuhusu Ukarimu na Sala

Masomo Kuhusu Ukarimu na Sala

SALA LUKA 10:38–11:13

  • YESU AWATEMBELEA MARTHA NA MARIA

  • NI MUHIMU KUENDELEA KUSALI

Kijiji cha Bethania kiko kwenye mteremko wa mashariki wa Mlima wa Mizeituni, karibu kilomita tatu kutoka Yerusalemu. (Yohana 11:18) Yesu anaenda huko na kuingia katika nyumba ya dada wawili, Martha na Maria. Wao na Lazaro ndugu yao ni marafiki wa Yesu, na wanamkaribisha kwa uchangamfu.

Ni pendeleo kutembelewa na Masihi. Martha anataka kumwandalia Yesu vizuri, basi anaanza kutayarisha chakula kitamu. Huku Martha akiendelea na kazi, Maria, dada yake, anaketi miguuni pa Yesu na kumsikiliza. Baada ya muda Martha anamwambia Yesu: “Bwana, hujali kwamba dada yangu ameniacha nishughulike peke yangu? Mwambie aje anisaidie.”—Luka 10:40.

Badala ya kumkemea Maria, Yesu anamshauri Martha kwa kuhangaikia sana maandalizi ya kimwili: “Martha, Martha, unasumbuka na kuhangaikia mambo mengi. Ni vitu vichache tu vinavyohitajiwa au kimoja tu. Maria alichagua fungu zuri, nalo halitaondolewa kwake.” (Luka 10:41, 42) Naam, Yesu anaonyesha kwamba si muhimu kutumia muda mwingi kutayarisha vyakula vingi. Mlo usio na vitu vingi unatosha.

Martha ana nia nzuri. Anataka kuonyesha ukarimu. Lakini kwa kuhangaikia sana chakula, anakosa maagizo yenye thamani kutoka kwa Mwana wa Mungu! Yesu anakazia kwamba Maria alifanya uamuzi wa hekima ambao utamletea manufaa ya kudumu na pia tunapata somo ambalo sisi sote tunapaswa kukumbuka.

Pindi nyingine, Yesu anafundisha somo tofauti ambalo pia ni muhimu. Mwanafunzi fulani anamuuliza: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali, kama vile Yohana alivyowafundisha wanafunzi wake.” (Luka 11:1) Tayari Yesu alikuwa amewafundisha kusali karibu mwaka mmoja na nusu uliopita kwenye Mahubiri yake ya Mlimani. (Mathayo 6:9-13) Hata hivyo, huenda mwanafunzi huyo hakuwapo wakati huo, basi Yesu anarudia mambo makuu. Kisha anatoa mfano ili kukazia umuhimu wa kuendelea kusali.

“Ikiwa mmoja wenu ana rafiki, naye aende kwake katikati ya usiku na kumwambia, ‘Rafiki, nikopeshe mikate mitatu, kwa sababu rafiki yangu amekuja kwangu kutoka safarini nami sina kitu cha kumpa.’ Lakini yule aliye ndani amjibu: ‘Acha kunisumbua. Tayari mlango umefungwa, nami na watoto wangu tumelala. Siwezi kuamka nikupe chochote.’ Ninawaambia ingawa hataamka na kumpa chochote kwa sababu yeye ni rafiki yake, kwa hakika ataamka na kumpa kwa sababu anaendelea kumwomba.”—Luka 11:5-8.

Yesu hamaanishi kwamba Yehova hayuko tayari kujibu maombi, kama yule rafiki. Badala yake, anaonyesha kwamba ikiwa rafiki asiyetaka atakubali kwa sababu anaombwa kwa kuendelea, bila shaka Baba yetu mpendwa wa mbinguni atajibu maombi ya unyoofu ya watumishi wake waaminifu! Yesu anaendelea: “Ninawaambia, endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa. Kwa maana kila mtu anayeomba hupokea, na kila mtu anayetafuta hupata, na kila mtu anayepiga hodi atafunguliwa.”—Luka 11:9, 10.

Kisha Yesu anakazia jambo kuu kwa kulinganisha na baba wa kibinadamu: “Ni baba gani kati yenu ambaye mwana wake akiomba samaki, atampa nyoka? Au pia akiomba yai, atampa nge? Kwa hiyo, ingawa ninyi ni waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi nzuri, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:11-13) Huo ni uhakikisho bora sana kwamba Baba yetu yuko tayari kutusikiliza na kujibu maombi yetu!