Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 96

Yesu Amjibu Mtawala Kijana Aliye Tajiri

Yesu Amjibu Mtawala Kijana Aliye Tajiri

MATHAYO 19:16-30 MARKO 10:17-31 LUKA 18:18-30

  • TAJIRI AULIZA KUHUSU UZIMA WA MILELE

Bado Yesu anasafiri kupitia Perea kuelekea Yerusalemu. Kijana fulani aliye tajiri anamkimbilia na kupiga magoti mbele yake. Mwanamume huyo ni mmoja wa ‘watawala,’ labda ni msimamizi wa sinagogi au mshiriki wa Sanhedrini. Anauliza: “Mwalimu Mwema, ninapaswa kufanya nini ili niurithi uzima wa milele?”—Luka 8:41; 18:18; 24:20.

Yesu anamjibu hivi: “Kwa nini unaniita mwema? Hakuna aliye mwema, isipokuwa mmoja, Mungu.” Huenda mwanamume huyo kijana anatumia jina “mwema” kama jina la cheo, jinsi ambavyo marabi hufanya. Ingawa Yesu anafundisha vizuri, anataka mwanamume huyo ajue kwamba “Mwema” ni cheo cha Mungu peke yake.

Yesu anamshauri hivi: “Hata hivyo, ikiwa unataka kuingia katika uzima, zishike amri sikuzote.” Basi kijana huyo anauliza: “Amri gani?” Yesu ananukuu Amri tano kati ya zile Amri Kumi—kuhusu kuua, uzinzi, wizi, kutoa ushahidi wa uwongo, na kuwaheshimu wazazi. Kisha anaongezea amri iliyo muhimu zaidi: “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.”—Mathayo 19:17-19.

Mwanamume huyo anajibu hivi: “Nimeyashika yote hayo; nifanye nini zaidi?” (Mathayo 19:20) Huenda anafikiri kwamba anahitaji kufanya tendo fulani zuri la kishujaa, ambalo litamfanya astahili kupata uzima wa milele. Anapotambua unyoofu wa ombi lake, Yesu ‘anampenda’ mtu huyo. (Marko 10:21) Hata hivyo, mwanamume huyo anakabili kikwazo fulani.

Mtu huyo anapenda sana mali zake, basi Yesu anasema: “Bado unahitaji kufanya jambo moja: Nenda ukauze vitu ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha uje uwe mfuasi wangu.” Naam, mwanamume huyo anaweza kuwapa maskini pesa zake, ambao hawawezi kumlipa, kisha awe mwanafunzi wa Yesu. Lakini labda akimsikitikia, Yesu anamtazama anapoinuka na kuondoka akiwa amehuzunika. Kwa kuwa mtu huyo anapenda utajiri, yaani, “mali [zake] nyingi,” anakosa kutambua hazina ya kweli. (Marko 10:21, 22) Yesu anasema: “Itakuwa vigumu sana kwa wale walio na pesa kuingia katika Ufalme wa Mungu!”—Luka 18:24.

Wanafunzi wanashangazwa na maneno hayo na jambo ambalo Yesu anaongezea kusema: “Kwa kweli, ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano ya kushonea kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.” Jambo hilo linawafanya wanafunzi wake waulize: “Ni nani anayeweza kuokolewa?” Je, kuokolewa ni jambo gumu sana hivi kwamba mtu hawezi kulipata? Yesu anawatazama na kuwajibu: “Mambo yasiyowezekana kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.”—Luka 18:25-27.

Petro anaonyesha kwamba wamefanya uamuzi tofauti na yule mwanamume, anaposema: “Tazama! Tumeacha kila kitu na kukufuata; basi tutapata nini?” Yesu anataja matokeo ya uamuzi wao mzuri: “Katika uumbaji mpya, Mwana wa binadamu atakapoketi katika kiti chake cha ufalme chenye utukufu, ninyi ambao mmenifuata mtaketi katika viti vya ufalme 12, mkiyahukumu makabila 12 ya Israeli.”—Mathayo 19:27, 28.

Ni wazi kwamba Yesu anafikiria wakati ujao duniani kutakapokuwa na uumbaji mpya wa hali kama zilizokuwa katika bustani ya Edeni. Petro na wanafunzi wengine watathawabishwa kwa kutawala pamoja na Yesu juu ya dunia Paradiso, kwa kweli ni thawabu inayozidi jambo lolote wanaloweza kujidhabihu!

Hata hivyo, hawatathawabishwa tu wakati ujao. Wanafunzi wake wanathawabishwa hata sasa. Yesu anasema: “Hakuna yeyote ambaye ameacha nyumba, au mke, au ndugu, au wazazi, au watoto kwa ajili ya Ufalme wa Mungu ambaye hatapata mara nyingi zaidi wakati huu, na katika mfumo wa mambo unaokuja, uzima wa milele.”—Luka 18:29, 30.

Naam, kokote ambako wanafunzi wake wanaenda wanaweza kufurahia undugu pamoja na waabudu wenzao ambao ni wa karibu na wenye thamani kuliko uhusiano kati ya watu wa familia moja. Inasikitisha kwamba huenda yule kijana tajiri atakosa baraka hiyo na pia thawabu ya uzima katika Ufalme wa mbinguni wa Mungu.

Yesu anaongezea hivi: “Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho na wa mwisho watakuwa wa kwanza.” (Mathayo 19:30) Anamaanisha nini?

Yule mtawala kijana aliye tajiri ni kati ya watu wa “kwanza,” akiwa mmoja wa viongozi wa Wayahudi. Kwa kuwa anashika amri za Mungu, ana uwezo mkubwa na anatarajiwa kutimiza mengi. Lakini anatanguliza utajiri na mali kuliko kitu kingine maishani. Kinyume chake, watu wa kawaida wa nchi hiyo wanayaona mafundisho ya Yesu kuwa ya kweli na njia ya uzima. Kwa maneno mengine walikuwa wa “mwisho,” lakini sasa wanakuwa wa “kwanza.” Wanaweza kutazamia kuketi kwenye viti vya ufalme mbinguni pamoja na Yesu na kutawala juu ya dunia Paradiso.