Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 89

Afundisha Huko Perea Akiwa Njiani Kwenda Yudea

Afundisha Huko Perea Akiwa Njiani Kwenda Yudea

LUKA 17:1-10 YOHANA 11:1-16

  • UZITO WA KOSA LA KUKWAZA

  • SAMEHE NA UWE NA IMANI

Kwa muda fulani, Yesu amekuwa katika eneo la Perea, lililo “ng’ambo ya Yordani.” (Yohana 10:40) Sasa anasafiri kuelekea kusini huko Yerusalemu.

Yesu hayuko peke yake. Anasafiri pamoja na wanafunzi wake, na vilevile “umati mkubwa,” unaotia ndani wakusanya kodi na watenda dhambi. (Luka 14:25; 15:1) Pia, Mafarisayo na waandishi, ambao wanashutumu mambo ambayo Yesu anasema na kufanya, wako hapo. Wana mambo mengi ya kufikiria baada ya kumsikia Yesu akisimulia mifano kuhusu kondoo aliyepotea, mwana aliyepotea, na tajiri na Lazaro.—Luka 15:2; 16:14.

Labda akikumbuka jinsi alivyodhihakiwa na kukosolewa na wapinzani wake, Yesu anawaelekezea fikira wanafunzi wake. Anataja baadhi ya mambo aliyokuwa amefundisha huko Galilaya.

Kwa mfano, Yesu anasema: “Lazima vikwazo vije. Hata hivyo, ole wake mtu atakayevisababisha! . . . Jiangalieni ninyi wenyewe. Ndugu yako akitenda dhambi mkemee, na akitubu, msamehe. Hata akikutendea dhambi mara saba kwa siku, naye anarudi kwako mara saba akisema, ‘ninatubu,’ unapaswa kumsamehe.” (Luka 17:1-4) Huenda maneno hayo ya mwisho yanamkumbusha Petro swali alilouliza kuhusu kusamehe mpaka mara saba.—Mathayo 18:21.

Je, wanafunzi wataweza kutenda kulingana na maneno ya Yesu? Wanapomwambia Yesu, “Tusaidie tuwe na imani zaidi,” anawahakikishia hivi: “Kama mngekuwa na imani inayolingana na mbegu ya haradali, mngeuambia mti huu wa mforsadi, ‘Ng’oka ukapandwe baharini!’ nao ungewatii.” (Luka 17:5, 6) Naam, hata kiasi kidogo cha imani kinaweza kutimiza mengi.

Kisha Yesu anafundisha kuhusu umuhimu wa mtu kuwa na mtazamo wa unyenyekevu na wenye usawaziko kujielekea, anapowaambia hivi mitume: “Ni nani kati yenu aliye na mtumwa anayelima shamba au kuchunga wanyama, ambaye akirudi kutoka shambani, atamwambia ‘Njoo upesi, keti ule chakula’? Hapana. Badala yake atamwambia, ‘Nitayarishie chakula cha jioni, na ujifunge vazi la kazi ili unihudumie mpaka nitakapomaliza kula na kunywa, kisha unaweza kula na kunywa.’ Je, utamshukuru mtumwa huyo kwa sababu alifanya mambo uliyomwagiza? Vivyo hivyo, baada ya kufanya mambo mliyoagizwa, semeni: ‘Sisi ni watumwa wasiofaa kitu. Tumefanya kile tulichopaswa kufanya.’”—Luka 17:7-10.

Kila mtumishi wa Mungu anapaswa kuelewa umuhimu wa kutanguliza mapenzi ya Mungu. Isitoshe, kila mmoja anapaswa kukumbuka pendeleo lake la kumwabudu Mungu akiwa mshiriki wa nyumba yake.

Inaonekana kwamba baada ya hapo, mjumbe aliyetumwa na Maria na Martha anawasili. Wao ni dada za Lazaro, nao wanaishi huko Bethania ya Yudea. Mjumbe huyo anasema hivi: “Bwana, ona! yule unayempenda ni mgonjwa.”—Yohana 11:1-3.

Ingawa anapata habari kwamba Lazaro rafiki yake amekufa, Yesu halemewi na huzuni. Badala yake anasema: “Lengo la ugonjwa huu si kusababisha kifo, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kupitia huo.” Anakaa mahali hapo kwa siku mbili kisha anawaambia wanafunzi wake: “Twendeni tena Yudea.” Wanapinga wakisema: “Rabi, juzijuzi tu Wayudea walitaka kukupiga mawe, nawe unarudi huko tena?”—Yohana 11:4, 7, 8.

Yesu anawajibu hivi: “Kuna saa 12 za mchana, sivyo? Yeyote akitembea mchana hatajikwaa, kwa sababu anaona mwangaza wa ulimwengu huu. Lakini ikiwa yeyote anatembea usiku, atajikwaa kwa sababu hana nuru ndani yake.” (Yohana 11:9, 10) Inaonekana anamaanisha kwamba muda ambao Mungu ameweka kwa ajili ya huduma ya Yesu bado haujaisha. Hadi utakapokwisha, Yesu anahitaji kutumia kikamili muda wake mfupi uliobaki.

Yesu anaongezea hivi: “Rafiki yetu Lazaro amelala usingizi, lakini ninasafiri kwenda huko ili kumwamsha.” Labda wakifikiri kwamba Lazaro anapumzika tu na kwamba atapona, wanafunzi wanasema: “Bwana, ikiwa amelala usingizi, atapona.” Yesu anawaambia hivi waziwazi: “Lazaro amekufa . . . Lakini twendeni kwake.”—Yohana 11:11-15.

Akiwa anajua kwamba Yesu anaweza kuuawa huko Yudea, lakini akitaka kumuunga mkono, Tomasi anawahimiza hivi wanafunzi wenzake: “Sisi pia, twendeni tukafe pamoja naye.”—Yohana 11:16.